Wewe Unafurahishwa na Mambo Anayochukia Mungu?
MHUDUMU Mkristo na mkewe walikuwa na tikiti za kuingia mchezo uliopasa kuwa wa kuigiza mchezo mmoja ulioandikwa na mwandikaji mashuhuri Shakespeare. Walakini, walipokwenda kwenye jumba la maonyesho wakakuta kwamba mchezo huo ulijaribiwa ukawa hauna matokeo mazuri sana na kwa hiyo mchezo mwingine wa kisasa ukachukua nafasi hiyo. Wengi wa watazamaji walikuwa watu wazee-wazee, wenye mapato ya kiasi na wengine wenye utajiri mwingi, kwa maana jumba hilo la maonyesho lilikuwa moja la majumba mazuri zaidi ya jiji la New York.
Baada ya kuutazama mchezo kwa dakika zipatazo tatu nne hivi mhudumu huyo akamgeukia mkewe na kumwuliza, “Uko tayari?” Mke alijua moja kwa moja jambo alilofikiria mumewe, kwa hiyo akasema “Ndivyo,” kisha wote wawili wakainuka na kuondoka nje. Kwa sababu gani? Mwanzo wa mchezo huo ulikuwa na maneno machafu-machafu ajabu, tena ishara za mwili zilifanywa kwa njia iliyowafanya wakajisikia hawakutaka tena kuvumilia hali hiyo yenye kuvunja heshima. Nyakati nyingine, pia, mashahidi wa Kikristo wa Yehova wamelazimika kuchukua hatua kama hiyo ya mume na mke huyo, kwa sababu walikwenda kukuta mambo tofauti na yale yaliyotangazwa mapema.
Mungu anachukia nini? Yeye anachukia yote yaliyo mabaya. Kati ya mambo mengine, yeye anachukia ‘moyo ambao unatunga mipango ya hila yenye madhara na nyayo zilizo katika haraka ya kukimbilia ubaya.’ (Mit. 6:16-19, NW) Kwa sababu yeye anachukia mambo yote yaliyo mabaya atawahukumu vikali wote wanaozoea uchafu usiopatana na adili.—Ebr. 13:4.
Hakuna wakati mwingine uliotangulia ambao umepata kuwa na uchafu mwingi sana unaovunja adili kila upande kama siku hizi. Sinema, michezo ya kuigiza jukwaani, maonyesho ya televisheni, vitabu na magazeti, vyote hivyo vinachochea nyege za watu wengi wapendao uasherati na mambo machafu.
Kwa nini hali ya mwili wa kibinadamu inaelekea sana hivyo kufurahia mambo anayochukia Mungu? Ni kwa sababu ya mwanzo mbaya tuliopewa na wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. Kwa sababu wao waliingilia mwendo wa uchoyo, kutokutii na uasi “mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake.” Alipokwisha kusahihishwa kuhusu dhambi nzito alizomtenda Yehova, Mfalme Daudi aliandika hivi: “Mimi naliumbwa [nilitokezwa nje kwa maumivu ya kuzaa, NW] katika hali ya uovu; mama yangu alinichukua mimba hatiani.”—Mwa. 8:21; Zab. 51:5; 2 Sam. 12:7-14.
Raha ambayo wanadamu wasio wakamilifu wanapata kutokana na mambo ambayo Mungu anachukia inaweza kufananishwa na tamaa nyingi ya kutaka peremende au vitu vyenye sukari ambayo mtu mwenye ugonjwa wa sukari huwa nayo. Sana-sana watu wanapata ugonjwa huo wa mwili kushindwa kuyeyusha vitu vyenye wanga na sukari kwa kuwarithi wazazi, ingawa unaweza kuongezeka haraka sana na kuwa mbaya sana mtu asipotumia busara katika kula na kunywa au unaweza kuharakishwa na mambo mengine. Kwa sababu dawa-dawa zilizo katika mwili wa mgonjwa zinashindwa kufanya kazi kwa njia nzuri, mtu huyo anatamani sana kitu kile kile asichopaswa kukila. Hiyo inatukumbusha mstari mmoja ulioandikwa na Shakespeare: “Mapendo yako ni hamu ya kutaka kula ya mtu mgonjwa, ambaye hutamani vingi ambavyo vingeongeza uovu wake.” Naam, sawa na vile hali fulani za magonjwa zinavyofanya mtu atamani vitu ambavyo vingeufanya ugonjwa uwe mbaya zaidi, ndivyo maelekeo yetu ya kutokukamilika tuliyorithi yanavyotuinamisha kuelekea mabaya.
Tusithubutu kuiachia nafasi tamaa yo yote ya kutaka kujifurahisha na mambo mabaya. Kwa sababu gani? Kwa sababu tutazoea sana kufanya hivyo mpaka tujikute tukiwa na maelekeo ya kuzidi kufanya hivyo, halafu wakati kishawishi chenye nguvu kitakapotokea tutashindwa nacho na kuanguka, kisha tuwe na huzuni ya muda mrefu sana.
Hata mtume Paulo alijikaza sana katika kupambana na hali hii. Ndiyo sababu yeye aliandika hivi: “Lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo. Basi nimeona sheria hii, ya kuwa kwangu mimi nitakaye kutenda lililo jema, lipo lililo baya. Kwa maana naifurahia sheria ya Mungu . . . lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu, na kunifanya mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu.”—Rum. 7:19, 21-23.
Ni jambo gani litakalotulinda? Ni kuchukia sana zaidi mambo anayochukia Yehova na kuyachukia kikweli, naam, kujisikia tukitaka kutapishwa nayo: “Chukieni lililo ovu kiasi cha kutaka kutapika.” (Rum. 12:9, NW) Si jambo jepesi kufanya hivyo. Ni kama vile alivyoeleza mwandikaji mmoja mwanamke aliyetatizwa sana kuacha kuvuta sigara: “Nawezaje kuchukia kitu kile kile kinachonipa raha?” Lakini mtu anaweza kukaza nia na kuzidi kujiambia mwenyewe akichukie na kutokutaka kabisa kukiona kilicho kibaya, kiovu, chenye madhara, chenye kuleta uharibifu, kitu kisicho cha hekima. Mtume Paulo alichukua hatua ya kutengeneza hali yake, kama vile alivyoandikia kundi jingine la Kikristo: “Mimi naupiga-piga ngumi mwili wangu na kuufanya kama mtumwa, ili, nikiisha kuhubiri wengine, mimi mwenyewe nisije nikakataliwa kwa njia fulani.”—1 Kor. 9:27, NW.
Hiyo haina maana ya kwamba kwa halisi Paulo aliupiga-piga makonde mwili wake jinsi Martin Luther alivyofanya alipokuwa mtawa wa kiume, akiucharaza (akiupiga) mwili wake mijeledi mpaka damu ikatiririka. Bali, Paulo alijitia adabu; alijizoeza kujiweza sana sana, kwa njia iliyokazwa kikiki. Kwa sababu ya kufanya hivyo angeweza kuandika hivi: “Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, ili utumishi wetu usilaumiwe; bali katika kila neno tujipatie sifa njema, kama watumishi wa Mungu; . . . katika kuwa safi, . . . katika upendo usio unafiki.” Sisi tunahitaji kufanya vivyo hivyo.—2 Kor. 6:3, 4, 6.
Tunaamriwa tumpende Mungu kwa moyo wetu wote na nafsi yote, akili zetu zote na nguvu zetu zote. Ikiwa tunampenda Mungu kikweli tutataka kuepuka mambo yote yasiyompendeza. (Marko 12:30, NW) Yeye ni mtakatifu naye anatutaka tuwe watakatifu. (1 Pet. 1:15, 16) Vilevile inatupasa tuepuke kupendezwa na nafsi zetu kwa kiasi kisichofaa. Mungu anatuamuru tujipende wenyewe, lakini pia anatuamuru tumpende jirani yetu kama tujipendavyo. (Marko 12:31) Lazima tuendelee kujiambia kwamba kuingilia jambo lililo baya hakufai hata kidogo. Ni kama vile Neno la Mungu linavyolieleza jambo hili: “Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna. Maana yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu; bali yeye apandaye kwa [roho], katika [roho] atavuna uzima wa milele.”—Gal. 6:7, 8.
Kukuza tabia za kufikiri zinazofaa kutatusaidia. Acheni tujihadhari na mambo tunayosoma, vitu tunavyotazama, mambo tunayoziacha akili zetu ziendelee kuyafikiria. Kuisoma Biblia kila siku kutatusaidia, hata kuyaingiza maandiko ya Biblia akilini kiasi cha kuweza kuyasema neno kwa neno. Wala haitupasi kusahau kwamba sala inaleta faida nyingi. Lifanye liwe zoea lako kusali. “Katika kusali, mkidumu.” Yesu alituwekea sisi mfano mwema, kwa maana imeandikwa hivi kumhusu yeye: “Umependa haki, umechukia maasi.”—Rum. 12:12; Ebr. 1:9.
Kuna thawabu gani ya kutia jitihada hizo? Tukifanya hivyo tutaona yakitimia upande wetu maneno yale ambayo mtume Paulo aliendelea kuyasema: “Utauwa hufaa kwa mambo yote; yaani, unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.” Hiyo maana yake ni kutembea katika ile barabara ya kujitia adabu iliyo nyembamba na yenye magumu, lakini barabara hiyo inatokeza amani ya akili na uradhi sasa, na mwisho wayo ni uzima wa milele.—1 Tim. 4:8; Mt. 7:13, 14.