Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 10/1 kur. 8-13
  • Tutachagua Tengenezo Jipi—la Yehova au la Shetani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tutachagua Tengenezo Jipi—la Yehova au la Shetani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JINA LAKE NI NINI?
  • Kaa Salama Ukiwa Sehemu ya Tengenezo la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Katika Umoja na Muumba wa Tengenezo la Ulimwengu Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Kuamini Tengenezo lishindalo la Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Tengenezo la Yehova Lenye Kusonga Mbele
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 10/1 kur. 8-13

Tutachagua Tengenezo Jipi—la Yehova au la Shetani?

“Chagueni hivi leo mtakayemtumikia.”​—Yos. 24:15.

1, 2. (a) Leo uchaguzi ni kati ya mambo yapi mawili, nao uhitaji wa kuamua jambo hilo ni wenye uharaka namna gani? (b) Karne kumi na tisa zilizopita, ni uchaguzi wa nani uliohusu matokeo juu ya ulimwengu wote, naye mtu huyo alifanya uchaguzi gani?

LEO uchaguzi ni kati ya matengenezo mawili makubwa zaidi yaliyopo. Kulingana na historia, hilo si jambo jipya, walakini leo uhitaji wa kufanya uchaguzi unaofaa ni jambo la haraka zaidi ya wakati mwingine wo wote. Miaka elfu mbili iliyopita mtu aliyeishi wakati huo, ambaye uchaguzi wake kuhusiana na ulizo hilo ungekuwa na matokeo makubwa sana juu ya ulimwengu wote, alikabiliwa na uhitaji wa kufanya uchaguzi huo.

2 Mashahidi wawili wa jambo hilo la hakika, watu wawili wenye kutafuta mambo ya kweli ya historia, yaani, Mathayo Lawi, aliyekuwa mtoza kodi, na Luka, daktari, wanatupa ushuhuda wa kuthibitisha ukweli wa jambo hilo. Mtu aliyeishi wakati huo ambaye macho ya ulimwengu wote yalikuwa yameelekezwa kwake alikuwa Yesu Kristo wa Mashariki ya Kati. Mathayo Lawi anatuambia kwamba Shetani Ibilisi alimwonyesha “milki zote za ulimwengu, na fahari yake, akamwambia, Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia.” Yesu hakukanusha kwamba tengenezo la ulimwengu lilikuwa la Shetani, walakini bila kusita alikataa kitu hicho alichopewa na Shetani. (Mt. 4:8-10) Yesu alikataa kuliacha tengenezo ambalo tayari alikuwa sehemu yake na hivyo ajifanye kuwa sehemu ya tengenezo la Shetani.

3. Katika Ufunuo uliopewa Yohana, Shetani Ibilisi alifananishwa na nini, nazo sehemu za tengenezo lake ni gani?

3 Mshiriki wa kibinafsi wa Yesu Kristo, yaani, aliyekuwa mvuvi hapo kwanza, Yohana, mwana wa Zebedayo, aliandika kile ambacho sasa kimepangwa kiwe kitabu cha mwisho cha Biblia. Katika kitabu hicho adui, Shetani Ibilisi, anafananishwa na kiumbe ambaye Yohana asingeweza kuwaza kwa akili yake mwenyewe. Kwa hiyo chini ya uongozi wa roho Yohana anamfananisha akiwa “joka kubwa jekundu, alikuwa na vichwa saba na pembe kumi, na juu ya vichwa vyake vilemba saba.” (Ufu. 1:1, 9, 10; 12:3) Kiumbe huyo mwenye maumbo yasiyo ya kawaida anaitwa “yule joka . . . mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani.” Baada ya vita​—ebu waza—katika mbingu zisizoonekana, au makao ya roho, joka huyo wa mfano “akatupwa hata [duniani], na malaika zake wakatupwa pamoja naye.” (Ufu. 12:7-9) Malaika hao wa kishetani waliopigania upande wa Shetani ni sehemu ya tengenezo lake la roho.

4. (a) ‘‘Mnyama” anayetoka baharini, kama anavyosimuliwa katika Ufunuo, sura ya 13, anafananisha nini? (b) Maoni ya ulimwengu wa wanadamu kuhusu “mnyama” huyo ni nini, nao watajulishwa ukweli wapi na namna gani?

4 “Vilevile Shetani Ibilisi ana sehemu ya kibinadamu ya tengenezo lake. Je! sisi ni sehemu yake au tunaliunga mkono? Katika Ufunuo, sura ya 13, linaonyeshwa likiwa mnyama-mwitu anayetoka baharini. Ulimwengu wa wanadamu wanamtendeaje kiumbe huyo wa mfano? Sikiliza: “Yule joka akampa mnyama nguvu zake na kiti chake cha enzi na uwezo mwingi. . . . Dunia yote ikamstaajabia mnyama yule. Wakamsujudu [wakamwabudu, NW] yule joka kwa sababu alimpa huyo mnyama uwezo wake; nao wakamsujudu yule mnyama, wakisema, Ni nani afananaye na mnyama huyu? Tena ni nani awezaye kufanya vita naye?” (Ufu. 13:2-4) Waabudu hao wa sehemu ya kidunia ya tengenezo la Shetani lionekanalo watajulishwa ukweli, maana, kulingana na Ufunuo 19:11-21, Yesu Kristo aliyetukuzwa pamoja na tengenezo la majeshi yake ya kimalaika watapigana na “mnyama” kwenye Har–Magedoni na kumharibu.​—Ufu. 16:14-16.

5. Mpaka vita hiyo kwenye Har–Magedoni ifike, ni taratibu gani ya mambo inayoendelea kuwapo?

5 Mpaka wakati huo ufike, yale ambayo mtume Paulo anazungumza juu yake katika Waefeso 2:2, NW, yanaendelea kuwapo, “taratibu ya mambo ya ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa, roho inayotenda kazi sasa katika wana wa kuasi.” Vilevile, katika 2 Wakorintho 4:4, NW, Paulo anasema kwamba “mungu wa taratibu hii ya mambo amepofusha akili za wasioamini.” Kwa kusudi gani? “Ili mwangaza wa habari njema zenye utukufu juu ya Kristo, ambaye ni mfano wa Mungu usipate kung’aa kwa kupenya.”

6. (a) Kulingana na Waefeso 6:11-18, Wakristo wana lazima ya kupiga vita ya namna gani? (b) Je! hiyo inamaanisha kwamba hakuna sehemu ionekanayo ya tengenezo la Shetani ambayo twapaswa kushindana nayo?

6 Paulo anafunua tengenezo la Ibilisi lionekanalo katika Waefeso 6:12, NW, ambapo twasoma hivi: “Tunako kushindana mweleka, si juu ya damu na nyama, bali juu ya serikali, juu ya mamlaka, juu ya watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho yenye uovu katika mahali pa kimbinguni.” Hapo Paulo hasemi kwamba hakuna sehemu ionekanayo ya kidunia ya tengenezo la Shetani. Yeye anatukumbusha tu kwamba sisi tukiwa Wakristo hatupigani vita ya jeuri juu ya wanadamu waonekanao wa tengenezo la Shetani ili tulipindue. Yesu Kristo, alipokuwa na mwili duniani, hakujaribu kupindua tengenezo la Shetani, nao wafuasi wake hawapaswi kujaribu kufanya hivyo, maana wakifanya jitihada hiyo wangekuwa wakipoteza wakati wao nao wangeshindwa. Wanapaswa kuendelea kupiga vita ya kiroho ili wasifanywe sehemu ya tengenezo la Shetani, na ili wafanye jambo hilo wanahitaji kujichukulia nguo na silaha za vita ambazo Paulo anasimulia katika Waefeso 6:11-18.

7. (a) Ukweli wa kwamba Shetani ana tengenezo unathibitisha nini kuhusu Mungu, na kwa sababu gani? (b) Jambo hilo lilionyeshwa namna gani katika mfano wa Yesu juu ya shamba ambalo liliingiliwa likapandwa na adui ya mpanzi?

7 Hatuwezi kukana kwamba Shetani ana tengenezo lenye nguvu lisiloonekana na lenye kuonekana. Shetani Ibilisi anaigiza kwa kusudi la kudanganya, na ukweli wa kwamba ana tengenezo unathibitisha kwamba mpinzani wake mkuu, Yehova Mungu, ana tengenezo pia. Kwa hiyo Shetani mwenye kuigiza amedanganya umati mkubwa wa watu wafikiri kwamba wanakubali, kufuata na kujiunga na kitu kinachofaa. (2 Kor. 11:13-15) Ili uwe kielelezo cha jambo hilo, fikiria mfano wa Yesu juu ya ngano na magugu. Magugu yalipotokea kwanza yalikuwa yanafanana kabisa na ngano hata kwamba wakati huo wa mapema wa ukuzi ilikuwapo hatari ya kung’oa mimea ya ngano badala ya magugu yaliyopandwa na Ibilisi. (Mt. 13:24-30, 36-43) Yesu alieleza kwamba magugu, yanafananisha “wana wa yule mwovu; yule adui aliyeyapanda ni Ibilisi.”

8. Kulingana na barua ya kwanza ya Yohana na barua ya pili ya Paulo aliyowaandikia Wathesalonike, magugu hayo ya mfano yanafananisha nini?

8 Katika mavuno yanayoendelea sasa wakati wa ‘mwisho wa taratibu hii ya mambo,’ magugu ya mfano ni mpinga Kristo aliyetabiriwa. Katika barua yake ya kwanza, iliyoandikwa karibu na mwisho wa karne ya kwanza, mtume Yohana anaandika, akisema hivi: “Kama vile mlivyosikia kwamba mpinga Kristo yuaja, hata sasa wapinga Kristo wengi wamekwisha kuwapo . . . Huyo ndiye mpinga Kristo, yeye amkanaye Baba na Mwana.” (1 Yohana 2:18, 22) Jambo hilo linapatana na yale ambayo mtume Paulo aliandika karibu miaka 50 mapema kuhusu siku ya Yehova. Yeye alisema hivi: “Haiji, usipokuja kwanza ule ukengeufu; akafunuliwa yule mtu wa kuasi, mwana wa uharibifu.” Bila shaka, Paulo hakuwa anazungumza juu ya mtu halisi, maana aliendelea kusema hivi: “Ile siri ya kuasi hivi sasa inatenda kazi; . . . [kuwapo kwa mtu wa kuasi ni kulingana na] kutenda kwake Shetani, kwa uwezo wote, na ishara na ajabu za uongo; na katika madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea; kwa sababu hawakukubali kuipenda ile kweli, wapate kuokolewa.”​—2 The. 2:3, 7-10.

9. (a) Ni kwa namna gani “siri ya kuasi” ilivyo kazi ya Shetani? (b) Ni kwa namna gani Jumuiya ya Wakristo ilivyo sehemu ya Babeli Mkuu?

9 Kutokana na maneno hayo ni wazi kwamba mpinga Kristo, mtu kafiri wa kuasi, “siri ya kuasi,” ni kitu kilichotokezwa kwa ufundi na Shetani kikiwa ni tengenezo. Ni mwigizo wa Ukristo ulio tengenezo na hivyo ni mpinzani wake. Ukiwa unachukua mahali pa Ukristo wa kweli ulio tengenezo, unaonekana kwa namna ya Jumuiya ya Wakristo ya kisasa, jina hilo likiwa linamaanisha milki ya Ukristo. Kwa hakika hilo ni jina la kudanganya, maana Jumuiya ya Wakristo ndio sehemu yenye nguvu zaidi ya Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, chini ya utawala wa Shetani Ibilisi.

10. Kwa msaada wa maneno ya Yohana na Paulo, kwelI kweli Jumuiya ya Wakristo ni nini leo, na kila tengenezo lililo mshiriki wake linadai kuwa nini?

10 Kwa msaada wa yale ambayo mitume Paulo na Yohana walisema, Jumuiya ya Wakristo ni ukengeufu kutoka kwa kundi la kwanza la kweli la Yesu Kristo, kwa kweli ni uasi wa kidini wake. Tofauti na kundi la Kikristo la karne ya kwanza, leo Jumuiya ya Wakristo ina matengenezo ya kimadhehebu zaidi ya elfu moja, kila moja likiwa linadai kuwa la Kikristo, wonyesho wa Ukristo wa Biblia.

JINA LAKE NI NINI?

11. Karibu karne moja iliyopita, wachapaji wa gazeti Mnara wa Mlinzi walichagua waitwe kwa jina gani?

11 Kuhusu matengenezo hayo ya kidini yaliyogawanyika ambayo yanafanyiza Jumuiya ya Wakristo, toleo la gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Februari wa 1884 (karibu karne moja iliyopita) lilisema maneno yafuatayo chini ya kichwa “Jina Letu”:

Wasomaji wapya katika sehemu zote za nchi sikuzote wanauliza: Mnajiita jina gani? Je! ninyi ni ‘Wabaptisti Halisi’ (waamini wa ubatizo wa maji)? Je! ninyi ni ‘Wamisionari Wabaptisti’? Je! ninyi ni ‘Wayunivaseli’ (waaminio walimwengu wote wataokolewa)? Je! ninyi ni ‘Waadventisti’ (waaminio kuja kwa pili kwa Kristo)? Je! ninyi ni ‘Wamethodisti Halisi’ (waaminio wokovu kwa wote)? n.k., n.k. Mara kadha wa kadha tumejaribu kuonyesha msimamo wetu wazi-wazi, na sasa twajaribu kufanya hivyo kwa maneno machache.

“Sisi si sehemu ya tengenezo lo lote la kidunia; hivyo, madhehebu yote yakitajwa, tutajibu, Sivyo, kwa yote. Tunashikamana na tengenezo la kimbinguni tu—‘ambao majina yao yameandikwa mbinguni.’ (Ebr. 12:23, NW; Luka 10:20.) Watakatifu wote wanaoishi sasa, au ambao wameishi wakati wa kizazi hiki, walikuwa wa tengenezo la kanisa letu: wote hao ni Kanisa moja, na hakuna jingine linalokubaliwa na Bwana. Basi tengenezo lo lote la kidunia linalojiingiza katika umoja huo hata kidogo linapingana na mafundisho ya Maandiko nalo linapingana na mapenzi ya Bwana—‘ili wawe na UMOJA.’ (Yohana 17:11)”

12. Likionyesha kwamba washiriki wa kundi la Kikristo waliobatizwa ni sehemu ya tengenezo la Mungu, toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Machi 1883 lilisema nini?

12 Likionyesha kwamba washiriki safi, waliobatizwa wa kanisa lililozaliwa kwa roho, au kundi, wana umoja na sehemu isiyoonekana ya kimbinguni ya tengenezo la Mungu, toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Machi wa 1883, ukurasa wa 6, lilisema yafuatayo:

“Lakini, ingawa haiwezekani kwa mtu wa asili kuliona tengenezo letu, kwa sababu hawezi kufahamu mambo ya Roho ya Mungu, twatumaini kwamba mnaweza kuona kwamba Kanisa la kweli ni tengenezo linalofaa kabisa, nalo lina utaratibu unaofaa kabisa wa kutenda. . . .

“Kwa kutambua tengenezo hili, ambalo ni la Roho, na kutotaka kuungana vyo vyote na ulimwengu, ni nani asiyeweza kuliona na kulifahamu, tuko tayari kuchukua suto la watu walio tofauti. . . .

“Tunamwamini sana Nahodha wetu; nalo tengenezo hili kamilifu, lisiloonekana na ulimwengu, linapiga hatua kufikia ushindi wa kweli na wa utukufu.”

13. (a) Katika mwaka 1904 Sosaiti ilichapisha kitabu kipi, nao msingi wa kichwa chake ulikuwa maandiko gani? (b) Kichwa cha Funzo la Nne la kitabu hicho kilikuwa gani, na sehemu yake ilisema nini?

13 Katika mwaka 1904 Sosaiti ilichapisha kitabu chenye kichwa “Kiumbe Kipya” (Kiingereza). Kichwa cha kitabu hicho kilikuwa na msingi wa maandiko ya Biblia yafuatayo: “Basi mtu ye yote akiwa ndani ya Kristo, yeye ni kiumbe kipya: vitu vya kale vimepita; tazama, vitu vyote vimekuwa vipya.” (2 Kor. 5:17, Authorized Version) “Maana katika Kristo Yesu kutahiriwa hakufai kitu, wala kutotahiriwa, ila kiumbe kipya.” (Gal. 6:15, AV) Funzo la Nne la Kitabu cha 6 katika Studies in the Scriptures, ukurasa 195, linaanza kwa kusema hivi: “Kwa kuwa Kiumbe Kipya hakitafikia ukamilifu au kumalizika kwake mpaka wakati wa Ufufuo wa Kwanza, tengenezo lake halitakamilishwa mpaka tu wakati huo utakapofika. Hesabu ya hekalu inaonyesha jambo hilo: sasa tunaitwa tukiwa mawe yaliyo hai, au tunaalikwa kwenye mahali pengi katika hekalu tukufu, na, kama Mtume anavyoeleza (1 Pet. 2:5), tunakuja kwa Yesu, ambaye, akiwa wakili wa Baba, anaunda, anachonga, anaweka mahali pake na kupiga sulu (kung’arisha) mahali pengi katika Hekalu tukufu la wakati ujao—mahali pa kukutania kati ya Mungu na ulimwengu.” Kwa kufaa, kichwa cha Funzo au Sura ya Nne ni “Tengenezo la Kiumbe Kipya.”

14. (a) Mambo yaliyoonwa wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza yaliwahusuje wale waliokuwa wametoka Babeli Mkuu na wakashirikiana na Sosaiti? (b) Ni usemi gani unaohusiana na mazungumzo haya uliopata kuwa jambo kuu?

14 Habari hiyo inayotangulia inaonyesha watu waliokuwa wametoka Babeli Mkuu na wakashirikiana na Sosaiti maoni waliyokuwa nayo kabla ya Vita ya Ulimwengu ya 1914 kuanza. Baada ya kupatwa na magumu katika pambano hilo la ulimwengu, washiriki washikamanifu wa “kiumbe kipya” cha Mungu walijikuta wanapingana zaidi kuliko hapo mbele na Babeli Mkuu. Ufahamu wao wa kiroho kuhusu unabii mwingi wa Biblia ambao ungetimizwa karibuni tangu 1914 ukawa wazi zaidi. Kusanyiko lililofuata baada ya vita hiyo kuu lilifanywa huko Cedar Point, Ohio, U.S.A., Septemba 1-8, 1919, nao wakaanza kufahamu sehemu za kazi ya Mungu ambayo ilikuwa ingali mbele. Usemi “tengenezo la Mungu” ukawa jambo kuu!

15. (a) Wakati wa kusanyiko la pili la Cedar Point, hotuba kuu ya “Siku Yenyewe” ilihusu unabii gani hasa? (b) Katika hotuba hiyo, ni matengenezo gani yenye kupingana yaliyotofautishwa?

15 Katika Septemba wa 1922 kusanyiko la pili lilifanywa huko Cedar Point, Ohio. Siku ya Ijumaa, Septemba 8, ambayo ilikuwa imepangwa kuwa “Siku Yenyewe,” J. F. Rutherford, ambaye wakati huo alikuwa msimamizi wa Sosaiti, alitoa hotuba yake yenye kutokeza sana ambayo msingi wake ni Mathayo 4:17 (UV), “Ufalme wa mbinguni umekaribia.” Alizungumza kwa urefu juu ya unabii wa Isaya, sura ya 6, kuhusu matumizi yake ya kisasa. Maneno yake yenye kutaja tengenezo hilo adui yanastahili kuchapishwa tena:

“Yehova, mtawala mkuu wa ulimwengu wote, ambaye utawala wote ni wake kwa haki, alipanga jamii ya kibinadamu ikombolewe tena na kuokolewa naye akafanya taifa la Israeli liwe tengenezo lenye kufananisha jambo hilo. Kupitia kwa taifa hilo alifanya dini ya kweli iwe tengenezo, akatoa amri kwamba wanapaswa kumwabudu yeye akiwa Mungu wa pekee wa kweli. Shetani, mpinzani, Mungu wa kuigiza, alifanya watu waliokuwa wanazunguka Israeli wawe tengenezo la dini ya uongo, naye akawafanya wamwabudu yeye na maibilisi wengine. Nguvu inayotumiwa na Yehova juu ya watu wake ni roho takatifu. Kifungo kinachofunganisha Shetani na wafuasi wake ni roho mbovu. Kwa sababu ya kushindwa na hila zake Israeli walishindwa naye. Mungu alitoa amri juu ya taifa hilo, naye akafikiliza amri hiyo mwaka 606 K.W.K.; na hapo Shetani akawa mungu wa ulimwengu huu. Vilevile yeye anaitwa mkuu wa uwezo wa hewa, hivyo kuonyesha tengenezo lake lisiloonekana na lenye kuonekana. . . .

“Wakuu wa kifedha na watawala wenye nguvu wa dunia walikusanyika Paris kwa mkutano wa kufanya amani, na viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wa kudai wakiwa pamoja nao; nayo matokeo yake yakawa ni kutokeza Ushirika wa Mataifa, kitu cha mwisho cha Ibilisi cha kuchukua mahali pa ufalme wa Masihi. Jumuiya ya Wakristo ya kujidai sasa ilikuwa inashirikiana na matengenezo makubwa ya kibiashara na ya kisiasa, na pia ilijivunia jambo hilo; nalo kanisa la kudai (ambalo sasa ni sehemu ya tengenezo la ibilisi, likiwa halina kibali cha kutumika katika daraka la ukuhani) likajitokeza kuchoma uvumba. . . .

“. . . Walakini je! viongozi hao wa kidini na makundi yao yanayounga mkono tengenezo la ibilisi watasikia? Nabii wa Bwana anajibu hivi: ‘Kusikia watasikia hakika, bali hawatafahamu. . .

16. Msemaji alimalizia hotuba yake yenye kichwa Ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo kwa kutoa ombi gani?

16 Kulingana na andiko ambalo alitoa kichwa chake cha habari juu ya ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo, J. F. Rutherford alimalizia hotuba yake yenye kuchochea kwa kusema hivi:

“Utangazeni ujumbe kote kote. Lazima ulimwengu ujue kwamba Yehova ni Mungu na kwamba Yesu Kristo ni Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana. Hii ndiyo siku ya siku zote. Tazameni, Mfalme atawala! Ninyi ndio mawakili wa kumtangaza. Kwa hiyo mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.”​—Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), Novemba 1, 1922, kurasa 331-337.

17. Kwa sababu ya “utaratibu wa shambani” mzuri tangu 1922, kumetokea nini lijapokuwapo ongezeko la idadi ya watu tangu wakati huo, na hivyo Mashahidi wa Yehova wametoa ushahidi juu ya nini?

17 Katika toleo lake la Desemba 15,1922, chini ya kichwa kidogo “Utaratibu wa shambani,” Mnara wa Mlinzi ulisema hivi katika ripoti yake ya kila mwaka: “Njia bora ambayo yapasa kutolewa kwa ushuhuda ulio wa lazima inategemea sana jitihada za utaratibu zinazofanywa shambani.” (Ukurasa 389) Tangu mwaka huo wa mapema uliofuata vita kuu (1922) idadi ya watu ulimwenguni imeongezewa wakaaji wa dunia elfu mbili milioni. Watangazaji wa Mfalme wa Yehova aliyewekwa wameongezeka pia. Kwa msaada wa ushuhuda mzuri ambao wametoa kufika sasa, mashahidi walio wakf na kubatizwa wa Yehova wametoa ushahidi usiofutika juu ya msimamo wao kuhusiana na ulizo la wakati huu, “Tutachagua tengenezo jipi, la Yehova au la Shetani?”

[Picha katika ukurasa wa 9]

Yesu Kristo aliyetukuzwa, pamoja na tengenezo lake la majeshi ya kimalaika, ataharibu “mnyama” kwenye Har–Magedoni

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki