Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 8/1 kur. 4-5
  • Yanayompata Mvutaji wa Sigara

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yanayompata Mvutaji wa Sigara
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAMBO YA HAKIKA JUU YA UVUTAJI WA SIGARA
  • SIGARA SALAMA?
  • Kwa Nini Uache Kuvuta Sigareti?
    Amkeni!—2000
  • Wauzaji wa Kifo—Je! Wewe Ni Mnunuzi?
    Amkeni!—1990
  • Mamilioni ya Uhai Yakitokomea Moshini
    Amkeni!—1995
  • Sigareti—Je, Wewe Huzikataa?
    Amkeni!—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 8/1 kur. 4-5

Yanayompata Mvutaji wa Sigara

PICHA hiyo ya tangazo la kibiashara inavutia na kupendeza. Ziwa lenye kung’aa la mlimani limepigwa picha pamoja na pakiti nzima ya sigara inayokuelekea kabisa wewe, uliye msomaji. Njia hiyo ya kutoa matangazo ya kibiashara ni yenye matokeo sana. Inashirikisha kuvuta sigara na maono yanayopendeza. Kila mwaka mabilioni ya fedha yanatumiwa kujaribu kushirikisha uvutaji wa sigara na mambo yenye kuvutia maishani. Walakini kusudi la jambo hilo ni nini?

MAMBO YA HAKIKA JUU YA UVUTAJI WA SIGARA

Mwaka 1979, Shirika la Uchunguzi wa Mapafu la Kanada lilifanya wengi watambue ukweli liliposema hivi waziwazi: “Kila mwaka Wakanada 50,000 wanakufa mapema kutokana na uvutaji wa sigara. Wengine wengi wanaendelea kuishi wakiwa na mapafu yasiyofanya kazi na mioyo inayolemewa na kazi.”

Mwaka 1979, daktari mkuu wa upasuaji wa United States, Dakt. Julius B. Richmond, alitoa ripoti ndefu yenye kutaja “uthibitisho mwingi sana” kwamba kuvuta sigara kunahatirisha afya. Ripoti hiyo ilikadiri kwamba, kila mwaka, kuvuta sigara kunaua Waamerika karibu 350,000. Vilevile, katibu mdogo wa afya wa serikali ya Uingereza, Sir George Young, hivi karibuni alisema kwamba kila mwaka kuvuta sigara kunatokeza vifo 50,000 katika Uingereza.

Hesabu hizo kubwa za vifo zinapatikanaje? Ni kwa kulinganisha hesabu ya vifo vya wavutaji sigara na wasiovuta sigara. Kuhusu uchunguzi wa kindani wa mamilioni ya watu, kitabu Encyclopedia Americana kilitoa maelezo haya: “Kwa kila vifo 100 vya wasiovuta sigara wakati wa kipindi cha kuchunguzwa, vifo 168 vilitokea kati ya kikundi cha wavutaji wa sigara; yaani, vifo vya ziada vilikuwa 68.”

Walakini je! ushuhuda huo ni hakika? Ndiyo. ‘‘Hakuna shaka juu ya mambo hayo ya hakika,” ndivyo linavyosema Shirika la Uchunguzi wa Mapafu la Kanada. “Maelfu ya uchunguzi wa uangalifu yamethibitisha hayo. Hakuna shirika lo lote kubwa la utibabu au afya linalotilia shaka hayo.” Gazeti Science 80, lililochapwa na Shirikisho la Amerika la Kuendeleza Sayansi, linakubali hivi: “Ushuhuda wa kwamba sigara zinafupiza maisha ni mwingi mno; uhusiano huo umethibitishwa kabisa kama mwingineo wo wote katika utibabu.”

Uchunguzi wenye kuthibitisha umewezeshwa na hesabu kubwa ya watu ambao wamevuta sigara katika sehemu kubwa ya maisha yao. “Kwa kurudia kuangalia hayo,” ndivyo anavyoandika John Cairns, mtaalamu wa chembe za viumbe na mtaalamu wa donda baya, “ni kana kwamba jamii za [nchi za] Magharibi zilijitokeza kuendesha jaribio kubwa lenye kuongozwa vizuri juu ya kutokea kwa donda baya, zikaleta vifo vya watu milioni kadha na kutumia watu wazo kama wanyama wa kufanyia majaribio hayo.”

Ndiyo, mamilioni ya maisha—mamilioni mingi, mengi— yamefupizwa na kuvuta sigara. “Uchunguzi wa utibabu,” ndivyo kitabu The World Book Encyclopedia, kinavyoeleza, “unaonyesha kwamba kwa wastani urefu wa maisha ya mvutaji sigara unapungua miaka mitatu kufika minne ya mtu asiyevuta sigara. Urefu wa maisha ya mvutaji sigara kwa wingi—mtu anayevuta pakiti mbili au zaidi za sigara kwa siku moja—waweza kupungua miaka minane ya mtu asiyevuta sigara.”

Zikiwa na jitihada za kupunguza hatari, sigara zinazoitwa “salama zaidi” zinauzwa. Walakini je! kweli kweli ni salama? Ni kwa njia gani kuvuta sigara kunavyomdhuru mvutaji sigara?

SIGARA SALAMA?

Sumu ya nicotine na visehemu vidogo vya moshi wa sigara—ambavyo kwa njia isiyo sahihi sana huitwa lami ya sigara—kwa wazi ndivyo vinavyotokeza maradhi kwa sehemu kubwa. Kwa hiyo lami ya sigara na sumu ya sigara (nicotine) vimepunguzwa sana katika moshi wa sigara. Kwa kweli, lami ya sigara imeondolewa kabisa katika namna fulani za sigara, jambo linalokaziwa mara nyingi na matangazo ya kibiashara ya sigara. Sigara zenye lami kidogo na sumu kidogo nyakati nyingine zimesifiwa kuwa “salama.” Kichwa kikuu katika ukurasa wa mbele katika gazeti Atlanta Constitution kilitangaza hivi: “Pakiti moja ya Sigara Fulani kwa Siku Yaweza Kuwa ya salama.”

Walakini mambo ya hakika ni nini? Jambo moja ni kwamba sigara zenye lami kidogo zimeongezwa vitu vya kuzikoleza. “Kama kusingekuwako vikolezaji vyo vyote katika sigara hizo zenye lami kidogo na sumu kidogo, hungeonja cho chote,” ndivyo alivyoeleza Peter Micciche, daktari mkuu wa madawa ya tumbako. Vikolezaji hivyo ni nini? Ni ‘siri za kibiashara’ zinazojulikana tu na makampuni ya tumbako na wenye kuwaletea vikolezaji hivyo. Hata hivyo vikolezaji hivyo vya madawa vyaweza kuwa hatari kwa afya pia, kama ambavyo mchanganuzi mmoja alivyosema: “Hujui kama kwamba baadhi ya vitu hivyo ni vibaya zaidi ya lami.”

Vilevile, ushuhuda unafunua kwamba, wakati wavutaji wa sigara wanapovuta sigara zenye lami kidogo na sumu kidogo, wanavuta sigara zaidi na kukalisha moshi huo muda mrefu zaidi mapafuni. Wanafanya hivyo ili kutosheleza tamaa yao ya sumu ya sigara, ambayo ni dawa ya kulevya ambayo yaweza kulevya zaidi ya bhangi ya heroin. Basi, kwa sababu ya mazoea hayo yaliyobadilishwa ya uvutaji wa sigara, wavutaji sigara wanaweza kupata kutoka kwa sigara zenye lami kidogo na sumu kidogo karibu kadiri ile ile ya vitu hivyo vyenye kudhuru kama vile katika sigara nyinginezo.

Zaidi ya hayo, sehemu hatari zaidi ya moshi wa sigara yaweza kuwa hewa ya carbon monoxide wala si lami ya sigara au sumu ya sigara. Na sigara fulani zenye lami kidogo na sumu kidogo zinatokeza moshi wenye carbon monoxide zaidi ya namna zile za kawaida!

Wachunguzi wawili wa Denmark, Profesa Poul Astrup na Dakt. Knud Kjeldsen, walichapisha mambo waliyogundua kuhusiana na matokeo ya carbon monoxide katika moshi wa sigara. Juu ya msingi wa ushuhuda mwingi wa majaribio, walikata kauli kwamba “carbon monoxide, wala si nicotine, ndiyo sehemu yenye sumu ya maana sana katika ongezeko la hatari kwa wavutaji sigara la kuzibika kwa mishipa ya damu na maradhi ya moyo.” Na yapaswa kuangaliwa kwamba vifo vingi vinavyotokezwa na uvutaji wa sigara huwa ni kwa sababu ya mishipa ya damu na maradhi ya moyo, wala si donda baya.

Akili yapaswa kuonyesha kwamba kuvuta ndani moshi wa sigara kunaharibu njia inayopitia hewa inayopumuliwa. Nao ushuhuda unathibitisha kwamba ndivyo ilivyo. Nywele ziitwazo cilia katika umio za hewa zinaharibiwa zisiweze kupunga huku na huku ili kufagia viini na uchafu. Vilevile, moshi unapunguza uwezo wa mapafu wa kujiondolea uchafu uliopumuliwa ndani. Hiyo inamaanisha kwamba wavutaji sigara wanahatirishwa zaidi na maradhi yanayotokana na vitu vinavyochukuliwa na hewa.

Kweli kweli, ni udanganyifu kudokeza kwamba sigara yo yote ni “salama.’’ Kama ambavyo afisa mkuu wa afya katika United States, Dakt. Julius Richmond alivyosema: “Hakuna hesabu zo zote po pote katika ushuhuda mwingi wa kisayansi juu ya hatari za uvutaji wa sigara zinazotoa tumaini lo lote kwamba kuna kitua kama sigara salama au kiasi salama cha kuvuta sigara.” Dakt. Richmond alimalizia hivi: “Sigara salama tu ni ile isiyowashwa.”

Lakini hata ikiwa wewe si mvutaji wa sigara, je! uko salama kutokana na madhara yanayoletwa na moshi wa watu wengine?

[Picha katika ukurasa wa 4]

WANADAMU WENYEWE WAMETUMIWA KAMA WANYAMA WA KUFANYIA MAJARIBIO KUTHIBITISHA KWAMBA KUVUTA SIGARA NI HATARI

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki