Je! Wakumbuka?
Umesoma matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi kwa uangalifu? Ikiwa ndivyo, bila shaka utayakumbuka mambo haya:
● Twapaswa kuyaelewaje maneno ya mtume Paulo katika Matendo 20:18-21?
“Tangu siku ya kwanza” alipoingia Asia, Paulo ‘alitoa ushuhuda kikamilifu.’ Alifanya jambo hilo ‘waziwazi na nyumba kwa nyumba,’ akiwatafuta watu wenye kufikiria mambo ya kiroho, kisha kuwafunza kwa ukawaida na baadaye kufanya ziara za uchungaji kama ilivyokuwa lazima. Yote hayo yanatoa kielelezo bora kwa kazi ambayo Mashahidi wa Yehova wanafanya leo.—12/15/79 kur. 11-13.
● Sababu gani Yeremia alimtaja Yehova kuwa “mfalme wa mataifa”?—Yer. 10:7.
Yehova ndiye Mfalme mwenye kutokeza, aliye Mkuu Zaidi, Yule ambaye anawatawala wafalme wengine wote. Aliye Juu Zaidi ameuonyesha ufalme wake ulio bora sana kwa kuchukua hatua juu ya watawala wa mataifa, kama vile wakati ule alipowapa Waisraeli ushindi juu ya Wafalme Sihoni na Ogi.—2/1/80 kur. 8, 9.
● Sababu gani Yeremia alisema ‘umenipumbaza, Ee Yehova’?—Yer. 20:7, NW.
Yeremia alipumbazwa katika njia yenye faida. Neno la Mungu lilikuwa limekuwa na uongozi wenye kushawishi juu yake. Yehova alikuwa amejithibitisha kuwa mwenye nguvu zaidi kuliko udhaifu wa Yeremia, kumwezesha nabii huyo avumilie katika utumishi huo wa kimungu mpaka kumalizika kwake.—2/15/80 kur. 5, 6.
● Tini “nzuri” na “mbovu” zinazotajwa katika Yeremia 24:1, 2 zinapatikana kutoka kwa mti gani, nazo zinafananisha nini?
Tini za mfano zilitoka kwa taifa la Israeli. Zile “tini nzuri” zilifananisha mabaki yenye kutubu ya taifa hilo, hali zile “tini mbovu” zilifananisha wale wasioaminika. Utimizo wa kisasa unapatikana katika Wakristo wa kweli, tofauti na Jumuiya ya Wakristo isiyotubu.—3/1/80 kur. 5, 6.
● Sababu gani kweli juu ya utawala wa Kristo wa miaka 1,000 imepotoshwa?
Wakati wa karne ya kwanza W.K. mitume walikuwa na nguvu zenye kuzuia ambazo zilihifadhi usafi wa fundisho la Kikristo. Hata hivyo, si muda mrefu baada ya wao kufa uasi wa imani ulipotokea. Jambo hilo liliongoza mwishowe kwenye usitawi wa wingi wa maoni ya kimadhehebu yenye kutofautiana.—4/1/80 kur. 5, 6.