Kuepuka Msiba Wa Kulalwa Kinguvu
Watu wanaweza kufaidika na mambo yanayowapata. Walakini inapokuwa ni kulalwa kinguvu (kuingiliwa, kunajisiwa), ni vema zaidi kupata masomo kutokana na yale yaliyowapata wengine, badala ya wewe mwenyewe kulalwa kinguvu. Kwa kusudi hilo, visa viwili vifuatavyo vinasimuliwa, navyo ni vya kweli.
Huyo msichana alikuwa tineja mwenye kuvutia, mshiriki wa jamaa kubwa iliyokuwa ikiishi kwenye ujamii wa mashambani. Hata hivyo, yeye hakuridhika na ushirika wa watu wa nyumbani mwao. Yeye alikuwa na tabia ya kwenda nje peke yake kutembelea baadhi ya wasichana waliokuwa wakiishi kwenye eneo hilo.
Haijulikani wazi kabisa makusudi yake ya kufanya ziara hizo yalikuwa nini. Kwa wazi yeye alitaka kuwa na hesabu kubwa zaidi ya rafiki wasichana. Hata hivyo kijana mmoja wa kiume huko alimwona. Kama msichana huyo alikuwa ametangulia kufahamiana naye na kufanya jambo fulani la kumtaka, haijulikani. Hata hivyo, katika pindi hiyo, kijana huyo alimlazimisha kufanya ngono.
Inaelekea kulalwa kinguvu hivyo hakukutangulia kupangwa, walakini kuna kisa cha kulalwa kinguvu kwa msichana mwingine kulikotangulia kupangwa. Mwanamume mmoja kijana alikuwa amekuza tamaa ya kufanya ngono pamoja na dada yake wa mzazi mmoja tofauti. Siku moja akajifanya kuwa ni mgonjwa, na akamwuliza babaye ampeleke dada yake kwenye nyumba yake ili amtayarishie chakula. Walipokuwa peke yao, alimkamata msichana huyo. Msichana huyo ajapomsihi sana, yeye alimshinda nguvu na akamlala kinguvu.
Wengine wenu mmetangulia kusoma visa hivyo vya kulalwa kinguvu. Wasichana hao walikuwa Dina, binti ya Yakobo, na Tamari, binti ya Daudi. Masimulizi hayo yameandikwa katika Biblia.—Mwanzo 34:1-7; 2 Samweli 13:1-14.
UHALIFU WENYE KUONGEZEKA KWA HARAKA SANA
Kulalwa kinguvu kumekuwa jambo lenye kutokea mara nyingi sana leo. Inaelekea sababu kubwa inayotokeza jambo hilo iko wazi. Ngono na jeuri vinaonyeshwa kwa wingi katika televisheni na sinema, katika redio, magazeti, majarida na vibao vya matangazo. Katika miji, mashambani—karibu kila mahali mtu anakokwenda—kuna ngono haramu na jeuri. Na watu wanatenda yale wanayoona na kusikia. Masimulizi ya Biblia juu ya ulimwengu uliotangulia gharika ya duniani pote yanafaa siku zetu kabisa: “Ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani . . . na dunia ikajaa jeuri.”—Mwanzo 6:1-5, 11; NW; Yuda 6, 7.
Inaelekea jeuri iliyokuwako wakati huo ni pamoja na mashambulizi ya kulazimisha kufanya ngono, kama ilivyo leo. “Kulalwa kinguvu kunaongezeka kwa haraka sana kuliko uhalifu mwingineo wa jeuri katika Amerika,” ndivyo kitabu The World Book Encyclopedia kinavyosema. “Maofisa wanakadiri kwamba hesabu kamili ya kulalwa kinguvu ni angaa mara nne ya hesabu inayoripotiwa.” Kwa kuwa kulalwa kinguvu kunakoripotiwa ni kama 70,000 kwa mwaka mmoja, hesabu kamili yaweza kuwa imezidi sana robo milioni. Hiyo maana yake ni kwamba kulalwa kinguvu kunatokea kila dakika mbili katika Amerika!
