Twashukuru Kwamba Yehova Alijibu Sala Zetu
Kama ilivyosimuliwa na Angelo Clave
“FURAHINI katika tumaini. Vumilieni dhiki. Dumuni katika sala.” Kukumbuka shauri hilo kumenisaidia kufurahia maisha ya kumtolea Yehova utumishi wa wakati wote.—Rum. 12:12, NW.
Nikiwa mchanga zaidi kati ya watoto sita, nilizaliwa katika mwaka 1936 katika kisiwa kidogo cha Anda karibu na sehemu ya watalii ijulikanayo sana kama Visiwa Mia Moja katika Pangasinan, Filipino. Nyumba yetu ya miti na mianzi, ikiwa nusu kilometre (maili 0.3) toka baharini, ilikuwa imezungukwa na maua na miembe, jambo lililochangamsha macho na sehemu za kuonjea za ulimi. Kwa kuhuzunisha, baba yangu alikufa nilipokuwa mwenye umri wa miaka mitatu peke yake. Licha ya huzuni ya kumpoteza mumewe, mama yangu alikuwa anahangaika sana juu ya namna ya kutulea katika njia bora zaidi. Alikuwa na kashamba ambako kangejaza mchele ghala lililokuwa nyuma ya nyumba yetu. Yeye alikuwa mwanamke aliyejitoa kabisa kwa ajili ya mambo ya kidini aliyoamini akiwa mshiriki wa Kanisa Huru la Filipino.
Katika mwaka 1945, muda mfupi tu baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili kuiharibu Filipino, mabadiliko yenye kuleta matokeo makubwa yalianza wakati wa ziara ya wanawake wawili vijana ambao walikuwa wakitangaza kwamba ufalme wa Mungu ulikuwa ndio tumaini pekee la wanadamu. Mama yangu hakupendezwa, walakini ndugu yangu mkubwa Presalino aliwakaribisha kwa shauku hao mashahidi wawili wa Yehova na kuzungumza pamoja nao vichwa vingi vya Biblia tangu asubuhi mpaka usiku wa manane. Siku iliyofuata, Presalino alimwalika binamu wangu Eduardo aende pamoja naye alipokuwa akiwarudisha wanawake hao nyumbani kwao kwa mashua.
Ndugu yangu na binamu yangu waliporudi siku chache baadaye, walimwambia kila mtu kwa shauku kwamba walikuwa wamebatizwa kama Mashahidi wa Yehova! Kwa shauku Presalino alieleza kwamba ufalme ule ambao tulikuwa tumeuomba mara nyingi katika Sala ya Bwana ungeletea watu wengi uzima wa milele katika dunia iliyo paradiso. (Mt. 6:9, 10; Luka 23:43) Mama yangu, ingawa kwanza hakupendezwa, alisadikishwa baada ya muda mfupi kwamba hiyo ilikuwa kweli. Mara moja aliondoa nyumbani mwetu msalaba na sanamu za Yusufu, Mariamu na “watakatifu” wengine. Vilevile aliacha kutafuna popoo. Miezi michache baadaye, baba ya wale wasichana wawili Mashahidi alikuja kututembelea. Alisisimuka kuona kikundi kikijifunza Biblia chini ya uongozi wa Presalino. Kisha watu kumi na wawili walibatizwa, kutia ndani mama yangu, ndugu wawili, dada yangu na shemeji wawili wa kike. Muda mfupi, wakafanyiza kundi. Wawili wa ndugu zangu, pamoja na binamu yangu Eduardo, waliwekwa kuwa waangalizi.
Katika shule yetu ya wanafunzi wapata 120, nilidhihakiwa mara nyingi kwa sababu ya imani yangu yenye kukua. Watoto wote wa Mashahidi wa Yehova walikazwa kwa sababu ya kukataa kushiriki katika vitendo vya kuabudu sanamu shuleni. Mwishowe mikazo hiyo ilinizuia nisipate elimu ya juu ya kilimwengu. Jambo hilo lilikatisha tamaa. Walakini, mama yangu alinisaidia nimtegemee Yehova na kusitawisha uhusiano wangu pamoja naye kwa sala na kujifunza Biblia zaidi. Matokeo yakawa nini? Nilipokuwa mwenye umri wa miaka 15 nilikuwa kati ya 522 waliobatizwa katika Aprili 22, 1951, katika kusanyiko la taifa la Quezon City.
