Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 8/15 kur. 4-7
  • Unaweza Kuridhika na Fungu Lako Maishani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Unaweza Kuridhika na Fungu Lako Maishani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MFANO UNAOONYESHA KUTOSHEKA
  • ONYO LINALOTOLEWA NA MIFANO YA KUTOKUWA NA URADHI
  • JE! WEWE UNARIDHIKA?
  • Je, Inawezekana Kuwa na Uradhi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Je, ‘Umejifunza Siri’ ya Kuridhika?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Pata Uradhi kwa Kutumia Kanuni za Biblia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Kutosheka Ni Mradi Unaofaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 8/15 kur. 4-7

Unaweza Kuridhika na Fungu Lako Maishani?

“KAMA malaika wawili wangetumwa toka mbinguni, mmoja aongoze ufalme, na yule mwingine afagie barabara, hawangekuwa na maelekeo ya kutaka kubadilisha kazi zao.” Ndivyo alivyosema kiongozi wa kidini Mwingereza John Newton karne mbili zilizopita. Hiyo ilikuwa njia mojayapo ya kuonyesha namna ya kuridhika na fungu la mtu maishani.

Lakini kuridhika kunatia nini ndani? Ni maono ya ndani ya uradhi mwingi na wenye kuendelea wa hali za mtu nao unaonyeshwa kwa kutonung’unika au kutotafuta makosa. Kamusi moja inalieleza neno “uradhi” kuwa “akili tulivu: kutosheka sana sana na fungu la mtu maishani.” Vipi wewe? Ndani-ndani, je! unatamani ungekuwa na kazi tofauti, nyumba tofauti, mwenzi tofauti? Je! inakuwa kwamba tamaa zako zinakuwa zenye nguvu sana hata zikufanye ukose usawa?

Kuridhika hakumaanishi tusitie jitihada sana tufanye hali zetu ziwe bora. Kuridhika hakupaswi kuzuia uwezo wa kufanyiza mambo, kujiacha bila vitu vya kutosha kuturuzuku siku baada ya siku. Lakini kunamaanisha kwamba tusitamani sana kitu kufikia hatua ya kujikuta tumo kati ya wanung’unikaji wasio na furaha.

MFANO UNAOONYESHA KUTOSHEKA

Fikiria mfano wa mtume Mkristo Paulo. Alikuwa raia wa Roma na kwa hakika akiwa ametoka katika jamaa maarufu ya Kiebrania, alijifunza sheria miguuni pa Gamalieli mwenye elimu nyingi naye akaheshimiwa na Mafarisayo wenzake. Lakini ilitokea nini? Aliitwa na Yehova Mungu kupitia kwa Mwana Wake awe mhubiri wa “habari njema.” Ili ajiruzuku na kuepuka kuwa mzigo kwa wengine katika kundi la Kikristo, Paulo alifanya kazi kwa mikono yake. Hilo lilimwezesha asafiri kama alivyotaka mji baada ya mji, po pote ambapo utendaji wake wa umisionari ulimtaka aende. Kazi yake akiwa mwevanjelisti ilimletea mateso mengi, hata kupigwa, kupigwa mawe na kupigwa mijeledi. Lakini je! alikuwa mwenye kuridhika?

Katika barua yake aliyowaandikia Wafilipi, Paulo aliandika hivi: “Nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo. Nimejifunza kuwa radhi na hali yo yote niliyo nayo.” (Flp. 3:8; 4:11) Ndiyo, mtume Paulo alipata uradhi wa kweli katika utumishi wake wa uaminifu aliomtolea Mungu.

ONYO LINALOTOLEWA NA MIFANO YA KUTOKUWA NA URADHI

Hata hivyo, wengine walikosa uradhi, nayo matokeo yakawa yenye msiba. Mwanamke wa kwanza, Hawa, alikuwa na mume mkamilifu, makao mazuri katika bustani iliyo paradiso, namna mbalimbali za chakula kwa wingi, uangalizi wa upendo kutoka kwa Baba na Mungu wake wa kimbinguni, na mataraja ya kuishi milele. Hata hivyo wakati Mjaribu alipotangaza kwamba Mungu alikuwa anamzuia kitu kilichokuwa chake kwa haki, mwanamke huyo alimwamini naye akakosa kuridhika na fungu lake. Alichagua mwendo uliompa hali ya kujitegemea na nafasi ya kujiwekea kanuni zake kwa habari ya yaliyo mema na yaliyo mabaya. Uchaguzi huo ulimletea taabu na kifo tu. Ingekuwa vizuri zaidi kwake kuendelea kuridhika, akiwa ananyenyekea kwa mume wake, na zaidi ya yote, kwa Mungu wake!

Karne nyingi baadaye, wakati Yehova Mungu alipokuwa akiongoza watu wake kupitia jangwani, mara nyingi kutoridhika kulitokea. Katika pindi moja, wakuu 254 wa Israeli walikosa kuridhika na fungu lao, nalo jambo hilo likatokeza uasi wa moja kwa moja juu ya Musa na Haruni. “Ninyi inawatosha. . . N’nini basi kujitukuza juu ya mkutano wa [Yehova]?” Jibu la Musa lilionyesha sababu ya kukosa uradhi. Twasoma hivi: “Je! mwaona kuwa ni jambo dogo kwenu . . . mfanye utumishi wa maskani ya [Yehova] . . . ? nanyi je! mwataka na ukuhani pia?” (Hes. 16:1-10) Matokeo yakawa nini? Wengi wao wakauawa kwa moto; wengine wakamezwa na ardhi.

Dema, mfanya kazi mwenzi pamoja na Paulo alikosa kuridhika kwa sababu ya hali tofauti. Alikuwa pamoja na mtume huyo wakati wa kufungwa kwake mara ya kwanza katika Roma. Walakini wakati wa kufungwa kwa Paulo mara ya pili, ‘Dema alimwacha kwa sababu aliipenda taratibu ya mambo iliyopo.’ (2 Tim. 4:10, NW) Hivyo akakosa uradhi wa kweli.

JE! WEWE UNARIDHIKA?

Namna gani wewe? Ikiwa ndiwe unayetafutia jamaa yako riziki, je! unakosa kuridhika? Bila shaka kuna mambo mengi yanayoweza kumsumbua Mkristo—udanganyifu katika bei zilizo juu, kuonewa kwa maskini na wenye uhitaji, upendeleo, licha ya kazi nyingi sana ambazo zinafanywa kwa kuwa ni kawaida tu. Mtu anaweza kuridhikaje chini ya hali kama hizo? Ni vema kukumbuka kwamba haupo peke yako. Watumishi waaminifu wa Mungu katika nyakati za kale walikabili matatizo ayo hayo, na njia ambayo waliyakabili kwa kufanikiwa imeandikwa katika Biblia ili kututia moyo.

Kwa mfano, alikuwako Mlawi Asafu, mwombaji na mpiga-muziki mwenye kujulikana sana. Yeye aliandika hivi: “Naliwaonea wivu wenye kujivuna, nilipoiona hali ya amani ya wasio haki. Katika taabu ya watu hawamo, wala hawapati mapigo pamoja na wanadamu.” Basi, akaanza kujisemea hivi: “Hakika nimejisafisha moyo wangu bure, nimenawa mikono yangu kwa kutokukosa.”​—Zab. 73:3, 5, 13.

Kwa kweli Asafu alikuwa anajiuliza hivi: ‘Kuna faida gani kujaribu kufanya yaliyo haki? Wajapofanya mabaya wengine wanaendelea vizuri. Sababu gani nisifanye hivyo?’ Lakini ndipo alipojua kwamba kuwaza kwake kulikuwa kwenye makosa. Alipokuwa hekaluni pamoja na waabudu wengine wa Yehova, akatambua kwamba ufanisi wa waovu ni wa muda tu.​—Zab. 73:15-19.

Ingawa tunaweza kuhuzunishwa na ubaya unaotuzunguka, twaweza kupata faraja kutokana na uhakika wa kwamba kuna siku ya kutoa hesabu. (Matendo 17:31) Katika taratibu hii ya mambo, kuna mengi sana yasiyoweza kugeuzwa. “Yaliyopotoka hayawezi kunyoshwa,” ndivyo inavyosema Biblia. (Mhu. 1:15) Kwa hiyo, tusipoweza kugeuza mambo kwa kutumia njia zinazofaa, kwa hekima tunamngojea Yehova Mungu atende katika wakati wake alioweka. Hivyo tunaendeleza uradhi wetu.

Namna gani nyumba yako? Je! inakupa uradhi? Hakika, washiriki wenye upendo wa jamaa wanaweza kuleta uradhi. Baada ya kufanya kazi sana katika siku, ni faraja kama nini kwa mwanamume kuingia katika nyumba yake yenye amani na kufurahia ushirika wa mke wake na watoto wake! Mithali ya Biblia inasema vizuri sana jambo hilo, inaposema hivi: “Chakula cha mboga penye mapendano; ni bora kuliko ng’ombe aliyenona pamoja na kuchukiana.”​—Mit. 15:17.

Jamaa ya kiroho ambayo washiriki wake ni wenzi walio mashahidi wa Yehova vilevile inasaidia sana ili kuendelea kuwa na uradhi. Ni vema kama nini kushirikiana na watu ambao ni wanyofu, wenye haki na wenye kupenda! Je umepata kuona kwamba kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kunakufanya usahau matatizo yanayovunja moyo?

