Neno la Mungu Li Hai
Je! Wewe Utasikiliza Shauri?
JE! UMEKWISHA kupokea shauri, kama unavyomwona kijana huyu hapa akipokea? Pengine uliambiwa kwamba mashirika fulani ni mabaya, au kwamba mwendo fulani hasa ungeweza kuelekeza kwenye matata na ungeweza hata kukufanya umkasirishe Mungu. Je! ulisikiliza? Jambo lililowapata watu wa Mungu wa nyakati za kale linaonyesha jinsi lilivyo jambo la maana kusikiliza shauri kwa makini.
Baada ya kuwakomboa Waisraeli kutoka Misri, Mungu aliwaagiza wasishirikiane na waabudu wa miungu mingine. Yeye alisema hivi: “Usifanye maagano [au, mapatano] pamoja nao, wala pamoja na miungu yao.” Wala waabudu hao wa miungu ya uongo hawangeruhusiwa wakae katika nchi hiyo. Sababu aliyotoa Mungu ilikuwa kwamba “wasije wakakufanya kunitenda mimi dhambi.” (Kutoka 23:32, 33) Hata hivyo, kabla tu ya kwenda kwenye Nchi ya Ahadi, Waisraeli wengi hawakutii shauri hilo. Ikawaje?
Nabii wa uongo Balaamu alifanya wanawake wa Moabu na Midiani, unaowaona hapa, wawaalike Waisraeli kwenye karamu ya chakula kinono na divai. Kwa kweli, lilikuwa jambo la upumbavu kwao kukubali mwaliko huo kutoka kwa waabudu wa uongo. Inaweza kuwa wengi wao walishauriwa wasiende. Haidhuru, wakaenda.
Kwenye karamu hiyo Waisraeli walistarehe kwa sababu ya kula na kunywa. Vilevile, inaelekea kulikuwako dansi ya kuonyesha hali ya kufanya ngono iliyochezwa na wanawake Wamoabi na Wamidiani, ambayo iliamsha nyege za wanaume. Wakaacha kujihadhari, hata kwamba wanawake hao wakawavuta wafanye ngono pamoja nao. Hata waliwafanya Waisraeli wainamie miungu ya uongo. Matokeo yakawa nini?
Hasira ya Yehova iliwaka juu ya watu wake, na akapeleka tauni juu yao. Hata mmoja wa Waisraeli alimleta Kozbi, binti ya mkuu Mmidiani, ndani kabisa ya kambi ya Waisraeli. Yeye alimleta kwenye hema yake ili afanye ngono pamoja naye. Lakini Finehasi, mwana wa kuhani mkuu Mwisraeli, akaingia haraka na kuwadunga wote wawili kwa mkuki. Ndipo Yehova akakomesha tauni hiyo. Hata hivyo, Waisraeli 24,000 walikufa kwa sababu hawakusikiliza shauri.—Hesabu 25:1-15; 31:16.
Je! unaweza kuona hali kama hiyo leo? Ipo. (1 Wakorintho 10:11) Sasa tuko karibu kabisa na taratibu mpya ya Mungu aliyoiahidi, tuko tayari kuingia ndani yayo sawa na Waisraeli walivyokuwa karibu kuingia ndani ya Nchi ya Ahadi. Tukiamua kutokana na mifano ya wakati uliopita, tungemtazamia Shetani ajaribu nini? Ndiyo, kuingiza watu wa Mungu katika hali ambazo zingewafanya wafanye uasherati, ili Yehova awahukumu hawafai kuingia katika taratibu mpya yake yenye haki.
Kwa hiyo unapopewa shauri la kuepuka hali zinazoweza kukuelekeza ufanye uasherati, utafanya nini? Uwe mwenye hekima. Sikiliza shauri!