Yehova wa Majeshi’ Aenda Kuokoa!
1. Kwa kuwa kuna wapinzani, ili kuletea wanadamu faraja yenye kudumu itamaanisha nini kwanza?
MSIBA wa ulimwengu uko mbele pasipo kuepukika! Lakini bila shaka matokeo yake ya ulimwenguni pote yataponywa baadaye. “Habari njema” kuhusu jambo hilo zimeenezwa duniani pote na wanaume na wanawake waliojitoa sana na ambao wameaminishwa ujumbe wenye utukufu wa faraja yenye kudumu kwa wanadamu. Habari yao ni yenye kutegemeka, kwa kuwa yatoka kwa Yeye ambaye anahangaikia sana hali ya wanadamu kuliko mtu mwingine ye yote katika mbingu yote na dunia. Kwa furaha, mtu huyo ana uwezo kamili wa kuleta faraja wanayohitaji wanadamu wote. Kwa kweli, yeye amekusudia kufanya hivyo. Walakini kufanya hivyo kutamaanisha apigane na wote wanaopinga kusudi lake, itakuwa vita itakayopita vita vyote!
2. Kulingana na Isaya 59:15b, mpiga-vita huyo mwenye ushindi ni nani?
2 Nabii Isaya anatujulisha huyo mpiga-vita mwenye kushinda ni nani akiwa chini ya uongozi wa roho anaposema hivi: “Naye [Yehova] akaona hayo, akachukizwa kwa kuwa hapana hukumu ya haki.”—Isa. 59:15b.
3. Kusema kwa njia ya mfano, dunia hii ni nini kwa Yehova akiwa Mfalme, na hata hivyo, yeye ameonyeshaje kupendezwa na yale yanayotukia juu yake?
3 Siku hizi watu kwa jumla hawafikiri kwamba Muumba mbingu na dunia anaangalia sana mambo ya kibinadamu. Na kwa sababu gani Muumba asifanye hivyo? Jambo moja kati ya mambo ya mwisho aliyoandika nabii Isaya ni usemi huu: “[Yehova] asema hivi, Mbingu ni kiti changu cha enzi, na dunia ni mahali pa kuweka miguu yangu.” (Isa. 66:1) Hivyo, basi, je! haimpasi Mfalme huyu, anayekalia kiti chake cha enzi juu ya uumbaji wote, apendezwe na dunia mahali pa kuweka miguu yake na yale yanayotendeka huko? Yeye ameonyesha kwamba anapendezwa. Namna gani?
4. Yehova alionyeshaje kupendezwa na yale yanayotendeka katika mahali pake pa kuweka miguu katika siku za Nuhu mwenye kumwogopa Mungu?
4 Uhakika wa kwamba leo hatuna maji yaliyotandaa yakining’inia juu angani kuizunguka dunia yetu na hivyo kufunika mwangaza wa jua, wa mwezi na wa nyota ni kwa vile Yehova aliona yale yaliyokuwa yakitendeka hapa chini mahali pake pa kuweka miguu akachukua hatua. Aliyaachilia maji hayo yaliyokuwa yakining’inia juu ya mahali pa kuweka miguu yake, si kwamba asafishe miguu yake, bali ili aondoe hali mbaya miongoni mwa wanadamu wote. Habari iliyoongozwa na Mungu yasema hivi: “[Yehova] akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote. . . . [Yehova] akasema, Nitamfutilia mbali mwanadamu niliyemwumba usoni pa nchi, . . . Lakini Nuhu akapata neema machoni pa [Yehova].” (Mwa. 6:5-8) Sisi sote ni wadeni wa Nuhu huyu mwenye kumcha Mungu, kwa sababu yeye na jamaa yake, nafsi nane zote pamoja, walijenga safina kwa amri ya Yehova na wakiwa ndani yake wakapita salama gharika hiyo ya duniani pote, ili tupate kuwa wazao wao.
5. (a) Kuharibiwa kwa Sodoma na Gomora kwaonyeshaje kupendezwa kwa Yehova? (b) Uharibifu huo pamoja na Gharika ni wonyesho wa nini?