Na bado makosa mengine ya kulazimisha kufanya ngono hayapangwi kuwa ni kulalwa kinguvu. Kuhusu jambo hilo msosholojia (mtaalamu wa hali ya ujamii wa watu) Richard Gelles wa Chuo Kikuu cha Kisiwa cha Rhode anatoa maelezo haya: “Sidhani kuna ndoa isiyokuwa na visa vya mke kulalwa kinguvu nyakati nyingine, ikiwa katika ndoa hiyo mume humpiga mkewe. Kwaweza kuwa kuna visa 400,000 kila mwaka vya wake wanaolalwa kinguvu na waume zao, walakini ukitia ndani kulalwa kinguvu baada ya kutishwa—kutishwa kutendwa jeuri—kwaweza kuwa milioni kadha.”
Lakini lenye kusikitisha zaidi ni hesabu ya makosa ya kufanya ngono na vijana—mara nyingi wakiwa ni watoto tu. Makumi ya maelfu wanalalwa kinguvu kila mwaka. Katika kitabu cha karibuni The Sex Offender (Mtu Anayeingilia Watu Kinguvu), Bart Belin anaandika hivi: “Inakadiriwa kwamba mmoja kati ya wasichana sita atashambuliwa kabla ya umri wa [miaka] kumi na sita.”
Binti ya Yakobo, Dina, yaelekea alikuwa mwanzoni-mwanzoni mwa miaka ya utineja alipolazimishwa afanye ngono. Ni kwa sababu gani Biblia inasimulia juu ya uhalifu wenye kutokeza msiba kama huo? Mtume Paulo anatoa jibu, kwa kusema: “Kwa kuwa yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi.”—Warumi 15:4; 1 Wakorintho 10:11.
Ni masomo gani tunayoweza kupata kutokana na masimulizi hayo ya Biblia?
JIFUNZE KUTENDA KWA AKILI
Dina alikosa kutenda kwa akili. Biblia inasema kwamba alizoea kwenda nje kuwaona binti za nchi hiyo.’ (Mwanzo 34:1, NW) Wakaaji wa nchi ya Kanaani walikuwa mafasiki, na kwa wazi ukahaba ulikuwa ni jambo la kawaida. (Mwanzo 34:31; 38:21) Kwa wazi Dina hakupaswa kujipeleka akachangamane nao. Inaelekea wazazi wake walikuwa wamemwonya asishirikiane na wasichana wa nchi hiyo. Kama walifanya hivyo, yeye alikataa kusikiliza, na jambo hilo likatokeza matata.
Vivyo hivyo, wanawake vijana wengi leo wanalalwa kinguvu kwa sababu ya kujiingiza isivyo lazima kwenye hali zinazoelekea kuwafanya wajiachilie waingiliwe. Wenye kutembea wakiomba-omba lifti (wabebwe kwa motokaa) wanafanya hivyo. Katika mtaa wa Multonomah huko Oregon inaripotiwa mtu mmoja analalwa kinguvu kila siku. Na zaidi ya nusu ya wanaolalwa kinguvu ni vijana wasichana wanaoomba-omba lifti wanapotembea!
Wanaume wengi wanatafuta mtu wa kufanya ngono nao, na wanawaza kwamba mwanamke anayeomba lifti anajitolea kufanya ngono kwa kufanya hivyo. Hayo yamekuwa maoni ya kawaida. Kwa mfano, hakimu mmoja wa California, akieleza sababu gani shtaka la kulala kinguvu liliondolewa, aliandika hivi: “Halingekuwa jambo la upumbavu kwa mwanamume aliye katika hali ya mshtakiwa hapa kusadiki kwamba mwanamke [mwombaji lifti] angependa kufanya ngono.” Maoni hayo yanaweza kuonekana kuwa yasiyo ya huruma na yenye kosa, walakini yanaonyesha mambo yalivyo kikweli katika ulimwengu wa leo.
Ingawa mwanamume hana haki ya kulazimisha mwanamke afanye ngono naye, chini ya hali yo yote, wanawake wanahitaji kuwa wenye akili kuhusu jinsi vitendo vyao vinavyoonwa na wanaume. Mwana wa mkuu aliyemlala Dina kinguvu huenda ikawa aliwaza kwamba, kwa kujijasirisha akiwa peke yake, Dina alikuwa msichana mwenye kujiachilia atendwe lo lote. Pengine alikata maneno kwamba ziara zake hazikuwa tu za kuja kuwaona rafikize wasichana, bali kumwona yeye hasa. Kwa hiyo pengine yeye alisadiki kwamba kwa kweli Dina alitaka alichokipata.
KUWA NA AKILI LEO
Leo kuna uhitaji mkubwa zaidi kwa wanawake kuepuka tabia ambayo huenda wanaume wakafahamu vibaya kuwa ni mwaliko wa kufanya ngono pamoja nao. Frederic Straska, ambaye amejifunza na kutoa hotuba kwa sehemu kubwa juu ya kulala kinguvu, alitoa maoni haya:
“Kwa njia isiyo ya moja kwa moja wanawake wanawashawishi wanaume wakati wo wote wanapofanya jambo lo lote hadharani linaloweza kuwafanya wengine wasadiki wamekwisha kufanya au wanafanya ngono na mtu fulani. Sana sana ninazungumza juu ya kuonyesha shauku za mapenzi hadharani, walakini kuna mambo mengine yanayoweza kutoa wazo hilo.
“Siku hizi, vijana wengi wanaume na wanawake wanaanza kuishi pamoja bila kuoana kisheria, na kwa hakika jambo hilo ni shauri lao. Walakini huenda kukawa wanaume fulani kuwazunguka ambao wanafikiri vingine. Wanaume hao wanawaza kwamba mwanamke ye yote mwenye nia ya kuishi pamoja na mwanamume fulani, na hata kulala naye pasipo kufunga ndoa, anaweza kushawishwa na wanaume wale wengine kwa urahisi.”
Kwa sababu ya wewe kuheshimu sheria za Mungu zinazohusu adili, bila shaka hungekubali kamwe kufanya ngono pamoja na mtu ambaye si mume au mke wako. Hata hivyo tabia fulani zaweza kuwafanya watu wafikiri kwamba wewe ni mwanamke anayependa kuchezewa-chezewa kwa mapenzi. Kwa mfano, ikiwa unakwenda kwenye mabaa (nyumba za pombe) au kwenye madisko (discotheque), ambako wanawake wenye tabia zinazotiliwa mashaka wanakwenda, ni wazi kwamba wanaume wangewaza kwamba wewe, pia, ni mwanamke wa aina hiyo.
Pia, kuvaa kwa njia isiyo ya kiasi, nguo zenye kuonyesha uchi kwaweza kuwashawishi au kuwakaribisha wanaume. Kuhusu jambo hilo, Biblia ina shauri lenye kufaa na lenye thamani sana. Inawashauri ‘wanawake wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri.’—1 Timotheo 2:9.
KATIKA HALI YA KUFANYA MATEMBEZI NA WANAUME
Kutumia akili ni jambo la maana hasa inapokuwa ni kufanya matembezi pamoja na mwanamume. Asilimia kubwa ya kulalwa kinguvu inatokea wakati wa pindi hizo. Na wengine wanasema wakati huo hasa ndipo kunapotokea visa hivyo. Kwa sababu gani?
Kwanza kabisa, ni kwa sababu huenda mwanamke huyo akaenda nje pamoja na mwanamume asiyeheshimu kanuni za adili za Biblia. Huenda akawaza kwamba yeye anatumainika kwa sababu ati anahudhuria mikutano ya kidini. Walakini jambo hilo peke yake si uhakikisho wa kwamba yeye anasadiki au kufanya yale yanayofundishwa na Biblia. Hata katika kundi la Kikristo la karne ya kwanza kulikuwako watu waliokuwa na makusudi mabaya. Juu ya hao mtume Petro aliandika hivi: “Wana macho yenye kujaa uasherati . . . nao wanatongoza nafsi zisizo imara.” (2 Petro 2:14, NW) Kwa hiyo ni jambo la maana kuamua makusudi ya kweli ya mwanamume kijana ni nini kabla ya kwenda kutembea naye.
Zaidi ya hayo, watu wengi huona matembezi ya wavulana na wasichana kuwa namna fulani ya mchezo, wala si njia ya kufahamiana na anayetazamiwa kuwa mwenzi wa ndoa. Walakini mara nyingi ni jambo gani linalotokea mwanamke anapokubali kwenda mahali fulani palipo peke yake akiwa na mwanamume, pengine wakibusiana na kukumbatiana? Kwa wanaume wengi katika ujamii wa watu leo wenye tabia zilizopotoka mchezo huo unaotangulia ngono ni “ahadi” ya kufanya ngono, nao watamlazimisha mwanamke atimize “ahadi” hiyo. Hata ikiwa mwanamume kijana anakusudia kujiendesha kwa heshima, kuamshwa nyege na kubusiana na kukumbatiana kwaweza kushinda makusudi yake mazuri na huenda akamlala kinguvu msichana huyo.
Namna gani maoni ya msichana katika hali kama hiyo? Namna gani wewe mwanamke kijana ukiruhusu hali kama hiyo itokee pamoja na mwanamume kijana unayependa? Inaweza kutokeza magumu yanayosimuliwa na mtaalamu Straska wa tendo la kulala kinguvu: “Kwa sababu ya uhakika wa kwamba huenda ukawa unatatizwa kumwambia mwanamume huyo hapana na pia kujiambia mwenyewe, huenda ukaona ugumu sana kuamua kama huko kwa kweli kulikuwa kulalwa kinguvu au hapana. Huenda ukataka kutuliza dhamiri yako kwa kujiambia [ulilalwa kinguvu].”
Usiwaze unaweza kucheza na matembezi pamoja na mwanamume kama kwamba ni mchezo fulani, au kujiingiza katika hatari kwa njia nyinginezo, pasipo kupatwa na matokeo mabaya. Mara nyingi wanawake vijana, kutia washiriki wa kundi la Kikristo waliodhani wanaiweza hali hiyo, wamepatwa na madhara mabaya sana. Uwe na hekima. Tumia akili. Jifaidi kutokana na masomo yanayotolewa na Maandiko, na uepuke hali ambazo zaweza kukuingiza katika ngono haramu (zisizo halali).
JIHADHARI
Vilevile, jifunze kutokana na mambo yenye kusikitisha yaliyompata Tamari, yule mwanamke kijana ambaye aliongozwa na ndugu yake wa mzazi mmoja tofauti, Amnoni, kwenye mahali pasipokuwa na watu akalalwa kinguvu. Kisa hicho kinaonyesha uhitaji wa kujihadhari, kutambua nia na maoni ya wengine kukuelekea. Kama Tamari angalitangulia kufahamu maoni ya Amnoni ya kutaka kufanya ngono pamoja naye, pengine angaliweza kuepuka kuingia katika hali alimoingia.
Bila shaka, mwanamke hawezi kutangulia kujua uwezekano wote wa jambo hilo kutokea. Kwa mfano, mwanamke kijana mmoja alikaa mwishoni mwa juma moja nyumbani mwa rafikiye msichana. Asubuhi, alipokuwa angali amelala, rafikiye msichana na mama yake walikwenda kununua mboga, wakamwacha nyumbani peke yake pamoja na baba. Baba huyo alikuja chumbani alimokuwa akipumzika msichana huyo na akaketi juu ya kitanda chake. Alipomwambia alitaka kufanya ngono pamoja naye, msichana huyo alishtuka na kuvurugika sana akili hata akashindwa kumpinga sana.
Hata hivyo, mwanamke huyo kijana angaliweza kufanya nini? Wewe ukiwa mwanamke, unaweza kufanya nini mtu akijaribu kukulala kinguvu? Kuna mambo mbalimbali anayoweza kufanya mwanamke.a
MWENDO BORA ZAIDI NA UNAOFAA
Zaidi ya yote, hapaswi kukubali atishike. Tangu mwanzo kabisa anapaswa kujulisha kwamba hatakubali ngono chini ya hali zo zote. Wawakilishi wa gazeti Star la Toronto, baada ya kushauriana na makao yanayoshughulikia hatari za kulalwa kinguvu katika Amerika na Kanada, kwa ujumla walisema habari hii yenye kufanana:
“Wakati wa hatari zaidi katika shambulio la kulalwa kinguvu ni dakika ya kwanza. Mwanamke asiposhindana kwa kutumia nguvu na akili wakati huo, nafasi zake za kuepuka shambulio la kulazimisha kufanya ngono zinazidi kuwa chache.”
Makao ya Kushughulikia Hatari ya Kulalwa Kinguvu ya Cleveland yalieleza hivi:
“Kwanza mwenye kulala kinguvu humchunguza atakayemshambulia ili aone nia yake itaelekea kuwa nini. Yeye hataki matata; anataka kumtisha mwanamke huyo pasipo kelele. Kwa kadiri ambayo mwanamke anaonekana kuogopa, ndivyo anavyoelekea sana kushambuliwa. Kadiri wakati upitavyo akiruhusu shambulio hilo liendelee, ndivyo anavyozidi kuwa ndani ya matata.”
Kwa hiyo mwanamke kijana aliyetangulia kutajwa angalipinga tisho hilo la kuingiliwa kinguvu mara moja, kwa uthabiti, kwa kukata maneno, wala si kama mtu asiyepinga kwa tendo lo lote, bila kujua atakalofanya. Pengine angalisema jambo kama hili: “Ungeonaje kama jambo hili ni bintiyo angekuwa akifanyiwa? Unajua, wengine wanafikiri binti yako nami tunafanana sana.”
Hata kama njia hiyo haingezuia shambulio, ikiwa yeye, tangu mwanzo, angalionyesha kuwa ni mpinzani imara na mwenye kufanya vita, bila shaka kulalwa kinguvu huko kungaliweza kuepukwa. Susan Brownmiller, mnenaji mkuu wa habari ya kulalwa kinguvu, anaeleza hivi:
“Wenye kulala watu kinguvu wanapata ujasiri kwa kadiri shambulio hilo linavyoendelea. Ndivyo ilivyo. Katika visa vingi, mshambuliaji anaanza akiwa na wasiwasi mwingi sana ingawa huenda mshambuliwa asijue hivi. Akiona kwamba amemwogopesha kabisa anayemshambulia, anakuwa na uhakika zaidi.”
Nyuma katika Machi 1974, gazeti Amkeni! (Kiingereza) lilisimulia jinsi mwanamume mmoja aliyekuwa na bastola alivyokuwa ameshika mateka Mashahidi wa Yehova wawili katika chumba kimoja cha hoteli. Alipokuwa akinyosha mkono amvue blauzi (nguo) msichana mmoja, msichana huyo alisema hivi kwa nguvu: “Hapana! Hapana! Acha kabisa we!” Msichana huyo alimwambia ikiwa angemgusa angepiga yowe kubwa ambalo hajapata kulisikia. Akaeleza kwamba kama hangefanya hivyo angeharibu uhusiano wake na Yehova Mungu na kundi la Kikristo. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 22:22-29.) Agizo lake thabiti: “Wewe usithubutu kunigusa wala kunikaribia” lilimzuia mtu huyo akashindwa na la kufanya.
Mwanamke huyo alifanya jambo linalofaa kulingana na Maandiko, na hili ndilo jambo bora zaidi kufanya. Mwanamke Mkristo ana daraka la kupinga, kwa maana suala la utii kwa sheria ya Mungu ya ‘kukimbia uasherati’ linahusika. (1 Wakorintho 6:18, NW) Haingefaa hata kidogo mwanamke aruhusu kulalwa kinguvu.
Kwa hiyo kuhusu kuepuka kulalwa kinguvu kuna masomo mengi tunayoweza kupata kutokana na yaliyowapata wale wa siku za kale za Biblia na watu wanaoishi leo. Kwa kuwa kulalwa kinguvu ndio uhalifu wenye kuongezeka kwa haraka zaidi katika sehemu fulani, hakika ni jambo la hekima kwa wanawake kufikiria yale wanayoweza kufanya ili kupinga.
[Maelezo ya Chini]
a Ili kupata mazungumzo marefu zaidi juu ya habari hiyo, ona toleo la Amkeni! la Machi, 1980.
[Picha katika ukurasa wa 3]
Dina alifanya urafiki na watu ambao hawakumtumikia Mungu
[Picha katika ukurasa wa 4]
Tamari alipatwa na jambo la kumvunjia heshima kwa kulalwa kinguvu na Amnoni, ndugu yake wa mzazi mmoja tofauti
[Picha katika ukurasa wa 5]
Kuomba lifti (ubebwe kwa motokaa) unapotembea kwaweza kuwa hatari
[Picha katika ukurasa wa 7]
Tangu mwanzo kabisa, mwanamke anapaswa kupinga kwa uthabiti mtu mwenye kulala kinguvu, ikiwa ni lazima na apige yowe