Matunda—Mazuri na Mabaya
“BWANA [Yehova, NW] akanionyesha, na tazama, vikapu viwili vya tini . . . Kikapu kimoja kilikuwa na tini nzuri sana, kama tini zilizotangulia kuiva; na kikapu cha pili kilikuwa na tini mbovu sana, zisizoweza kuliwa, kwa kuwa zilikuwa mbovu sana.”—YEREMIA 24:1, 2.
1. Yehova aliwaonyeshaje watu wake Israeli huruma, lakini wao waliitikiaje?
ULIKUWA ni mwaka wa 617 K.W.K. Ilikuwa miaka kumi tu kabla ya hukumu ya Yehova iliyostahiliwa kutekelezwa dhidi ya Yerusalemu na watu walo. Tayari Yeremia alikuwa amekuwa akihubiri kwa bidii kwa miaka 30. Ona maelezo dhahiri ya Ezra juu ya hali hiyo, kama yapatikanavyo kwenye 2 Mambo ya Nyakati 36:15: “BWANA, [Yehova, NW], Mungu wa baba zao, akatuma kwao kwa mikono ya wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma [tena na tena, NW]; kwa sababu aliwahurumia watu wake, na makao yake.” Na tokeo la jitihada hizo zote lilikuwa nini? Kwa kusikitisha, Ezra aendelea kusimulia katika mstari wa 16: “Lakini waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya BWANA [Yehova, NW] juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.”
2, 3. Simulia lile ono lenye kutokeza ambalo Yehova alimwonyesha Yeremia.
2 Je! hiyo ilimaanisha kwamba taifa la Yuda lingefutiliwa mbali kabisa? Ili kupata jibu, acheni tufikirie ono lenye maana sana ambalo sasa alipewa Yeremia na kurekodiwa katika sura ya 24 ya kitabu kinachoitwa kwa jina lake. Mungu alitumia vikapu viwili vya tini katika ono hili ili kufananisha matukio miongoni mwa watu wake wa agano. Hao wangewakilishwa na aina mbili za matunda tofauti, mazuri na mabaya.
3 Yeremia sura ya 24, mstari wa 1 na wa 2, husimulia yale ambayo nabii wa Mungu aliona: “BWANA [Yehova, NW] akanionyesha, na tazama, vikapu viwili vya tini, vimewekwa mbele ya hekalu la BWANA [Yehova, NW]; baada ya Nebukadreza, mfalme wa Babeli, kumchukua mateka Yekonia, mwana wa Yehoyakimu, mfalme wa Yuda, na wakuu wa Yuda, pamoja na mafundi na wafua chuma, kutoka Yerusalemu, na kuwaleta Babeli. Kikapu kimoja kilikuwa na tini nzuri sana, kama tini zilizotangulia kuiva; na kikapu cha pili kilikuwa na tini mbovu sana, zisizoweza kuliwa, kwa kuwa zilikuwa mbovu sana.”
Tini Nzuri Katika Ono
4. Lile ono la tini liliwawekea Waisraeli waaminifu ujumbe upi wenye kufariji?
4 Baada ya kumuuliza Yeremia kile alichoona, Yehova aliendelea kusema hivi katika mstari wa 5 hadi wa 7: “Kama zilivyo tini hizi nzuri, ndivyo nitakavyowaangalia mateka wa Yuda, niliowatoa katika mahali hapa, waende mpaka nchi ya Wakaldayo, wapate mema. Kwa maana [nitaweka jicho langu juu yao kwa njia nzuri, NW], wapate mema, nami nitawaingiza katika nchi hii tena; nami nitawajenga, wala sitawabomoa; nitawapanda, wala sitawang’oa. Nami nitawapa moyo, wanijue ya kuwa mimi ni BWANA, [Yehova, NW]; nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao; kwa maana watanirudia kwa moyo wao wote.”
5, 6. (a) Waisraeli fulani ‘walipelekwaje kwa wema’ hadi Kaldayo? (b) Yehova ‘aliwekaje jicho lake kwa njia nzuri’ juu ya Waisraeli waaminifu waliokuwa utekwani?
5 Kwa hiyo yaonekana kutokana na yale Yehova aliyosema hapa kwamba nyakati nzuri zaidi zilikuwa mbele, kwamba taifa la Yuda halingefutiliwa mbali kabisa. Lakini ni nini umaana wa kikapu hicho cha tini nzuri?