5 Kile kisa cha baadaye cha Sodoma na Gomora kinajulikana sana ulimwenguni pote. Kuharibiwa kwa miji hiyo ya Mashariki ya Kati yenye kufanya uasherati mbaya sana kulionyesha kwamba Yehova anapendezwa na mambo ya binadamu walio juu ya mahali pa kuweka miguu yake. (Mwa. 18:20, 21) Loti mwenye haki pamoja na binti zake wawili waliokolewa na moto huo uliokunya kutoka juu ukaiteketeza Sodoma na Gomora. Sababu gani? Ni kwa sababu, ijapokuwa waliishi katika Sodoma, Loti “alisikitishwa na mwenendo mbaya wa watu hao waasi,” na “moyo wake [wenye haki] ulikuwa katika wasiwasi mkuu aliposikia matendo yao maovu.” (2 Pet. 2:6-8, HNWW) Jambo lenye kupendeza juu ya hili ni kwamba kuharibiwa huko kwa Sodoma na Gomora kwa moto na kule kwa ulimwengu wa kale kwa Gharika kunalinganishwa katika njia fulani na mwisho wenye jeuri wa taratibu ya ulimwengu ya mambo iliyopo.—Luka 17:26-37; Mt. 24:36-39.
6. Ni kwa sababu gani kuenda-enda kwa macho ya Yehova pamoja na uwezo wake wa kuona si mambo ya kupuzwa?
6 Wasodoma (wafiraji) wa kisasa, ndiyo, vikundi vingine vya watu, hujipofusha wenyewe wakati wanapodhihaki yale yanayosemwa na Maandiko: “Macho ya [Yehova] hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.” Vilevile: “Macho ya [Yehova] yako kila mahali; yakimchunguza mbaya na mwema.” (2 Nya. 16:9; Mit. 15:3) Kwa sababu ya uwezo wake wa kutofautisha kati ya mwema na mbaya, ingeweza kusemwa juu ya Israeli hivi: “Kama [Yehova] wa majeshi asingalituachia uzao, tungalikuwa kama Sodoma, tungalifananishwa na Gomora.”—Rum. 9:29; Isa. 1:9.
7. Inastaajabisha kwa sababu watu wote wamekosa uwezo wa kufanya jambo gani, na ni kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova hawajitolei kufanya jambo hilo?
7 Katika siku za Isaya, wakati Yehova alipoutazama ufalme wa Yuda pamoja na mji wake mkuu Yerusalemu, ni mambo gani aliyoyaona yakiwa mabaya mbele zake? Yote haya: “Kweli imepunguka kabisa, na yeye auachaye uovu ajifanya kuwa mateka; naye [Yehova] akaona hayo, akachukizwa kwa kuwa hapana hukumu ya haki. Akaona ya kuwa hapana mtu, akastaajabu kwa kuwa hapana mwombezi.” (Isa. 59:15, 16a) Ole, ‘hapakuwa na mtu ambaye angestahili kutosheleza mahitaji ya wakati huo, hapakuwa na mwanadamu ambaye angeweza kuomba na kukomesha uongo, matendo yasiyo ya haki, udhalimu, hata katika “njia kuu” ambapo kesi zililetwa ili ziamuliwe. (Isa. 59:14) Hata leo kutoheshimu sheria ya kimungu na uhalifu unaoongezeka juu yake ni jambo linalostaajabisha, sana sana kwa kuwa Jumuiya ya Wakristo sasa imekuwapo kwa muda wa miaka zaidi ya 1,650 Mashahidi wa Yehova hawakuagizwa waonyoshe mambo. Hawangeweza kujiingiza na kufanya hivyo hata kama wangependa kufanya hivyo. Vipi, basi?
8. Ni nani anayejiona kuwa na wajibu wa kupigana vita na watenda mabaya duniani, naye amejipa jina gani linalomfaa tangu karne ya 12 kabla ya kuja kwa Kristo?
8 Hivi: ‘Yehova wa majeshi’ anayo vita ya kupigana. Lazima apiganie haki! Yeye haitegemei Mahakma ya Haki ya Mataifa Yote, hata kama vile asivyoweka mahakma kama hiyo ya kibinadamu ya kupatanisha mataifa. Wakati wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” inayokuja katika Har-Magedoni hautakuwa wakati wa kwanza ambapo amepigana na adui zake duniani. Tayari katika karne ya 12 kabla ya Kristo kuja, alikuwa akiabudiwa akiwa ‘Yehova wa majeshi.’ (1 Sam. 1:3, 11) Wakati nabii Isaya alipomwona katika njozi akiwa katika hekalu lake takatifu, ‘Yehova wa majeshi’ alikuwa amekalia kiti cha enzi kilichoinuliwa na kutukuzwa juu sana, ambacho kwa habari zake maserafi wenye mabawa sita waliruka-ruka juu yake, wakisema kwa kurudia-rudia: “Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, ni [Yehova] wa majeshi.” (Isa. 6:3, 5) Hapo hakuonyeshwa akiwa na vazi la kivita kama lile la Amiri-jeshi Mkuu, huku akifuatwa na majeshi yake.—Linganisha Ufu. 4:1-3.
9. Kwa sababu ya yale ambayo Yehova ameona yakiendelea katika karne hii, yeye anajitayarishia nini na kwa vifaa gani, kulingana na Isaya 59:16b-19?
9 Kwa sababu ya matukio ya ulimwengu tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza itokee katika mwaka 1914, limekuwa jambo lisiloepukika kwamba Hakimu wa dunia yote ajionyeshe mwenyewe kuwa ‘Yehova wa majeshi.’ Kwa sababu ya yale ambayo ameona yakifanyika wakati wa karne hii ya 20 W.K., yeye anajitayarisha kwa ajili ya vita. Isaya anamwonyesha akifanya hivyo katika maneno haya: Mkono wake mwenyewe ndio uliomletea wokovu; na haki yake ndiyo iliyomsaidia. Akajivika haki kama deraya kifuani, na chapeo cha wokovu kichwani pake, akajivika mavazi ya kisasi yawe mavazi yake, naye akavikwa [juhudi] kama joho. Kadiri ya matendo yao, kwa kadiri iyo hiyo atawalipa, ukali kwao wampingao, malipo kwa adui zake; naye atavirudishia visiwa malipo. Basi, wataliogopa jina la [Yehova] toka magharibi, na utukufu wake toka maawio ya jua; maana yeye atakuja kama mkondo wa mto ufurikao, uendeshwao kwa [roho] ya [Yehova].”—Isa. 59:16b-19.
10. Vita ya Yehova inayokuja itakuwa upeo wa vita inayopigwa na nani hapa duniani, navyo vifaa wanavyotumia hao vinatia ndani nini?
10 Vita inayokuja ya Yehova wa majeshi itakuwa ndiyo upeo wa vita yenye kuendelea ambayo Mashahidi wa Yehova wamelazimika kupigana na ambayo wameamriwa wajitayarishie kwa kuchukua silaha. Silaha zao ni za kiroho, nazo zatia ndani kujifunga kweli kiunoni, “dirii ya haki kifuani,” kufunga miguu ‘utayari wa habari njema za amani,’ “ngao ya amani,” “chapeo ya wokovu,” na “upanga wa [roho] ambao ni neno la Mungu.”—Efe. 6:11-17.
11, 12. (a) “Chapeo ya wokovu” anayovaa Yehova inamaanisha nini? (b) “Deraya” ya haki anayovaa inamaanisha nini, nalo jambo hilo latoa ahadi gani?
