Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 7/1 kur. 3-4
  • Mahitaji Wanayotazamia Watu Kutimiziwa na Serikali

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mahitaji Wanayotazamia Watu Kutimiziwa na Serikali
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAHITAJI TUNAYOTAKA YATOSHELEZWE
  • SEHEMU YA SERIKALI YA KUTIMIZA
  • NI NANI AWEZAYE KUTIMIZA MAHITAJI HAYO?
  • Serikali ya Mungu ya Amani
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Ufalme wa Mungu Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Kuwa Raia wa Serikali ya Mungu
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Namna Mahitaji Yetu Yatakavyojazwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 7/1 kur. 3-4

Mahitaji Wanayotazamia Watu Kutimiziwa na Serikali

ZAIDI ya miaka 200 iliyopita taifa fulani la watu lilijiona ni lenye kuonewa na serikali liliyokuwa likiishi chini yake. Katika kutangaza uhuru kutokana na serikali hiyo ya Uingereza, kiongozi wa nchi Mwamerika Thomas Jefferson aliandika juu ya “Haki fulani zisizoweza kutenganishwa,” kutia ndani “Uzima, Uhuru na kufuatia Furaha.”

Jambo ambalo serikali inatazamiwa kutimiza sasa, kama vile ilivyokuwa wakati huo, ni kutolea watu “haki” hizo. Ni watu wachache sana leo wanaofurahia maisha kamili, yenye kutosheleza, pamoja na uhuru na furaha. Ili kuyapata maisha hayo, wewe unafikiri ni mabadiliko gani yaliyo ya lazima?

Wengi wamelifikiria sana jambo hilo. Katika kitabu chao A Sane and Happy Life: A Family Guide, Madaktari Abraham na Rose Franzblau waliandika hivi: “Kama tungeomba watu wote ulimwenguni wapige kura na kushauriana na jamii ya wanadamu juu ya ulimwengu ambao sote tungependa kuishi ndani yake, inaelekea sana kwamba sote tungekubaliana juu ya matakwa fulani ya msingi.” Ni nini ‘matakwa au mahitaji hayo ya msingi?”

MAHITAJI TUNAYOTAKA YATOSHELEZWE

Kwanza, katika orodha madaktari hao waliandika “ulimwengu usio na vita.” Kweli kweli, sote twaweza kukubaliana na uhitaji huo wa kuondoa vita? Namna ilivyo msiba, ikinyonya uchumi wa mataifa na kulemaza na kuua wapendwa wetu! Walakini je! serikali yo yote inaweza kutimiza uhitaji huo wa kukomesha vita?

“Wa pili,” madaktari hao wakaandika, “ungekuwa ulimwengu usio na njaa, ambao njaa na uhitaji vingeondolewa milele.” O, namna tunavyokubaliana na uhitaji wa kuwapa wote chakula cha kutosha! Lingekuwa jambo zuri kama nini kutopatwa tena na njaa kali au kufa njaa, na kufahamu kwamba kila mwanadamu duniani ana chakula cha kutosha! Je! ni kutamani mengi mno kutazamia serikali itatue tatizo la upungufu wa chakula?

“Wa tatu,” wakaendelea madaktari hao, “ungekuwa ulimwengu usio na maradhi, ulimwengu ambao katika huo wote wangekuwa na nafasi ya kukua katika afya na kuishi siku zao pasipo magonjwa.” Bila shaka, sote tunatambua uhitaji wa kuwa na afya njema ili kufurahia maisha kabisa. Ingekuwa faraja yenye kuvutia namna gani kuishi katika ulimwengu ambao hakuna mtu anayekuwa mgonjwa, ambao hakuna mtu anayepatwa na mafua au maradhi mengine yo yote! Je! ni jambo gumu sana kwa serikali kuweza kutosheleza uhitaji huo?

Hata hivyo ili watu waweze kufurahia kweli kweli ‘maisha, uhuru na furaha,’ serikali yapaswa kuweza kutosheleza mahitaji mengine zaidi ya lazima. Katika ulimwengu ambao sote tungependa kuishi, madaktari hao wakaandika, ‘ungepatia watu kazi ili wapate kujiruzuku wenyewe na jamaa zao.’ Ndiyo, hakuna ukosefu wa kazi; bali utendaji wenye matokeo, wenye kutosheleza kwa wote. Je! serikali inaweza kutimiza uhitaji huo?

Wakiendelea, madaktari hao waliongeza hivi: “Ungekuwa ulimwengu ambao katika huo kila mtu angefurahia uhuru chini ya sheria, pamoja na haki ya hukumu kwa wote.” Vilevile, “kila mwanadamu angekuwa na nafasi ya kukuza kabisa uwezo na karama zake, na kuthawabishwa kwa ajili ya jitihada zake, pasipo kupendelea.” Bila shaka sote twakubaliana na uhitaji wa kuondoa uonevu mbaya sana wa leo, ukosefu wa usawa na upendeleo. Walakini je! serikali yo yote inaweza kufanya hilo?

Wengi wetu tutakubaliana kwamba kungali kuna mahitaji mengine yanayopaswa kutimizwa iwapo tutakuwa na ulimwengu ambao ungependeza kuishi ndani yake. Kama vile madaktari hao walivyosema: ‘Ulimwengu wa namna hiyo ungekuwa ambao katika huo watu wote wangekuwa na starehe ya kutosha kufurahia mambo mazuri maishani.’ Nao wakamalizia hivi: ‘Sifa kama vile ukamilifu, upendo, kutokuwa na choyo na kuhangaikia wanadamu wengine ndizo zingeonwa kuwa za thamani zaidi.’

Ijapokuwa kwa ujumla mahitaji hayo hayatimizwi leo, je! kweli kweli ni kutaka mengi sana kutazamia yatimizwe? Ni katika njia zipi mahitaji ya kweli ya wanadamu yanaweza kutimizwa?

SEHEMU YA SERIKALI YA KUTIMIZA

Katika kutunga Tangazo la Amerika la Uhuru, Thomas Jefferson aliandika hivi: “Ili kupata haki hizo [uzima, uhuru na kufuatia furaha], Serikali huanzishwa katikati ya Wanadamu.” Ndiyo, serikali nzuri ni jambo la lazima ili kutosheleza mahitaji ya wanadamu. Kama vile alivyoandika kiongozi wa kale wa kisiasa wa Amerika John C. Calhoun: ‘Asili ya wanadamu ni kwamba serikali ni ya lazima ili jamii iwepo, nayo jamii ni ya lazima ili mwanadamu awepo.’

Lakini serikali ni nini? Imefafanuliwa kuwa “uelekezo au uongozi wenye mamlaka.” Serikali hufanya na kufikiliza sheria kwa kusudi la kuongoza tabia za kibinadamu. Nasi twapaswa kushukuru kwa ajili ya jambo hilo, sana sana katika jamii yetu yenye matatizo makubwa. Kwa mfano, fikiria ni jambo gani ambalo lingetokea katika pembe ya barabara yenye kupitiwa na magari mengi kama mwendo wa magari usingeongozwa. Ingetokeza msiba.

Hata hivyo kuongoza mwendo wa motokaa ni jambo rahisi kwa kulinganisha. Ni jambo gumu zaidi sana kufikiliza sheria ili kuhifadhi amani kati ya watu, kuongoza ukuzaji na ugawanyaji wa chakula ili wote wawe na chakula kingi, kutoa utumishi ili kuendeleza afya nzuri ya kila mtu, kutoa kazi yenye kusudi kwa wote, na mambo mengine kama hayo. Ili kutimiza mahitaji yote hayo, na mengineyo mengi ambayo lazima yatoshelezwe ili watu wafurahie maisha kweli kweli, serikali yenye ustadi mwingi ni ya lazima.

NI NANI AWEZAYE KUTIMIZA MAHITAJI HAYO?

Muumba wa wanadamu anatambua uhitaji wa wanadamu wa serikali, kwa ajili ya “uelekezo au uongozi wenye mamlaka.” Kwa hiyo si jambo lisilotazamiwa kwamba Biblia inasema juu ya serikali iliyo chini ya uongozi wa Mungu. Kwa kweli, ahadi hiyo ya utawala wa Mungu ndilo fundisho kuu la Biblia. Pengine umeshangaa kwa kujifunza hilo.

Huenda ukauliza hivi: “Serikali ya Mungu inazungumzwa wapi katika Biblia?” Tafadhali chukua nakala ya Biblia, uifungue kwenye Isaya sura ya tisa, mistari ya sita na saba, Iwapo yako ni tafsiri inayotumiwa sana ya Union Version, inasema hivi:

“Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume; na uweza wa kifalme [serikali, AV] utakuwa begani mwake; naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi [serikali] yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe.”‏

Hapo nabii wa Mungu, Isaya alikuwa akizungumza juu ya kuzaliwa kwa wakati ujao kwa mtoto, mwana wa mfalme. Mwishowe huyo ‘mwana wa mfalme’ angekuwa mtawala mkuu, “Mfalme wa amani.” Angekuwa mwenye mamlaka juu ya serikali yenye ustadi kweli kweli, ambayo ingeleta amani isiyo na mwisho. Pengine unamtambua mtoto huyo. Akitangaza juu ya kuzaliwa kwake, malaika Gabrieli alisema kwamba angepaswa kuitwa Yesu, naye akaongeza hivi: “Atamiliki [kama mfalme] . . . , na ufalme wake utakuwa hauna mwisho.”​—Luka 1:31, 33.

Utendaji mkubwa wa kidunia wa Yesu Kristo na wanafunzi wake ulikuwa kuhubiri na kufundisha juu ya ufalme huo wa Mungu. Zaidi ya mitajo 140 inatolewa nao katika Biblia juu ya serikali hiyo. Kumbuka kwamba hata Yesu alifundisha wafuasi wake wamwombe Mungu: “Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”​—Mt. 6:9, 10.

Walakini utawala wa Ufalme huo utasimamishwa namna gani, nao utafanya kazi namna gani? Je! wanadamu watautokeza na kuuendesha? Je! wanadamu wanaweza kutoa serikali ambayo itatokeza ulimwengu ambao sote tungependa kuishi ndani yake?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki