Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 7/15 kur. 5-10
  • Jifanyie Jina Zuri Pamoja na Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jifanyie Jina Zuri Pamoja na Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WENYE KUOMBOLEZA WAFAIDIKA
  • USEMI WENYE KUSHANGAZA HATA ZAIDI
  • JAMBO JIPYA
  • Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Kwa Nini Ni Lazima Tujue Jina la Mungu
    Jina la Mungu Litakaloendelea Milele
  • Sehemu ya 1: Mafundisho ya Kikristo
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Jina la Mungu na Lako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 7/15 kur. 5-10

Jifanyie Jina Zuri Pamoja na Mungu

“Jina zuri ni jema kuliko marashi ya damani; na siku ya kufa ni njema kuliko siku ya kuzaliwa kwa mutu.”​—Muh. 7:1, Zaire Swahili Bible.

1. Kila mtu anajifanyia nini, na nyakati nyingine kuwapa wengine?

KILA mtu anafanya jambo zaidi ya lile analofanya, hata mtu asiyefanya lo lote. Mtu hufanyiza vyombo vizuri vya mbao, na zaidi ya hilo, anajifanyia jina la kuwa fundi stadi. Mwanamke anafanyiza chakula kitamu, na kujifanyia jina la kuwa mpishi mzuri. Mtu wa tatu hafanyi lo lote, naye anajifanyia jina la kuwa mvivu. Kila mtu anajifanyia jina. Na nyakati nyingine tunawapa wengine majina. Sauli na washiriki wake walimpa Daudi jina baya kwa kumkashifu. Daudi kwa zaburi zake alimpa Mungu jina zuri. Yehova alimwezesha Daudi ajifanyie jina zuri. Wengine wanaodai kumwakilisha Mungu wanampa jina baya kwa uongo wao wa kidini na matendo yao ya uasherati. Waabudu wa kweli wanampa Mungu jina zuri kwa maneno na matendo yao, na kwa kufanya hivyo wanajifanyia jina zuri pamoja na Yehova Mungu.​—Zab. 64:1-6; 1 Nya 17:8; Eze. 36:20-23.

2. Ni usemi gani unaoelekea kuwa wa kushangaza ulioandikwa katika Mhubiri, nalo ni shauri gani linaloufuata?

2 Kuna mstari fulani katika kitabu cha Biblia cha Mhubiri ambao unaonekana kuwa usemi wa kushangaza kwa wasomaji wengine: “Jina zuri ni jema kuliko marashi ya damani; na siku ya kufa ni njema kuliko siku ya kuzaliwa kwa mutu.” Hiyo yaweza kuwaje? Kifo chawezaje kuwa kizuri kuliko uzima? Ikiwa ungekuwa na nafasi ya kuchagua, je! hungependelea kuwa ukianza maisha yako kuliko kuwa ukifikia mwisho wake? Acheni tuusome tena mstari huu, pamoja na mistari inayoufuata:

“Jina zuri ni jema kuliko marashi ya damani; na siku ya kufa ni njema kuliko siku ya kuzaliwa kwa mutu. Ni heri kwenda kwa nyumba ya maombolezo kuliko kwenda kwa nyumba ya karamu: maana huu ni mwisho wa watu wote; naye aliye hai atautia moyoni mwake. Huzuni ni nzuri kuliko kucheka: maana kwa huzuni ya uso moyo unafurahishwa. Moyo wa wenye hekima umo nyumbani mwa maombolezo; lakini moyo wa wapumbafu umo nyumbani mwa furaha. Ni vizuri kusikia laumu ya wenye hekima, kuliko mutu kusikia wimbo wa wapumbafu. Maana kama kilio cha miiba chini ya chungu, ndivyo [na] kucheka kwa mupumbafu; hili vilevile ni la bule.”​—Mhu. 7:1-6, Zaire Swahili Bible.

3. (a) Ni desturi gani ya Israeli wa kale inayozungumzwa hapa, nalo ni wazo gani la wakati huo linalofariji zaidi? (b) Twajuaje kwamba jina linalotajwa hapa ni jina zuri?

3 Je! hiyo inaufanya ufahamike zaidi ule usemi wenye kushangaza wa kwamba siku ya kufa kwako ni njema kuliko siku ya kuzaliwa kwako? Inafanya hivyo ukijua wakati na kikao cha maneno hayo. Yanahusu desturi katika Israeli wa kale. Wakati nyumba fulani ilipompoteza mpendwa wao katika kifo, makao yao yalikuwa nyumba ya maombolezo. Ilikuwa desturi ya rafiki na jirani kuja na kutoa rambi-rambi. Wazo lenye kufariji zaidi lilikuwa kwamba siku ya kufa kwa mpendwa huyo ingekuwa bora kuliko siku ya kuzaliwa kwake—ikiwa alikuwa amejifanyia jina zuri pamoja na Mungu. Ni kweli kwamba katika Kiebrania cha asili, mstari wa kwanza wa fungu hili la maneno unasema “jina” tu badala ya “jina zuri.”a Hata hivyo, inafahamika kwamba jina hilo ni jina zuri. Hali moja na hiyo ni Mithali 22:1: “[Ni] heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi.” Tafsiri fulani huongeza neno “jema” kuonyesha ni jina la namna gani linalomaanishwa.b Kwa lazima jina hilo ni jina zuri, katika mahali kote kuwili, katika Mithali na katika Mhubiri 7:1; kama sivyo, hakuna usemi wo wote kati ya semi hizo mbili ambao ungekuwa na maana yo yote.

4. Ni nini tunachoweza kuwa nacho wakati wa kufa, ambacho hatukuwa nacho wakati wa kuzaliwa, na sababu gani?

4 Tuendeleapo kuishi, twajifanyia majina—majina mema au mabaya. Tukitenda kwa hekima machoni pa Mungu, twajifanyia jina jema pamoja na Mungu. Lakini jambo hilo lachukua wakati. Wakati wa siku ya kuzaliwa kwetu, hatujaishi wakati wa kutosha kujifanyia jina la namna yo yote. Zaidi ya hayo, sisi tunazaliwa tukiwa chini ya dhambi ya Adamu na tukiwa tumehukumiwa kifo. (Rom. 5:12) Kwa hiyo, ikiwa miaka mingi baadaye, wakati wa siku yetu ya kufa, tumejifanyia jina zuri pamoja na Mungu, tunacho kitu ambacho hatukuwa nacho wakati wa siku yetu ya kuzaliwa. Tuna jina ambalo Mungu atakumbuka wakati wa kufufua wafu chini ya ufalme wa Kristo. “Kuwakumbuka wenye haki huwa na baraka; bali jina la mtu mwovu litaoza.”​—Mit. 10:7.

WENYE KUOMBOLEZA WAFAIDIKA

5. Mwombolezaji aweza kutafakari (kufikiria) juu ya nini anapoketi katika nyumba ya maombolezo?

5 Lakini wakati Mwisraeli alipokwenda kwenye nyumba ya maombolezo ili kuwafariji waliofiwa, yeye pia alifaidika. Fikiria hilo tunaposoma tena baadhi ya ile mistari. “Ni heri kwenda kwa nyumba ya maombolezo kuliko kwenda kwa nyumba ya karamu: maana huu ni mwisho wa watu wote; naye aliye hai atautia moyoni mwake.” (Mhu. 7:2, ZSB) Si kwamba tu anaonyesha huruma zenye fadhili waliofiwa ambao wangali wanaishi, badala ya kufuatia anasa yake mwenyewe bila kujali, bali vilevile anafikiria uhakika wa kwamba katika nyumba hiyo mtu fulani amekufa, kwamba hilo si jambo lisilo la kawaida, kwamba kifo kinakuja kwa wote, na kwamba kitamjia yeye pia. Kijapo, je! siku hiyo ya kufa kwake itakuwa bora kuliko siku ya kuzaliwa kwake? je! atakuwa ametenda kwa hekima maishani mwake, ili kwamba kufikia siku ya kufa kwake atakuwa amekwisha jifanyia jina zuri pamoja na Mungu? Lazima walio hai waweke jambo hilo moyoni, wakati wangali na wakati wa kufanya badiliko, kwa kuwa jina zuri haliwezi kufanywa kwa dakika chache za mwisho kabla ya kufa.

6. Sababu gani, kuhusiana na jambo hili, huzuni ni bora kuliko kicheko?

6 “Huzuni ni nzuri kuliko kucheka,” yaendelea masimulizi hayo, “maana kwa huzuni ya uso moyo unafurahishwa,’ (Mhu. 7:3, ZSB) Badala ya kupoteza wakati kwa anasa ya kiwazimu, ni jambo bora zaidi kuchunguza maisha yako, uyafikirie makosa uliyofanya wakati uliopita uhuzunishwe na mabaya uliyotenda. Kufanya hivyo kutasitawisha hali ya moyo wako na kukusukuma ubadilishe njia zako na kuanza kutenda kwa hekima, badala ya kucheka-cheka muda wote wa maisha yako kama mpumbavu asiyejua kitu. “Moyo wa wenye hekima umo nyumbani mwa maombolezo; lakini moyo wa wapumbafu umo nyumbani mwa furaha.”​—Mhu. 7:4, ZSB.

7. (a) Jambo hilo laweza kumweka mwombolezaji katika hali gani ya akili? (b) Sababu gani kicheko cha wapumbavu kinafananishwa na kelele ya miiba chini ya chungu?

7 Zaidi ya hayo, “ni vizuri kusikia laumu la wenye hekima, kuliko mutu kusikia wimbo wa wapumbafu.” (Mhu. 7:5, ZSB) Kukutana na kifo, kama vile kwenye mazishi, ni jambo lenye kumfanya mtu afikiri nalo lapaswa limfanye mtu afikirie mwendo wake mwenyewe wa maisha. Vilevile laweza kumweka katika hali ya akili ya kusikiliza washauri wenye hekima. Lawama, hata inapotolewa kwa fadhili, ni vigumu kulivumilia, walakini ni bora kuliko kusikiliza wimbo au “sifa ya wapumbavu.” (The New English Bible) Kusikia na kuyatii makemeo yenye hekima yanayopatikana katika kurasa za Biblia kutatusaidia kujifanyia jina zuri pamoja na Mungu. Kupoteza wakati wetu tukisikiliza wapumbavu ni ubatili: “Maana kama kilio cha miiba chini ya chungu, ndivyo [na] kucheka kwa mupumbafu: hili vilevile ni bule.” (Mhu. 7:6, ZSB) Kutumia miiba kama kuni chini ya chungu hakutimizi lo lote. Miali yake inaruka-ruka na kufanya kelele, walakini upesi inamalizika huku miiba ikigeuka na kuwa majivu. Miiba haina nguvu za kutosha kuufanya moto uendelee mpaka nyama iishe kupikwa. Kelele hiyo yenye kujionyesha ni ya bure kama vile kicheko cha mpumbavu. Hakuna lo lote kati ya mambo hayo linalotimiza jambo lenye maana ya kudumu.

USEMI WENYE KUSHANGAZA HATA ZAIDI

8. Kwa kuwa na ufahamu mkubwa zaidi, sasa tunaona somo gani?

8 Kwa hiyo, tukiwa na ufahamu huo wingi zaidi, twaurudia ule usemi wa kwamba ‘siku ya kufa ni bora kuliko siku ya kuzaliwa.’ Twaona kwamba si wenye kushangaza tena bali ni somo lenye nguvu juu ya namna inavyotupasa kuishi maisha yetu ili tujifanyie jina zuri pamoja na Mungu. Ndipo siku ya kufa kwetu itakapokuwa bora kuliko siku ya kuzaliwa kwetu. Yaani, ikiwa siku ya kufa kwetu inatokea wakati wo wote. ‘Nini hilo?’ wengine wapaza sauti. ‘Ala! ikiwa siku ya kufa kwetu inatokea wakati wo wote? Wamaanisha huenda isije? Aa! huo ni usemi wenye kushangaza zaidi kuliko ule wa kwamba kifo ni bora kuliko kuzaliwa!’

9. Macho yako yanaona hali gani, nayo yanapaswa kuona nini kweli kweli?

9 Kwa mara nyingine, inahusu kufahamu wakati ambao katika huo tunaishi. Je! wewe una macho yenye kuona, kuona kweli kweli? Bila shaka wewe unaona kwamba nyakati ni za hatari na zenye magumu, kwamba watu wengi ni wenye kujifikiria wenyewe tu na wenye majivuno, kwamba ndoa zinavunjika na jamaa kuharibika, kwamba kupunja na kusema uongo na uvunjaji wa sheria wenye jeuri uko kila mahali, na kwamba hata wengi miongoni mwa wale wanaodai kuwa Wakristo wanajionyesha kuwa wanafiki. Walakini je! macho yako yanaona yanayomaanishwa na mambo hayo? Timotheo wa Pili 3:1-5, 13 hutuambia yanavyomaanisha:

“Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao. Lakini watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika.”

