Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 6/15 kur. 3-8
  • Ukristo wa Kisasa Ni wa Kweli Kiasi Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ukristo wa Kisasa Ni wa Kweli Kiasi Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JE! WEWE NI MKRISTO WA KWELI?
  • Ukristo na Matendo ya Dini ya Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Wewe Umepata Kukatishwa Tamaa na Kibandiko?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Je! Dini za Ulimwengu Zinatoa Uongozi Unaofaa?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Wakristo wa Kweli Ni Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 6/15 kur. 3-8

Ukristo wa Kisasa Ni wa Kweli Kiasi Gani?

WAKATI wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, Mholanzi Hanz van Meegeren aliuzia Mjeremani mmoja picha iliyosemekana kuwa ndiyo picha ya zamani zaidi inayojulikana ya Jan Vermeer, mchoraji Mholanzi wa karne ya 17. Ilitukuzwa kuwa kitu cha ufundi mkubwa. Mwishoni mwa vita van Meegeren alikamatwa kwa sababu aliuzia adui mchoro huo uliofanywa kwa ustadi mwingi sana. Ebu wazia namna washtaki wake walivyoshangaa alipokiri kwamba alikuwa amenakili huo ‘mchoro wa ustadi mwingi sana wa Vermeer,’ bila kupewa kibali ya kufanya hivyo. Alithibitisha alikuwa ameinakili tu kwa kupiga brashi (kuchora) picha nyingine ya “Vermeer” akiwa gerezani!

Kisa hicho kinaonyesha nini? Kwamba si nyakati zote sahihi au kibandiko kinapomaanisha kwamba kitu ni cha kweli. Huenda kikawa kimenakiliwa kwa njia haramu (bila kibali na kwa ubandia tu). Katika habari ya uchoraji, jambo hilo linagunduliwa kwa kuchunguza kwa uangalifu njia iliyotumiwa kuchora na vifaa vilivyotumiwa, kwa kulinganisha mambo hayo na yale yanayoonekana katika picha za mchoraji wa kwanza, kwa kulinganisha mchoro unaotiliwa mashaka na ule mchoro wa kweli.

Leo mamia ya mamilioni ya watu wanatumia “kibandiko” au “sahihi” ya Ukristo. Labda wewe ni mmoja wao. Lakini unaweza kujuaje kama wewe ni Mkristo wa kweli, kama wewe ndiwe kile kitu halisi? Kwanza, chunguza mwenendo wako na imani zako kwa kuzilinganisha na maandishi ya Biblia yanayoonyesha mafundisho ya Yesu Kristo na mitume wake. Halafu, chunguza namna Wakristo wa kwanza walivyoyatumia mafundisho hayo. Tatu, changanua namna ya dini yako mwenyewe uone kama inalingana na kielelezo kilichowekwa na Kristo. Sasa jiulize mwenyewe, Je! dini yangu ni Ukristo wa kweli? Je! mimi ninaifuata kwa mazoea?

Ili kukusaidia katika uchanganuzi wako, acha turudie kujikumbusha pande kadha za msingi zinazohusu mwenendo ambazo zitathibitisha Ukristo wa kweli ni nini.

VITA: Yesu Kristo alisema: “Wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.”​—Mathayo 26:52.

Mtume Paulo aliandika hivi: “Msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo mema machoni pa watu wote. Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote.” “Pendo halimfanyii jirani neno baya.” (Warumi 12:17, 18; 13:10) Yeye alisema hivi pia: “Ingawa tunaenenda katika mwili, hatufanyi vita kwa jinsi ya mwili; maana silaha za vita vyetu si za mwili.”​—2 Wakorintho 10:3, 4.

Tertuliano, mwandikaji Mkristo aliyezaliwa miaka zaidi ya 100 baada ya kifo cha Kristo, anatusaidia kuona namna maoni ya Wakristo wa kwanza yalivyokuwa kuhusu vita na kushiriki ndani yake: “Mimi nafikiri ni lazima kwanza tuulize kama vita inafaa hata kidogo kwa Wakristo. . . . Je! litachukuliwa kuwa jambo halali kisheria kuwa na upanga, hali Bwana anatangaza kwamba yeye anayetumia upanga atatoweka kwa upanga? Na je! mwana wa amani atashiriki katika pigano na hali hata haimstahili kumshtaki mtu kisheria?”

Jumuiya ya Wakristo imekuwa na kumbukumbu la namna gani juu ya kutafuta amani na kuidumisha? Dini uliyolelewa ndani yake ina msimamo gani kuhusu suala hili? Jiulize hivi: Ni mataifa gani yaliyovianzisha vile vita vya ulimwengu viwili vilivyoua watu wengi sana na kutaabisha wengine katika karne hii? Je! ni mataifa ya Kiislamu, ya Kihindu au ya Kibuddha? Hapana, vilianzishwa na yale yanayoitwa ati mataifa ya Kikristo ya Ulaya, nayo yalifanya hivyo kwa kuhimizwa na wanasiasa Wakatoliki na Waprotestanti pamoja na viongozi wa kidini. Basi, yanafaa sana maelezo ya mtangaza-habari za radio aliye mwandikaji pia, Malcolm Muggeridge, ambaye aliandika hivi: “Katika vita mbalimbali vya nyakati zetu Kanisa limesisitiza ya kwamba Mungu amekuwa upande wetu, nalo limebariki kabisa njia zo zote za kupiga vita hivyo ambazo majemadari na wanasiasa wameona zinafaa. . . . Mmoja wa semi zenye hekima zaidi za mwanzilishi wa dini ya Kikristo ulikuwa kwamba ufalme Wake si sehemu ya ulimwengu huu.”

UHALIFU NA MAKOSA: Kristo alifundisha hivi: “Mpende jirani yako kama nafsi yako.”​—Mathayo 22:39.

Ni mtu gani mwenye akili timamu anayetaka kunyang’anywa mali zake, apigwe au auawe? Kwa msingi huo hakuna Mkristo wa kweli anayeweza kutenda mambo kama hayo ya uhalifu juu ya mwanadamu mwenzake, kwa maana Kristo alisema: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.”​—Mathayo 7:12.

Mtume Petro alitaja mambo wazi katika shauri lake: “Mtu wa kwenu asiteswe kama mwuaji, au mwivi, au mtenda mabaya.”​—1 Petro 4:15.

Tertuliano anasema nini juu ya mwenendo wa Kikristo katika siku zake? “Katika orodha zenu ndefu za wale walioshtakiwa juu ya matendo mengi mbali-mbali ya ukatili, je! mwuaji ye yote wa watawala, mkata-vibeti [mwizi wa mifukoni] ye yote, mwanamume ye yote mwenye hatia ya . . . utongozi, au mwenye kuiba nguo za wenye kuoga, [amepata] kuandikwa jina lake katika orodha hizo akitajwa kuwa ni Mkristo? . . . Sikuzote watu wenu ndio wanaomiminika gerezani . . . Hampati Mkristo ye yote huko, isipokuwa kama amefungwa kwa sababu yeye ni Mkristo tu; au kama mmoja amefungwa huko kwa sababu ya kutenda jambo jingine, huyo hawi ni Mkristo tena.”

Hali ya uhalifu wa sasa iko namna gani katika mataifa ‘ya Kikristo’? Kuna ongezeko kubwa sana la uhalifu, wafungwa wamesongamana katika magereza na watu wanaogopa kutembea nje kwenye barabara katika miji mingi kwa sababu kuna maelekeo ya kushambuliwa na wahalifu. Je! si kweli kwamba wengi wa majambazi na wahalifu hao wangali wana “kibandiko cha Ukristo” kama inavyoshuhudiwa na uhakika wa kwamba wanaipokea Misa, au sakramenti ya Waumini? Hata Misa Kuu zimesherehekewa kwa niaba ya watu wanaojulikana kuwa wenye ghasia. Imekuwa ni kama hakuna hatua yo yote ya kuwatia watu adabu inayochukuliwa kusafisha kanisa kwa kuondoa wasiostahili. Je! hizo ndizo shuhuda za kuutambulia Ukristo halisi?

KUTOA MIMBA: Hapa tena tunaweza kuitumia kanuni ya mwenendo iliyotolewa na Yesu: “Sikuzote tendeeni wengine kama vile ninyi mngependa wao wawatendee ninyi.”​—Mathayo 7:12, The New English Bible.

Je! wewe unataka kufa? Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili Wanazi waliua mamilioni ya watu katika kambi zao za mateso. Ukitazama yaliyotendwa huko nyuma, je! wewe ungalichagua kuwa mmoja wa watu hao waliouawa kama ungalikuwako? Vijusu (vitoto visivyozaliwa) havina uchaguzi wa kujifanyia vyenyewe, sawa na watu hao waliouawa. Tena vinauawa kwa makumi ya mamilioni kila mwaka. Agizo la mtume Petro linaihusu hali hiyo: “Mtu wa kwenu asiteswe kama mwuaji.”​—1 Petro 4:15.

Katika habari hii maelezo ya Wakristo wa karne ya pili, Tertuliano na Athenagora, yanatoboa mambo wazi: “Kwa habari yetu, kwa kuwa uuaji umekatazwa mpaka milele, sisi hatuna ruhusa ya kuangamiza hata kijusu kilicho katika tumbo la uzazi.” (Tertuliano) “Na wakati tunaposema kwamba wanawake wale wanaotumia dawa za kulevya ili kutoa mimba wanafanya uuaji, na lazima watamtolea Mungu jibu kwa sababu ya utoaji-mimba, sisi tutawezaje kuua na hali si jambo la kanuni kufanya hivyo?” (Athenagora)

Tarakimu zenye kustaajabisha zinatolewa kuonyesha mimba ambazo zimetolewa katika mataifa ‘ya Kikristo’ yaliyo mengi katika nchi za Uzunguni. Kwa mfano, tarakimu rasmi ya mimba zilizotolewa katika United States (Amerika) wakati wa mwaka wa 1978 pekee ilikuwa 1,157,776! Katika Netherlands na Jamhuri ya Mwungano wa Ujeremani inahesabiwa kwamba asilimia 25 za mimba zinatolewa kwa ruhusa iliyopatikana kisheria au njia haramu. Tarakimu ya nchi ya Kikatoliki ya Ufaransa ni asilimia 50. Tunapolinganisha habari zilizotangulia kutajwa za Wakristo wa kwanza na takwimu hizi zenye kuhuzunisha sana, tuna haki ya kuuliza, Je! “Wakristo” wa kisasa wanaotoa mimba, na makanisa yanayoachilia mazoea hayo yaendelee, ni Wakristo kweli?

ADILI KATI YA WANAUME NA WANAWAKE Mwanzilishi wa Ukristo alitamka hivi: “Ndani ya mioyo ya watu hutoka mawazo mabaya uasherati, . . . uzinzi, . . . ufisadi . . . Haya yote yaliyo maovu . . . yamtia mtu unajisi.”​—Marko 7:21, 22.

Paulo misionari Mkristo anakubali kwamba mambo hayo yanatia mtu unajisi (uchafu), kwa maana anaandika hivi; “Waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, . . . wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti.”​—1 Wakorintho 6:9, 10.

Sasa acha turudi nyuma tena kwenye mambo yaliyozoewa na Wakristo wa karne ya pili: “Sisi tuko mbali sana na kuzoea ngono za ovyo-ovyo, hivi kwamba si halali kati yetu kuhusika hata kutupia mwanamke jicho lenye tamaa.” (Athenagora) “Mkristo hujizuia asihusike na wanawake . . . Mume Mkristo hana la kufanya na mwanamke ye yote isipokuwa mke wake mwenyewe.” (Tertuliano)

Je! Jumuiya ya Wakristo ya kisasa imefuata kielelezo cha mwenendo kilichowekwa na Wakristo wa kwanza kuhusu adili Je! ‘njia na vifaa vinavyotumiwa’ vinaonekana kuwa vya namna moja vikilinganishwa na kielelezo cha kwanza? Katika habari hii, Malcolm Muggeridge aliyetajwa hapo mwanzoni alivutwa kuandika hivi “Katika mambo kama talaka, kulalana kwa mwanamume na mwanamume na ile inayoitwa Adili Mpya maelekeo ya sasa yanatofautiana sana na hali ya Ukristo wa kwanza; mara nyingi wanakanisa walio mashuhuri hawajali.”

Katika milki ya Jumuiya ya Wakristo uasherati, uzinzi na tendo la wanaume kulalana na wenzao na wanawake hivyo hivyo ni matendo yaliyoenea kote kote. Magonjwa ya kisonono na kaswende yanayotokana na mambo hayo yamesambaa kote. Je! huo ndio Ukristo wa kweli? Au hiyo inaonyesha kwamba tunashughulika na kitu cha bandia, kiigizo ovyo tu?

KUHUSIKA KATIKA SIASA: Kristo alisema hivi juu ya wafuasi wake: “Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” Vilevile alisema hivi mbele ya Pilato: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. . . . Ufalme wangu si wa kutoka chanzo hiki.”​—Yohana 17:16, UV; 18:36, NW.

Katika Roma wa kale cheo cha kisiasa na dini ya serikali ni mambo yaliyoshirikishwa pamoja. Wakristo wa kwanza walikuwa na maoni gani juu ya hali hiyo? Kitabu Encyclopaedia Britannica kinaeleza hivi: “Wakristo wa karne tatu za kwanza waliikataa kabisa dini ya serikali ya Roma , . . Wakristo walijichukua kuwa raia za mji wa kimbingu uliokuwa ukija na wakajichukua kuwa wahaji na wageni duniani . . . kuwa washiriki wa Ufalme wa Mungu . . . ambao ulikuwa ukimaliza kufungamana kwake na ulimwengu huu unaopita na hivyo pia ukamaliza kufungamana kwake na taratibu yake ya kisiasa.”

“Ukristo” wa kisasa unahusianaje na siasa? Uko katika hali ya mgawanyiko tangu juu hata chini. Kuna viongozi wa kidini wanaohusika na karibu kila chama cha kisiasa kilichopo, tangu mapadri Wakatoliki wanaounga mkono Ukomunisti katika Spania na Latin Amerika mpaka wachungaji Waprotestanti wanaotumika katika bunge la Uingereza au wanaojishirikisha na chama kisichotaka mapinduzi ya siasa katika United States. Watu wenye habari wanajua sana kwamba makumi machache ya miaka iliyopita viongozi wa kidini wamekuwa wakijishusha sana, isipokuwa wachache tu kati yao, ili watii tawala za Kinazi na Kifashisti katika Ujeremani, Italia na Spania.

Watu wa Jumuiya ya Wakristo wamegawanyikana na walio waaminifu wana ushikamanifu kwa vyama vya kisiasa vilivyo tofauti na vya wale wengine. Mwandikaji Mspania wa karne ya 20 aliye pia mwanachuo, Miguel de Unamuno, alisema kweli kabisa alipoandika hivi: “Nchi alikozaliwa Mkristo si ya ulimwengu huu.” “Ukristo unapasa kujiepusha na siasa.” Badala ya kujiepusha, mwandikaji Mwingereza wa habari za jarida, Anthony Lejeune, alivutwa kuandika kwamba: “Mapadri wamekuwa wengi sana siasani. . . . Ikiwa kazi ya Kanisa ni kueleza watu mambo ya ulimwengu tu, kuna faida gani kwenda kwenye Kanisa?”

Pia, namna gani vile vyeo vya kurairai viongozi wa kidini vinavyotumiwa katika makanisa mengi sana? Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninyi msiitwe Rabi [“Mkuu wangu; Mtu wangu aliye bora kabisa”​—majina yanayofanana na vyeo vya wahubiri kama “Reverendi,” “Reverendi Mkubwa Zaidi,” N.K.], maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni.” (Mathayo 23:8, 9) Hiyo inaonyesha wazi kwamba haikukusudiwa kuwe na tofauti ya viongozi wa kidini na watu wa kawaida tu katika Ukristo wa kweli.

KUHUBIRI “HABARI NJEMA”: Katika Mahubiri yake juu ya Mlima Yesu alisema: “Ninyi ni nuru ya ulimwengu. . . . Nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.”​—Mathayo 5:14-16.

Kitia-moyo hicho cha kuangaza kwa maneno na matendo kimerudiwa katika maneno haya ya mtume Paulo: “Kwa njia yake [Yesu], na tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake.” (Waebrania 13:15) Kila mfuasi wa Kristo amewekewa pendeleo na wajibu wa kuzihubiri “habari njema” za Kikristo.

Je! Wakristo wa kwanza ‘waliliungama jina lake’ mbele ya watu wote wakiwa jamii? Au waligandamizwa mara tu baada ya kufa kwa mitume ilipotokea jamii ya viongozi wa kidini? Mtajo unaofuata uliotolewa katika kitabu cha Dakt. Neander, History of the Christian Religion and Church during the Three First Centuries, unajibu ulizo hilo:

“Selso [wa karne ya 2 W.K.], mwandikaji wa kwanza mwenye kupinga Ukristo, anafanya dhihaka akidharau jambo la kwamba wafanya kazi wa kikawaida tu, washona viatu, wakulima, watu wajinga-wajinga kabisa wa kishamba, walikuwa wahubiri wenye juhudi wa ile Gospeli ati.”

Sasa jiulize mwenyewe maulizo haya yenye kuchunguza moyo: Je! dini yangu inanitia moyo na kunitayarisha kwa bidii nihubiri imani zangu za Kikristo? Je! roho (kusudi) ya Ukristo wangu inanichochea niende kwenye nyumba za watu wale wengine nikatafute wale wanaohitaji Ukristo wa kweli? Kama sivyo, ni dini ipi ya Kikristo inayotimiza amri hiyo iliyotolewa na Kristo?​—Mathayo 24:14; Matendo 1:8; 1 Wakorintho 9:16.

JE! WEWE NI MKRISTO WA KWELI?

Inahitajiwa kabisa kila mtu anayedai kuwa Mkristo ajibu ulizo hilo kwa kukubali. Kwa sababu gani? Kwa sababu kupata kwake kibali ya Mungu kutategemea namna anavyolijibu. Ukristo si imani tupu tu au kibandiko, bali ni njia ya maisha. Je! njia yako ya maisha inaonyesha unafuata mfano wa Kristo? Je! mazoea yako ya kidini yanapatana na ubora ambao Biblia inaonyesha Wakristo wa kwanza walikuwa nao, kama tulivyoona sasa hivi?

Mtume Paulo anatutolea ukaribishi huu: “Jitieni wenyewe kwenye uthibitisho, mwone kama ninyi mnaishika ile Imani. Jijaribuni wenyewe.” (2 Wakorintho 13:5, The Twentieth Century New Testament) Kwa kusudi hilo, tunakukaribisha uichunguze orodha fupi inayofuata, huku ukifungua katika Biblia yako mwenyewe maandiko yaliyoonyeshwa.

1. Je! wewe unashiriki kuonyesha ushikamanifu kwa vyama vya kitaifa au vya kisiasa vinavyoleta migawanyiko kati ya wenye kujiita Wakristo?​—1 Wakorintho 1:10; Yohana 18:36; Yakobo 1:27.

2. Wewe unaielezaje maana ya upendo wa Kikristo?​—1 Wakorintho 13:4-8.

3. Je! unajaribu kuonyesha kwa matendo upendo wa kweli kwa jirani yako? Unauonyeshaje?​—Mathayo 22:39; Yohana 13:34, 35.

4. Je! wewe ni mwenye fadhili, mwenye huruma nyororo na je! unawasamehe wengine?​—Waefeso 4:31; Warumi 12:10.

5. Katika maisha yako ya kila siku, je! unaepuka kusema uongo, kuiba, kupunja watu (kuwadanganya) na kutumia usemi wa tabia chafu-chafu na wa matusi?​—Waefeso 5:3-5; 4:25-31.

6. Je! wewe una maelekeo ya kufikiri kwamba si jambo la maana sana kufuata adili katika mambo yanayohusu wanaume na wanawake?​—Marko 7:20-23.

7. Je! una maelekeo ya kula na kunywa kupita kiasi?​—Mithali 23:20, 21; Waefeso 5:18.

8. Je! wewe unajaribu kuwaeleza wengine imani ya kweli ya Kikristo kwa maneno na matendo?​—Warumi 10:9, 10;1 Wakorintho 9:16.

Umefikia neno gani la mwisho? Je! leo kuna Wakristo halisi kweli? Je! wewe unawajua wo wote wanaojaribu kwa bidii kuishi kama Kristo na wakati ule ule wanajitahidi sana kuwaeleza jirani zao imani yao ya Kikristo na njia ya maisha? Je! dini yako mwenyewe kwa uhakika inafundisha na kuzoea Ukristo wa kweli? Au dini hiyo ni kibandiko tu au sahihi yenye kuvuta macho tu?

Ikiwa wewe mpaka sasa hujawajua Mashahidi wa Yehova kibinafsi, tunapendekeza uwatazame walivyo katika ujirani wako kisha uone kama wanadhamiria kwa bidii kulinganisha maisha yao na viwango vya Biblia vilivyozungumzwa hapo juu. Ikiwa hujui mahali walipo, sisi tutafurahi kukusaidia uwasiliane nao.​—Isaya 43:10-12; Matendo 11:26.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki