Ulimwengu Uliumbwa kwa Kusudi Tukufu
KAMA ilivyotajwa mapema, kwa muda mrefu watu wametazama angani na kujiuliza, ‘Kwa nini vitu hivi vyote vipo?’ Mwanamuziki mmoja mwenye kipawa alionyesha shukrani kwa kuimba hivi: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake.”—Zaburi 19:1.
Ulimwengu wetu maridadi sana pia hutufanya tuhisi vivyo hivyo. Kwa mfano, baada ya safari ya angani, mwanaanga Charles M. Duke, Jr., alisema: “Dunia ndiyo kitu maridadi zaidi angani, ikiwa na rangi zake zote za ardhi, bahari, na mawingu.” Aliongezea kusema: “Kuitazama dunia kwenye anga jeusi kulikuwa jambo lililonivutia kwelikweli.”
Unahisije unapotazama anga jangavu lililotapakaa nyota? Au utazamapo mandhari fulani duniani ambayo ni maridadi sana kiasili? Je, wewe hujiuliza jinsi ilivyopata kuwapo, au kwa nini ipo?
Ajulisha Kusudi Lake
Yehova alimwuliza Yobu swali hili: “Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya nchi?” (Ayubu 38:4) Swali hilo lilikuwa la kumnyenyekeza Yobu, kwa kuwa bila shaka hakuwako wakati huo wa uumbaji. Lakini, muda mrefu kabla ya wakati wa Yobu, Mungu aliwaumba wana wanaofanana na yeye—watu wa roho, malaika. (Zaburi 104:4, 5) Basi akiendelea kumwuliza Yobu maswali kuhusu dunia, Mungu akauliza: “Ni nani aliyeliweka jiwe lake la pembeni, hapo [malaika walipoimba] pamoja, na wana wote wa Mungu walipopiga kelele kwa furaha?” —Ayubu 38:6, 7.
Kwa nini kulikuwa na furaha kuu hivyo miongoni mwa malaika wakati dunia ilipowekewa misingi? Kwa sababu inaonekana kwamba dunia ilikuwa kitu cha kipekee kati ya vitu ambavyo Mungu alikuwa ameumba. Labda hata Mungu aliwapa malaika mwono fulani wa kimbele juu ya kusudi lake tukufu kuhusu dunia. Baadaye, Yehova aliwafunulia wanadamu kwamba “hakuiumba [dunia] ukiwa, [bali] aliiumba ili ikaliwe na watu,” ndiyo, ikaliwe na kufurahiwa na wanadamu hata milele.—Isaya 45:18.
Baada ya kuwaumba mwanamume na mwanamke, Yehova alijulisha kusudi lake kuhusu dunia alipowaagiza wenzi hao wa kwanza: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.” (Mwanzo 1:28) Mungu aliwaumba wenzi wa kwanza wakiwa na uwezo wa kimwujiza wa kuzaa watoto, na alikusudia dunia yote ijae watu wakamilifu wanaodhihirisha sifa nzuri za Muumba wao.
Ni kweli kwamba karibu kila sehemu inakaliwa na watu duniani, lakini hawaishi duniani kwa njia inayomletea Muumba sifa. Wanadamu wako katika hali mbaya ya ugonjwa na kifo, nao hawatunzi ifaavyo dunia na wanyama wake. Yehova aliwaumba wanadamu wakiwa wakamilifu, na alikusudia kwamba baada ya muda fulani dunia yote iwe chini ya familia ya wanadamu waadilifu, wote wakiishi pamoja katika dunia paradiso.
Tunaweza kuwa na uhakika kwamba kusudi hilo litatimizwa. Kwa nini? Kwa sababu ya ahadi ya Yehova kwamba yale anayoyakusudia ‘atayafanya.’ (Isaya 46:11; 55:11) Neno lake latuhakikishia hivi: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” (Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4) Wengi wanaweza kukumbuka kwamba Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, alimwahidi mtenda-dhambi mwenye toba aliyekufa kando yake: “Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:43) Hiyo itatimizwaje?
Jinsi Kusudi la Mungu Litakavyotimizwa
Kristo aanzapo kutawala dunia kabisa, mtenda-dhambi huyo atafufuliwa apate uhai duniani chini ya utawala wa kimbingu ambao tumesali kwa muda mrefu. (Zaburi 72:1, 5-8; Mathayo 6:9, 10; Yohana 18:36, 37; Matendo 24:15) Lakini, kabla ya wafu kufufuliwa, wote wanaokataa kumwabudu Mungu wataondolewa duniani. Biblia inaahidi hivi: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele.” Na inaongezea hivi: “Utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
Kwa hakika Muumba wa ulimwengu huu wetu mtukufu ambaye ana hekima yote aweza kutimiza kusudi lake la kufanya dunia hii ijae watu wanaodhihirisha sifa zake nzuri! (Mwanzo 1:27) Ili wanadamu wapate fursa ya kujifunza jinsi Mungu atakavyotimiza jambo hili, yeye ameandaa kitabu ambacho watu kila mahali wanaweza kusoma.a Ona jinsi mtu mmoja wa huko Dayton, Ohio, Marekani, anavyokifafanua kitabu hicho:
“Sitaweza kumaliza kusoma kitabu hiki maishani mwangu. Kinaanza kwa kufafanua jinsi makao yetu maridadi yalivyoharibiwa na uasi. Yakafuata maafa, msiba, huzuni, uuaji, na kifo. Familia iongezekapo, kukata tamaa na huzuni nayo yazidi. Karne zazidi kuyoyoma, mataifa yainuka na kuanguka, maelfu ya watu nao wapita, kila hisia ya mwanadamu yadhihirika, tokea chuki ya ndani hadi upendo wa mfia-imani. Tumaini, likianza kama taa hafifu, laongezeka na kuwa kubwa. Serikali kamilifu itarudisha makao yetu maridadi. Mtawala wake ni Mfalme, Kristo Yesu. Serikali hiyo ni Ufalme wa Mungu. Na familia hiyo ni jamii ya wanadamu. Kitabu hicho ni Biblia!”
Twakutia moyo uchunguze kitabu hiki chenye maana zaidi, Biblia. Na zaidi, twakualika uchunguze kindani mambo yanayothibitisha kwamba ulimwengu na sehemu zake nyingi haukutokea wenyewe tu. Utapata uchunguzi wa kindani wa suala hilo katika kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? Kwenye ukurasa wa 32 wa gazeti hili, unaweza kuona jinsi ya kupokea kitabu kimoja.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 10]
“Kitu maridadi zaidi angani”
[Picha katika ukurasa wa 10]
NASA photo