10. Masikio yako yanasikia nini, nayo yanapaswa kufahamu jambo gani zaidi?

10 Je! wewe unayo masikio yanayosikia, yanayosikia kweli kweli? Bila shaka umekwisha kusikia habari za vita, njaa, matetemeko ya ardhi pamoja na magonjwa ya kipuku, mambo ambayo yametaabisha ulimwengu tangu mwaka 1914. Unajua kuvunjika-vunjika kwa adili kunakotaabisha ulimwengu wote. Nawe umesikia habari njema za ufalme wa Kristo zinazohubiriwa na Mashahidi wa Yehova, pamoja na mateso yaliyowapata kwa sababu ya kutangaza kwamba ufalme huu wa miaka elfu umekaribia. Walakini, je! masikio yako yanasikia yanayomaanishwa na mambo haya? Yanafahamu ukweli wa kwamba mambo hayo yalitabiriwa na Yesu yakiwa ishara ya mwisho, alipoulizwa na wanafunzi, wake, “Twambie, Mambo hayo yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya mwisho wa taratibu ya mambo?”​—Mt. 24:3, NW.

11. Wadhihaki wanasema nini, na kwa kufanya hivyo wanatoa nini?

11 Je! moyo wako unaona yanayomaanishwa na hayo yote, au umefanywa kuwa mgumu na ushupavu unaokufanya useme “Mambo hayo yote yamepata kutokea hapo mbeleni”? Wale wanaodhidaki wanatokeza sahemu nyingine ya ile ishara kuonyesha kwamba twaishi wakati wa “siku za mwisho.” Kuwapo kwao kulitabiriwa katika 2 Petro 3:3, 4, NW: “Katika siku za mwisho watakuja wadhihaki pamoja na dhihaka yao, wakiendelea kulingana na tamaa zao wenyewe na kusema: ‘Ku wapi huku kuwapo kwake kulikoahidiwa? Kwani, tangu ile siku mababu zetu walipolala usingizi wa mauti, mambo yote yaendelea sawasawa kama yalivyokuwa tangu mwanzo wa kuumba.’”

JAMBO JIPYA

12. Ni jambo gani ambalo ni jipya sasa katika historia ya ulimwengu?

12 Walakini, bila shaka moyo wako unaona uhakika wa kwamba unapofikiria kuchafuliwa duniani pote kwa sayari yetu wafahamu kwamba ‘mambo yote HAYAENDELEI sawasawa kama yalivyokuwa tangu mwanzo wa kuumba.’ Wanadamu hawajakuwa hapo mbeleni na uwezo wa kuharibu dunia isiwe sayari ya kukaliwa. Wanao uwezo huo sasa nao wanautumia kufanya jambo ilo hilo! Wanasayansi wamewapa wanaviwanda ufundi uliotazamiwa kuwa baraka kwa wanadamu wote, walakini baraka hiyo imegeuka ikawa laana, kadiri inavyoyachafua mazingira, nayo magonjwa ya kufisha yanaenea kote duniani. Hewa tunayovuta inachafuliwa, udongo unaokuza chakula chetu unatiwa sumu, mito mingi na maziwa yanayotupa maji ya kunywa yanakufa, nazo bahari zinakuwa jaa (mahali pa kutupia takataka) za mataifa yote!

13. Ni sehemu gani ya ile ishara ambayo juu yake wadhihaki hawawezi kusema, “Imekwisha tokea hapo mbeleni”?

13 Je! moyo wako unafahamu kwamba uwezo wa dunia wa kuendeleza uhai umo hatarini, kwamba jambo hilo halijapata kutokea hapo mbeleni, na ya kwamba wadhihaki hawawezi kupuza jambo hilo na kusema kwamba ni jambo lililotokea hapo mbeleni linalotokea tena? Wanaweza kutaka kufanya hivyo, kwa kuwa kuharibiwa huku kwa dunia kulitabiriwa pia kama sehemu ya ile ishara ya “siku za mwisho.” Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kilifunua jambo hilo karibu karne 19 zilizopita, katika sura ya 11, mstari wa 18: “Mataifa walikasirika, hasira yako nayo ikaja, na wakati ukaja wa kuhukumiwa waliokufa, na wa kuwapa thawabu . . . hao walichao jina lako, na wa kuwaharibu hao waiharibuo nchi.”

