Heshimu Mpango wa Yehova kwa Unyenyekevu Kama Malaika
JESHI la Ashuru, lenye zaidi ya wanaume 185,000, lilikuwa limepiga kambi katika nyanda za chini katika Libna kwenye upande mwingine wa nchi tambarare ya Yudea, zaidi ya maili 25 (kilometres 40) kutoka hapo. Miji mingi iliyoharibiwa na maiti zilizokatwa-katwa zilikuwa zimeanguka kote lilikopita jeshi hilo. Lengo la mwisho lilikuwa Yerusalemu.
Mfalme Hezekia Myudea alijua kwamba kukombolewa kwa njia za kibinadamu kusingewezekana. Msemaji wa Waashuru alikuwa ametoa mwito wajitoe na kukubali kushindwa kisha akarudi kwenye kambi ya Ashuru kule Libna. Walakini Hezekia alisihi kwa bidii: “Ee [Yehova], Mungu wetu, utuokoe na mkono wake, nakusihi, ili kwamba falme zote za dunia zipate kujua ya kuwa wewe ndiwe [Yehova] Mungu, wewe peke yako.” (2 Fal. 19:19) Jibu lilitolewa haraka sana, katika usiku uo huo ambao Hezekia alitoa sala.
Muda si muda ripoti ikamfikia Hezekia kwamba usiku uliopita malaika wa Yehova alikuwa ameua askari 185,000 katika kambi ya Waashuru huko Libna. (2 Fal. 19:35) Kama matokeo, Mfalme Senakeribu akarudi moja kwa moja mpaka Ashuru. Huo ulikuwa wonyesho wa nguvu wenye kutisha kama nini aliokuwa ameshuhudia!
WATUMISHI WANYENYEKEVU
Wanaume wenye ushujaa wa kivita wamejivunia matendo madogo zaidi. Walakini ni nini maoni ya malaika? Hawa “wana wa Mungu” wa kiroho ni mifano yenye kutokeza ya unyenyekevu. (2 Pet. 2:11; Ayubu 38:7) Chukua kisa cha malaika aliyeleta ujumbe aliyemtokea mtume Yohana katika njozi. Yohana alipokuwa karibu kumtolea ibada, malaika huyo alionya hivi: “Acha! Mimi ni mtumishi tu kama wewe na ndugu zako; sote tunauzingatia ukweli ule aliofunua Yesu.” (Ufu. 19:10, HNWW; 22:8, 9) Hivyo malaika huyo alikubali kwa unyenyekevu kwamba yeye alikuwa mtumwa wa Aliye Juu Zaidi. Ingawa alikuwa amepewa pendeleo kubwa la kupitisha ufunuo wa kimungu, alikubali kwamba ingekuwa vibaya kwake kupewa ibada yo yote kwa ajili ya kufanya sehemu yake akiwa mtumishi wa Mungu.
Yesu Kristo alitaja kwamba malaika hufurahi sana mtenda dhambi mmoja anapotubu. (Luka 15:7, 10) Hilo ni jambo lenye kutokeza kweli kweli, kwa kuwa mtu huyo anaingia katika njia ya kuwa mtawala katika ufalme wa kimbinguni. Mahali pa kuona wivu juu ya pendeleo hilo wasilostahili wakipewa waliokuwa watenda dhambi hapo kwanza, malaika wanathamini haki ya Mungu ya kutumia wanadamu ambao, kupitia kwa yale ambayo wamepata duniani, wanatayarishwa kutumikia kama wafalme na makuhani wenye huruma. (Linganisha Waebrania 4:15; 5:8, 9.) Wakiwa wanathamini pendeleo la kuruhusiwa kumtumikia Yehova katika cheo cho chote, malaika wanatumikia kwa unyenyekevu warithi wa Ufalme wenye taraja. (Ebr. 1:14) Kwa kweli, hata wanaongoza wahubiri wapate wale wanaomtafuta Mungu.—Linganisha Matendo 8:26-38.
Malaika wanakubali kwamba hakuna nafasi ya kujikweza katika jamaa ya Mungu, iwe mbinguni au duniani. Je! hilo halitutii nguvu tujitahidi kutofanya ‘lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu akimhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yetu’? (Flp. 2:3) Je! tunakubali kwa unyenyekevu mpango wa Yehova katika kundi la Kikristo, tukiheshimu watu wasiokamilika wanaotumikia kama waangalizi? (Ebr. 13:17) Na nini maoni yetu kuelekea waamini wenzetu? Je! Tunawaheshimu na kuwaonyesha fadhili, kujapokuwa kutokamilika kwao? Alipokuwa akizungumza na Abrahamu, mjumbe wa kimalaika wa Yehova alisema hivi, “tafadhali.” (Mwa. 13:14, NW) Je! tunaheshimu watoto, wake, waamini wenzetu hivyo? Malaika hawakujitafutia faida katika kushughulika na wanadamu wasiokamilika. Twapaswa kuwa kama wao.
Kuhusiana na mazishi ya Musa, twapata kisa kingine cha kutii kwa unyenyekevu. Kulikuwako mashindano kati ya malaika mkuu Mikaeli na Ibilisi aliyedai kwamba mwili wa Musa haukuwa mali ya Yehova. Mikaeli alishughulikaje na jambo hilo? Je! alimwonyesha chuki ya madharau mpinzani huyo ambaye ndiye aliyetokeza taabu za wanadamu? (Mwa. 3:1-5) Hasha, “hakuthubutu kumhukumu Shetani kwa matusi; ila alisema: ‘Mungu mwenyewe na akukaripie.’ “(Yuda 9, HNWW) Malaika huyo mkuu aliheshimu mpango wa Yehova wa hukumu, akaepuka kujitanguliza.—Linganisha Yohana 5:19, 30.
Wakifuata mfano wa Mikaeli, waume na akina baba Wakristo wanapaswa kuepuka kuwa wakali au wenye kuamuru katika kutatua masuala ya jamaa, nao wazee wa kundi wanapaswa kuwa waangalifu wasitumie vibaya mamlaka yao kwa kutendea wenye kukosa kwa ukali. (1 Pet. 3:7; 5:1-3) Wale wanaotoa kweli zenye kuokoa uhai kutoka Neno la Mungu kwa hakika wasingetaka kutusi watu wasioitikia bali watamwachia Yehova hukumu ambaye “huutazama moyo.”—1 Pet. 3:8-12; 1 Sam. 16:7.
KUVUMILIA KWA UAMINIFU
Kuheshimu kwa unyenyekevu mpango wa Yehova kuliwezesha malaika wavumilie kwa uaminifu katika migawo yao ya utumishi. Akiwa njiani kwenda kwa nabii Danieli akiwa na ujumbe wa pekee kutoka kwa Mungu, malaika mmoja alipata upinzani mkali. “Mkuu wa ufalme wa Uajemi alinipinga siku ishirini na moja,” malaika huyo alimwambia Danieli baadaye. Akithamini maana ya kumletea mtumishi huyo wa Mungu wa kidunia ujumbe huo, alishindana na upinzani kutoka kwa mkuu wa kishetani asiyeoonekana wa Uajemi kwa siku 21, hata malaika mkuu Mikaeli alipokuja kumsaidia.—Dan. 10:12-14.
Kama malaika huyo, “kushindana kwetu si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya . . . majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.” (Efe. 6:12) Jitihada ya nguvu inatakiwa ili kupinga majeshi ya kishetani yenye kusudi la kuharibu urafiki wetu pamoja na Yehova na kukomesha kutangazwa kwa ufalme wa Mungu. Kuheshimu na kuthamini utawala wa Yehova kutatusaidia kupata ushindi kwa msaada wa roho takatifu.—Ufu. 12:17.
Pindi kwa pindi, huenda tukavunjwa moyo na maoni yasiyofaa ya washiriki wa jamaa au rafiki. Malaika, pia, wamekazwa na waasi. Kabla ya gharika kuu ya siku za Noa malaika fulani waliangukia tamaa zisizofaa. Waliacha ‘makao yao yanayofaa’ mbinguni, wakatwaa miili ya kibinadamu nao wakaingia kwenye uhusiano usio wa kawaida pamoja na wanawake. (Yuda 6, NW) Wengi wa wana wa kiroho wa Mungu, yajapokuwa hayo, walikataa kuvutwa na mwendo wa kutokuaminika wa washiriki hao waasi wa jamaa ya Yehova. Zaidi ya miaka 2,000 baadaye, Danieli aliona njozi ya nyua za kimbinguni. Aliona malaika wangapi? ‘Kulikuwako maelfu elfu wakimtumikia, na elfu kumi mara elfu kumi wakisimama mbele zake.’ (Dan. 7:10) Kama malaika hao wenye haki, usikubali kuvutwa na maoni ya watu wenye kujipendeza. Mifano hiyo ya uaminifu na ikutie moyo.—1 The. 1:7.
UTHAMINI UPENDO WA MUNGU
Yehova aliwaumba malaika na wanadamu wakiwa na uwezo wa kumwonyesha upendo akiwa Baba yao na pia Mwenye Enzi Kuu. Adui mkuu wa Mungu alikuwa malaika mmoja aliyefurahia faida za upendo wa Yehova; hata hivyo alishindwa kuitikia kwa kuthamini. Kukosa unyenyekevu kuliongoza kwenye kutamani umaarufu na hatimaye uasi.—1 Tim. 3:6.
Je! yote hayo hayapaswi kuwa onyo kitia-moyo kwetu? Iwapo malaika, wanaoshindwa kutafakari kwa kuthamini upendo wanaoonyeshwa na Yehova wameangukia tamaa mbaya, namna gani sisi? Kama vile kundi kubwa la malaika waaminifu katika njozi ya Danieli, tutakuwa macho kuona sababu za kumshukuru Yehova kwa ajili ya kutupa mapendeleo kila siku? Na tuthamini nafasi zetu za kumkaribia Mungu.
“Ni nani afananaye na [Yehova] miongoni mwa malaika [Targum]?” auliza mtunga zaburi. “Mungu huogopwa sana barazani pa watakatifu, ni wa kuhofiwa kuliko wote wanaomzunguka.” (Zab. 89:6, 7) Heshima hiyo ya kuogopa inasitawije mioyoni mwa malaika na wanadamu? Kwa kutafakari kila siku sifa nzuri ajabu za Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote kama zinavyofunuliwa katika kazi zake za uumbaji na fadhili zake za upendo,
Mashahidi wa Yehova leo si wachache sana katika kumwabudu Mungu wa kweli. “Walio pamoja nasi ni wengi kuliko wa walio pamoja nao,” Biblia inatuhakikishia. (2 Fal. 6:16) Katika jitihada zetu za kumpendeza Yehova, tunashiriki pamoja na wingi wa malaika wanaomwabudu Mungu yule yule. Viumbe hao wenye nguvu wanapendezwa nasi kwa fadhili, wakati wote wakiwa tayari kutusaidia tusimame imara kwa ajili ya Yehova. (Zab 34:7) Basi, uwe na moyo, kupitia kwa mfano wa wana hao wa Mungu wanaoheshimu mpango wa Yehova kwa unyenyekevu. Tukiwa pamoja nao, na tuendelee kujinyenyekeza kwa mapenzi ya Baba yetu wa kimbinguni mkarimu.