Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 11/1 kur. 3-7
  • Sala ya Mfungwa llijibiwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sala ya Mfungwa llijibiwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAISHA YA HAPO KWANZA NA MAVUTANO YALIYONIPATA
  • KUWAPATA WATU WA YEHOVA
  • KUJITAYARISHA KUWA WAKRISTO WA KWELI
  • KUENDELEA KUWA WENYE SHUGHULI KATIKA UTUMISHI WA YEHOVA
  • KUMTANGULIZA YEHOVA
  • KULEA WATOTO WETU
  • KUFURAHIA MAPENDELEO YA UTUMISHI
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Vita Haikukomesha Kazi Yetu ya Kuhubiri
    Amkeni!—2001
  • Kumtumikia Mungu Nyakati za Magumu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 11/1 kur. 3-7

Sala ya Mfungwa llijibiwa

Kama llivyosimuliwa na Isaac V. Espeleta

MWAKA wa 1945, wakati majeshi ya Amerika yalipokuwa yamekwisha kuvijia Visiwa vya Ufilipino na kuvishambulia, mimi na wenzangu 11 tulikamatwa na Wajapani. Tulifungiwa katika vijumba vya gereza vya mabati vyenye ukubwa unaolingana na vibanda vidogo vya kufungia mbwa. Wakati wa mchana, vilitutoa jasho jingi ajabu, na usiku, vikatugandisha kwa baridi ya ajabu.

Baadaye wenzangu waliulizwa-ulizwa maswali kisha wakauawa wote. Ingawa mimi niliulizwa maswali mengi sana muda wa siku 45 na kuteswa-teswa mara tatu, sikukubali kwamba makosa niliyoshtakiwa yalikuwa ya kweli. Nilikuwa nimejionea kwamba kama mtu aliteswa-teswa kisha akakubali makosa yake, alichapwa risasi papo hapo au akauawa kwa kuchomwa jisu kubwa linalokuwa limeunganishwa na bunduki. Basi, mimi nilijaribu kujiponyoa kwa kuvumilia kuteswa-teswa.

Mumo humo, ndani ya kijumba hicho kidogo cha gereza, nilimpelekea Yehova Mungu sala nikaahidi kwamba, nikiweza kuepuka kifo, ningemtafuta yeye na kutumia maisha yangu yote nikimtumikia. Lakini kabla sijasema mengi zaidi juu ya nilivyomtafuta Yehova, acha nieleze sababu ya kufungwa kwangu na kilichonifanya nimpe Yehova ahadi hiyo.

MAISHA YA HAPO KWANZA NA MAVUTANO YALIYONIPATA

Jamaa yetu ilikuwa ya Wakatoliki na tuliishi katika mji mdogo wa Biñan, karibu kilomita 30 (maili 19) kusini mwa Manila. Mtu aliyekuwa na mavutano makubwa katika maisha yangu ya ujana alikuwa babu wa upande wa baba. Alikuwa ameacha kupendezwa na Kanisa Katoliki na badala yake akapendezwa na Biblia. Yeye aliniwekea msingi wa kufuata mazoea mazuri ya kuyasoma Maandiko, nami nitazidi kupiga asante nyakati zote kwa sababu ya yeye kunisaidia hivyo.

Nilipozidi kupata umri mkubwa, kiu yangu ya kusoma iliongezeka sana. Wakati vita ya ulimwengu ya pili ilipovifyatukia Visiwa vya Ufilipino, vifaa vya kusoma katika Kiingereza vilikosekana kabisa. Halafu, siku moja, nikaona nakala ya kitabu Riches bila kutazamia, kitabu kilichopigwa chapa na Sosaiti. Lo! furaha, mwishowe sasa nilikuwa na kitu cha kusoma! Kitabu hicho kilikuwa na habari za kufurahisha sana.

Lililonivutia zaidi ni kwamba Mungu ana jina la kibinafsi, Yehova. Nililiangalia jina hilo katika Biblia ambayo nilikuwa nimepewa na babu. Ndiyo, lilikuwamo. Hakika jina la Mungu lilikuwa Yehova. (Kutoka 6:3; Zaburi 83:18) Walakini, vita ilinizuia kuendeleza maarifa mapya niliyokuwa nimepata.

Miaka kadha kabla ya hapo nilikuwa nimeoa, yaani, katika mwaka wa 1936. Kuufikia wakati huo wa vita nilikuwa nimekwisha kuwa na watoto watatu wadogo wa kulisha. Nikawa nikisafiri kwenda Luzon ya kusini nikanunue miti ya mbao za ufundi na ya kutumia kama kuni. Hiyo ikawa ni sehemu moja ya kazi yangu ya kimwili. Huko katika misitu nilikokwenda walikuwa wakijificha watu wenye kupinga ukaaji wa Wajapani katika nchi yao. Wakaniandika niwe mtu wao wa kuwaenezea vitabu, na wakati wa vita hiyo nikawa mpeleka-habari wa siri.

Mwaka Wa 1945, Wajapani walitia mashaka juu ya kazi yangu ya siri wakanikamata. Uzuri ni kwamba kabla ya hapo tulikuwa tumekwisha kuharibu vitabu vyenye kufundisha mambo ya mapinduzi. Lakini wakati wa zile saa nilizokaa peke yangu katika kile kijumba cha gerezani, akili yangu ilizidi kumrudia yule Mungu niliyekuwa nimesoma habari zake—Yehova.

Basi ikawa kwamba Wajapani walishindwa kupata uthibitisho halisi kwamba mimi ni mwenye hatia. Waliniachilia, na moja kwa moja nikawaunga mkono Waamerika katika shughuli yao ya upinzani. Lakini niliumia tena mikononi mwa Waamerika waliponishuku kwamba mimi nilikuwa mpelelezi wa Wajapani! Walakini, kukaa kwa Wajapani katika Visiwa vya Ufilipino kulikoma, basi shauku yangu ya utukuzo wa kitaifa ikakoma, pia. Hata hivyo, sikuisahau ahadi niliyokuwa nimemtolea Mungu. Moja kwa moja nikaanza kumtafuta Yehova.

KUWAPATA WATU WA YEHOVA

Mimi na Pablo Quiohilag, aliyekuwa rafiki yangu tangu utotoni, tulitembelea makanisa mbalimbali, lakini hakuna hata moja lililoelekea kuwa na ujumbe unaofaa. Halafu, siku moja nikasikia mtu fulani akimhubiri Yehova. Nikamkaribisha kwenye uwanja wa nyumba yangu katika Biñan nikamwambia ahubiri hapo saa nyingi kama alivyotaka.

Mwaka wa 1947, mmoja wetu akasikia mtu mwingine pia akimhubiri Yehova. Safari hii alikuwa ni mmisionari Mkanada Vic White, mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alikuja kusema na sisi tuliokuwapo nami nikachaguliwa nimtafsirie atakayosema. Tukapata kujua kwamba yule mtu aliyekuwa amekuja kuhubiri katika Uwanja wa nyumba yangu hakuwa tena mmoja wa Mashahidi wa Yehova, bali alikuwa ametengwa na ushirika kabla ya vita. Habari hizo zilitugutusha tukafikia hatua ya kuamua ni jambo gani tutakalofanya.

Karibu na wakati huo tulipata habari za kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova ambalo ndilo lingekuwa la kwanza kufanyiwa Manila baada ya vita. Mimi nilihudhuria naye Vic White akanijulisha kwa mwangalizi wa tawi, Earl K. Stewart. Baadaye, kwenye afisi ya tawi, yeye alitueleza tungepaswa kufanya nini ndipo tuwe Mashahidi wa Yehova. Ni wazi kwamba moja la mambo tuliyopaswa kufanya ni kutimiza daraka la Mkristo la kushiriki katika utendaji wa kuhubiri nyumba kwa nyumba. Niliporudi Biñan, mimi na wenzangu wote tuliacha kushirikiana na yule mtu aliyetengwa na ushirika kisha tukaamua kuanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova.

KUJITAYARISHA KUWA WAKRISTO WA KWELI

Ndipo Kundi la Biñan lilipozaliwa. Lakini yalikuwako maulizo mengi ya kujibiwa. Kwa mfano, washiriki walio wengi wa kikundi chetu, waliopata watu 15 wakati huo, walikuwa wamebatizwa na yule mtu aliyetengwa na ushirika aliyekuwa akituhubiri. Sasa tukajiuliza: “Je! tubatizwe tena, au namna gani?” Wengine waliwaza kwamba hatukupaswa kufanya hivyo, kwa maana Biblia inataja “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja.” (Waefeso 4:5) Sisi tulikuwa tumekwisha kubatizwa mara moja, basi tukajiuliza sababu gani kubatizwe tena? Lakini mimi niliwaza nikaona kwamba “ubatizo mmoja” unaotajwa unapasa kabisa ufanywe kwa kushirikiana na ile “imani moja.” Kwa kuwa sasa tulikuwa tumeipata imani iliyo ya kweli, ilitupasa tubatizwe upya kwa kushirikiana na wale walioishika imani hiyo. Ndivyo tulivyofanya.

Sasa ikawa lazima tupambane na tatizo la kuhubiri nyumba kwa nyumba. Tungeanzaje? Hakuna mmoja wetu aliyejua. Basi Paulo Quiohilag na mimi tukaenda pamoja mlango kwa mlango. Kabla ya kufikia kila nyumba, tukawa tukitupa juu sarafu (peni moja au shilingi na kadhalika) na kuiacha ianguke. Ilipoanguka ikiwa imetazama upande ambao haukuchaguliwa na yule mwingine, huyo ndiye aliyepaswa kuhubiri nyumba hiyo! Hata nashindwa kukumbuka tulihubiri kwa kusema nini, lakini kwa uhakika Yehova alituongoza tumsifu mbele ya watu wengi tujapokuwa na ujuzi mdogo sana.

Mwishowe, ndugu wawili wenye ujuzi kutoka Betheli, kina Salvador Liwag na Vic Amores, wakatumwa waje kutusaidia. Walituonyesha namna ya kuwapa watu ushuhuda na kuongoza mikutano. Mimi nikaanza kuuhudhuria mkutano wa utumishi wa kundi la Santa Ana mjini Manila siku za Alhamisi, ili nipate ujuzi wa kuendesha kipindi icho hicho kwa njia nzuri zaidi kwenye kikundi chetu kidogo kilichokutana siku za Ijumaa.

KUENDELEA KUWA WENYE SHUGHULI KATIKA UTUMISHI WA YEHOVA

Hivi majuzi, tulipokuwa tukielekea kwenye kusanyiko la wilaya, mke wangu alisema hivi kwa ghafula: “Tuliwezaje kutimiza jambo hilo?”

“Kutimiza jambo gani?” nikamwuliza.

“Unakumbuka kwamba eneo lote hili kuanzia Sucat, Muntinlupa, katika Rizal mpaka Cabuyao katika Laguna [kilomita karibu 40 (maili 25)] lilikuwa eneo letu Ia mahubiri?”

Miaka hiyo ya zamani hatukuwa na gari. Tulikuwa tukitembea kutwa nyingi tukitafuta wenye kupendezwa. Nyakati nyingine tulisafiri tukiwa na taa ya mafuta ili tuitumie kuongoza funzo la Mnara wa Mlinzi na kufanya mkutano wa watu wote giza lilipoingia.

“Siku hizi sina uwezo wa kufanya hivyo,” akasema mke wangu.

Labda hiyo ni kweli, kwa maana sasa yeye anaugua ugonjwa wa kufura na kuuma kwa vifundo vya mifupa kunakozidi kuumiza mtu kadiri wakati upitavyo. Lakini tulipokuwa na nguvu za ujana, tulizitumia katika utumishi wa Yehova. Miaka hiyo ya zamani mimi nilikuwa nikiamka saa 10 alfajiri na mapema siku sita kwa juma ili nifike kazini mjini Manila kabla ya saa mbili ya asubuhi. Saa za usiku nilikuwa nikitoka kazini na kuelekea moja kwa moja kwenye mafunzo yangu ya Biblia. Nyakati nyingine nilifanya hivyo kwa kutembea kilomita 16 (maili 10) niweze kufikia nyumba ya mwenye kupendezwa kisha kilomita nyingine 16 za kurudi nyumbani. Majira ya mvua, mimi nilikuwa nikifika nyumbani saa 7 ya usiku mara nyingi mwili wangu ukiwa umelowanishwa na mvua, halafu baada ya kulala saa tatu tu naamka niende kazini.

Wakati uo huo, pia, nilipata pendeleo la kulitafsiri gazeti Watchtower katika kilugha cha kwetu, yaani, Kitagalogi. Ni kama vile mke wangu alivyouliza, “Tuliwezaje kutimiza jambo hilo?” Iliwezekana kwa kusaidiwa na Yehova, ama sivyo isingaliwezekana. (Wafilipi 4:13) Lakini ni baraka ‘kuzidi sana kutenda kazi ya Bwana.’​—1 Wakorintho 15:58.

KUMTANGULIZA YEHOVA

Nyakati nyingine, kumtanguliza Yehova maishani mwetu kulihusu kujinyima mambo fulani, lakini hatukupata hasara. Vita ilipokwisha nyumba yetu katika Biñan ilibaki ikiwa kijumba ovyo tu. Basi tukaweka akiba ya fedha tuweze kuwa na nyumba nzuri zaidi, na mwishowe tukawa tumekusanya peso 500 (karibu shilingi 2,500 kwa kulinganisha na fedha za siku hizo). Lakini ndipo mazungumzo yalipotokea ikaonekana kwamba Jumba la Ufalme lenye kufaa lilihitajiwa. Ikaelekea kuwa kwamba ni kama mimi pekee niliyekuwa na fedha. Basi nikamwambia Ndugu Jose Nava hivi: “Nenda kamwambie mke wangu akupe zile peso 500.” Akapewa fedha hizo na mke wangu bila malalamiko nasi tukajenga Kijumba cha Ufalme kizuri.

Hata hivyo, muda mfupi baadaye Yehova alituwezesha kuijenga nyumba yetu, nasi tukaishi humo kwa starehe mpaka mwaka wa 1954. Hapo ndipo ilipoharibiwa na mchwa hata ikahitaji kutengenezwa. Muda mfupi tu baada ya kupanga kuitengeneza ikawa wazi kwamba kile Kijumba cha Ufalme cha zamani hakikuwa tena na nafasi ya kulitosha kundi lenye kuendelea kupanuka. Kwa mara nyingine tena, mke wangu akatoa fedha zote tulizokuwa tumeweka akiba bila kulalamika, nasi tukazitoa zitumiwe kujenga jumba jipya kando ya barabara kuu ya mji. Walakini, kwa mara nyingine Yehova alituwezesha upesi kuijenga upya nyumba yetu. Hatukupata hasara kwa sababu ya kumtanguliza (kumweka kwanza).​—Mathayo 6:33.

Miaka kadha baadaye, nilipokuwa nimejishughulisha sana na ujenzi wa Jumba la Ufalme la tatu, mke wangu aliniambia: “Unapenda sana kujifurahisha na mambo yanayokuingiza katika gharama kubwa sana. Sina habari juu ya mtu mwenye kufanya kama wewe.”

“Mambo gani?” nikamwuliza.

“Kujenga Majumba ya Ufalme,” akasema, akichekelea kwa furaha.

KULEA WATOTO WETU

Wakati mwana wetu wa mwisho alipozaliwa mwaka wa 1956, tulikuwa tumekwisha kupata wavulana wanne na wasichana sita. Walipokuwa wadogo, nyakati zote tulilizungumza andiko la siku la Biblia pamoja nao. Pia tukaona uhitaji wa kuwa na funzo la kawaida la jamaa. Vilevile, tulikuwa tukienda katika utumishi wa shambani tukiwa jamaa nzima. Tulijitahidi kwa nguvu zetu zote tulee watoto wetu katika “ile nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.”​—Waefeso 6:4, NW.

Matatizo makubwa yalitufikia. Lakinj tulipata baraka nyingi! Watoto wetu wote walipainia nyakati mbali mbali, wakatumikia wakiwa watangazaji wa Ufalme wa wakati wote. Binti yangu aliye mkubwa zaidi alitumikia pamoja na wafanya kazi wa huko Betheli miaka kadha kabla hajaolewa na kuwa na jamaa yake. Wasichana wetu watatu wa kwanza walikuwa kati ya mapainia wa pekee wa kwanza katika Visiwa vya Ufilipino, na mmoja amekuwa akitumikia kwa uaminifu muda wa miaka mingi akiwa mmisionari nchini Thailand. Watoto wetu wote, kasoro mmoja, wamesimama imara katika imani.

Binti yangu aliye wa pili kwa ukubwa alipokea mgawo wake wa kwanza wa kuwa painia wa pekee alipokuwa na umri wa miaka 17. Alipokwisha kuondoka nyumbani akaanze mgawo huo, alituandikia barua ambayo ninapoikumbuka machozi yanajaa machoni kila mara. Alisema kwamba alipokuwa mdogo alinihesabu mimi kuwa baba aliye mkatili zaidi ya mababa wote. Lakini sasa alijua kwamba kama sisi wazazi wake tusingalisimama imara kumtia nidhamu (mazoezi ya adabu), hata siku moja asingalifurahia pendeleo zuri sana la utumishi wa painia wa pekee (ambalo baadaye lilifanya apewe mgawo wa umisionari katika nchi ya mbali). Kwa hiyo, sisi wazazi Wakristo tusiwanyime watoto wetu nidhamu. (Mithali 22:6) Wanaihitaji, na katika miaka itakayofuata watakuja kuithamini.

KUFURAHIA MAPENDELEO YA UTUMISHI

Mimi nimefurahia mapendeleo mengi kwa kushirikiana na watu wa Yehova. Kwa mfano, nilipendelewa kupanga mambo ya vyakula kwenye makusanyiko ya kwanza-kwanza katika Visiwa vya Ufilipino. Kwa muda wa miaka mingi, mimi nilipata pendeleo zuri la kulitafsiri gazeti The Watchtower katika kilugha changu mwenyewe. Tena, sisi tumekuwa tukikitazama kile kikundi kidogo cha watu 15 kikiongezeka na kuwa makundi makubwa 11 yenye kusitawi sana.

Pendeleo jingine lilinifikisha ndani ya Gereza la Taifa la Kurekebishia Tabia za Watu, karibu na nyumbani kwangu. Mara kwa mara, wafungwa wa huko wanaiandikia Sosaiti, wakitaka msaada wa kiroho. Mara nyingi barua wanazoandika zinaletwa kwangu, na tangu mwaka wa 1947 mimi nimekuwa nikiwaongoza wafungwa wenye kupendezwa wajifunze Biblia kwa ukawaida. Hivyo, muda wa miaka hiyo, watu karibu 50 wamesimama upande wa Yehova na wakabatizwa wakiwa wangali gerezani. Nilikutana na 23 kati yao kwenye kusanyiko moja la wilaya. Walipofunguliwa, wengine wao wakawa mapainia, na vilevile waangalizi wenye kusafiri, na sasa wengi wanatumikia wakiwa wazee.

Mtu mmoja ambaye sikutazamia kamwe kumkuta gerezani ni yule mtu aliyetengwa na ushirika ambaye ndiye aliyekuwa wa kwanza kunihubiri mimi habari za Yehova. Alikuwa amekamatwa kwa shtaka la kujiunga na Wajapani kuipinga nchi yake. (Baadaye, alisamehewa kisha akaachiliwa.) Alipokuwa gerezani, alihudhuria mikutano niliyokuwa nikiongoza huko akiwa mnyenyekevu. Miaka mingi baadaye, katika mwaka wa 1975, mimi nilikuwa mmoja wa halmashauri ya hukumu iliyofikiria ombi lake la kurudishwa. Basi, baada ya miaka karibu 40 ya kuwa katika hali ya kutengwa na ushirika, aliweza kwa mara nyingine kushirikiana na watu wa Mungu kwa uhuru.

Muda wa miaka yote hiyo, mke wangu amenisaidia kweli kweli—akawa mwunga-mkono mshikamanifu katika utumishi wa Mungu. Sasa sisi wawili tunaweza kutazama nyuma na kuona kwamba tumemtumikia Yehova kwa muda wa miongo inayozidi mitatu (miaka zaidi ya 30). Kwa kuwa mimi nilimtafuta Yehova nikampata, ninaendelea kuitimiza ile ahadi niliyoifanya miaka mingi iliyopita nikiwa katika kambi ya gereza la Wajapani. Napiga asante kubwa sana kwa kumpata Yehova Mungu wakati wa miaka yenye matokeo mazuri sana maishani mwangu na kwa kuweza kuitumia katika utumishi wake!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki