“Nuru Yenu na Iangaze”
WANAFUNZI wa Yesu wanapaswa kuangaza kama taa zenye mwangaza mwingi katika ulimwengu huu, wakielekeza wanadamu wenzao kwenye njia inayoongoza kwenye umilele wa maisha ya furaha. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Mwana wa Mungu alisema: “Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima. Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani. Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.”—Mt. 5:14-16.
Mwenendo ulio mfano bora wa wanafunzi wa Kristo unapaswa uwafanye waonekane tofauti na watu wasiofahamiana na ujumbe wa Biblia. Fadhili, subira, ustahimilivu, upendo na sifa nyinginezo bora zao zapaswa kuwafanya waonekane kuwa nuru katika ulimwengu huu mkatili, usio na upendo. Hata hivyo, ili wengine wapate kujua sababu ya mwenendo wao wa kusifika, Wakristo wanapaswa kuwa watangazaji wa masadikisho yao. Hiyo ndiyo sababu mashahidi wengi wa Yehova wanaweka kando wakati kila juma ili watembelee jirani zao wakiwa na ujumbe wenye kufariji wa Neno la Mungu. Pamoja na hayo, wanatumia’ vizuri nafasi zao za kushiriki maarifa yao pamoja na ye yote wanayekutana naye wanaposhughulika na mambo yao ya kila siku maishani.
UJAPOKUWAKO UPINZANI
Sikuzote si rahisi kwa watumishi wa Mungu kuangaza kama nuru. Mara nyingi wanadhihakiwa na kuwa vitu vya kuchukiwa. Ujumbe wanaotangaza—kwamba karibuni ufalme wa Mungu utaponda-ponda hii taratibu mbovu ili kutayarisha kuleta Taratibu Mpya—haupendwi na ulimwengu. Wale wanaopendelea kuishi maisha bila kumwamini Yehova Mungu na Mwanawe hawataki kusikia ujumbe wa Biblia. Wanaupinga na hata huenda wakafaulu kufanya marufuku ipigwe juu ya utendaji wa watu wa Mungu. Vilevile, Mkristo akifanya mabadiliko maishani mwake awe bora anaweza kudhihakiwa. Mtume Petro alisema jambo hilo, akasema: “Kwa sababu hamwendelei kukimbia pamoja nao [walimwengu] katika mwendo huo wa hali ile ile ya upujufu, wanatatizwa na kuendelea kuwatukana ninyi.”—1 Pet. 4:4, NW.
Kujikumbusha historia ya hivi karibuni kunaonyesha kwamba ndivyo ambavyo imekuwa kwa Mashahidi wa Yehova. Kwa furaha, hiyo haijawasimamisha, wakiwa kama jamii, wasiendelee kutenda kulingana na maneno ya Yesu kwamba ‘waangaze nuru yao.’ Wanakubali kwamba si wakati kamwe kwa Wakristo kuficha nuru yao kwa woga, kana kwamba ni “kuiweka chini ya pishi.” Hata hali ziweje, kweli inahitaji kuangaza katika maneno na matendo ya watumishi walio wakf wa Yehova.
Bila shaka, hiyo haimaanishi kwamba kwa kukosa kiasi mtu angepuza hali zisizofaa ambazo analazimika kutimiza utendaji wake wa Kikristo akiwa chini yazo. Yesu Kristo alishauri kwamba wafuasi wake wajiendeshe kwa hekima katika ulimwengu wenye uadui. Yesu aliwaambia hivi mitume wake: “Angalieni, mimi nawatuma kama kondoo kati ya mbwa-mwitu; basi iweni na busara kama nyoka, na kuwa watu wapole kama hua. Jihadharini na wanadamu.” (Mt. 10:16, 17) Hivyo, katika nyakati za magumu, tahadhari inahitajiwa tunapotafuta watafutaji wanyofu wa Mungu.
SABABU GANI UPENDEZWE?
Lakini sababu gani tupendezwe sana na kuangaza nuru yetu? Biblia inaonyesha kwamba Muumba ameweka siku ya kutoa hesabu, au hukumu, kwa wanadamu wote. (Matendo 17:31) Ili siku hiyo ya hukumu ituletee baraka, twahitaji msimamo unaokubaliwa naye. Msimamo huo unaokubalika unawezekanaje? Twahitaji imani ambayo inatusukuma kufanya yote tuwezayo ili kusaidia wengine wawe na waendelee kuwa wanafunzi wa kweli wa Kristo.
Angalia namna mtume Paulo alivyohusianisha jambo hilo la hukumu na maana ya kuhubiri kunakotegemezwa na mwenendo wenye kusifika. Aliandika hivi: “Kwa maana imetupasa sisi sote kudhihirishwa mbele ya kiti cha hukumu cha Kristo, ili kila mtu apokee ijara ya mambo aliyotenda, kwamba ni mema au mabaya. Basi tukiijua hofu ya Bwana, twawavuta wanadamu.”—2 Kor. 5:10, 11.
Paulo alikubali mamlaka isiyolinganika ambayo Yehova Mungu alikuwa amempa Mwanawe. Yesu Kristo sasa ana ‘mamlaka yote mbinguni na duniani.’ (Mt. 28:18) Kuhusu uwezo wake wa kuhukumu, Mwana wa Mungu alitangaza hivi: “Baba hamhukumu mtu ye yote, bali amempa Mwana hukumu hiyo.” (Yohana 5:22) Hukumu ya Yesu Kristo haitakuwa na kosa nayo itakuwa ya mwisho. Hawezi kudanganywa na sura ya nje wala maneno ya werevu. Kwa njia ya unabii ilisemwa hivi juu yake: “Hatahukumu kwa kuyafuata ayaonayo kwa macho yake, wala hataonya kwa kuyafuata ayasikiayo kwa masikio yake; bali kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili.” (Isa. 11:3, 4) Kweli kweli, kuna sababu nzuri kuwa na woga unaofaa wa hakimu huyo mashuhuri anayestahili mwenye mamlaka yote ya kutoa maamuzi ya mwisho. Si kwamba tu sisi binafsi tunataka kutenda katika njia inayoonyesha imani yetu kwake akiwa hakimu, bali pia twataka kuvuta wengine wachukue hatua za lazima ili wapate hukumu nzuri kutoka kwake.
Kwa wazi, basi, watu wa rangi zote, mataifa na kabila wanahitaji kujua wanayopaswa kufanya kusudi siku inayokaribia haraka sana ya kutoa hesabu iwe kwa faida yao. Hiyo inakaziwa vizuri sana katika maneno haya: “‘Kila mtu atakayeliitia jina la Yehova ataokolewa.’ Hata hivyo, watamwitaje yeye ambaye hawajamwamini? Nao, watamwaminije yeye ambaye hawajasikia juu yake? Nao, watasikiaje pasipo mtu wa kuhubiri?”—Rum. 10:13, 14, NW.
Kwa sababu ya kuthamini maana ya kutangaza “habari njema,” mashahidi wengi wa Yehova wanashiriki katika utumishi wa painia msaidizi, wakitoa angaa saa 60 wakati wa mwezi fulani wakitangaza kweli ya Biblia. Hiyo imeongoza kwenye baraka nyingi. Kwa mfano, kama miaka mitatu iliyopita, kulikuwako Shahidi mmoja katika Dacca, Bangladesh. Kisha Shahidi mwingine, akiwa pamoja na mkewe, alikuja kwenye mji huo kwa ajili ya mkataba wa kazi. Wenzi hao waliooana walianza kushiriki ujumbe wa Biblia kwa juhudi pamoja na wengine, na karibuni hesabu ya watangazaji wa Ufalme ikaongezeka ikawa nane. Kati ya hesabu hiyo, wawili walitumikia wakiwa mapainia wasaidizi kwa ukawaida. Nini kilitokezwa na utendaji huo ulioongezwa? Kama mwaka mmoja uliopita zaidi ya mafunzo ya Biblia 20 yalikuwa yakiongozwa kwa watu wenye kupendezwa, na wengi wao walikuwa wakihudhuria mikutano iliyokuwa imepangwa.
Tukiamini kweli kweli kwamba siku ya kutoa hesabu inakaribia wakati wote, je! hiyo haipaswi kujionyesha katika tamaa ya kuarifu watu juu ya uhakika wa tukio hilo? Maarifa ya kwamba utasimama mbele ya Hakimu aliyewekwa na Mungu yanaongozaje maisha yako? Je! unalifanya kuwa azimio lako kuwaza, kusema na kutenda katika njia ambayo itavutia dhamiri njema ya wanadamu wenzako? Je! unaweka wakati kando kwa ukawaida ushiriki pamoja na wengine kweli za Neno la Mungu? Je! moyo wako unakuchochea uzungumze nyakati nyinginezo vilevile? Iwapo unajitahidi kwa bidii kuwa kama Mwana wa Mungu katika kuwaza, kusema na kutenda, hakika utakuwa ukiishi kwa kupatana na shauri lake: “Nuru yenu na iangaze.”