SALA ZANGU ZA KUWA MHUBIRI WA WAKATI WOTE ZAJIBIWA
Kusanyiko hilo lilichochea tamaa yangu ya kuwa painia, kama wanavyoitwa watangazaji wa Ufalme wa wakati wote. Wakati wa safari ya kurudi na katika mazungumzo ya jamaa, hilo ndilo lililokuwa jambo kubwa akilini mwangu na katika sala zangu. Ingawa kwanza mama yangu hakukubali, mwishowe aliniruhusu niwe painia wa “likizo” kwa miezi kadha. Miezi hiyo michache ilikuwa yenye kuthawabisha sana, nayo ilitia nguvu azimio langu la kuwa painia wa kawaida.
Katika Machi 1, 1953, mradi wangu ulitimizwa. Hivyo nikaanza kujifunza lugha mpya—Iloko. Sababu gani jambo hilo lilikuwa la lazima? Kuna zaidi ya lugha 87 katika Filipino nami ni Mbolinao, lakini katika eneo langu la kutolea ushuhuda kulikuwako Wailoko wengi. Hiyo ilikuwa lugha ya kwanza ya lugha nyingi mpya ambazo ningepaswa kujifunza ili nifundishe watu zaidi kweli ya Biblia. Wakati wote, nimemtegemea sana Yehova anisaidie, nikiomba kwamba abariki jitihada zangu.
Nilipata kuona jambo lisilo la kawaida nilipokuwa nikifanya kazi pamoja na Kundi la Ilogmalino katika kijiji kidogo kinachopakana na ufuo wenye changarawe nyeupe katika Bahari ya China. Mwanamume kijana niliyempata nyumbani mwake alikasirika sana alipofahamu nilikuwa Shahidi hata kwamba akanifukuza akinionya nisirudi tena. Juma iliyofuata mwangalizi wa mzunguko mwenye kusafiri alitutembelea nasi tukawa tukienda katika nyumba zilizokuwa katika eneo hilo. Pasipo kufahamu jambo nililoliona, mwangalizi huyo wa mzunguko aliniambia nianze nyumba ile ile ambayo yule mwanamume kijana alikuwa mwenye uadui sana.
Wazo langu la kwanza lilikuwa kuiacha nyumba hiyo; walakini baada ya kumwomba Yehova niliamua kwenda mara nyingine. Lo! ilikuwa ajabu namna gani! Mwanamume huyo kijana alisikiliza kwa uangalifu, akakubali kujifunza Biblia naye akaja kwenye mkutano wake wa kwanza katika juma hiyo. Alifanya maendeleo ya haraka ya kiroho naye akabatizwa katika kusanyiko moja miezi michache tu baadaye. Ni jambo gani lililokuwa limetokeza badiliko hilo la ghafula kwa juma moja tu? Baada ya kunitendea vibaya sana, alipatwa na msiba. Akiliona jambo hilo kuwa ni adhabu, aliamua angaa kuwa mpole kwa Shahidi mwingine ambaye angemwona. Ndivyo alivyofanya, naye akapendezwa na aliyosikia.
Watatu kati yetu mapainia walitumia mara nyingi mashua ya kuvulia samaki ya futi 20 (metre 6) ili kutembelea visiwa vya karibu na kutoa hotuba. Tulipokuwa tukirudi nyumbani usiku mmoja, hali ya hewa ilibadilika ghafula. Tukawa matatani! Mawimbi makubwa yaliitosa majini hiyo mashua nasi tukalazimika kuogelea katika bahari hiyo iliyochafuka, mwendo wa kilometre mbili (maili 1.25) kwenye ufuo. Kwa njia fulani mpwa wangu wa kiume nami tulipata nguvu za kumsaidia mpwa wangu wa kike, na ijapokuwa tulipoteza vitu vyetu, tulifika salama salimini kwenye ufuo. Tulimshukuru Yehova kwa kutupa uhai wetu.
Mgawo wangu uliofuata ulikuwa katika mji uliokuwa mbali zaidi kutoka nyumbani. Huko nilishuhudia ukweli wa maneno ya Yesu: “Kila mtu aliyeacha nyumba, au ndugu wa kiume, au wa kike, au baba, au mama, au watoto, au mashamba, kwa ajili ya jina langu, atapokea mara mia na kuurithi uzima wa milele.” (Mt 19:29) Ndugu na dada hao walikuwa wafadhili na wenye kupenda sana hata kwamba baada ya muda mfupi tulifurahia uhusiano wa karibu ulio mzuri na wenye kujenga. Uhusiano ulikuwa wenye nguvu sana hata kwamba baadaye wakati nilipoondoka kwenda kwa mgawo wangu wa kwanza wa painia wa pekee katika Mkoa wa Bulacan hakuna ye yote wetu aliyeweza kuzuia machozi yaliyotiririka katika nyuso zetu tulipokuwa tukisema kwaheri.
Katika migawo yangu miwili iliyofuata nilikuwa na wenzi wawili tofauti nami nikajifunza namna ya kuishi na kushirikiana na watu wenye nyutu tofauti. Wa kwanza wa migawo hiyo ulinifanya nijifunze lugha nyingine, Tagalog, lugha ya taifa. Katika wa pili wa migawo hiyo, nilipata kwa mara ya kwanza furaha ya pekee ya kusaidia kuanzisha kundi jipya. Jambo hilo lilichukua zaidi ya miaka miwili ya kazi ya bidii, sala za wakati wote na kumtegemea Yehova ‘anayekuza vitu.’—1 Kor. 3:5-9.
MAPENDELEO MENGINE YA UTUMISHI
Kushukuru kwangu kuliongezeka wakati, baada ya miaka mitatu katika utumishi wa painia wa pekee, nilipowekwa nifanye ziara za mzunguko kwa makundi 20, kutia ndani mji wangu wa nyumbani. Je! waweza kuwazia furaha yangu nikienda kwenye funzo la Biblia pamoja na mama yangu na kumsaidia afundishe mtu mwingine kweli ambazo yeye mwenyewe wakati mmoja alisita-sita kukubali? Baada ya miaka miwili katika kazi ya kuzunguka, kulikuwako furaha ya namna nyingine, kwani Lucrecia nami tulioana katika Januari 17, 1962. Kutumika kwake kama painia wa kawaida na wa pekee kwa miaka saba u nusu kulikuwa kumetoa ushuhuda wa upendo wake wa kumtumikia Yehova, naye ameendelea kuwa mwenye kusaidia na kutia moyo katika miaka ambayo imefuata tangu wakati huo. Hakika, hiyo ni sababu nyingine ya kumshukuru Yehova!—Mit. 19:14.
Wakati mwingi kufanya ziara za kuzunguka lilikuwa jambo gumu, lakini lilithawabisha sana. We! ili kufika Kijiji cha Agumanay tulipaswa kukazana kupanda kwenye milima katika kijia chenye kuteleza kwa saa 12! Walakini ilikuwa furaha kama nini baada ya kufika kuona kwamba wengi wa wakaaji wa kijiji hicho walikuwa Mashahidi wa Yehova! Walitukaribisha kwa nyimbo za kumsifu Yehova—nyimbo ambazo wenyewe walikuwa wametunga. Kila siku, karibu 50 wa ndugu hawa maskini walikwenda pamoja nasi tulipokuwa tukitembelea vijiji vya karibu ili kueneza habari njema za Ufalme.