11 Kwa ajili ya vita ijayo ya ulimwengu wote Yehova anavaa “chapeo cha wokovu kichwani pake,” lakini, badala ya kuvaa ’dirii ya haki kifuani,” yeye anavaa ’deraya” ya haki. Bila shaka, yeye hahitaji vifaa vya namna hiyo vya kumlinda, kwa kuwa yeye ni mwenye nguvu zote na hawezi kufa, hawezi kuangamia. Kwa hiyo hapa usemi wa mfano tu umetumiwa kufananisha jambo fulani. Kuvaa “chapeo cha wokovu kichwani pake” kunaonyesha kwamba yeye anafikiria akilini mwake wokovu wa kusudi lake, na zaidi sana faida za ufalme wake wa Kimasihi. Hakuna jambo ambalo adui watafanya katika kushambulia kusudi lake liweze kupiga na kuondoa kutoka kichwani pake kusudi la wokovu au kumpiga apoteze fahamu zake juu yake, na kumfanya asilifikirie. Kwa habari ya “deraya” ya haki yenye kupindika, kuivaa kiunoni kunaonyesha kwamba kupenda kwake haki hakuwezi kuhalifiwa. Hakuna shambulio lo lote juu ya kusudi lake la kitheokrasi litakaloweza kumaliza kujitoa kwake kwa moyo wote kwa yaliyo haki.
12 Ni kama vile ilivyoandikwa: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki, Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kum. 32:4) Kulingana na “ahadi yake,” yeye atapigana mpaka “mbingu mpya na dunia mpya” zisimamishwe, ambazo katika hizo “haki itakaa.”—2 Pet. 3:13, NW.
13. (a) “Mavazi ya kisasi” anayovaa Yehova yanamaanisha nini? (b) ‘Juhudi anayojivika kama joho’ inamaanisha nini?
13 Yehova atapigana vita akiwa Mlipa-Kisasi. Ndiyo sababu ameonyeshwa kama akijivika “mavazi ya kisasi yawe mavazi yake.” Mashahidi wake duniani wameagizwa ‘watangaze . . . siku ya kisasi upande wa Mungu wetu.’ (Isa. 61:1, 2, NW) Kujivika “[juhudi] kama joho” kunamaanisha kwamba juhudi yake itamsukuma mbele, si kiwazimu, bali kwa heshima kama ile aliyokuwa nayo mtu ambaye katika wakati wa kale alivalia “joho.” Atawalipa adui zake matendo yanayolingana na yale waliyowatenda wale waliosimama imara kwa ajili ya kusudi lake la kitheokrasi. Hata matengenezo madogo, yaliyo peke yake kama kwamba ni “visiwa” yatapata haki yake.
14. (a) Ushindi wenye utukufu wa Yehova utakuwa na matokeo gani kwa wakaaji wa dunia? (b) Ni kwa sababu gani hakuna jambo litakalomzuia Yehova asiendelee kusonga mbele mpaka ajipatie ushindi kwenye Har-Magedoni?
14 Kwa sababu ya vita yenye utukufu atakayopigana, wakaaji wa dunia kutoka mashariki mpaka magharibi watalazimika kumwogopa, tangu machweo ya jua mpaka macheo ya jua. Hakuna jambo litakalomzuia asisonge mbele mpaka ajipatie ushindi. “Maana yeye atakuja kama mkondo wa mto ufurikao, uendeshwao kwa [roho] ya [Yehova].” Itakuwa kama vile ilivyokuwa katika siku za Mwamuzi Baraka na Debora, wakati Yehova alipoufanya “mto wa Kishoni” ufurike na kuyagharikisha majeshi yenye kushambulia ya Mfalme Yabini yaliyokuwa yakiongozwa na Sisera, amiri-jeshi wake mkuu. (Amu. 4:7, 13; 5:21) Katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har-Magedoni, yeye atamtumia Mwanawe anayetawala Yesu Kristo akiwa amiri-jeshi wake, kama vile Ufunuo 19:11-21 unavyoonyesha. Wakati wa vita hiyo roho ya Yehova yenye kuendesha itajionyesha kuwa yenye nguvu zaidi kuliko makombora yote ya atomiki au ya nuklea yatakayolipuliwa wakati huo au yatakayokuwa yamelundikwa duniani.
Mkombozi na Agano Lake
15. Kupitia kwa Isaya, kwa kurudia-rudia Yehova anajitangaza kuwa Mkombozi wa nani?
15 Kwa kurudia-rudia ‘Yehova wa majeshi’ anajitangaza kuwa Mkombozi, au Go·elʹ, wa watu wake wateule, ambao ndio waliokuwa watu wa Isaya. Kwa watu hao wa mfano Isaya aliambiwa aseme hivi: “Usiogope, Yakobo uliye mdudu, nanyi watu wa Israeli; mimi nitakusaidia, asema [Yehova], na mkombozi wako ni Mtakatifu wa Israeli.” Na Tena: “Sasa, [Yehova] aliyekuhuluku, Ee Yakobo, yeye aliyekuumba, Ee Israeli, asema hivi, Usiogope, maana nimekukomboa; . . . Ninyi ni mashahidi wangu, asema [Yehova], na mtumishi wangu niliyemchagua; . . . [Yehova], Mkombozi wenu, Mtakatifu wa Israeli, asema hivi; Kwa ajili yenu nimetuma ujumbe Babeli nami nitawashusha [vifungo vya gereza].”—Isa. 41:14; 43:1, 10-14; 44:6, 24; 48:17; 49:26; 54:5, 8; 60:16; 63:16.
16. Mtume Paulo anatumia wapi sehemu ya maneno ya Isaya 59:20, 21, naye anahusianisha utimizo kamili wa unabii huo na kukamilishwa kwa jambo gani?
16 Kama miaka 23 hivi baada ya kufa, kufufuliwa na kupaa kwa Yesu Kristo, mtume Paulo alitumia sehemu ya maneno ya Isaya 59:20, 21 akaonyesha yana utimizo katika nyakati za Ukristo. Yeye anatoa maelezo hivi: “Kama yasemavyo Maandiko matakatifu: ‘Mkombozi atakuja kutoka Sayuni, atauondoa uovu wa Yakobo. Hili ndilo agano nitakalofanya nao wakati nitakapoziondoa dhambi zao.’” (Rom. 11:26-27, kupatana na Septuagint Version ya Kigiriki) Mtume Paulo anaonyesha utimizo kamili wa unabii huo ukiwa katika wakati ujao wakati ambapo hesabu kamili ya washiriki wa jamii ya Ufalme chini ya Yesu Kristo itakapokuwa imekamilishwa, yaani, washiriki 144,000. Hao ndio Waisraeli waliofanishwa, Waisraeli wa kiroho, walio katika agano jipya pamoja na Yehova Mungu. Wao ni kama hesabu kamili ya matawi katika mzeituni wa mfano. (Rum. 11:17-26) Wakati wa Mungu wa utimizo wa mwisho umetufikia sisi!
17. Ni wakati gani mabaki ya Waisraeli wa kiroho yalipojiuza utumwani, naye Mkombozi wao alikuja kuwakomboa kutoka wapi?
17 Kama vile Waisraeli wa siku za Isaya, Waisraeli wa kiroho walijiuza wenyewe kwa sababu ya matendo yao maovu wakaja katika utumwa wa milki ya dini ya uongo, yaani, wa Babeli Mkuu, na wa hawara zake za kilimwengu. (2 Fal. 17:17; 1 Fal. 21:20, 25) Mfano wenye kutokeza sana wa hilo ulitokea katika wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ya 1914-1918. Ili Waisraeli wa kiroho waliokuwa kifungoni waweze kupata uhuru tena wa kumtumikia Mungu wao pasipo kizuizi na woga, kulikuwa na lazima ya Mkombozi ajitokeze kwa ajili yao. Alitokea, akiwa Yehova mwenyewe. Kwa tendo lake la wakati wake la kutokea akiwa hivyo, aliwakomboa kwa ajili ya utumishi wake. Kama vile Sayuni katika siku za Isaya ulivyokuwa mlima wenye kutokeza zaidi ambao juu yake ulisimama Yerusalemu ukiwa ndio mji mkuu wa ufalme huo, Sayuni uliofananishwa ndiko ambako kutoka huko Yehova angekuja ili aokoe jamii ya Ufalme. (Ufu. 14:1; Isa. 24:23; 52:7) Ndipo mabaki ya Waisraeli na makosa yao ya kumkosea Yehova, wakajitenga kabisa na uhusiano wote na Babeli Mkuu.—Ufu. 18:4.
18. Kuhusiana na jambo hilo, Yehova anamtumia nani kama mdogo wake, naye huyo anaonyeshwa akipigana katika vita gani?
18 katika utendaji wake Yehova alimtumia Mwanawe Yesu Kristo kama mdogo wake au “mjumbe wa agano.” (Mal. 3:1) Akiwa Koreshi Mkuu Zaidi, Yesu Kristo alifungua kwanza mabaki ya Israeli wa kiroho na kisha wenzi wao kutoka kwa Babeli Mkuu. (Isa. 44:28-45:7) Katika Ufunuo 19:11-21 anafananishwa akiwa yeye ambaye anapigana moja kwa moja katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye Har-Magedoni.
19. Ni nini yaliyo masharti ya “agano” ambalo Yehova anafanya na Isaya Mkuu Zaidi, Yesu Kristo, kwa niaba ya mabaki waliokombolewa wa Waisraeli wa kiroho?
19 Akiwa Isaya Mkuu Zaidi, Yesu Kristo ndiye Nabii ambaye Yehova alifanya agano pamoja naye kwa niaba ya mabaki ya Waisraeli wa kiroho waliokombolewa. Agano hilo linaligana na ahadi katika Isaya 59:21: “Roho yangu iliyo juu yako, na maneno yangu niliyoyatia kinywani mwako, hayataondoka kinywani mwako, wala kinywani mwa wana wako, wala kinywani mwa wajukuu wako, asema [Yehova], tangu leo na hata milele.”—Linganisha matendo 3:22, 23.
20. Roho ya Yehova imekuwa juu ya Isaya mkuu Zaidi kwa kadiri gani, na ni jambo gani linalothibitisha kwamba leo maneno ya Yehova hayajaondolewa vinywani mwa “wana” ambao Yehova alimpa Yesu Kristo?
20 Tangu wakati huo nabii Isaya na “wana” wake wa asili wametoweka kutoka duniani. Walakini, Isaya aliye Mkuu Zaidi, Yesu Kristo angali anaishi akiwa mtu asiyeweza kufa, akiwa katika mkono wa kuume wa Mungu huko mbinguni. Roho ya Yehova inamkalia kwa wingi sana. (Isa. 61:1-3; Luka 4:16-21) Vilevile, “maneno” ya Yehova yamewekwa kinywani mwake, ili ayanene hasa duniani pote. Kwa ajili ya hilo yeye ameyatia maneno hayo vinywani mwa “wana” wa kiroho ambao Yehova amempa. Matokeo ya jambo hilo yamekuwa kwamba habari njema za ufalme wa Mungu uliosimamishwa zimehubiriwa ulimwenguni pote.—Mt. 24:14.
21. (a) Tangu mwaka 1395, ni nani ambao wameuchukua ujumbe wa siku za leo vinywani mwao? (b) Ni wakati gani ambapo ‘Yehova wa majeshi’ atalazimika kuja kuokoa, akijishuhudia mwenyewe kuwa nini?
21 Tangu mwaka 1935 “mkutano mkubwa” wamekuwa wenzi wa mabaki ya Waisraeli wa kiroho. Wameuchukua ujumbe wa Ufalme, navyo vinywa vyao vimeutangaza kwa sauti kuu, pamoja na onyo juu ya kisasi cha kimungu juu ya adui za Mungu. (Ufu. 7:9-17) Adui hao wangali wanajaribu kuukomesha ujumbe wa Ufalme. Wakishindwa kufanya hivyo, adui hao walioghadhibika watafanya shambulio la mwisho juu ya wote walio washikamanifu kwa ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo. Bila shaka, wakati huo, kuliko wakati mwingine wo wote uliopita, ‘Yehova wa majeshi’ atalazimika kuja kuokoa. Atafanya hivyo kupitia kwa amiri-jeshi wake, Yesu Kristo “Mfalme wa wafalme.” Aa, basi, njoo, Ee ‘Yehova wa majeshi,’ nao ushindi wako wenye utukufu wote kupitia kwa Kristo na udumu katika maandishi yote ya kihistoria yasiyofutika ya mbingu yote na dunia uwe ushuhuda wa milele wa kuondolewa lawama ukiwa Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote asiyeweza kupingwa!
—Kutoka The Watchtower Nov. 15, 1980.