6 Yekonia, au Yehoyakini, alikuwa amekuwa mfalme wa Yuda kwa miezi mitatu na siku kumi tu kabla ya yeye kusalimisha Yerusalemu kwa hiari kwa Mfalme Nebukadreza. Miongoni mwa wale waliochukuliwa mateka hadi utumwani pamoja naye alikuwa Danieli na waandamani wake watatu Waebrania Hanania, Mishaeli, na Azaria, kutia na Ezekieli. Uhai wao ulihifadhiwa na mfalme wa Babiloni, hivyo ingeweza kusemwa kwamba Yehova aliwaona mateka hao wote kana kwamba walikuwa wakiondoshwa kwa wema hadi nchi ya Wakaldayo. Je! uliona kwamba Yehova aliahidi pia ‘kuweka jicho lake juu yao kwa njia nzuri’? Hilo lilitimizwaje? Miaka 80 baadaye, katika 537 K.W.K., Yehova alifanya Mfalme Sairasi (Koreshi) atoe amri iliyoruhusu mabaki ya wazao wao warudi kwenye nchi ya Yuda. Wayahudi hao waaminifu walijenga upya jiji la Yerusalemu; walijenga hekalu jipya kwa ajili ya ibada ya Mungu wao, Yehova; nao walirudi kwake kwa moyo wao wote. Kwa hiyo katika hayo yote, hao mateka na wazao wao walikuwa kwa Yehova kama tini nzuri sana za mapema.
7. Jicho la Yehova lilikuwa juu ya jamii ya Yeremia ya kisasa ‘kwa njia nzuri’ wakati gani na jinsi gani?
7 Huenda ukakumbuka kwamba katika makala inayotangulia juu ya maneno ya kiunabii ya Yeremia, tulijifunza kwamba yana maana kwa ajili ya karne yetu ya 20. Na ndivyo ilivyo na sura ya 24. Katika ile miaka yenye msukosuko ya Vita ya Ulimwengu 1, watumishi wengi wa Yehova waliojiweka wakfu walikuja kuwa chini ya uvutano wa Babiloni Mkubwa kwa njia moja au nyingine. Lakini jicho la Yehova lenye kulinda sana ‘lilikuwa juu yao kwa njia nzuri.’ Na hivyo ilikuwa kwamba kupitia Sairasi Mkuu Zaidi, Kristo Yesu, Yehova alivunja uwezo wa Babiloni Mkubwa juu yao na akawaingiza hatua kwa hatua katika paradiso ya kiroho. Waisraeli hao wa kiroho waliitikia na wakamrudia Yehova kwa moyo wao wote. Kisha, katika 1931, wao walishangilia kukubali jina Mashahidi wa Yehova. Kwa kweli, sasa ingeweza kusemwa kwamba walikuwa kama kikapu cha tini nzuri sana machoni pa Yehova.
8. Ni katika njia gani Mashahidi wa Yehova wameupiga mbiu kotekote utamu kama ule wa tini wa ujumbe wa Ufalme?
8 Na Mashahidi wa Yehova hawajakosa kusudi la fadhili isiyostahiliwa ya Mungu katika kuwaweka huru kutoka katika Babiloni Mkubwa. Wao hawawanyimi wengine utamu kama ule wa tini wa ujumbe wa habari njema za Ufalme, bali wameupiga mbiu kotekote kwa kutii maneno ya Yesu kwenye Mathayo 24:14, NW: “Habari njema hizi za Ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa, kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” Na matokeo yamekuwa nini? Zaidi ya watu 4,700,000 wenye mfano wa kondoo ambao si Waisraeli wa kiroho wamejiweka huru na Babiloni Mkubwa!
