Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 12/15 kur. 20-22
  • ‘Kuwaogopa Wanadamu Kunaleta Mtego’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Kuwaogopa Wanadamu Kunaleta Mtego’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Kuhofu Mungu, Si Wanadamu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kuogopa Mungu Je! Kunaweza Kukunufaisha Wewe?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Sitawisha Moyo wa Kumhofu Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Sababu Tano za Kumwogopa Mungu na Si Mwanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 12/15 kur. 20-22

‘Kuwaogopa Wanadamu Kunaleta Mtego’

JOHN na Helen waliendelea kupendezwa na habari walizoambiwa kwenye mlango wao na Shahidi mwenye kusema nao asubuhi moja ya Jumapili. Walisisimuka kuyasoma maneno haya ya Ufunuo 21:4 kwenye Biblia yao wenyewe: “Naye [Yehova Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” Kwa kuwa wao wenyewe walikuwa wapenda amani, walitaka kujua jinsi wangeweza kufurahia kuishi chini ya hali hizo nzuri ajabu. Moja kwa moja funzo la Biblia likapangwa.

Nyakati za usiku za Jumatano tatu zilizofuata, lilikuwa jambo la kupendeza kuwaona vijana wawili hao waliooana wakiuliza na kujibu maulizo wakati funzo la Biblia lilipoongozwa katika nyumba yao. Woo-we, furaha hiyo ikawa ya juma tatu tu! Ile juma ya nne, hawakumfungulia Shahidi mlango alipogonga hodi. John na Helen walikuwa wameamua kuacha funzo lao la Biblia. Kwa sababu gani? Je! ni kwa sababu walikuwa wameacha kuuamini uwezo wa Mungu? Je! walikuwa wameanza kutilia mashaka uhalisi wa Biblia na ukweli wayo? Je! wao hawakupendezwa tena na kuishi chini ya hali bora? Haikuwa hivyo. Hizo sizo zilizokuwa sababu? Wao waliacha kujifunza kwa sababu ya kuogopa wanadamu. Naam, walinaswa na mtego wa woga. Karne nyingi zilizopita, yule mwanamume mwenye hekima aliyeongozwa na Mungu alitoa onyo juu ya woga huo, akisema: “Kuwaogopa wanadamu huleta mtego.”​—Mit. 29:25.

Ni kweli kwamba sisi sote tumezaliwa tukiwa na tamaa ya kupendwa na wengine, kunenewa mambo mema na jirani zetu, rafiki zetu na watu ambao huonana nasi. Walakini, ni jambo la hatari sana kuacha kanuni za wengine ziongoze maamuzi yaliyo ya maana zaidi katika maisha yetu. Ikiwa mtu anajisikia kwamba ni lazima atimize kwa njia zote mambo anayotazamiwa kufanya na watu wa mtaa wake, na kuishi kulingana na kanuni za watu hao, huyo atakuwa mtumwa wa kujipatanisha na matakwa yao. Na tamaa yenye nguvu ya kutaka kukubaliwa na wengine inaweza kuzuia sana mtu asichukue hatua za uhakika awe mtumishi wa Mungu.

Watu wengi leo hawampendi Mungu, hawamheshimu wala hawamwogopi. Ama hawana tamaa ya kujifunza habari zake, ama wanatia shaka juu ya hata kama yeye yuko. Kwa hiyo, huenda mtu akafanyiwa dhihaka na kuacha kuheshimiwa na wengine kwa sababu anaonyesha anapendezwa na Biblia. Ni wazi kwamba katika mkazo kama huo, kuogopa mwanadamu kungefanya iwe vigumu sana mtu azidi kufanya maendeleo ya kiroho.

Matokeo mabaya sana ya kukubali kushindwa kwa sababu ya kuogopa mwanadamu yameonyeshwa vizuri katika kisa cha Mfalme Sauli wa Israeli ya kale. Wakati nabii Samweli alipomkabili amwulize habari za kushindwa kwake kuyatimiza maagizo ya kimungu katika shughuli kubwa ya kuwashambulia Waamaleki, Sauli alikubali hivi: “Naliwaogopa wale watu, nikaitii sauti yao.” Matokeo ya mwendo huo yalikuwa nini? Yeye aliambiwa: “Umelikataa neno la [Yehova], [Yehova] naye amekukataa wewe, usiwe [usiendelee kuwa, NW] mfalme wa Israeli.”​—1 Sam. 15:24,26.

Ikiwa hatutaki tukataliwe na Mwenye Nguvu Zote, tunahitajiwa kabisa tujitahidi kuhangaikia zaidi msimamo wetu mbele zake kuliko msimamo wetu mbele ya wanadamu. Biblia inasema: “Kumcha [Yehova] ndio mwanzo wa hekima.” (Zab. 111:10) Kumcha (kumwogopa) hivyo kunafaa nako kunatokana na tamaa ya moyoni ya kujisikia hutaki kumchukiza Aliye Juu Zaidi. Kunalinganika na nia ya mwana mtiifu kuelekea baba mwenye upendo. Mwana hataki kufanya lo lote linaloweza kumhuzunisha baba yake au linaloweza kuleta lawama juu ya jina lake zuri. Basi, imekuwa vizuri kwamba njia moja ya kumwogopa Mungu ni kuchukia mambo anayoyachukia, na kupenda mambo anayoyapenda. —Mit. 8:13.

Ili kumwogopa Mungu, mtu anahitajiwa akumbuke kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kumpa yeye uzima wa milele na kumtunza nyakati zote na chini ya hali zote. Mtunga zaburi mwenye kuongozwa na Mungu alionyesha maoni yanayofaa kuhusu jambo hilo wakati alipoandika hivi: “Usiogope mtu atakapopata utajiri, na fahari ya nyumba yake itakapozidi. Maana atakapokufa hatachukua cho chote; utukufu wake hautashuka ukimfuata.” (Zab. 49:16, 17) “Hao wanaozitumainia mali zao, na kujisifia wingi wa utajiri wao; hakuna mtu awezaye kumkomboa ndugu yake, wala kumpa Mungu fidia kwa ajili yake.” (Zab. 49:6, 7) Walakini, Mwenye Enzi Kuu Ipitayo Zote anaweza kusaidia mtu apite hali zenye majaribu makali sana na hata kumwokoa na kifo. (Zab. 49:15) Kwa kweli, Mungu anatutolea uhakikisho huu: “Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.”​—Ebr. 13:5.

Hata kama wanadamu wakituua, hawawezi kutuzuia tusiinuliwe kutoka kwa wafu. Wao hawawezi kutuondolea haki yetu ya kuwa watu walio hai. Anayeweza ni Mungu Mwenye Nguvu Zote peke yake. Kwa sababu hiyo, Yesu Kristo aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Msiwe wenye kuogopa wale wauuao mwili lakini hawawezi kuiua nafsi; bali badala yake iweni na woga wa huyo ambaye anaweza kuharibu nafsi na mwili pia katika Gehena.”​—Mt. 10:28, NW.

Basi, kwa uhakika hata hakuna sababu kubwa ya kuogopa malawama au dhihaka za wanadamu wanaoweza kufa. Neno la Yehova kupita kwa Isaya linatutia sana moyo kwa habari hii. Tunasoma hivi: “Nisikilizeni, ninyi mjuao haki, watu ambao mioyoni mwenu mna sheria yangu; msiogope matukano ya watu, wala msifadhaike kwa sababu ya dhihaka zao. Maana nondo itawala kama vazi, na funza atawala kama sufu.”​—Isa. 51:7, 8.

Tunapoufikiria ukubwa wa Muumba na kuutofautisha na udogo wa mwanadamu, tunasaidika tuwe huru tuache kuogopa wanadamu. Machoni pa Yehova Mungu, mataifa yote ni kitone kidogo sana cha maji katika ndoo au kivumbi chepesi sana juu ya mizani. (Isa. 40:11-15) Loo! ungekuwa upumbavu namna gani kuogopa kitone cha maji ambacho si kitu kikubwa au kisehemu kidogo sana cha vumbi badala ya kumwogopa Mtengenezaji ulimwengu mzima wenye vitu vya kustaajabisha mno!

Tunaweza pia kutiwa moyo na uhakika wa kwamba wengine wamefaulu kujizuia wasiogope mwanadamu. Petro mtume wa Kikristo aliwakumbusha waamini wenzake kwamba “mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani.” (1 Pet. 5:9) Naam, sisi hatuko peke yetu katika kusimama imara tumtetee Yehova Mungu kwa kukabiliana na mikazo ya wanadamu.

Ungekuwa upumbavu mkubwa kweli kweli kuogopa kwa sababu ya wanadamu, kujaribu kupendeza wanadamu na huku tukimchukiza Muumba Mwenye Nguvu Zote. Kwa sababu John na Helen hawakumtumaini Yehova, wao walipoteza furaha yao. Tunatumaini kwamba siku moja kabla ya ile “dhiki kubwa” inayoendelea kuja wao na wengine walio kama wao watapata uhakika wenye nguvu wamtumaini Aliye Juu Zaidi na kuwa na maoni kama ya mtunga zaburi, aliyesema: “[Yehova] ni nuru yangu na wokovu wangu, nimwogope nani? [Yehova] ni ngome ya uzima wangu, nimhofu nani?”​—Zab. 27:1.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Je! dhihaka zitasimamisha funzo hili la Biblia?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki