Je! Mileani (Miaka Elfu) ya Amani Ni Ndoto Tu?
“Ile Milki ya Tatu ambayo ilizaliwa Januari 30, 1933, ingeendelea kwa miaka elfu, akajisifu Hitler, na katika usemi wa Nazi iliitwa ‘Milki ya Miaka Elfu.’ “—The Rise and Fall of the Third Reich, by W. Shirer.
WEWE wajua ilivyotukia. Ndoto ya Hitler ya miaka elfu (au mileani) haikutimizwa. Walakini je! wewe wajua kwamba watu wengi wamekuwa wakitazamia mbele kwenye utawala wa miaka elfu halisi ya amani? Dakt. W. Lee wa Chuo Kikuu cha Dublin alisema hivi: “Makisio ya kilimwengu na ya kidini yana ndoto yao ya Mileani.”
Mara nyingi “ndoto” hiyo imetia ndani imani katika Wakati Mzuri sana utakaorudishwa katika wakati ujao. Kwa mfano, ukizuru Iran, waweza kusikia habari juu ya “Wakati Mzuri Sana pasipokuwa na makosa, ugonjwa na mauti.” Bushmen (watu wanaokaa msituni) wa Afrika Kusini husema juu wa wakati uliopita wakati ambapo wanadamu na wanyama waliishi Pamoja kwa amani. Kikiripoti juu ya imani hizi, kitabu The Encyclopedia of Religion and Ethics kinasema kwamba Wazo la “Wakati Mzuri Sana wa wakati ulipita, uliopotezwa kwa sababu ya makosa ya mwanadamu,” mara nyingi ulifungamanishwa na “tumaini la kwamba mambo yatakuwa mazuri zaidi katika wakati ujao,”
Lakini je! matumiani kama hayo ni ndoto tu? Ebu fikiria mambo yanayokujia kila siku—ripoti juu ya uvunjaji wa sheria, kupanda kwa bei ya vitu, uchafu, ghasia za raia pamoja na vita. Ni watu wachache sana ambao wangeona katika mambo haya msingi wo wote wa kuamini juu ya enzi ijayo ya amani na ufanisi. Ripoti ya Septemba 1976 juu ya mkutano wa Chuo cha Mataifa Yote cha Masomo juu ya enzi ijayo ya amani na ufanisi. Baden, Austria, ilisema hivi: “Wale watu wanaotumia wakati wao wakijifunza juu ya mambo ya hakika yanayoongoza kwenye vita [hawana] tena hata ufumbuzi wa kukisia wa kupata kile kilichoahidiwa wakati mmoja kama kizazi cha amani.”
Hata hivyo, unaweza kusoma jambo fulani katika Biblia linalotoa sababu nzito ya kufikiri kwamba mileani ya amani si jambo la kutupiliwa mbali kama ndoto tu. Zaidi ya hayo, inatoa ahadi ya mambo ambayo, yakitimizwa, yangefanya maisha zetu ziwe zenye maana na zenye kufurahisha zaidi. Karibu na mwisho wa Biblia utaona haya:
“[Naye malaika] akamshika yule yoka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu; . . . asipate kuwadanganya mataifa tena, hata ile miaka elfu itimie. . . . Naye [Mungu] atafuta kila chozi katika macho [ya wanadamu], wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufu. 20:1-3; 21:4.
Maelezo hayo yajaposikika kuwa yenye kupendeza sana, ni kwa sababu gani tuna sababu zaidi ya kutazamia yatimizwe kuliko lo lote la yale matumaini mengine mileani kutia na ile Milki ya Nazi ya Miaka Elfu? Kuna sababu moja yenye nguvu. Mileani hii ya amani imeahidiwa na Yehova Mungu. Pindi moja, wakati mtu mmoja alipomwambia Yesu kwamba jambo fulani lilionekana kutowezekana, Mwana wa Mungu alijibu hivi: “Yasiyowezekana kwa wanadamu yawezekana kwa Mungu.”—Luka 18:27.
Lakini je! Biblia yasema kweli kweli kwamba Mungu ataleta katika wakati ujao miaka elfu halisi ya amani hapa duniani? Je! ndivyo inavyotupasa kufahamu yale yanayosemwa na Maandiko? Kwa sababu ya kupendezwa na uwezekano wa baraka za ajabu kwa ajili yetu sisi wenyewe na jamaa zetu, yatupasa tuhakikishe kama mileani hiyo ya amani ni zaidi ya ndoto tu.