Tini Mbaya Katika Ono
9. Ni nani waliowakilishwa na zile tini mbaya za ono la Yeremia, na ni lazima wapatwe na nini?
9 Lakini vipi juu ya kile kikapu cha tini mbaya katika ono la Yeremia? Sasa Yeremia aelekeza uangalifu kwenye maneno ya Yehova yapatikanayo kwenye Yeremia sura ya 24, mstari 8 hadi 10: “Na habari za tini zile mbovu, zisizoweza kuliwa, kwa kuwa ni mbovu sana; hakika, asema BWANA, [Yehova, NW], ndivyo nitakavyomtoa Sedekia, mfalme wa Yuda, na wakuu wake, na mabaki ya Yerusalemu, waliosalia katika nchi hii, na hao wanaokaa katika nchi ya Misri. Naam, nitawatoa watupwe huko na huko katika falme zote za dunia, wapate mabaya; wawe kitu cha kulaumiwa, na mithali, na dhihaka, na laana, katika mahali pote nitakapowafukuza. Nami nitatuma upanga, na njaa, na tauni, kati yao, hata watakapopotelea mbali katika nchi niliyowapa, wao na baba zao.”
10. Kwa nini Yehova alimwona Sedekia kuwa ‘tini mbaya’?
10 Kwa hiyo kwa kweli Sedekia alikuwa ‘tini mbaya’ machoni pa Yehova. Si kwamba tu aliasi dhidi ya Mfalme Nebukadreza kwa kuvunja kiapo cha kuwa mwaminifu-mshikamanifu alichokuwa amefanya kwa mfalme huyo kwa jina la Yehova bali yeye pia alikataa katakata huruma za Yehova zilizotolewa kupitia Yeremia. Kwa kweli, hata alifanya Yeremia akatiwa gerezani! Haishangazi kwamba Ezra amalizia mtazamo wa mfalme huyo kama vile afanyavyo kwenye 2 Mambo ya Nyakati 36:12: “Akafanya yaliyo mabaya machoni pa BWANA, [Yehova, NW], Mungu wake; wala hakujinyenyekesha.” Katika macho ya Yehova Sedekia na wale waliobaki katika Yerusalemu walikuwa kama kikapu cha tini mbaya, zilizooza!
Tini Zilizooza za Kitamathali Katika Siku Zetu
11, 12. Ni nani wanaotambulishwa kuwa tini mbaya leo, nao watapatwa na nini?
11 Sasa tazama huku na huku katika ulimwengu leo. Je! wafikiri twaweza kupata kikapu cha ufananisho cha tini mbaya? Acheni tufikirie mambo hakika kwa kulinganisha siku zetu na zile za Yeremia. Katika karne hii ya 20, Yehova ametumia jamii ya Yeremia, mabaki ya wapakwa, kuyaonya daima mataifa juu ya hasira yake inayokuja kwenye dhiki kubwa. Yeye amehimiza vikundi vya mataifa vimpe yeye utukufu unaostahili jina lake, vimwabudu kwa roho na kweli, na kukiri Mwanae anayetawala, Kristo Yesu, kuwa Mtawala halali wa dunia. Itikio limekuwa nini? Kama vile katika siku za Yeremia. Mataifa yanaendelea kufanya yaliyo mabaya machoni pa Yehova.
12 Lakini ni nani wanaochochea mtazamo huo wa uasi? Ni nani wanaoendelea kudhihaki wajumbe hao wa Mungu walio kama Yeremia kwa kutilia shaka mamlaka yao ya kutenda wakiwa wahudumu wa Mungu? Ni nani wanaoendelea kudharau Neno la Mungu? Ni nani leo wamechochea sehemu kubwa ya mnyanyaso dhidi ya Mashahidi wa Yehova? Jibu liko wazi kwa wote kuona—ni Jumuiya ya Wakristo, hasa makasisi! Na ebu tazama matunda yote mabaya, yaliyooza ya Jumuiya ya Wakristo yaliyozungumziwa katika makala inayotangulia. Oh, Ndiyo, kwa kweli kuna kikapu cha ufananisho cha tini mbaya duniani leo. Kwa kweli, Yehova asema kwamba hayawezi ‘kulika kwa ubovu wayo.’ Maneno ya Yehova kupitia Yeremia yarudiwa hadi siku yetu: ‘Watafikia mwisho wao’! Hasira ya Yehova dhidi ya Jumuiya ya Wakristo haitapata kiponyo.
Somo Lenye Kutuonya Sisi
13. Kulingana na maneno ya Paulo yapatikanayo kwenye 1 Wakorintho 10:11, twapaswa kuelewaje ono la vikapu viwili vya tini?
13 Tunapochunguza maana hasa ya ujumbe wenye kuonya uliopuliziwa wa Yeremia, twayakumbuka maneno ya mtume Paulo kwenye 1 Wakorintho 10:11: “Basi mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya [mfumo wa mambo, NW].” Je! sisi binafsi tumezingatia moyoni onyo linalotolewa kwetu na ono hilo la vikapu viwili vya tini? Yale ambayo tumekuwa tukizungumzia ni sehemu ya maana ya mambo yaliyopata Israeli yakiwa kielelezo chenye kutuonya sisi.
14. Israeli liliitikiaje utunzi wororo wa Yehova?
14 Mwishowe, acheni tukumbuke maneno ya Yehova kwa Mfalme Daudi kuhusu Israeli, kwenye 2 Samweli 7:10: “Nitawaagizia mahali watu wangu Israeli, nami nitawapanda.” Yehova aliwatunza watu wake Israeli kwa wororo, katika kila njia. Kulikuwa na kila sababu ya Waisraeli kutokeza matunda mazuri maishani mwao. Yale waliyotakiwa kufanya tu ni kusikiliza mafundisho ya kimungu kutoka kwa Yehova na kutii amri zake. Lakini, ni wachache tu kati yao waliofanya hivyo. Wengi wao walikuwa wakaidi na wakengeufu sana hivi kwamba walitokeza matunda mabaya, yaliyooza.
15. Israeli la kiroho leo pamoja na waandamani walo wenye mfano wa kondoo wameitikiaje huruma ya Yehova?
15 Basi, namna gani juu ya siku yetu? Yehova ameonyesha huruma nyingi kuelekea mabaki ya Israeli wa kiroho na waandamani wao wenye mfano wa kondoo. Jicho lake limekuwa juu yao daima tangu ukombozi wao wa kiroho katika 1919. Kama alivyotabiri kupitia Isaya, wao hupokea maagizo ya kimungu kila siku kutoka kwa Mfundishaji mkuu zaidi katika ulimwengu wote mzima, Yehova Mungu. (Isaya 54:13) Ufundishaji huo wa kimungu unaotolewa kupitia Mwanae mpendwa, Yesu Kristo, umetokeza amani nyingi miongoni mwao na umewaingiza hatua kwa hatua katika uhusiano wa karibu zaidi na Yehova. Hilo hutuandalia sisi sote hali ya kiroho iliyo nzuri kama nini ili tupate kumjua Yehova, kumsikiliza, na kisha kuendelea kutokeza matunda mazuri maishani mwetu—matunda yanayoleta sifa kwa Yehova! Uhai wetu wenyewe wahusika!
16. Kila mmoja wetu aweza kutumiaje kibinafsi lile ono la vikapu viwili vya tini?
16 Lakini ijapokuwa fadhili yote isiyostahiliwa ya Mungu, bado kuna baadhi ya wale wanaokuwa waasi na wenye mioyo migumu, kama vile wengi walivyofanya katika Yuda la kale, na ambao hutokeza matunda mabaya, yaliyooza maishani mwao. Hilo ni lenye msiba kama nini! Yeyote kati yetu na asisahau somo lenye kuonya tulilofafanuliwa wazi kwa vikapu hivyo viwili vya tini pamoja na matunda yavyo—mazuri na mabaya. Kadiri hukumu ya Yehova inayostahiliwa dhidi ya Jumuiya ya Wakristo yenye kuasi imani ikaribiavyo zaidi na zaidi, na tuzingatie moyoni himizo hili la mtume Paulo: “Mwenende kama ulivyo wajibu wenu kwa BWANA, [Yehova, NW], mkimpendeza kabisa; mkizaa matunda kwa kila kazi njema.”—Wakolosai 1:10.
Kupitia “Matunda—Mazuri na Mabaya” na mafungu 1-4 ya “Ugomvi wa Yehova na Mataifa”
◻ Kikapu cha tini nzuri chawakilisha nini?
◻ Kile kikapu katika ono cha tini mbaya kimekuja kudhihirikaje?
◻ Ujumbe wa Yeremia watuandalia somo jipi lenye kuonya?
◻ Ni nini uliokuwa umaana wa mwaka 607 K.W.K.? na 1914 W.K.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kama tini nzuri, watu wa Mungu wametokeza matunda matamu ya Ufalme
[Picha katika ukurasa wa 15]
Jumuiya ya Wakristo imekuwa kama kikapu cha tini mbaya