Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 7/15 kur. 10-15
  • Jifanyie Jina Lako Zuri Sasa!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jifanyie Jina Lako Zuri Sasa!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UHITAJI WA UONGOZI
  • NAMNA YA WATU TUNAOPASWA KUWA
  • SASA NDIO WAKATI WAKO!
  • Dini
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Maoni Yanayofaa Ni Ulinzi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Kufanya Kazi ya Yehova Katika Njia ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Sehemu ya 1: Mafundisho ya Kikristo
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 7/15 kur. 10-15

Jifanyie Jina Lako Zuri Sasa!

“Kitu cho chote mukono wako unachopata kufanya, ukifanye kwa nguvu zako zote; maana hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima ndani ya kaburi, pahali unapokwenda.”​—Mhu. 9:10, Zaire Swahili Bible.

1. Ni wakati gani ambapo lazima tujifanyie jina zuri pamoja na Mungu?

NAMNA gani wengine wakisema, ‘Lakini namna gani mwisho usipokuja wakati wa maisha yangu? Wakati wa karne zote zilizopita watu walikuwa wakifikiri kwamba mwisho ungekuja wakati wa maisha yao nao haukuja’? Bila kujali uhakika wa kwamba mataraja yao hayakutimizwa, wakati wa maisha ya wengi wao ulikuwa bado ndio wakati wa kujifanyia jina zuri pamoja na Mungu, kwa kumwamini Mwana wa Mungu, ili wapate kufufuliwa kwenye uzima wa milele katika “siku ya mwisho.” (Yohana 6:40; 11:24) Wakati mrefu kabla ya hizi “siku za mwisho” zilizopo, mtume Paulo aliweza kusema: “Tangu sasa na kuendelea nimewekewa taji ya haki.” Wakati wo wote anapoishi mtu, huo ndio wakati wake wa kujifanyia jina zuri, mwisho wa ulimwengu uwe karibu au mbali.​—2 Tim. 4:8, NW; Ebr. 11:4-38.

2. (a) Je! kuna kitu cho chote, kitu cha kimwili au kinginecho, tunachoweza kuchukua wakati wa kufa? (b) Kwa hiyo ni onyo gani la upole linalofaa?

2 “Alivyotoka tumboni mwa mamaye, atakwenda tupu-tupu kama alivyokuja; asichume kitu cho chote kwa ajili ya kazi yake, hata akichukue mkononi mwake.” (Mhu. 5:15) Kusema kwa habari ya mambo ya kimwili, hakuna kitu cho chote mtu anayekufa ‘anachoweza kuchukua mkononi mwake.’ Walakini, anaweza kuchukua kitu peke yake kilicho cha thamani yenye kudumu anachoweza kujifanyia katika maisha haya—jina zuri pamoja na Mungu. Wakati kila mmoja wetu anapoishi, huo ndio wakati wetu wa kujifanyia jina zuri pamoja na Mungu. Utumie vizuri wakati huo! Ukomboe! Ununue! “Kitu cho chote mukono wako unachopata kufanya, ukifanye kwa nguvu zako zote; maana hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima ndani ya kaburi, pahali unapokwenda.” Sana sana sasa, wakati wa mwisho wa hii taratibu ya mambo, wakati ambapo wengi wanaoishi huenda wasife kamwe, ndio wakati wetu wa kufanya kwa nguvu zetu zote yale ambayo mikono yetu inapata kufanya katika utendaji wa Kikristo.​—Mhu. 9:10, ZSB.

