Maswali kutoka kwa Wasomaji
● Je! lingekuwa kosa kwa Mkristo kutumia vidude vyenye kugongana na kutokeza mlio mzuri kama wa kengele vinapovumishwa na upepo ndani ya nyumba yake?
Watu wengi wametumia vidude vya namna hiyo kufanya nyumba yao iwe na milio mizuri ya kimuziki. Upepo unapovuma, vile vitu vya kioo, chuma au mbao vinagongana na kutokeza mlio. Walakini, katika nchi fulani kuna desturi ya kuweka vidude vya namna hiyo kwa wazo la kwamba vitazuia pepo waovu (mashetani) wasiingie ndani ya nyumba. Ni wazi kwamba Mkristo asingetumia vidude hivyo kwa kusudi hilo. Kwa hiyo ikiwa nchi au mtaa ambamo mtu anakaa ina imani ya ushirikina, lisingekuwa jambo la hekima kuwa na vidude hivyo ndani ya nyumba. Kwa njia hiyo hakuna mtu atakayekwazwa wala kuwa na maoni ya kwamba Mashahidi wa Yehova wanatumia vidude vyenye kugonganishwa na upepo kwa kusudi lisilopatana na Maandiko.—1 Wakorintho 10:31-33.
Walakini, ikiwa kusudi la mtu la kuweka vidude hivyo nyumbani halihusiani hata kidogo na dini ya uongo, ushirikina wala ushetani, na havitaelekea sana kuwapa wengine maoni mabaya juu ya namna vinavyotumiwa nyumbani, hili ni jambo rahisi la kuamuliwa na mtu binafsi.