Msiba Unapotokea
KWA wazi jamaa hiyo haikuwa na mali nyingi. Hata hivyo walikuwa na vitu vingi sana walivyopaswa kuwa na shukrani kwa ajili yavyo. Shamba lao lilikuwa linazaa, hali ya hewa ilikuwa yenye joto la kutosha katika sehemu kubwa ya mwaka, nao walikuwa na mahali pazuri.
Mji wao wa Naini ulikuwa katika mahali penye kupendeza katika nchi tambarare yenye rutuba ya Esdraeloni kwenye upande wa kaskazini-magharibi wa Kilima cha More. Ikiwa nyumbani mwao jamaa hiyo ingeweza kutupa macho juu ya bonde enye majani ya chanikiwiti na kuona vilima vyenye misitu mizuri vya Galilaya vikiwa umbali wa maili chache tu. Na, kwa kuinuka juu sana kule-e-e mbali kilionekana kilele chenye kufunikwa na theluji cha Mlima Hermoni na milima ya Lebanoni. Ilipendeza kama nini mwishoni mwa siku kuketi nje juu ya nyumba na kuangalia mandhari hiyo—wakiwa wao watatu tu—mwanamume huyo, mkewe na mwana wao mchanga!
Halafu siku moja msiba ukatokea—mwanamume huyo akafa. Lilikuwa jambo lenye kuhuzunisha kama nini! Sasa jioni zile zenye utulivu walizokuwa pamoja hazingekuwapo tena. Hata hivyo, mwanamke huyo akafarijiwa na uhakika wa kwamba alikuwa angali na mwanawe. Matumaini, tamaa na matazamio yake yakawa yanategemea wakati ujao wa mwana huyo. Kwa njia hiyo akapata tena maana na kusudi maishani.
Lakini kwa mara nyingine msiba ukatokea. Mwana huyo akafa. Sasa hakuwapo mtu ambaye angejipatia faraja kwake. Huzuni ya mjane huyo ilikuwa nyingi huku maiti ya mwanawe ikiwa inatayarishwa ikazikwe.
Pengine unafahamiana na maono ya ndani ya kuachwa upweke yanayoletwa na kifo cha mpendwa. Unaweza kushuka moyo na kujiona hoi kama nini! Hakika kifo ni adui mwenye kuleta uchungu. Katika pindi hizo, mtu anahangaikia sana wakati ujao wa waliokufa. Je! kweli kweli wana tumaini?
Ebu waza, kama mtu angekuja atwae mkono wa mpendwa wako na amrudishe kwako akiwa hai na mwenye afya tena. Ungekuwa mwenye furaha kama nini! Lingekuwa jambo zuri ajabu!
‘Lakini hiyo haiwezekani,’ huenda ukasema. Ni kweli kwamba jambo hilo halijapata kutokea katika maisha yetu. Hata hivyo limepata kutokea hapo mbeleni. Wanawake wamewapata tena watu wao waliokufa kupitia ufufuo.
Jambo hilo lilitokea wakati gani? Sababu gani twaweza kuliamini? Linamaanisha nini kwetu leo?