Namna ya Kuacha Kuvuta Sigara
KWANZA kabisa, lazima mvutaji sigara atake kuacha kikweli. Anahitaji kichocheo chenye nguvu. Jacquelyn Rogers, mwanzilishi wa Smokenders, tengenezo la kusaidia wavutaji sigara waache, anasema kwamba anachochea watu. “Tunawafanya watu waamini wanaweza kuacha,” ndivyo anavyosema. Wavutaji sigara wengi wanashindwa kuacha kwa sababu ya kutia shaka—wanatilia shaka uwezo wao wa kufaulu.
Je! mipango mbalimbali ya kuzuia uvutaji wa sigara na mchanganyo wa madawa unaweza kusaidia kuacha? Kwa wazi mambo hayo yamesaidia wengine. “Singeweza kuacha pasipo msaada,” ndivyo alivyosema mvutaji sigara kwa wingi. Walakini ni kama Dakt. Niel Solomon, aliyetunga mvutaji sigara huyo sindano vitamini, madawa na dawa ya novocaine, alivyokubali kuhusiana na utibabu huo: “Hakuna mwujiza wo wote kuhusiana na jambo hilo. Iwapo hutaki kuacha, haiwezi kufaulu.”
NIA YA KUTAKA KUACHA
Ndiyo, kufaulu kunategemea kwa sehemu kubwa nia na azimio la mvutaji sigara kutaka kuacha. Pasipo kuazimia huko, hakuna suluhisho lo lote la kuzuia uvutaji sigara litakalofaulu. Walakini akiwa nayo, mtu anaweza kuacha pasipo kulipia suluhisho lo lote la kuzuia uvutaji sigara. Asilimia 29 ya waliokuwa wavutaji sigara hapo kwanza waliacha pasipo misaada yo yote ya namna hiyo. Ni kama ilivyosemwa katika gazeti World Health: “Jambo kubwa katika kufaulu au kushindwa sikuzote litakuwa ni nia ya mvutaji sigara. Sehemu iliyobaki ni kufanya rekebisho.” Lakini mtu anaweza kupataje nia ya kutaka kuacha?
Kwa wengi, kujikumbusha wakati wote kwamba kuvuta sigara kunaua kumewapa nia hiyo. Ni kama daktari wa Miami kusini anayekubali alipenda kuvuta sigara, alivyosema: “Sababu pekee inayonifanya nisivute sigara ni woga.” Mipango mingine * inayofanywa ya kuzuia kuvuta sigara inasitawisha woga huo, ikikazia umizo baya sana linaloletwa mwilini na uvutaji sigara. Tabibu wa magonjwa ya akili David M. Fineman alieleza namna kuona mambo yasiyofaa kulivyomsaidia, pamoja na wengine, aache: “Nilikuwa nikivuta moshi wa sigara na kupiga akilini umizo la mara moja ambalo mwili wangu ulikuwa unapata. Kwa akili nilijaribu kuwaza juu ya hayo.
Hata hivyo, njia hiyo haitoi kichocheo cha kutosha kwa wengine kuacha. Kama vile mke anayefanya kazi nyumbani alivyoeleza: “Kama ningemwendea daktari naye aniambie kwamba ningekufa kwa ajili ya donda baya nisipoacha kuvuta sigara singeacha. Kuvuta sigara ndilo lililokuwa jambo kuu maishani mwangu, jambo la maana kwangu kuliko chakula. Nilivuta sigara wakati wote. Hata nilikuwa nikitembea hapa na hapa nyumbani nikiwa na kile kisahani cha kuwekea majivu ya sigara mkononi mwangu.” Ni kichocheo gani chenye nguvu zaidi kinachoweza kusaidia wavutaji sigara wazoelevu sana waache?
Mwanamke huyo mwenye kufanya kazi nyumbani wa New York alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo kujifunza kwamba kuvuta sigara kulikatazwa na sheria ya Mungu hakukumpa nia ya kutosha aache. “Nilitaka kuacha,” ndivyo alivyosema, “walakini nilikuwa mzoelevu sana. Sikuwa na nguvu za kufanya hivyo.”
Alieleza jambo ambalo mwishowe lilimfanya aazimie kuacha. “Mume wangu alikubali kweli za Biblia alizokuwa akijifunza, akaacha kuvuta sigara naye akabatizwa. Nilishukuru sana! Sikutaka kufanya jambo lo lote lituzuie tusimtumikie Yehova Mungu kwa njia yenye kukubalika na kupata uzima wa milele katika taratibu yake mpya ya mambo, kwa hiyo nikaazimia kuacha pia.” Naye aliacha!
MISAADA YA KUACHA
Kuna misaada ya kutegemeza nia yako ya kuacha. Msaada wa maana zaidi ni ule anaotoa Mungu. Mwanamke huyo mwenye kufanya kazi nyumbani wa New York aliyetangulia kutajwa alieleza hivi: “Nilitoa sala kwa Yehova bila kukoma na kwa msaada wake nikashikilia azimio langu la kutovuta sigara tena.” Hata hivyo wengine hutoa sala lakini wasiweze kuacha. Tatizo ni nini?
Laweza kuwa ni wakati sala zao zinapotolewa. Mvutaji sigara mmoja alisali asubuhi na usiku ili apate nguvu, na, baada ya kudhoofika na kuvuta sigara, akawa akitoa sala kwa Yehova ili kumwambia anasikitika kwa ajili ya aliyofanya. Rafiki mmoja wa Kikristo alimwuliza hivi: “Je! wakati unaomhitaji Mungu zaidi si ni ule unaponyosha mkono uchukue sigara? ” Wakati mwanamume huyo alipoanza kutoa sala wakati kama huo, alipata msaada wa kuacha kuvuta sigara!
Rafiki wenye kutegemeza, sana sana wale ambao wameshinda zoea la kuvuta sigara na hivyo ambao wanaweza kuthibitisha kwamba jambo hilo linawezekana, ni misaada bora sana. Wajulishe juu ya uamuzi wako wa kuacha kuvuta sigara, na uwaulize wakutegemeze.
Njia bora ya kuacha ni nini? Je! ni kwa kupunguza hesabu ya sigara unazovuta kila siku, hivyo kuacha polepole? Au je! ni kwa kuweka siku fulani na kuacha ghafula siku hiyo?
Tofauti na ambavyo Wengi wanafikiri, uchunguzi wa kindani wa waliokuwa wa-vutaji wa sigara ulionyesha kwamba, kwa kuacha ghafula wavutaji sigara wanaweza kushinda dalili zinazofuatana na kuacha kuvuta sigara. Wachunguzi Saul M. Shiffman na Murray E. Jarvik wa Chuo Kikuu cha California huko Los Angeles wanaeleza kwamba kupunguza polepole kwaweza “kuendeleza muda mrefu maumivu [ya wavutaji sigara] kwa kuongeza nguvu pindi kwa pindi dalili na tabia yao ya kuvuta sigara. Kwa kweli, hali hiyo yenye kuendelea ya kuacha itarudisha hali hiyo mbaya na kurudia kadiri ile ile ya uvutaji wa sigara.”
Siku chache za kwanza baada ya kuacha zaweza kuwa ngumu zaidi. Kwa hiyo, ili kukusaidia, fikiri juu ya faida za kutovuta sigara. Mojayapo ni fedha zinazookolewa. Zaweza kuwa nyingi sana! “Sasa nimekuwa nikiweka kila siku shilingi 15 ndani ya kobo la kahawa—fedha ambazo hapo kwanza nilikuwa nikitumia kununua sigara,” ndivyo alivyoandika mwanamume mmoja. “Nadhani katika miezi 12 inayokuja zitakuwa zaidi ya shilingi 5,520, ambazo zatosha kumununulia mke wangu koti la manyoya au kitu kingine.”
Kwa nia yenye nguvu, wavutaji sigara wengi wameacha kwa juma moja au karibu na hapo, wakivumilia maumivu ya kwanza ya kuacha. Walakini, kama ambavyo gazeti World Health linavyosema, “sehemu ngumu inaanza, sikuzote ikianza kati ya juma la kwanza na la tatu. Ndipo kurudia hali ya kwanza kunapoanza.” Kwa hiyo vita hiyo inapaswa kuendelea!
Wakati wo wote unapohitaji sigara vuta pumzi nyingi ndani mara mbili au tatu. Uwe na vitu vingine vya kutafuna karibu. Tafuna vitu kama zabibu, njugu na mbegu za alizeti, ama tafuna karati ama chew gum (switi-gamu). Kunywa maji zaidi—vinywaji vya afya kama vile maji ya matunda au ya mboga au maji ya kawaida tu. Vilevile, kula chakula kilichosawazika cha afya.
Kujizoeza zaidi kwaweza kuwa msaada kweli kweli. Pengine jaribu kukimbia-kimbia, kuendesha baisikeli au kuogelea. Jipe mazoezi mengi. Pumzika vya kutosha. Lala mapema ili akili isichoke. Kaza fikira juu ya namna ya kujistarehesha. Iwapo unataka kweli kweli, unaweza kuacha kuvuta sigara!
SABABU GANI KUACHA KUNASTAHILISHA JITIHADA HIYO
Faida za kuacha ni nyingi. Zinatia ndani afya na taraja la maisha marefu zaidi, walakini zipo nyingi. Aliyekuwa mvutaji sigara wakati mmoja alisema hivi: “Nimegundua kwa mara nyingine raha zote za kawaida na zisizotaka mambo mengi zilizopo, za kuonja, kwa mfano. Kutembea msituni, kwanijulisha harufu zote hazinukii namna ile ile—kuna namna mbali-mbali; ni kama kuingia katika mazingira mapya kabisa.”
Hata hivyo, faida kubwa zaidi ni kujua kwamba kwa kuacha unajiondolea zoea lisilompendeza Mungu, na jirani wengi wako pia. Iwapo unataka msaada wa kuacha kuvuta sigara kwa sababu unataka kibali ya Yehova Mungu, waandikie wachapaji wa Mnara wa Mlinzi. Watafurahi kukutumia nyumbani mwako mhudumu anayestahili ambaye atafurahi kukupa habari zaidi ya Kimaandiko na kukupa tegemezo la kiadili ili kukusaidia uache.