14. Ni kwa sababu gani umati mkubwa wa watu katika siku za Yesu, na sasa umati mkubwa wa watu katika siku zetu, wanashindwa kutii lile onyo?

14 Ikiwa macho yako yanaona kweli kweli, nayo masikio yako yanaona kweli kweli, nao moyo wako haukufanywa kuwa mgumu, utafahamu kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” na kwamba mwisho wa hii taratibu mbovu ya mambo unakaribia. Walakini umati mkubwa wa wanadamu haufahamu jambo hili, sawasawa na vile umati mkubwa katika siku za Yesu haukufahamu ujumbe wake wa onyo. Yale aliyowaambia, akitumia maneno ya unabii wa Isaya, yanahusu wanadamu leo:

“Kwa kuwa wakitazama hawaoni, na wakisikia hawasikii, wala kuelewa. Na neno la nabii Isaya linatimia kwao, likisema, Kusikia mtasikia, wala hamtaelewa; kutazama mtatazama, wala hamtaona. Maana mioyo ya watu hawa imekuwa mizito, na kwa masikio yao hawasikii vema, na macho yao wameyafumba; wasije wakaona kwa macho yao, wakasikia kwa masikio yao, wakaongoka, nikawaponya.”​—Mt. 13:13-15.

15. Ni nani wanaoweza kufurahi sasa, na wakiwa na tumaini gani?

15 Katika mstari unaofuata, Yesu anaongeza maneno haya kwa ajili ya wafuasi wake: “Lakini, heri macho yenu, kwa kuwa yanaona; na masikio yenu, kwa kuwa yanasikia.” Wale leo walio na macho na masikio na mioyo inayofahamu na kuona na kusikia kwamba sisi tunaishi katika “siku za mwisho” waweza kuwa wenye furaha kweli kweIi. “Mambo hayo yaanzapo kutokea,” wanaambiwa, “changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.” (Luka 21:28) Wengine kati ya wale wanaoishi katika “siku za mwisho” huenda wasikutane kamwe na siku ya kufa kwao. Yesu alilinganisha wakati huu na siku za Noa. Kama vile Noa na jamaa yake walivyohifadhiwa hai wakaipita gharika iliyoharibu ulimwengu huo mwovu, ndivyo na leo wale wanaotenda kwa hekima na kujifanyia jina zuri pamoja na mungu hawataona kifo wakati Yehova Mungu aiharibupo hii taratibu mbovu ya mambo katika vita yake ya Har–Magedoni. Kwa hiyo si kusema lisilowezekana kusema kwamba huenda wengine wasiione kamwe siku ya kufa kwao. Badala yake, ni kuonyesha tumaini litokalo kwa Mungu.

16, 17. Watu hukataa kuelekeana na jambo gani, nalo ni jambo gani lililo la maana sana sasa kwetu sisi?

16 Katika Israeli wa kale, mtu angeweza kutoa sababu kwamba yeye alikuwa na muda wote unaobaki wa maisha yake wa kujifanyia jina zuri pamoja na Mungu. Mtu huficha uhakika wa kwamba anaweza kufa kesho. Wengine wachanga zaidi yake watakufa, lakini sivyo yeye. Sikuzote yeye anaona miaka michache inayobaki ya yeye kuishi. Kuwaza kwa namna hiyo ni kosa wanalofanya wanadamu, kosa lenye hatari. Ingekuwa hivyo hata kwa mtu katika Israeli wa kale, walakini ni kosa lenye hatari hata zaidi kwetu sisi leo. Sisi hatuishi katika nyakati za kawaida, wakati tungetazamia kuishi muda wa kawaida wa maisha wa miaka 70 au 80. Sisi tumo katika “siku za mwisho.” Kifo cha taratibu ya mambo kinakaribia. Ni jambo la maana sana kwetu kutii maneno haya ya Waefeso 5:15-17: “Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima, bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana [nyakati] hizi ni za uovu. Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya [Yehova].”

17 Sasa ndio wakati wa kujifanyia jina zuri pamoja na Mungu, wakati ungali hai, kabla haijaja siku ya kufa kwako.

[Maelezo ya Chini]

a Angalia tafsiri ya New World.

b Authorized Version, American Standard Version, The New English Bible, n.k.; angalia pia tafsiri ya New World, maneno ya chini.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Siku ya kufa ni bora kuliko siku ya kuzaliwa—hiyo yaweza kuwaje?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Siku ya kufa yawezaje kuwa bora kuliko hii?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki