Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 12/15 kur. 4-7
  • Mizizi ya Krismasi ya Kisasa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mizizi ya Krismasi ya Kisasa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Msingi Wenye Kasoro
  • Ufisadi Waingizwa
  • Sikukuu ya Kimataifa
  • Kubadilishwa kwa Krismasi
  • ‘Penda Kweli na Amani’
  • Je! Ni Lazima Wewe Usherehekee Krismasi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Krismasi—Kwa Nini Inapendwa Sana Katika Japani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Krismasi—Mbona Husherehekewa Hata Mashariki?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Krismasi (Noёl) Ilianza Zamani Sana
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 12/15 kur. 4-7

Mizizi ya Krismasi ya Kisasa

KWA mamilioni ya watu ulimwenguni pote, majira ya Krismasi ni wakati wa mwaka wenye shangwe sana. Ni wakati wa milo ya bei ya juu, mapokeo yenye kuheshimiwa kwa sababu ya ukale wake, na wa kuwa pamoja kifamilia. Sikukuu ya Krismasi pia ni wakati ambapo marafiki na jamaa huonea shangwe kubadilishana kadi na zawadi.

Hata hivyo, miaka 150 iliyopita, Krismasi ilikuwa sikukuu tofauti sana. Katika kitabu chake The Battle for Christmas, profesa wa historia Stephen Nissenbaum aandika hivi: “Krismasi . . . ilikuwa wakati wa unywaji wa kupindukia wakati ambapo kanuni zilizoongoza tabia ya watu hadharani ziliachwa kwa muda kwa kupendelea ‘kanivali’ isiyo na vizuizi, aina fulani ya sherehe ya Desemba iliyo kama sherehe ya kabla ya Kwaresima.”

Kwa wale ambao huitazama Krismasi kwa kicho chenye staha, ufafanuzi huo huenda ukawashtusha sana. Kwa nini yeyote angechafua sikukuu ambayo yadai kuadhimisha kuzaliwa kwa Mwana wa Mungu? Huenda jibu likakushangaza.

Msingi Wenye Kasoro

Tangu ilipoanzishwa karne ya nne, Krismasi imezingirwa na ubishi. Kwa mfano, kulikuwa na lile swali juu ya siku ya kuzaliwa kwa Yesu. Kwa kuwa Biblia haitaji siku wala mwezi wa kuzaliwa kwa Kristo, tarehe mbalimbali zimedokezwa. Katika karne ya tatu, kikundi kimoja cha wanatheolojia Wamisri kiliweka siku hiyo kuwa Mei 20, huku wengine wakipendelea tarehe za mapema zaidi kama vile Machi 28, Aprili 2, au Aprili 19. Kufikia karne ya 18, kuzaliwa kwa Yesu kulikuwa kumeshirikishwa na kila mwezi wa mwaka! Basi, Desemba 25 ilichaguliwaje mwishowe?

Wasomi walio wengi hukubali kwamba Desemba 25 iliagizwa na Kanisa Katoliki kuwa siku ya kuzaliwa kwa Yesu. Kwa nini? “Yaelekea sana sababu,” chasema kichapo The New Encyclopædia Britannica, “ni kwamba Wakristo wa mapema walitaka hiyo tarehe isadifiane na msherehekeo wa kipagani wa Roma uliotia alama ‘siku ya kuzaliwa kwa jua lisiloshindwa.’” Lakini kwa nini Wakristo ambao walikuwa wamenyanyaswa na wapagani kwa zaidi ya karne mbili na nusu kwa ghafula waliwaachia nafasi wanyanyasaji wao?

Ufisadi Waingizwa

Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alionya Timotheo kwamba “watu waovu na walaghai” wangepenya ndani ya kutaniko la Kikristo na kuwaongoza vibaya watu wengi. (2 Timotheo 3:13) Uasi-imani huu mkubwa ulianza baada ya kifo cha mitume. (Matendo 20:29, 30) Baada ya ule uitwao kwa kawaida mgeuzo wa imani wa Konstantino katika karne ya nne, idadi kubwa ya wapagani ilijiunga kwa wingi na namna ya Ukristo ulioenea wakati huo. Kukiwa na matokeo gani? Kitabu Early Christianity and Paganism chataarifu hivi: “Kile kikundi cha waamini wenye bidii kwa kweli ambacho kwa kulinganishwa ni kidogo kilipotea katika umati mkubwa wa wenye kudai kuwa Wakristo.”

Maneno ya Paulo yalithibitika kuwa kweli kama nini! Ilikuwa ni kana kwamba Ukristo wa kweli ulikuwa ukimezwa na ufisadi wa kipagani. Na hakuna mahali popote ambapo uchafuzi huo ulikuwa dhahiri kuliko katika kusherehekea sikukuu mbalimbali.

Kwa kweli, sherehe tu ambayo Wakristo wameamriwa waadhimishe ni ile ya Mlo wa Jioni wa Bwana. (1 Wakorintho 11:23-26) Kwa sababu ya mazoea ya ibada ya sanamu yaliyoshirikishwa na misherehekeo ya Roma, Wakristo wa mapema hawakuishiriki. Kwa sababu hiyo wapagani wa karne ya tatu waliwashutumu Wakristo, wakisema hivi: “Hamzuru maonyesho; hamjihusishi na maonyesho ya hadharani; mwakataa karamu za watu wote, na kukirihi mashindano matakatifu.” Kwa upande mwingine, wapagani walijigamba hivi: “Twaabudu miungu kwa uchangamfu, kwa karamu, nyimbo na michezo.”

Kufikia katikati ya karne ya nne, kuguna kwa wapagani kulitulia. Jinsi gani? Wakristo bandia zaidi na zaidi walipopenya ndani ya kundi, mawazo ya uasi-imani yalizidi. Jambo hilo liliongoza kwenye kuridhiana na ulimwengu wa Roma. Kikieleza juu ya hilo, kitabu The Paganism in Our Christianity chataarifu hivi: “Ilikuwa ni sera hususa ya Kikristo kuidhibiti na kuipa umaana wa Kikristo misherehekeo ya kipagani ambayo pokeo lilifanya ipendwe na watu.” Ndiyo, uasi-imani mkubwa ulikuwa ukitokeza madhara yake. Utayari wa wale waitwao Wakristo isivyofaa wa kukubali rasmi sherehe za kipagani sasa ulileta kiasi fulani cha ukubalifu ndani ya jumuiya. Punde si punde, Wakristo walipata kuwa na misherehekeo mingi ya kila mwaka kama vile wapagani wenyewe. Haishangazi kwamba Krismasi ilikuwa ya kwanza kabisa miongoni mwa hiyo misherehekeo.

Sikukuu ya Kimataifa

Namna ya Ukristo wenye nguvu ilipoenea kotekote Ulaya, watu wengi zaidi na zaidi walianza kusherehekea Krismasi. Kanisa Katoliki lilikubali maoni ya kwamba lilikuwa jambo lifaalo kuendeleza msherehekeo wenye shangwe katika kuiheshimu siku ya kuzaliwa kwa Yesu. Basi, mwaka wa 567 W.K., Baraza la Tours “likatangaza siku zile 12 kuanzia Krismasi hadi Epifania kuwa majira yenye utakatifu na ya kusherehekea.”—The Catholic Encyclopedia for School and Home.

Upesi Krismasi ilitwaa sehemu nyingi kutoka misherehekeo ya mavuno ya kilimwengu ya Kaskazini mwa Ulaya. Kusherehekea kuliendelea kuwa kwa kawaida zaidi ya uchaji kwa maana washerehekeaji walijitia mno katika ulafi na ulevi. Badala ya kuteta dhidi ya mwenendo mlegevu, kanisa liliukubali. (Linganisha Waroma 13:13; 1 Petro 4:3.) Mwaka wa 601 W.K., Papa Gregory wa Kwanza alimwandikia Mellitus, mmishonari wake huko Uingereza, akimwambia “[asi]komeshe shughuli hizo za sherehe za kipagani, lakini kuzirekebisha zifae sherehe ya ibada ya Kanisa, kubadili tu sababu ya sherehe hizo kuwa msukumo wa Kikristo bali si wa kipagani.” Hivyo ndivyo aripotivyo Arthur Weigall, aliyekuwa wakati mmoja mkaguzi mkuu wa mambo ya kale wa serikali ya Misri.

Katika Enzi za Kati, waliotaka marekebisho walihisi uhitaji wa kuteta dhidi ya mazidio hayo. Walipeleka maagizo mengi sana dhidi ya “kutumiwa vibaya kwa sherehe ya Krismasi.” Katika kitabu chake Christmas in America—A History, Dakt. Penne Restad asema hivi: “Makasisi fulani walikazia kwamba jamii ya kibinadamu isiyokamilika ilihitaji majira ya kutojizuia kabisa na ya kuzidi mno katika tamaa za asili, maadamu hayo majira ya kuzidi mno yaliendelezwa chini ya uangalizi wa Kikristo.” Wazo hilo liliongeza tu hali ya mvurugo. Ingawa hivyo, hilo halikubadili hali ya mambo sana, kwa maana desturi za kipagani zilikuwa tayari zimeunganishwa kwa ukaribu sana na Krismasi hivi kwamba watu walio wengi hawakupenda kuziacha. Mwandikaji Tristram Coffin, alisema hivi: “Kwa ujumla watu [walikuwa] wakifanya tu lile walilokuwa wa[me]fanya sikuzote na kuikazia uangalifu mdogo mijadala ya waadilishi.”

Kufikia wakati Wazungu walipoanza kufanya Amerika iwe koloni, Krismasi ilikuwa sikukuu yenye kujulikana sana. Na bado, Krismasi haikukubaliwa katika hizo koloni. Warekebishaji Wapiuriti waliiona hiyo sherehe kuwa ya kipagani na kuipiga marufuku huko Massachusetts kati ya mwaka wa 1659 na wa 1681.

Baada ya hayo marufuku kuondolewa, kusherehekea Krismasi kuliongezeka kotekote katika hizo koloni, hasa kusini mwa New England. Hata hivyo, kwa kufikiria wakati uliopita wa sikukuu hiyo, si jambo la kushangaza kwamba watu fulani walihangaikia kujitumbuiza zaidi ya kumheshimu Mwana wa Mungu. Desturi moja ya Krismasi iliyokuwa hasa yenye kuvuruga ni ile ya ulevi. Vikosi vya vijana wenye ghasia vilikuwa vikiingia katika nyumba za majirani wenye mali na kudai chakula na kinywaji cha bure kwa kutisha kuwakenga wakikataa. Ikiwa mwenye nyumba alikataa, kwa kawaida alilaaniwa, na nyumba yake kuharibiwa pindi kwa pindi.

Hali katika miaka ya 1820 ziliharibika kiasi cha kwamba “michafuko wakati wa sherehe ya Krismasi” ilipata kuwa “tisho kali la kijamii,” asema Profesa Nissenbaum. Katika majiji kama New York na Philadelphia, wamiliki-ardhi wenye mali walianza kuajiri walinzi ili kulinda mashamba yao. Hata yasemwa kwamba Jiji la New York liliunda kikosi chake cha kwanza cha polisi wa kulipwa kufuatia fujo zenye jeuri katika majira ya Krismasi ya mwaka wa 1827/1828!

Kubadilishwa kwa Krismasi

Karne ya 19 ilileta mabadiliko yasiyo na kifani kwa jamii ya kibinadamu. Watu, bidhaa, na habari zilianza kusafiri kwa wepesi zaidi kwa kuwa mfumo wa barabara na wa njia za reli uliibuka. Mvuvumko wa kiviwanda ulitokeza nafasi nyingi za kazi, na viwanda vilitokeza kwa haraka na kwa ukawaida ugavi wa bidhaa za biashara. Ujenzi wa viwanda ulileta matatizo ya kijamii yaliyo mapya na yenye utata, ambayo hatimaye yaliathiri jinsi Krismasi ilivyosherehekewa.

Kwa muda mrefu watu wametumia sikukuu kuwa njia ya kuvitia nguvu vifungo vya familia, na Krismasi hutumiwa vivyo hivyo. Kwa kuyafanyia marekebisho mapokeo fulani ya Krismasi yaliyo ya zamani zaidi, wenye kuikuza walibadili Krismasi kwa matokeo kutoka kuwa msherehekeo usiotulia, ulio kama wa kanivali na kuwa sikukuu yenye msingi wa familia.

Kwa kweli, mwisho-mwisho wa karne ya 19, Krismasi ilikuja kuonwa kuwa namna fulani ya suluhisho la maovu ya maisha ya kisasa ya Marekani. “Kati ya sikukuu zote,” asema Dakt. Restad, “Krismasi ilikuwa kifaa kamili cha kusafirishia dini na hisia za kidini hadi nyumbani na cha kusahihisha mazidio na kutofaulu kwa ulimwengu wa watu wote.” Aongeza kusema hivi: “Kupeana zawadi, kuonyesha hisani, hata kusalimiana kirafiki salamu ya sikukuu na kule kuremba na kufurahia mti wa kijani kibichi uliowekwa katika sebule au, baadaye, katika jumba la shule ya Jumapili, kuliwaunganisha wao kwa wao washiriki wa kila familia ifanyizwayo na baba, mama na watoto, na kuwaunganisha na kanisa, na jamii.”

Vivyo hivyo, watu wengi leo husherehekea Krismasi kama njia ya kuthibitisha kupendana kwao na ya kusaidia kudumisha muungano wa familia. Bila shaka, zisizo za kuachiliwa, ni zile pande za kiroho. Mamilioni ya watu husherehekea Krismasi kwa kuheshimu kuzaliwa kwa Yesu. Huenda wakahudhuria ibada za pekee za kanisa, wakaweka mandhari za Kuzaliwa kwa Yesu nyumbani, au wakatoa sala kumshukuru Yesu mwenyewe. Lakini Mungu hulionaje jambo hilo? Je, yeye huyakubali mambo hayo? Fikiria kile Biblia isemacho.

‘Penda Kweli na Amani’

Alipokuwa duniani, Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yeye lazima waabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Yesu aliishi kulingana na maneno hayo. Alisema kweli sikuzote. Alimwiga Baba yake kikamili, “BWANA [“Yehova,” NW] Mungu wa kweli.”—Zaburi 31:5; Yohana 14:9.

Kupitia kurasa za Biblia, Yehova amefanya ieleweke wazi kwamba yeye huchukia namna zote za udanganyo. (Zaburi 5:6) Kwa kufikiria hilo, je, si jambo lililo kinyume kwamba sehemu nyingi sana zenye kushirikishwa na Krismasi zaashiria mambo yasiyo ya kweli? Kwa mfano, fikiria ile hekaya juu ya Santa Klaus. Je, umewahi kumweleza mtoto ni kwa nini Santa hupendelea zaidi kuingia kupitia dohani badala ya kupitia mlangoni, kama iaminiwavyo sana katika nchi nyingi? Na je, Santa huyazuruje mamilioni mengi hivyo ya nyumba katika usiku mmoja tu? Vipi juu ya kulungu arukaye? Mtoto ajuapo kwamba amedanganywa juu ya kuamini kwamba Santa ni mtu halisi, je, jambo hilo halidhoofishi itibari ya mtoto katika wazazi wake?

Kichapo The Catholic Encyclopedia chataarifu wazi hivi: “Krismasi . . . ilivuta desturi za kipagani.” Hivyo basi ni kwa nini Kanisa Katoliki na makanisa mengine ya Jumuiya ya Wakristo huendelea kudumisha sikukuu ambayo desturi zake si za asili ya Kikristo? Je, jambo hilo halionyeshi kuruhusu mafundisho ya kipagani?

Alipokuwa duniani Yesu hakuwatia watu moyo wamwabudu. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Ni Yehova Mungu wako ambaye lazima uabudu, na ni kwake peke yake lazima utoe utumishi mtakatifu.” (Mathayo 4:10) Vivyo hivyo, baada ya utukuzo wa kimbingu wa Yesu, malaika alimwambia mtume Yohana “[a]abudu Mungu,” akionyesha kwamba hakukuwa na mabadiliko yoyote kuhusiana na jambo hilo. (Ufunuo 19:10) Hilo laongoza kwenye swali, Je, Yesu angekubali ujitoaji wa kiibada ambao huelekezwa kwake, bali si kwa babake, wakati wa Krismasi?

Kwa wazi, mambo ya hakika juu ya Krismasi ya sasa hayapendezi sana. Krismasi hasa ni sikukuu ya kubuniwa yenye uthibitisho mwingi unaoonyesha kwamba ina wakati uliopita uliopotoka. Hivyo basi, kwa kutegemea dhamiri safi, mamilioni ya Wakristo wameamua kutosherehekea Krismasi. Kwa kielelezo, kijana mmoja aitwaye Ryan asema hivi kuhusu Krismasi: “Watu husisimuka sana juu ya siku kadhaa za mwaka wakati ambapo familia hupata kuwa pamoja na wote ni wenye furaha. Lakini ni nini lililo la pekee sana juu ya hilo? Wazazi wangu hunipa zawadi mwaka wote!” Kijana mwingine, mwenye umri wa miaka 12, asema hivi: “Sihisi nimenyimwa. Mimi hupokea zawadi mwaka wote, si katika siku moja ya pekee wakati ambapo watu huhisi wamewajibika kununua zawadi.”

Nabii Zekaria aliwatia moyo Waisraeli wenzake ‘wazipende kweli na amani.’ (Zekaria 8:19) Ikiwa sisi, kama Zekaria na kama watu wengine waaminifu wa zamani, ‘twapenda kweli,’ je, haitupasi kuepuka sherehe ya kidini isiyo ya kweli ambayo humfedhehesha “Mungu aliye hai na wa kweli,” Yehova?—1 Wathesalonike 1:9.

[Picha katika ukurasa wa 7]

“Sihisi nimenyimwa. Mimi hupokea zawadi mwaka wote”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki