Habari Njema Kutoka Sehemu Zenye Matata
MARA kwa mara barua zinapokewa katika afisi za Sosaiti zikiuliza hali ya Wakristo wenzi wa wenye kuziandika ikoje katika nchi ambako kumekuwa na mateso makali. Wao wanaendeleaje? Je! wanaendelea kumtumikia Yehova kwa ushikamanifu? Je! wana uhitaji wa chakula na mavazi?
Kwa kujibu, tunasema hivi: Kwa wingi Mashahidi wa Yehova katika nchi hizo wanasimama imara katika imani. Wanaendelea kwa ushikamanifu kutafuta nafasi za kuongea na wengine juu ya mambo matukufu ya uufalme wa Yehova. Na kupatana na neno lake la ahadi, Yehova anabariki jitihada zao za kupata mahitaji ya lazima ya maisha.—Luka 12:22-31.
Hata wawe wametendwa mambo gani na watawala, Mashahidi wa Yehova wanakumbuka yale ambayo mtume Paulo alimwandikia Timotheo mshirika mwenzake: “Basi . . . nataka dua, na sala, na maombezi, na shukrani zifanyike kwa ajili ya watu wote; kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka, tuishi maisha ya utulivu na amani, katika utauwa wote na ustahivu.” (1 Timotheo 2:1, 2) Kupatana na sala hiyo, Mashahidi wanadhamiria kujitahidi watii sheria zote ambazo hazipingani na amri za Mungu. Hasa wanakuwa na juhudi ya kufanya mapenzi ya Mungu, yaani, kueleza wengine habari njema zinazohusu ufalme wake.
Mgeuzo Mzuri wo Moyo
Ni vizuri kuona kwamba serikali nyingine zimegeuza moyo wazo kuelekea Mashahidi wa Yehova katika miaka ya karibuni, zikawapa ukubali wa kuwatambua kisheria pamoja na uhuru baada ya miaka mingi ya kuonewa na wakuu. Mifano miwili yenye kutokeza ni nchi za Spania na Ureno, ambako watawala wenye kutumia nguvu waliagiza Mashahidi wapigwe marufuku. Wakati marufuku katika Spania ilipoondolewa mwaka wa 1970, walikuwako Mashahidi 11,000 wenye kutenda kazi huko. Sasa, miaka 12 baadaye, hesabu hiyo imeongezeka ikawa 50,000!
Sasa wenye mamlaka katika Spania wana maoni gani juu ya Mashahidi? Kisa cha hivi majuzi katika mji wa Barcelona kinaonyesha nia yao. Katika kichapisho rasmi, serikali ya mitaa iliwahesabu Mashahidi katika lawama la ujumla la madhehebu fulani zinazoendeshwa huko sasa ambazo hazifuati kanuni. Lakini rufani ilipoombwa kwa maafisa wa mji, bila kukawia waliomba msamaha na wakachapisha sahihisho katika ukurasa wa kwanza wa gazeti lililofuata. Lilisema hivi: “Tunataka kuwajulisha kwamba Shirika hili [la Mashahidi wa Yehova] linaheshimiwa sana sana na Jumba Kuu la Mji wa Barcelona na hata na idara zake za kiserikali.”
Hali iliyo katika Ureno ni ya kuvutia pia. Mwaka wa 1962, wakati wamisionari sita walipofukuzwa nchini, Mashahidi watendaji wa huko walikuwa 1,285 tu. Na sasa ni zaidi ya 22,000 wakilinganishwa na idadi ya watu karibu 9,500,000. Hicho ni kiasi cha Shahidi mmoja kwa kila wakaaji 438.
Ijapokuwa walikuwa wamepewa uhuru mwaka wa 1974, Mashahidi wa Ureno hawakuwa wameweza kufanya kusanyiko la mzunguko katika mji fulani wa kusini. Shukrani zinamwendea meya mwenye kutaka kuona wakipewa uhuru ambaye aliingilia jambo hilo kisha wakapewa ruhusa ya kutumia Jumba la Maonyesho la Serikali ya Mtaa wa huko. Kwenye mkutano wa kwanza wa baraza uliolifuata kusanyiko, meya huyo na wanabaraza wengine waliwapongeza Mashahidi kwa sababu ya mipango yao yenye utaratibu mzuri na utendaji wao wa kusafisha mahali pa kusanyiko lilipokwisha.
Katika mji mwingine wa Ureno Mashahidi walijitolea wamimine saruji sakafuni na kuitandaza kwenye kibanda cha maonyesho ya ukulima, ambapo walipanga kufanyia kusanyiko. Mashahidi 70 walikuja wakaifanya kazi hiyo kwa siku moja. Meya alivutiwa hata akasema hivi: “Sikuamini jambo kama hilo lingeweza kufanyika. Ninyi mnaruhusiwa kufanya makusanyiko mengi kama mnavyopenda katika kibanda hiki, bila malipo, kwa muda wa miaka mitatu inayokuja!”
Shughuli zo Mitaa na Kazi ya Kusaidia Wenye Shida
Hata sehemu ambako mateso yanaendelea, Mashahidi wa Yehova wanaendelea kutoa sala kuhusu watawala ili waweze kuwa na maoni yenye usawaziko zaidi na ya kuvumilia utendaji mbalimbali wa Mashahidi. Hakuna roho ya kuwaonea uchungu. Kwa kweli, wao wanazishiriki shughuli za kujitolea kusaidia mitaa katika nchi nyingi za namna hiyo.
Kwa mfano, katika mtaa mmoja wa Kiafrika mipango miwili ya watu kujisaidia wenyewe itayarishwa, yaani, kujenga barabara moja na shule moja. Kazi ilipasa kuanzwa saa kumi na mbili ya asubuhi. Mashahidi walifika kabla ya saa hiyo wakaanza kazi bila kuiacha. Wanakijiji wengine walifika wamechelewa na kazi yao haikuwa nzuri sana. Walianza kugombana-gombana. Akina ndugu waliendelea kufanya kazi ili waimalize. Tangu wakati huo watu wa ujirani huo wamekuwa wakiwaheshimu Mashahidi kwa bidii yao ya kujali kazi.
Kutoka nchi nyingine ya Kiafrika ambako Mashahidi wamevumilia mateso inakuja ripoti hii: “Kwa mambo ya kimwili, ndugu zetu walio katika kambi za uzuizi . . . wameweza kujitafutia mengi ya mahitaji yao muda wa mwaka wote. Wamekuwa na mavuno mazuri. Hata hivyo, kumekuwa na uhitaji wa lazima kusaidia wengine wenye shida, sana-sana kwa upande wa mavazi na dawa, nayo Sosaiti imefurahia kutoa misaada hiyo.”
Kwa kweli, ulimwenguni pote kila kundi la Mashahidi wa Yehova linachukua hatua zinazohitajiwa kabisa kusaidia wale walio na shida za kweli kati yao. Wakati misiba mikubwa inapotokea katika taifa, misaada inakusanywa-kusanywa bila kukawia kupitia afisi ya tawi ya nchi hiyo na afisi za matawi jirani ya Sosaiti.—Matendo 2:44-47; 6:1-6.
Watu Wafanywa Wawe na Maoni Yanayofaa
Kama vile ilivyokuwa kwa Wakristo wa kwanza, Mashahidi wa Yehova wamepewa sifa mbaya magazetini. Wayahudi fulani katika Roma walimweleza mtume Paulo habari ambazo wao walizijua juu ya Wakristo katika wakati wao : “Katika habari za madhehebu hiyo imejulikana kwetu kwamba inanenwa vibaya kila mahali.” (Matendo 28:22) Hata hivyo, sehemu ambako wakuu wa kisiasa wamekuwa na nafasi ya kuwajua Mashahidi uso kwa uso, mara nyingi matokeo yamekuwa ya kuwatendea inavyofaa. Kwa sababu gani? Kwa sababu wanaona wazi kwamba wao wanashughulika na watu wenye maisha safi na wanaotii sheria, watu wanaosaidia kuleta hali bora za kijamii kwa kuwapa maendeleo ya tabia watu ambao wanajifunza Biblia nao. Hiyo ni wazi katika habari zilizopokewa kutoka Jamhuri ya Gambia, iliyo katika pwani ya magharibi ya Afrika. Ripoti hiyo inasema hivi: “Kazi nzuri inafanywa katika magereza, na Mashahidi wa Yehova ndicho kikundi cha pekee cha kidini kinachoruhusiwa kuingia katika maeneo ambamo watu hukatazwa kuingia, kwa sababu wao wamekuwa na mafanikio mazuri katika kusaidia wafungwa wageuze maisha yao.”
Katika nchi nyingine ya Kiafrika ambako Mashahidi hawajapewa ukubali rasmi wa kuwatambua, inaripotiwa hivi: “Wenye mamlaka wanawaheshimu sana akina ndugu. Ilichangamsha moyo kuwasikia wakuu wakisema habari za ndugu zetu na kuwasifu kwa ajili ya unyofu na bidii yao ya kazi.”
Mashahidi wa Yehova wanatoa sala kwa bidii ili watu wa hali zote za maisha wapate kujua Yehova Mungu na Kristo Yesu. Basi wao wataendelea kuzihubiri habari njema za serikali ya Ufalme wa Mungu kwa watu wenye vyeo vya namna zote za hali ya kijamii, kutia na wale “wenye mamlaka.” Wao watatoa sala pia kwa ajili ya watu hao ili ‘tuendelee kuishi maisha ya utulivu na amani, katika utauwa wote.’—1 Timotheo 2:1, 2; Yohana 17:3.