Mashahidi Mpaka Kwenye Sehemu Ya Mbali Zaidi Ya Dunia
1. Dakika zenye kutokeza zaidi katika historia ya wanadamu zilikuwa nini?
HAKIKA zilikuwa dakika zenye kutokeza zaidi katika historia ya wanadamu. Kabla ya hapo, kuagana hakukuwa kumepata kuwa kwenye kugusa moyo zaidi. Mwana wa Mungu alikuwa anakaribia kuacha wafuasi wake duniani, asipate kuonekana tena nao akiwa na nyama. Ulikuwako wakati wa kuuliza ulizo moja tu, kutoa jibu moja tu. Juu ya habari gani? Mazungumzo hayo ya mwisho yangehusu wafuasi wa Kristo hata mwisho wa taratibu ya mambo iliyopo!
2. Ni ulizo gani la mwisho ambalo Yesu aliulizwa kabla ya kuondoka duniani asirudi tena, na sababu gani jibu lake linatupendeza sana?
2 Ulizo la mwisho ambalo wanafunzi wa Yesu walimwuliza lilikuwa hili: “Bwana, unarudisha ufalme wa Israeli wakati huu?” Makusudi yao hasa ya kuuliza jambo hilo tunaweza kuwazia tu. Hata matazamio yao yawe yalikuwa nini, jambo moja ni wazi: walitaka kujua wakati makusudi ya Mungu kuhusiana na Ufalme yangetimizwa. Nani awezaye kuwalaumu? Wao si ndio waliokuwa wa kwanza wala wa mwisho kutaka kukombolewa haraka. Basi maelezo ya Yesu, ndiyo, maneno yake ya mwisho kabisa kabla ya kuondoka duniani asirudi tena, yanatuvutia sana sisi leo.
MGAWO AMBAO KRISTO ALITOA ALIPOKUWA AKIONDOKA
3, 4. (a) Yesu alijibu namna gani? (b) Yesu aliwapa wanafunzi wake somo gani lenye sehemu mbili?
3 Yesu alijibu hivi: “Si shauri lenu kupata kujua nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe; lakini ninyi mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu ninyi, na ninyi mtakuwa mashahidi wangu mimi katika Yerusalemu na katika Yudea yote na katika Samaria na kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” Masimulizi hayo yanaongeza hivi: “Na alipokwisha kusema mambo hayo, walipokuwa wakitazama, aliinuliwa nalo wingu likamfunika wasimwone.”—Matendo 1:6-9, NW.
4 Maana ya maneno ya kuagana ya Yesu ilikuwa na sehemu mbili. Kwanza, kwa busara, lakini kwa uthabiti, aliwaambia wanafunzi wake kwamba wakati wa kutimizwa kwa makusudi ya Yehova haukuwa juu yao. Hivyo alithibitisha yale aliyokuwa ametangulia kusema katika unabii wake juu ya mwisho wa taratibu ya mambo. (Mt. 24:36; Marko 13:32-37) Kisha akaendelea kuwaonyesha jambo ambalo kuanzia wakati huo na kuendelea lingekuwa juu yao. Kwanza wangekuwa mashahidi Wakristo katika Yerusalemu, ambapo walikuwa wameambiwa wangojee kwa wakati huo (Matendo 1:4), kisha katika Yudea yote na Samaria na, mwishowe, “kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” Wangepokea “nguvu” kupitia kwa roho takatifu.
5. “Nguvu” ilikuja juu ya wanafunzi wa Yesu wakati gani, nayo iliwachochea wafanye nini?
5 “Nguvu” hiyo ilikuja juu yao juma moja na nusu baadaye, siku ya Pentekoste. Mitume na wanafunzi wengine walikuwa wamekaa Yerusalemu kwa kutii, na katika siku hiyo ya sikukuu “wote pamoja walikuwa mahali pamoja.” Ghafula, “wote wakajawa na roho takatifu nao wakaanza kusema kwa lugha tofauti, kama ambavyo roho iliwapa ya kusema.” Walisema, “juu ya mambo mazuri sana ya Mungu,” bali si kunong’oneza maneno yasiyofahamika. —Matendo 2:1, 4, 11, NW.
“KATIKA YERUSALEMU”
6. Wakristo hao waliotiwa mafuta walianzaje kutimiza mgawo wao, walakini kukiwa na upinzani gani?
6 Wakristo hao waliotiwa mafuta karibuni mara moja walianza kutimiza mgawo waliokuwa wamepewa na Kristo aliyefufuliwa. Kwanza walihubiri “katika Yerusalemu”; wakiwa wanapingwa. Viongozi wa kidini na viongozi wa mji wa Wayahudi waliwafanyia hila, wakasema:
“Tutawafanyia nini watu hawa? Kwa sababu, hakika, ishara yenye kutokeza imetokezwa nao [kuponywa kwa mtu aliyelemaa], ambayo ni wazi kwa wakaaji wote wa Yerusalemu; nasi hatuwezi kuikanusha. Hata hivyo, kusudi isienezwe mbali zaidi kati ya watu, na tuwaambie kwa vitisho wasiseme tena kwa msingi wa jina hili [Yesu] kwa mtu ye yote.” Matendo 4:16, 17, NW.
7. (a) Kwa sababu hiyo wanafunzi wa Yesu walitendaje? (b) Mpinzani wa kidini alitoaje uthibitisho kwamba Wakristo wa kwanza walikuwa wakitimiza mgawo wao kwa uaminifu?
7 Kristo alikuwa amesema hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu mimi.” Baraza Kuu ya Kiyahudi iliwatisha Wakristo wa kwanza “wasiseme tena kwa msingi wa jina hili.” Wao walitii nani? Kwa heshima waliwaambia hivi watesi wao: “Sisi hatuwezi kuacha kusema juu ya mambo ambayo tumeona na kusikia.” (Matendo 4:18-20, NW) Waliendelea kutoa ushuhuda. Ingawa mitume walifungwa, baada ya kufunguliwa kimwujiza wakati wa usiku “wakaingia kwenye hekalu kulipopambazuka na kuanza kufundisha.” (Matendo 5:17-21, NW) Ni juhudi kama nini! Kwa mara nyingine wakakamatwa.
“Wakawaleta na kuwasimamisha mbele ya jumba la Baraza Kuu. Naye kuhani mkuu akawahoji na kusema: ‘Tuliwaambia kabisa msiendelee kufundisha kwa msingi wa jina hili, na bado, tazameni! mmeujaza Yerusalemu mafundisho yenu.’ “(Matendo 5:27, 28, NW)
Pasipo kujua, mheshimiwa huyo wa kidini alishuhudia uhakika wa kwamba Wakristo hao wa kwanza walikuwa wakitimiza kwa uaminifu sehemu ya kwanza ya mgawo wao waliopewa na Kristo. Walikuwa mashahidi wake wenye juhudi “katika Yerusalemu.”
8. Wakristo hao walikuwa ‘wameujazaje Yerusalemu mafundisho yao, nao walipata matokeo gani?
8 Baada ya kupigwa mijeledi na kuamriwa ‘waache kusema kwa msingi wa jina la Yesu,’ Wakristo hao “wakaenda zao toka Baraza Kuu, wakifurahi kwa sababu walikuwa wamehesabiwa wanastahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake.” Badala ya kuvunjika moyo, “kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.” (Matendo 5:40-42, NW) Angalia kwamba ‘waliendelea’ kutoa ushuhuda “nyumba kwa nyumba.” (New World Translation; New International Version) Ingawa hesabu yao ilikuwa ndogo, ni kwa njia hiyo waliweza ‘kuujaza Yerusalemu mafundisho yao.’ Njia hiyo ilileta matokeo mazuri sana. “Basi neno la Mungu likaendelea kukua, na hesabu ya wanafunzi ikaendelea kuongezeka sana katika Yerusalemu.”—Matendo 6:7, NW.
KUSONGA MPAKA SAMARIA NA YUDEA
9. Kazi ya kutoa ushuhuda ilisonga mpaka Yudea na Samaria chini ya hali gani?
9 Walakini Wakristo wa kwanza hawangeweza kuachia hapo. Walipaswa kuwa mashahidi wa Kristo “katika Yudea yote na katika Samaria” vilevile. Kwa kweli, sehemu ya kwanza ya mgawo wao iliyotimizwa kwa juhudi ndiyo iliyoongoza watimize sehemu ya pili ya kazi yao ya Kikristo. Upinzani juu ya utoaji wao wa ushuhuda katika Yerusalemu ulifikia kilele chake wakati wa kuuawa kidini kwa Stefano, nalo hilo likatokeza wimbi la mateso juu ya kundi la mashahidi Wakristo katika Yerusalemu. Kusudi la upinzani huo wenye jeuri lilikuwa kunyamazisha mashahidi hao wa Kristo. Mahali pake, uliipa kazi ya kutoa ushuhuda kichocheo na kuieneza mahali ambapo Kristo alitaka ifike. “Wote isipokuwa mitume walitawanyika kote kote katika mikoa ya Yudea na Samaria.” Nao Wakristo hao waliotawanywa walifanya nini katika maeneo hayo? “Wakaenda kote katika nchi hiyo wakitangaza habari njema za lile neno.”—Matendo sura 7; 8:1, 4, NW.
10. Mitume walifanya nini waliposikia kwamba “Samaria ilikuwa imekubali neno la Mungu,” naye Petro alitumia ‘ufunguo’ gani?
10 Upesi habari zikafikia “mitume katika Yerusalemu” kwamba “Samaria ilikuwa imekubali neno la Mungu.” Wakitenda kulingana na hali hiyo, mitume wakatuma wawili kati yao, Petro na Yohana, wakaimarishe kazi njema iliyokuwa imefanywa na Wakristo hao waliotawanywa, kutia Filipo mhubiri wa habari njema. Akitumia mapendeleo ya pekee ambayo Kristo alikuwa amempa, Petro alifungulia Wasamaria njia ya kuwa Wakristo waliozaliwa na kutiwa mafuta kwa roho, walioitwa kushiriki pamoja na Kristo katika “ufalme wa mbinguni.” (Mt. 16:18, 19; Matendo 8:14-17, NW) Masimulizi katika Matendo yanaendelea hivi: “Walipokwisha kutoa ushuhuda kikamilifu na kusema neno la Yehova, . . . wakaenda wakitangaza habari njema katika vijiji vingi vya Wasamaria.” (Matendo 8:25, NW) Ndivyo ilivyokuwa kwa Samaria!
11. Kuna ushuhuda gani kwamba “Yudea yote” ilipewa ushuhuda vizuri?
11 Kwa habari ya Yudea, bila shaka Wayudea wengi walikuwako Yerusalemu siku ya Pentekoste nao wakapokea ushuhuda mzuri uliotolewa na Wakristo waliokuwa wametiwa mafuta karibuni, sana-sana uliotolewa na Petro. (Matendo 2:9, 14-36) Vilevile twajua kwamba kabla ya wimbi hilo la mateso kutokea juu ya Wakristo katika Yerusalemu, “makutano ya watu wa miji iliyoko kandokando ya Yerusalemu wakakutanika, wakileta wagonjwa, nao walioudhiwa na pepo wachafu; nao wote wakaponywa.” (Matendo 5:16) Wakaaji hao wote wa Yudea wakapewa ushuhuda juu ya Yesu. Akitaja juu ya kipindi kilichofuata kuongolewa kwa Paulo, Luka anaandika hivi: “Kundi katika Yudea yote na Galilaya na Samaria likaingia katika kipindi cha amani, likijengwa.” (Matendo 9:31, NW) Karibu miaka 15 baadaye Paulo aliandikia Wakristo katika Thesalonika hivi: “Maana ninyi, ndugu, mlikuwa wafuasi wa [makundi] ya Mungu yaliyo katika [Yudea]. (1 The. 2:14) Hakika, Wakristo wa kwanza walitimiza kwa juhudi mgawo wao waliopewa na Kristo wa kuwa mashahidi wake “katika Yerusalemu na katika Yudea yote na Samaria.”
“MBALI KWENYE MIISHO YA DUNIA”
12. Mbegu za upanuzi wa wakati ujao zilipandwaje siku ya Pentekoste?
12 Hata hivyo, mgawo wa kuaga wa Yesu ulikuwa zaidi ya hayo. Ulisema hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Yudea yote na Samaria, na mbali kwenye miisho ya dunia.” (Matendo 1:8, The New English Bible) Kuna ushuhuda kwamba jina la Kristo lilishuhudiwa kati ya Wayahudi wa Diasporaa mapema, hata kabla ya mwaka 36 W.K.—mwaka ambao kwa mara nyingine Petro alitumia pendeleo lake alilopewa na Kristo, wakati huu akafungulia Mataifa wasiotahiriwa nafasi ya kuingia katika Ufalme. (Mt. 16:18, 19; Matendo sura 10) Jambo moja ni kwamba wale Wayahudi 3,000 na waongofu pia ambao walibatizwa wakawa Wakristo siku ya Pentekoste 33 W.K. hawakuwa wakaaji wa Yerusalemu na Yudea peke yake. Wengi wao walikuwa wametoka sehemu za mbali sana kama vile Parthia, Umedi, Elamu na Mesopotamia (Iran na Iraq za Kisasa), Asia Ndogo (Uturuki ya kisasa), Afrika ya Kaskazini na Italia. (Matendo 2:8-11) Baada ya kurudi kwenye makao yao katika kontinenti tatu za Asia, Afrika na Ulaya, Wakristo hao waliokuwa wameongolewa karibuni bila shaka walitoa ushuhuda juu ya jina la Kristo, angaa kwa Wayahudi wengine na waongofu katika nchi zao. Hivyo mbegu za upanuzi wa wakati ujao zilipandwa apo hapo katika Pentekoste.
13. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba ushuhuda wa Kikristo ulitangulia kutolewa mahali kwingine zaidi ya Yudea na Samaria?
13 Na zaidi, tunasoma katika Matendo 11:19 hivi: “Wale waliotawanyika kwa sababu ya ile dhiki iliyotukia kwa habari ya Stefano [wakati fulani baada ya Pentekoste, lakini kabla ya kuongolewa kwa Paulo katika mwaka 34 au 35 W.K.], wakasafiri hata Foinike na Kipro na Antiokia [ya Shamu] wakasema na Wayahudi.” Hiyo inathibitisha kabisa kwamba hata kabla ya kuhubiri huko kufikia watu wasio Wayahudi, Kristo alikuwa akihubiriwa mbali zaidi ya Yudea na Samaria.
14. Kutoa ushuhuda kwa njia ya utaratibu kati ya watu wasiotahiriwa inaelekea kulianzia wapi? Eleza.
14 Mara tu Petro alipokwisha kutumia mwingine wa “funguo za ufalme wa mbinguni” ili kufungulia watu wasiotahiriwa nafasi za kuingia katika Ufalme, katika mwaka 36 W.K., njia ilikuwa wazi kutoa ushuhuda wa Kikristo kwa watu wote, ndiyo! “mbali kwenye miisho ya dunia.” (NE) Inaonekana kwamba kutoa ushuhuda kwa njia ya utaratibu kati ya Mataifa wasiotahiriwa kwa mara ya kwanza kulianzia Antiokia ya Shamu, ambayo wakati huo ilikuwa mji mkuu wa tatu katika ulimwengu, kufuata Roma na Aleksandria. Mambo yalitokea hivi: Wakati fulani baada ya mwaka 36 W.K., lakini kabla ya 44 W.K., “baadhi ya hao [Wakristo] walikuwa watu wa Kipro na Kirene [katika Afrika ya Kaskazini], nao walipofika Antiokia wakasema na Wayahudi wa [Kigiriki], wakihubiri habari njema za Bwana Yesu. Mkono wa [Yehova] ukawa pamoja nao; watu wengi wakaamini, wakamwelekea Bwana.”—Matendo 11:20, 21.
15. (a) Kundi la Yerusalemu lilifanya nini juu ya hali hiyo mpya, na sababu gani uchaguzi wao ulifaa? (b) Wakati wa miaka kadha iliyopita Paulo alikuwa akifanya nini? (c) Sababu gani habari ya kundi la kwanza la Antiokia inavutia hasa?
15 Utendaji wa juhudi wa kuhubiri kati ya Wakristo hao waliotoka Kipro na Kirene kati ya watu wasio Wayahudi ulibarikiwa na Yehova. “Kundi lililokuwa Yerusalemu” likatuma mjumbe wa pekee aende kaskazini mwa Shamu akashughulikie hali hiyo mpya. Walichagua Barnaba, mwenyewe akiwa Myahudi mwenye kusema Kigiriki kutoka Kipro. Baada ya kutia moyo wanafunzi hao wapya wa Kristo, Barnaba akaenda Tarso kumchukua Paulo, ambaye alikuwa ametumia miaka kadha tu ‘akitangaza habari njema juu ya imani’ katika Shamu na Kilikia, sasa ni upande wa kusini-mashariki wa Uturuki. (Linganisha Matendo 9:26-30 na Wagalatia 1:18-23.) “Hivyo ikawa kwamba kwa mwaka mzima [inaelekea katika mwaka 45 W.K.] wao [Barnaba na Paulo ] wakakusanyika pamoja nao kundini [ambalo sasa washiriki wake walikuwa Wayahudi pamoja na Mataifa] wakafundisha kundi kubwa, na ni katika Antiokia ndipo kwa uongozi wa Mungu wanafunzi walipoitwa Wakristo kwa mara ya kwanza.”—Matendo 11:22-26, NW.
16, 17. (a) Kazi ya kutoa ushuhuda ilipanuliwaje toka Antiokia ya Shamu? (b) Paulo na Barnaba walitaja unabii gani ili kutetea utendaji wao, nao unabii huo ulihusu nani hapo kwanza? (c) Jambo hilo linatupa msaada wa kufahamu Matendo 1:8 kwa njia gani?
16 Kwa miaka 10 hivi Antiokia ya Shamu ikawa makao makuu ambapo kutoka hapo utendaji mwingi wa umisionari ulifanywa, chini ya uongozi wa roho takatifu. (Matendo 13:1-4; 14:26; 15:35, 36; 18:22, 23) Paulo, pamoja na wamisionari wenzake wengine, walifanya ziara tatu za kutoa ushuhuda mbali ambazo zilieneza Ukristo kote kote Asia Ndogo na Ugiriki. Walimhubiri Kristo kwa Wayahudi na Mataifa. Pindi moja, Paulo na Barnaba walitetea tendo hilo mbele ya kikundi cha Wayahudi wenye hasira, wakasema:
“Ilikuwa lazima neno la Mungu lisemwe kwenu kwanza. Kwa kuwa mnalitupilia mbali nanyi hamwonyeshi mnastahili uzima wa milele, tazameni! twageukia mataifa. Kwa kweli, Yehova ametupa sisi amri katika maneno haya, ‘Nimekuweka wewe uwe nuru ya mataifa mpaka kwenye mwisho wa dunia.’ “
Luka anaongeza hivi: “Wakati wale wa mataifa waliposika hayo, wakaanza kufurahi na kutukuza neno la Yehova, na wote wale waliokuwa na maelekeo yanayofaa uzima wa milele wakawa waamini.”—Matendo 13:46-48, NW.
17 Kwa kutaja unabii wa Mtumishi wa Kimasihi (Isa. 42:6; 49:6) na kuonyesha unavyohusu utendaji wao, Paulo na Barnaba walionyesha kwamba wao na Wakristo wenzao walikuwa ‘badala ya Kristo’ kweli kweli, ambaye Yehova alikuwa amempa mgawo wa kuleta “nuru” na “wokovu” “kwenye sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—2 Kor. 5:20, NW; Matendo 1:8, NW; linganisha Isaya 49:5-9 na Luka 2:25-32.
MGAWO WA MUDA MREFU
18. Twajua nini juu ya jitihada za Wakristo wa kwanza za kuwa mashahidi “kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia”?
18 Kama ambavyo tumekwisha kuona, kitabu cha Matendo kinaonyesha juhudi ambayo mitume na Wakristo wa kwanza walifanya kutimiza mgawo wao wa kutoa ushuhuda waliopewa na Kristo katika Yerusalemu, Yudea, Samaria na mbali kadiri ambavyo wangeweza kufika kuelekea “miisho ya dunia.” Kwa mfano, tunajua kwamba mtume Petro alikuwa shahidi mwaminifu wa Kristo mbali upande wa mashariki katika Babeli, na kwamba Paulo alitoa ushuhuda mbali upande wa magharibi katika Italia na hata pengine Spania.—1 Pet. 5:13; Matendo sura 28; Rum. 15:23-28.
19. Hata hivyo, ni jambo gani linaloonyesha kwamba mgawo wa kuaga wa Kristo aliowapa Wakristo ungehusu wakati wa leo, nalo ni ulizo gani linalotokea?
19 Lakini ni wazi kabisa kwamba mgawo wa kuaga wa Kristo wa kuwa mashahidi “kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia” ulihusu wakati mrefu zaidi. Kulingana na unabii wa Yesu mwenyewe, ulihusu zaidi ya wakati wa mitume, kufika wakati wa “mwisho wa taratibu ya mambo” wenyewe. (Mt. 24:3, 14, NW) Hata hivyo, limekuwa jambo lenye kutia nguvu na imani kurudia mfano mzuri uliowekwa na Wakristo wa kwanza. Sasa ulizo hili latokea: N’nani leo wanaotimiza kazi hiyo njema iliyoanzwa na mitume, na ni kwa njia gani wamekuwa mashahidi wa Kristo na Baba yake wa kimbinguni, kwa halisi “kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia”? Tutaona katika makala inayofuata.
[Maelezo ya Chini]
a “Kutapanywa” kwa Wayahudi baada ya uhamisho wa Ashuru na Babeli.
[Blabu katika ukurasa wa 10]
“Tazameni! mmeujaza Yerusalemu mafundisho yenu”
[Blabu katika ukurasa wa 11]
‘Wakaenda wakitangaza habari njema kwa Wasamaria’
[Picha katika ukurasa wa 9]
“Mtakuwa mashahidi wangu mimi . . . kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Matendo 1:8, NW.
SAMARIA
YERUSALEMU
YUDEA