Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● Kazini pangu kila mwajiriwa hupewa bakshishi (zawadi) ya Krismasi. Kwa kuwa mimi siiamini Krismasi, je! inanipasa kuikataa bakshishi hiyo?
Hiyo inategemea ni nini hasa inayomaanishwa na bakshishi hiyo na jinsi kuikubali kunavyoweza kuonwa.
Kama vile ambavyo tumekwisha kuonyesha mara nyingi, Krismasi pamoja na sikukuu nyinginezo za Jumuiya ya Wakristo hazina msingi wa Biblia. Kwa kweli, zimechukuliwa kutoka kwa ibada isiyo ya Kikristo.a Biblia inawaamuru Wakristo waadhimishe mwadhimisho mmoja tu wa kidini, kifo ,cha Kristo kinachoadhimishwa mara moja tu kila mwaka.—Luka 22:19, 20.
Je! kukubali “bakshishi ya Krismasi” kungemaanisha kwamba mtu huyo anashiriki katika kuadhimisha sikukuu hiyo? Pengine sivyo. Huenda ikawa kwamba bakshishi hiyo haionwi ikimaanisha kwamba kila mtu anayeipokea anaadhimisha Krismasi. Huenda tajiri akawa ameamua tu kuwapa waajiriwa wake wote sehemu ya mapato ya kampuni mwishoni mwa mwaka wakati ambapo wengi wao wangethamini sana sana kupata kiasi fulani cha fedha watumie kama wapendavyo. Bakshishi hiyo yaweza kuwa ushuhuda wa shukrani kwa ajili ya utumishi uliotolewa kwa kipindi chote cha mwaka, na vilevile kama kichocheo cha kuendelea kufanya kazi vizuri pamoja na kudumisha uhusiano mzuri kati ya tajiri na wafanya kazi. Tajiri aweza kuwapa waajiriwa wote bakshishi hiyo, bila kujali kama wengine, kama vile Wayahudi, Waislamu au wengineo, hawaiamini Krismasi. Kwa hiyo wakati wenyewe wa kutolewa kwa zawadi hiyo au jina ambalo limekuja kushikamanishwa nayo, kwa lazima halina maana kwamba mmoja wa Mashahidi wa Yehova hawezi kuikubali.
Vilevile, hata ikiwa mwenye kutoa zawadi anafanya hivyo katika wakati fulani kwa sababu ya imani ya kidini, haimaanishi kwamba inadhaniwa kwamba mwenye kuipokea anashiriki maoni hayo ya kidini. Mara nyingi mfanya kazi mwenzi au mshiriki wa jamaa humwambia mmoja wa Mashahidi wa Yehova, ‘Najua kwamba wewe husherehekei Krismasi (au, sikukuu nyingineyo), hata hivyo bado nataka kukupa zawadi hii.’ Ikiwa dhamiri ya Mkristo haitamsumbua akikubali zawadi hiyo, aweza kuamua kuipokea na kuonyesha shukrani bila kutaja sikukuu hiyo. (Matendo 23:1) Mwendo uo huo umefuatwa na Wakristo wengi wanapotolewa zawadi na mtu asiyejua juu ya imani yao. Pengine, wakati mwingine, wakati haitaelekea kumwudhi sana mtu huyo, Mkristo huyo atataja kwa busara kwamba yeye hasherehekei sikukuu hiyo ya kidini naye aweza kueleza kwa njia ya fadhili na ya upole kwamba ndiyo sababu yeye hatoi zawadi zo zote za sikukuu.—1 Pet. 3:15.
Walakini ikiwa zawadi inatolewa kwa kusudi lililo wazi la kuonyesha kwamba Mkristo si imara katika imani yake au kwamba anaweza kuvunja ukamilifu wake ili ajipatie kitu fulani, basi ni wazi kwamba inafaa kuikataa. Inawapasa Wakristo wamwabudu Yehova Mungu. Yeye peke yake twamtolea utumishi mtakatifu.—Mt. 4:8-10.
[Maelezo ya Chini]