3. Ni maarifa sahihi gani yaliyo ya maana sana, nayo yaweza kutimiza jambo gani?

3 Ikiwa tutajifanyia jina zuri pamoja na Mungu lazima tufikirie mambo mawili: yaliyo mabaya na yaliyo mema. Lazima tuache kufanya yaliyo mabaya tuanze kufanya yaliyo mema. Tutafanyaje hivyo? Lazima akili ihusike. “Mwache kufanyizwa kulingana na mtindo wa taratibu hii ya mambo,” akasema Paulo, “bali mgeuzwe kwa kubadili akili zenu.” (Rum. 12:2, NW) Anarudia jambo hilo katika Waefeso 4:23, NW: “Mpate kufanywa wapya katika nguvu yenye kuendesha akili zenu.” Nayo nguvu hiyo inaonyeshwa katika Wakolosai 3:9, 10, NW: “Uvueni ule utu wa kale, pamoja na mazoea yake, mkajivike wenyewe utu mpya, ambao kupitia kwa maarifa sahihi ya kweli unafanywa upya kulingana na sura ya Yeye aliyeuumba.” Nguvu inayotendesha akili yako, inayoifanya upya akili yako na kukuongoza kwenye kibali ya Mungu ni maarifa sahihi ya Neno lake, Biblia.

4. Ni kwa sababu gani haitoshi kuacha tu kutenda mabaya, ni Jambo gani zaidi ambalo lazima lifanywe?

4 Kujikaza na kuazimia kuachana na mambo yaliyokatazwa hakuleti matokeo sikuzote. Namna gani ukifaulu kuachana nayo kwa muda? Bado hauko salama. Yesu alionyesha hilo kwa kutoa mfano. Roho mbaya alimtoka mtu mmoja, “nyumba” yake, na baadaye akarudi. Alipokuta nyumba haina mtu, akaiingia pamoja na roho wengine saba wabaya, “na mtu yule hali yake ya mwisho huwa mbaya kuliko ya kwanza.” (Mt. 12:43-45) Haikutosha kumwondoa yule roho mbaya katika ile nyumba; ilihitaji kujazwa ili roho hao wabaya wasiingie tena. Haitoshi tu kuacha kufanya mabaya na kuacha utupu—lazima tuanze kufanya yaliyo mema. Yasukumie mbali mabaya kwa kufanya yaliyo mema. “Mpingeni Shetani,” asema Yakobo, “naye atawakimbia. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:7, 8) Kutokuwa na la kufanya ni kumkaribisha Shetani; kuijaza akili kweli ni ulinzi.​—Flp. 4:8, 9.

UHITAJI WA UONGOZI

5. Ni kwa sababu gani kusoma Biblia ni jambo gumu kwa wengi, nalo tatizo hilo alimaliziwaje mtu fulani karne 19 zilizopita?

5 Leo katika ulimwengu wa dini na filosofia kuna mvurugo wa maoni yenye kupingana kuhusu yaliyo mema na yaliyo mabaya. Katika kutafuta-tafuta kwao, wengi wanajaribu kusoma Biblia lakini wanaiona kuwa ngumu kufahamu. Wao si ndio wa kwanza kuona hivyo. Karne 19 zilizopita Mwethiopia mmoja alikuwa akiendesha gari lake, huku akisoma kitabu cha Isaya. “Filipo [yule mhubiri wa injili] akaenda mbio, akamsikia anasoma chuo cha nabii Isaya; akanena, Je! yamekuelea haya unayosoma? Akasema, Nitawezaje kuelewa, mtu asiponiongoza?” Filipo alipanda garini akaenda pamoja naye akamwongoza.​—Matendo 8:26-35; 21:8.

6. Ni wapi tunapoweza kutarajia kupata ‘akina Filipo’ wa kisasa, na ni wapi tusipoweza kutazamia kuwaona?

6 Wako wapi ‘akina Filipo’ wa leo wanaostahili kuongoza wengine waamue kutokana na Biblia mwendo unaompatia mtu jina zuri pamoja na Mungu? Hawako katika dini za kawaida za Jumuiya ya Wakristo zilizoimarika na zenye kuheshimiwa, kama vile mtu fulani anavyoweza kutarajia. Filipo hakuwa mwandishi au Farisayo mwenye kuheshimiwa, bali alikuwa mmoja wa Wakristo waliodharauliwa, wakasingiziwa na kuteswa. Masomo ya kihistoria yanatufundisha kwamba taratibu za kidini zilizoimarika na kukubaliwa mara nyingi zinaanguka kwenye mtego wa kukubali filosofia za wanadamu nazo zina hatia ya kuchanganya maneno ya Mungu na filosofia hizo.

7. (a) Israeli wa kale walilichafuaje Neno la Mungu? (b) Ni kwa kadiri gani makanisa fulani ya kisasa pamoja na watu wake katika Jumuiya ya Wakristo wanaiga Israeli, katika kuhalifu maandiko?

7 Taifa la Israeli lilikuwa na sheria ya Yehova, walakini waliichafua ibada yao kwa kuiongeza ibada ya sanamu ya Baali yenye kutumia ngono, iliyokuwa ikifanyiwa vichakani na sehemu za juu. Mambo ya Nyakati cha Pili 33:17 huonyesha hivyo, kikisema: “Watu wakaendelea kutoa dhabihu katika mahali pa juu, ila wakamtolea [Yehova], Mungu wao tu.” Mchanganyiko huo wa ibada ya kweli na uongo ndio uliomfanya Eliya alaumu Israeli akisema: “Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini? [Yehova] akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! mfuateni yeye. (1 Fal. 18:21) Makanisa mengi pamoja na wanakanisa wengi leo huachilia vitabu vyenye kuonyesha picha za umalaya, sinema zenye kuonyesha ngono zisizo halali, watu wanaofanya ngono kabla ya kuoana, uzinzi pamoja na watu wa namna moja wenye kulalana—hata kufikia kadiri ya kukubali na kufanya mambo hayo anayokataza Mungu.​—Rum. 1:26, 27, 32; 1 Kor. 6:9, 10; Ufu. 21:8.

8. Liliporudi kutoka utumwa wa Babeli, taifa la Yuda lilichafua na kulitangua Neno la Mungu katika njia gani mpya?

8 Kwa sababu ya machukizo kama hayo Yuda ilikwenda uhamishoni katika Babeli. Iliporudi, ilichafua tena Neno la Mungu—wakati huu si kwa kufanya ibada ya sanamu yenye kutumia ngono, bali kwa kuongeza mapokeo na filosofia za wanadamu. Yesu aliilaumu taratibu yao ya kidini, waandishi na Mafarisayo, kwa ajili ya hayo, akitangaza hivi: “Mbona ninyi nanyi huhalifu amri ya Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu? Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, Watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami. Nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.”​—Mt. 15:3, 7-9.

9. Ni njia gani yenye nguvu ambayo katika hiyo Paulo alilinganisha wanabiashara wadanganyaji wa divai na wanadini wasioaminika?

9 Paulo alikuwa akilaumu kuchafuliwa kwa Neno la Mungu kwa filosofia za wanadamu aliposema hivi: “Tumekataa mambo ya aibu yaliyositirika, wala hatuenendi kwa hila, wala kulichanganya neno la Mungu na uongo.” Wanabiashara ya divai wa siku zake wenye kudanganya walikuwa wakiongezea divai kileo ambacho si bora au hata maji ili iongezeke na kuleta fedha zaidi. Vivyo hivyo, wanadini wengine waliliongezea neno la Mungu mapokeo na filosofia za wanadamu ili likubalike zaidi na watu wa ulimwengu. Walakini sivyo Paulo! “Sisi si kama wengi ambao huufanya ujumbe wa [neno la] Mungu kuwa kitu cha biashara;” akatangaza, “sisi tunahubiri kwa unyofu mbele ya Mungu, kama watu tuliotumwa na Mungu, tukiwa tumeungana na Kristo”​—2 Kor. 4:2; 2:17, HNWW.

10. Ni onyo gani alilotoa mtume Paulo, nalo limekuwa kweli namna gani?

10 Paulo alionya kwamba Ukristo ungeasi, na katika karne ya nne W.K. ulichafuliwa kwa njia mbaya sana na ya waziwazi kupitia kwa Konstantino, Mfalme Mrumi. (Matendo 20:29, 30) Kama matokeo kukawa na Ukristo uliochanganywa mafundisho ya mashetani yaliyoanzia Misri na Babeli—kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi, moto wa mateso, matohara, sala kwa ajili ya wafu, matumizi ya tasbihi na mengineyo. Mafundisho hayo ya kidini hayamo katika Biblia, walakini yalitiwa katika imani za yanayoitwa ati makanisa ya Kikristo. Yamo mle mpaka hivi leo. Zaidi ya hayo, makanisa ya kisasa ya Jumuiya ya Wakristo yamechafua Neno la Mungu hata zaidi: yameongeza uchambuzi unaojaribu kupunguza ukweli wa Biblia, na vilevile kisio la mageuzi lisilopatana na sayansi linalokataa kwamba Mungu ndiye Muumba mbingu na dunia na uhai!

11. Ni sifa gani tofauti pamoja na masadikisho yanayotambulisha wale walio ‘akina Filipo’ wa kisasa kuwa viongozi salama?

11 Basi, ni nani walio ‘akina Filipo’ wa kisasa walio viongozi salama. Wale wanaoamini kwamba Biblia ni Neno lililoongozwa na Mungu; wanaoliona kuwa taa ya miguu yao na mwanga wa njia yao; ambao hawaliongezei cho chote wala kutoa cho chote; wanaomwacha Mungu na Neno lake kuwa wa kweli wajapomfanya ‘kila mtu kuwa mwongo’; na wanaojitumikisha katika ‘kuhubiri habari njema hizi za ufalme katika dunia yote kuwa ushuhuda.’ (2 Tim. 3:16; Zab. 119:105; Kum. 4:2; Rum. 3:4; Mt. 24:14, NW) Wanaitumia Biblia ikiwa mamlaka yao, na kuwatia moyo wanaowasikiliza wawachunguze, bila kuamini neno lao tu, bali wakiliamini Neno la Mungu peke yake. (Matendo 17:11) Ili wewe ujifanyie jina zuri pamoja na Mungu, inakupasa uwe na lengo la kuwa kiongozi mwaminifu wa namna hiyo, ‘tayari sikuzote kujitetea mbele ya kila mtu anayetaka kwako sababu ya tumaini lililo ndani yako, lakini mkifanya hivyo pamoja na upole na heshima nyingi.’ Au, kama vile alivyosema Paulo: ‘Ujue jinsi ikupasavyo kumjibu kila mtu.’​—1 Pet. 3:15, NW; Kol. 4:6.

NAMNA YA WATU TUNAOPASWA KUWA

12. Ni jambo gani lililo la maana zaidi kwako kuliko kujifunza Neno la Mungu tu na kuwahubiri wengine?

12 Ili kujifanyia jina zuri pamoja na Mungu, haitoshi kujifunza tu na kujua majibu. Lazima tutumie maarifa hayo kwanza sisi wenyewe. Ili tufaidike kibinafsi lazima tuyatumie sisi wenyewe binafsi. Kama vile yule mtu katika Israeli wa kale katika nyumba ya maombolezo, lazima ‘tuyatie moyoni.’ (Mhu. 7:2) “Basi wewe umfundishaye mwingine, je! hujifundishi mwenyewe? Wewe uhubiriye kwamba mtu asiibe, waiba mwenyewe? Wewe usemaye kwamba mtu asizini, wazini mwenyewe?” Hata mtume Paulo alitangaza hivi: “Mimi naupiga-piga ngumi mwili wangu na kuufanya kama mtumwa, ili, nikiisha kuwahubiri wengine, mimi mwenyewe nisije nikakataliwa kwa njia fulani.” (Rum. 2:21, 22; 1 Kor. 9:27, NW) Ni jambo la maana zaidi kuliko yale tunayofanya. Swali ni, Sisi ni nini? Ni nini yule “mtu wa siri wa moyo”? “Ninyi yawapasa kuwa watu wa namna gani?”​—1 Pet. 3:4, NW; 2 Pet. 3:11, NW.

13. Yehova alirekebishaje kufikiri kwa Samweli juu ya kuamua namna watu walivyo?

13 Vile tulivyo haiamuliwi na vile tunavyoonekana nje. Nabii Samweli alitumwa kwa Yese akapake mafuta mmojawapo wa wanawe awe mfalme wa Israeli. Samweli alivutiwa na mwana mzaliwa wa kwanza mwenye maungo na mwenye nguvu, walakini Yehova akamwambia Samweli: “Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa. [Mungu] haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali [Yehova] huutazama moyo.”​—1 Sam. 16:7.

14. Ni ushuhuda gani zaidi unaotolewa kuonyesha kwamba sura za nje zaweza kudanganya, nalo jambo lililo la maana ni jambo gani?

14 Sura za nje ni zenye kudanganya. Yesu alisema kwamba waandishi na Mafarisayo walionekana kuwa wenye haki nje-nje, lakini ndani walikuwa wapotvu. (Mt. 23:3, 27, 28) Wayahudi wa siku za Paulo walifikiri kwamba ile ishara ya nje ya kutahiriwa ingewaokoa, walakini Paulo alisema hivi: “Yeye si Myahudi aliye Myahudi kwa nje tu, wala tohara siyo ile ya nje tu katika mwili; bali yeye ni Myahudi aliye Myahudi kwa ndani; na tohara ni ya moyo.” (Rum. 2:28, 29) Vilevile Paulo alionyesha mambo makuu ambayo angeweza kutimiza, kisha akaongeza, “[Lakini] kama sina upendo, hainifaidii kitu.” Lo lote tufanyalo ili tujifanyie jina zuri pamoja na Mungu lapasa liongozwe na upendo kutoka kwa moyo. “Mimi, [Yehova], nauchunguza moyo.” —1 Kor. 13:1-3; Yer. 17:10.

15. Inatupasa sisi kuwa watu wa namna gani?

15 Kwa hiyo, inatupasa sisi kuwa watu wa namna gani? Mtume Paulo anatoa orodha hii inayoonekana kuwa kubwa ya mambo yanayoamriwa kufanywa na mambo yanayokatazwa:

“Pendo na lisiwe na unafiki; lichukieni lililo ovu, mkiambatana na lililo jema. Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi; kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu; kwa bidii, si walegevu; mkiwa na juhudi katika roho zenu; mkimtumikia [Yehova]; kwa tumaini, mkifurahi; katika dhiki, mkisubiri; katika kusali, mkidumu; kwa mahitaji ya watakatifu, mkifuata ukarimu; katika kukaribisha wageni, mkijitahidi. Wabarikini wanaowaudhi; barikini, wala msilaani. Furahini pamoja na wafurahio; lieni pamoja na waliao. Mpatane nia zenu ninyi kwa ninyi. Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge. Msiwe watu wa kujivunia akili. Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote. Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena [Yehova]. Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema.”​—Rom. 12:9-19, 21.

16. Inatupasa kuepuka nini, na kutafuta nini?

16 Hiyo ndiyo namna ya watu tunayopaswa kuwa! Lingekuwa jambo lenye kuogopesha sana kama Mungu hangeturehemu mahali tunapopungukiwa kwa sababu ya udhaifu wetu. Hapa pana chanzo kikubwa cha msaada: shirikiana na watu walio na miradi kama yako. “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” “Msipotezwe. Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.” Jiepushe na milki ya ulimwengu ya dini ya uongo yenye uzinzi inayolichafua Neno la Mungu. “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake.” Dhamiri yake imechomwa hata hawezi kujiona kuwa na hatia, dhambi zake zijapofika mbinguni. Kama vile ilivyo kwa habari ya kahaba wa halisi, ndivyo ilivyo kwake: “Hivyo ndivyo mwendo wa mwanamke mzinifu; hula, akapangusa kinywa chake akasema, Sikufanya ovu.” Hivyo, ni jambo la maana kupata nguvu kwa kushirikiana na watu wanaotafuta kujifanyia jina zuri pamoja na Mungu, “tusiache kukusanyika pamoja kama ilivyo desturi ya wengine.”​—Mit. 13:20; 1 Kor. 15:33, NW; Ufu. 18:4; Mit. 30:20; Ebr. 10:25.

SASA NDIO WAKATI WAKO!

17, 18. Inatupasa kukaza fikira zetu juu ya nini sasa, na ni kwa sababu gani jambo hilo halipaswi kuahirishwa?

17 Kadiri mwisho wa taratibu mbovu ya Shetani ukaribiavyo, acheni tukaze fikira zetu juu ya ‘namna ya watu tunayopaswa kuwa,’ juu ya kufanya upya akili zetu, juu ya kuuvua kabisa ule utu wa kale na kujivika ule mpya, na juu ya kujifanyia jina zuri pamoja na Mungu ‘ili siku yetu ya kufa iwe bora kuliko siku ya kuzaliwa kwetu.’ (Mhu. 7:1) Au, kwa habari ya wale wanaotumaini kurithi dunia ya paradiso, iwe kwamba siku ya kufa haitakuja kamwe!

18 Lakini, pengine unafikiri kwamba mwisho ulipaswa kuwa umekuja kufikia sasa. Je! wewe unafikiri kwamba Bwana amekawiza kuja kwake? Je! wewe unaanza kulegeza mkono wako katika kazi ya maana ya kutangaza ufalme wa Mungu, au hata kuingilia mwenendo mbaya? Bila kujali wakati mwisho utakapokuja, huu ndio wakati ambapo mkono wako wapaswa kufanya lo lote unalopata la kufanya katika kujifanyia jina zuri pamoja na Mungu. Ye yote wetu huenda akatoweka kesho. Sisi ni kama ua linalonyauka, ukungu unaotoweka, kivuli kipitacho. (Ayubu 14:1, 2; Yak. 4:14) Mhubiri 9:12 huonya hivi: “Mwanadamu naye hajui wakati wake kama samaki wanaokamatwa katika nyavu mbaya, na mfano wa ndege wanaonaswa mtegoni, kadhalika wanadamu hunaswa katika wakati mbaya, unapowaangukia kwa ghafula.”

19, 20. (a) Zaidi ya kuishi maisha yenye adili safi sasa, ni Jambo gani linalohitajiwa? (b) Sababu gani ni Jambo la muhimu kuchukua hatua sasa?

19 Lazima sisi tufanye zaidi ya alivyofanya yule kijana aliyemwendea Yesu akiuliza namna anavyoweza kupata uzima wa milele. Kwa wazi, alikuwa akiishi maisha yenye adili safi, lakini hiyo haikuwa inatosha. Kuongezea haya, Yesu alimwambia hivi: “Njoo unifuate.” Yesu ndiye kielelezo. (Mt. 19:16-22; 1 Pet. 2:21) Si kwamba yeye aliishi kulingana na kanuni za Mungu za mwenendo mzuri; vilevile yeye alitangaza “habari njema ya ufalme” kwa wengine. “Tubuni,” akatangaza, “kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” “Naye Yesu alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji, akifundisha katika masinagogi yao, na kuhubiri habari njema ya ufalme.” (Mt. 4:17; 9:35) Wakati makutano walipotaka akae nao zaidi nao wakajaribu kumzuia, yeye alisema hivi: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia; maana kwa sababu hiyo nalitumwa.” Wakati alipowaona makutano waliokuwa “wamechoka na kutawanyika” kiroho, “aliwahurumia,” “akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Luka 4:43; Mt. 9:36; Marko 6:34) Aliwatuma mitume wake wakahubiri, akiwaagiza: “Katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia.”​—Mt. 10:7, 8.

20 Sasa sisi twaishi katika hizi “siku za mwisho” zenye hatari za taratibu hii ya Kishetani. “Muda ubakio si mwingi.” Ni jambo la muhimu sana kwetu kwamba tutangaze “habari njema.” (1 Kor. 7:29; 9:16) Sasa ndio wakati uliotabiriwa wa ‘habari hizi njema za ufalme zihubiriwe katika dunia yote inayokaliwa na watu kuwa ushuhuda, kabla ya mwisho kuja.’ (Mt. 24:14, NW) Hata wakati wa Yehova wa kuleta mwisho wa hii taratibu mbovu uwe wakati gani, usisahau hili kamwe: SASA wakati ungali unaishi; SASA kabla kifo kisichotazamiwa hakijakufikia; SASA ndio wakati wako wa kushiriki katika kuhubiri “habari hizi njema” na kujifanyia jina zuri pamoja na Mungu!

[Picha katika ukurasa wa 13]

Wakati wo wote anapoishi mtu, huo ndio wakati wake wa kujifanyia jina zuri

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki