Neno la Mungu Li Hai
Kwa nini Mungu aliumba dunia yetu?
SIKU moja Mungu alimwuliza Ayubu hivi: “Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya nchi?” Kwa kuwa wanadamu walikuwa hawajaumbwa bado, ni wazi kwamba Ayubu hakuwako wakati huo. Lakini “wana wa Mungu” mbinguni walikuwa wakitazama, nayo Biblia inasema ‘waliimba pamoja.’ Ndiyo, ‘walianza kupiga kelele kwa furaha’ katika pindi hii ya maana.—Ayubu 38:4, 7.
Ni jambo gani lililowafurahisha sana malaika hawa? Bila shaka walipata habari fulani juu ya kusudi la Mungu kwa dunia. Labda Mungu aliwaambia ataumba aina mpya za viumbe humo. Basi malaika wakafurahia kupaona mahali hapo pa kupendeza pakitayarishwa pawe makao ya milele ya jamaa ya kibinadamu.
Mwishowe, Mungu alipokwisha kufanyiza viumbe vingine, aliwaumba mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa. Ndipo alipowaweka mahali malidadi duniani penye kuitwa Bustani ya Edeni, na kuwaambia: ‘Zaeni watoto wengi ili wajaze dunia. Limeni dunia mkuze vitu, kisha tunzeni samaki, ndege na wanyama wote.’ (Mwanzo 1:28) Mungu aliwataka wanadamu waishi milele duniani wakiwa na furaha—Zaburi 37:29.
Walakini, Adamu na Hawa walimwasi Mungu. Basi magonjwa, taabu na kifo vikaipata jamaa nzima ya kibinadamu. (Warumi 5:12) Je! kufurahi kwa “wana wa Mungu” waliokuwa wametazama dunia ikitayarishwa kungekwisha kwa kukatishwa tumaini? Je! kusudi la Mungu kwa dunia lingekosa kutimia?
Sivyo, kwa maana kama Mungu asingetimiza kusudi lake ingekuwa kwamba amekubali ushinde. Yeye asingeweza kamwe kufanya hivyo! Yeye anatamka kwamba, “nitatenda mapenzi yangu yote.” (Isaya 46:10,11) Nayo Biblia inasema kwamba Mungu hakuiumba dunia “ukiwa,” bali “aliiumba ili ikaliwe na watu.”—Isaya 45:18.
Ni kweli kwamba sasa dunia imekaliwa na watu, lakini si kwa njia aliyokusudia Mungu. Kuna chuki. Kuna uhalifu. Kuna vita. Mamilioni ya watu wana njaa na magonjwa. Lakini Mungu aliiumba dunia yetu iwe makao yenye kufurahisha wanadamu milele. Na kweli ndivyo itakavyokuwa! Biblia inatabiri hivi: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4.