Walakini hali fulani za kuishi hutokeza hatari, na mwishowe nilipatwa na ugonjwa wa kufura ini. Jambo hilo lililazimisha badiliko kwenye utumishi wa painia wa pekee tangu Februari 1965 mpaka Julai 1966, nilipopona kutosha kurudia ziara za mzunguko, wakati huu katika Mkoa wa Tarlac katika Luzon ya kati. Huko Huks (magaidi) walifanya mambo yawe hatari, nao watu wengi walikuwa wameuawa. Ingawa rnikutano ya kawaida isingeweza kufanywa mara nyingi, iliwezekana kusaidia waamini wenzi kiroho kwa kuwatembelea nyumbani mwao. Siku moja, tulipokuwa tukila kiamsha-kinywa pamoja na ndugu mmoja na jamaa yake katika nyumba yao ndogo ya miti na mianzi yenye paa la mabati, lori mbili zenye askari ziliizunguka nyumba hiyo kwa ghafula. Bunduki zikiwa zimelenga, walituhoji, mmoja baada ya mwingine. Nilipata nafasi isiyopatikana mara nyingi ya kumweleza afisa mwenye amri juu ya “habari njema.” Kwa kutosheka kwamba sisi hatukuwa Huks, walienda zao. Kwa mara nyingine kumtumaini Yehova kulithawabishwa.—Mit. 29:25.
LUGHA NYINGINE YA KUJIFUNZA
Barua ya tarehe 31 Agosti, 1967, kutoka kwa Sosaiti ilitushangaza sana. Ilitualika tuchukue utumishi wa misionari katika Indonesia. Kwa njia ya sala, tulitafuta uongozi wa Yehova na kisha tukakubali mwaliko huo. Kwa hiyo ndivyo sisi, pamoja na Wafilipino wengine sita, tulivyofika Jakarta katika Februari 18, 1968.
Katika mikutano ya kwanza tuliyohudhuria iliyoongozwa katika Kiindonesia, niliyoweza kuwaambia ndugu na dada zangu wa kiroho yalikuwa “Selamat sore. Selamat datang. Silahkan masuk.” (“Habari ya alasiri. Karibu. Tafadhali ingia.”) Mtaala wenye uharaka katika lugha ya Kiindonesia ulianza mara moja. Mtaala huo ulipomalizika niliwekwa niangalie kundi jipya. Lilikuwa jambo gumu kwangu kama nini! Bila shaka, nilihitaji ‘kufanya maendeleo katika maarifa yangu ya lugha hiyo. Tuliona kwamba njia bora zaidi kujifunza ilikuwa kushiriki kwa bidii katika kazi ya kutoa ushuhuda nyumba kwa nyumba. Watu wa Jakarta walikuwa wakarimu na wenye kutoa msaada, nao walitukaribisha nyumbani mwao na kwa upole kujaribu kuyafahamu tuliyokuwa tukisema. Kwa njia hiyo tulifanya maendeleo ya haraka, kwa kuwa Kiindonesia kinafanana kidogo na lugha fulani za Filipino. Hivyo baada ya miezi nane peke yake, tulipewa mgawo wa kufanya ziara za mzunguko kwa mara nyingine, tukitumia Kiindonesia tulichokuwa tumejifunza karibuni.
Baada ya wakati fulani katika eneo la Jakarta, tulipewa mgawo wa kutembelea makundi yaliyokuwa katika kisiwa cha Sulawesi. Huko ukosefu wa njia za kusafiria na barabara mbaya-mbaya zilikuwa jambo lenye kujaribu, walakini kwa mara nyingine upendo wa ndugu ulistahilisha jitihada zetu. Katika kundi mojawapo mwanamke mmoja alimfikia mke wangu na kusema hivi: ‘Tafadhali niombeeni kwamba niweze kuvumilia mateso anayoniletea mume wangu kwa ajili ya kweli.’ Tulimtia moyo na kumfariji kwa Biblia na kumwombea, lakini baadaye tukapoteana na mwanamke huyo, kwa kuwa mume wake alihamia sehemu mbalimbali zilizokuwa peke yake ili amwondoe mbali mke wake walipokuwa Mashahidi. Miaka kadha baadaye, lilikuwa jambo la kushangaza kama nini kumwona mwanamke huyo kati ya wale waliobatizwa katika kusanyiko la mzunguko!
MKAZO WENYE KUONGEZEKA
Katika mwaka 1976, tulikuwa tunajaribu kutayarisha kusanyiko la ndugu wa Sulawesi katika Manado. Tuliomba majumba matano tofauti tofauti, lakini tukakatazwa. Mwishowe, jumba zuri lilipatikana walakini kodi yake ya (fedha za Indonesia) Rp260,000 (shilingi za Kenya 4,702 au Z1,567) ilizidi mapato yetu. Tulishangaa kama nini wakati mtu asiyeamini alipotoa mchango wa Rp100,000! Kisha mwamini mwenzetu akatoa mchango mkubwa, hivyo tukaweza kulipia jumba hilo. Kusanyiko zuri lilifanywa, nalo jambo lenyewe lilitokezwa na Mungu, kwa kuwa ndilo lililokuwa kusanyiko kubwa la mwisho la ndugu zetu katika sehemu hiyo, kwani upinzani kwa utendaji wetu uliongezeka.
Kwanza, tulikatazwa tusitembee nyumba kwa nyumba. Lakini akina ndugu walijifunza namna ya kuwapata watu ambao wangeweza kuzungumza nao. Hivyo, watu wengi wenye kupendezwa walipatikana nayo kazi ikazidi kufanya maendeleo.
Kisha tukakatazwa kukutanika katika nyumba za watu. Akina ndugu wakaanza kujenga Majumba ya Ufalme zaidi. Walakini katika Desemba 24, 1976, marufuku kamili ilitangazwa juu ya utendaji na mikutano ya Mashahidi wa Yehova wakiwa kama watu mmoja mmoja, vilevile wale wa shirika lao halali, Shirika la Wanafunzi wa Biblia la Indonesia. Tulifahamu kwamba hati zetu za kukaa nchini hazingefanywa upya, lakini tulifurahi kwamba hatukulazimishwa kuondoka mara moja. Tuliomba muda mrefu zaidi wa kukaa na mwishowe afisa mmoja wa uhamiaji alitupa siku nyingine 10. Siku iliyotangulia kuondoka kwetu, tulifanya mandari (karamu) pamoja na ndugu 200. Ilikuwa nafasi nzuri ya kutiana moyo. (Rum. 1:11, 12) Hivyo tukalazimishwa kuwaacha ndugu na dada zetu wapendwa wa Indonesia baada ya miaka tisa ya kutumikia pamoja nao yenye kuthawabisha.
KUTUMIKIA NCHI NYINGINE
Hata hivyo, tulipendezwa kwamba iliwezekana kutumikia Yehova mahali pengine—wakati huu ikiwa ni Taiwan. Kwa mara nyingine tukawa na funzo letu la lugha, lakini sasa katika Kichina cha Mandarin, lugha iliyo tofauti kabisa na yo yote tuliyokuwa tumejifunza. Ingawa ni lugha yenye sauti zenye kugeuka-geuka zenye kubadili maana ya maneno yenye sauti ile ile nayo haiandikwi katika herufi za Kilatini, tunafanya maendeleo. Kama vile katika nyakati zilizopita, twaomba msaada wa Yehova katika kuhubiri “habari njema za ufalme.” (Mt. 24:14 NW) Twafanya kazi katika mji wenye viwanda unaokua haraka wa Kaohsiung, wenye zaidi ya wakaaji 1,000,000. Kundi letu dogo lenye watangazaji 30 wa “habari njema” lina mgawo mkubwa sana. Lakini tu wenye furaha kama nini kuona zaidi ya maradufu ya hesabu yetu wakihudhuria mikutano ya Jumba la Ufalme!
Wakati wa karibu miaka 30 ambayo tumejitoa wakf kwa Yehova, mara nyingi zisizohesabika tumeona kwamba mwendo ambao mtume Paulo alishauri ndio ulio bora zaidi. Tukiwa tumetumia miaka 25 kati ya hiyo katika utumishi wa wakati wote, twafahamu kwamba mtu ‘akifurahi katika tumaini lililo mbele, akivumilia dhiki na kudumu katika sala’ baraka ya Yehova itatajirisha sana maisha yake.—Rum. 12:12, NW.