‘Lakini namna gani fungu langu?’ huenda mke wa nyumbani akauliza. Inahitaji jitihada yenye kuendelea ili kuendeleza uradhi wa kweli wakati huu ambapo mengi sana yanasemwa juu ya “uhuru wa wanawake.” Lakini je! wale wanaoongoza chama hicho wanaridhika kweli kweli? Wanawezaje kuridhika hali wanapuza uhakika wa kwamba sehemu iliyotolewa na Mungu kwa mke ni kuwa msaidizi na mkamilishaji, wala si ile ya kichwa au mshindani? (Mwa. 2:18) Mke anaweza kufanya mengi sana ili kutokeza furaha ya jamaa yote. Katika siku hizi za infuleshoni yenye kupanda juu sana, anaweza kupunguza matumizi kwa kununua vitu kwa hekima. (Mit. 31:14) Kwa kusema na kwa mfano, mke Mkristo anaweza kujenga watoto wake kiroho, akiwasaidia kuona maana ya kuishi kama wanafunzi wa Yesu Kristo.

Kwa kukaa katika mahali pake alipopewa na Mungu, mwanamke Mkristo anapata furaha ya mke mwema anayesimuliwa katika kitabu cha Mithali, ambapo twasoma hivi: “Mke mwema, ni nani awezaye kumwona? Maana kima chake chapita kima cha marijani. Moyo wa mumewe humwamini. . . . Humtendea mema . . . siku zote za maisha yake. . . . Huangalia sana njia za watu wa nyumbani mwake . . . Wanawe huondoka na kumwita heri; mumewe naye humsifu. . . . Mwanamke amchaye [Yehova], ndiye atakayesifiwa.”​—Mit. 31:10-30.

Namna gani ninyi vijana? Je! mnatosheka na fungu lenu? Leo vijana wanakabili matatizo magumu. Ufisadi, kudanganya na kutumia vibaya dawa za kulevya vimeongezeka sana. Vitu hivyo havipaswi kuwafanya mkose usawa, kuwafanya mkose kufuata uongozi na kuwafanya mwache shule. Kwa kuacha masomo yenu kabla ya wakati, huenda mkalazimika kutosheka na kazi yenye kulipa mshahara mdogo na hali za kazini ambazo ni zenye kuhuzunisha kuliko zile mnazokabili shuleni. Hivyo, jaribuni kufanya yote mwezayo shuleni, mkichagua namna ya mafunzo ambayo yatawasaidia kujiruzuku vema bila kumaliza kabisa nguvu zenu. Watumishi wa Mungu wanafanya vema kujitayarisha kwa ajili ya kazi ambayo itawaruhusu kutoa wakati wao mwingi na nguvu kusaidia wengine kiroho. Hiyo inatokeza furaha kubwa zaidi inayotokana na kutoa.​—Matendo 20:35.

Iwapo wewe ni mwabudu wa Yehova Mungu, unapokuwa ungali shuleni jaribu sana kufanya maendeleo ukiwa Mkristo. Tumia nafasi ya kutangaza “habari njema” shuleni na katika kushirikiana na washiriki wengine wa kundi. Wakati wa likizo za shule, fikiria kupanua sehemu yako katika kutangaza waziwazi “habari njema.” Unaweza kupata furaha ya kweli ya kutumikia kama painia-msaidizi. Usipuze kusoma Biblia vitabu ambavyo vimekusudiwa vikusaidie uifahamu vizuri. Kutangulia kujitayarisha vizuri kutakusaidia ushiriki kwenye mikutano ya kundi.

Je! kuna wo wote katika kundi lenu ambao ni wagonjwa, wasiojiweza au wazee? Je! unaweza kuwanunulia vitu dukani, au kuwatengenezea vitu au kuwasafishia nyumba? Je! kuna mtu asiyeona vizuri? Je! unaweza kutoa wakati kila juma wa kumsomea mtu huyo? Kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo kunamaanisha kuwatumikia wengine kama vile alivyofanya yeye. Ukijifunza kutumikia wengine wakati wa ujana wako, furaha na baraka zako zitakuwa nyingi.

Je! kuna mambo mapya ya kuleta uradhi wa kweli? Hapana, hakuna mambo mapya. Miaka zaidi ya 1,900 iliyopita mtume Paulo alitoa shauri linalotumika sasa kama ambavyo lilitumika wakati huo. Aliandika hivi: “Utauwa pamoja na kuridhika ni faida kubwa. Kwa maana hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu; ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo.”​—1 Tim. 6:6-8.

Basi, chukua wakati wa kutafakari juu ya fungu lako. Ni kweli kwamba huenda likawa bora, lakini pia laweza kuwa baya zaidi. Jitahidi kuridhika na uliyo nayo, bila kuhangaikia yale usiyokuwa nayo. Pata furaha kwa kufanya unayoweza kufanya ili kusaidia wengine kiroho na kuwa kitia-moyo kwao. Fanya hivyo, kama ambavyo wengi wamefanya, nawe waweza kuridhika na fungu lako maishani.

[Picha katika ukurasa wa 5]

‘Lakini namna gani fungu langu maishani?’ huenda mke anayefanya kazi nyumbani akauliza

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki