Asili Yake ni Wapi?
INGAWA dini za ulimwengu ni za namna nyingi sana, kuna mifanano fulani iliyoenea sehemu kubwa. Kwa mfano, dini za kichawi za Amerika ya Kusini, dini za kikabila za Afrika, dini zile kubwa za nchi za Mashariki, dini za maaborigini za Australia—kwa kweli, karibu dini zote—zinasadiki kwamba kuna sehemu ya kiroho ya mtu inayoendelea kuishi baada ya kufa kwa mwili wa nyama. Vilevile, dini nyingi zinasadiki juu ya kuwapo kwa roho zisizoonekana ambazo zinaweza kuwaletea wanadamu mema au mabaya.
Je! umepata kuona, vilevile, namna matumizi ya sanamu za kidini yalivyoenea sana? Vilevile, dini nyingi zinapiga bao au kufanya unajimu. Na hesabu kubwa ajabu ya dini katika historia yote zimekuwa na utatu wa miungu, sawa na ule Utatu wa Miungu wa Jumuiya ya Wakristo.
Je! unafikiri inawezekana kwamba dini hizo zote zilisitawisha mazoea kama hayo ya kidini bila kutegemeana? Au inaelekea zaidi kwamba zilipata mawazo yazo kutoka asili moja? Bila shaka, hilo ndilo jambo la akili zaidi. Walakini chanzo hicho kimoja kilikuwa nini?
Ili kujibu hilo, lazima tuzungumze juu ya ulizo, dini ilitoka wapi. Hayo ni mazungumzo ambayo wanafunzi wa historia hawafahamu vizuri. Kitabu The World Book Encyclopedia kinasema hivi: “Wanachuo fulani wamesitawisha mawazo fulani juu ya namna dini ilivyoanza katika nyakati zilizoitangulia historia iliyoandikwa. Hakuna wazo moja ambalo limekubaliwa kwa umoja na wanachuo wote.” Hata hivyo, kuna mamlaka bora inayotuambia juu ya asili ya dini. Mamlaka hiyo ni Biblia.
MWANZO WA HAYO YOTE
Kama unavyojua, Biblia ni kitabu ambacho wakati mmoja kilikuwa kinaheshimiwa na watu wengi. Kwa kusikitisha, katika siku hizi, watu wachache zaidi na zaidi wanaisoma. Hata hivyo tunapozungumza juu ya dini, hatuwezi kufanya hivyo kwa njia yenye kuridhisha tusipoiendea Biblia, kwa sababu kwa njia ya kidini imewaongoza zaidi wanadamu kupita kitabu kinginecho chote.
Vilevile, ukiachana na mambo mengine yote, maelezo ya Biblia ya jinsi dini ilivyoanza yanatumainika zaidi kwa sababu iliandikwa na watu walioishi karibu zaidi na matukio yenyewe hayo kuliko sisi. Ebu tuchunguze yale ambayo Biblia inasema na kulinganisha mambo tutakayoyagundua na mawazo fulani ya wanachuo wa kisasa.
Biblia inatuambia kwamba hapo kwanza wanadamu walimwamini Mungu mmoja tu. Hilo halikuwa wazo la mwanadamu mwenyewe. Kulingana na maandishi, Mungu alijijulisha kwa mwanadamu pale pale mwanzoni kuwa yeye ndiye Asili kuu ya uzima. Yeye alitoa msaada na uongozi ili mwanadamu afanikishe njia yake maishani. (Mwanzo 1:26—2:25) Kwa hiyo, yote yalianzia kwa dini moja. Basi, je! hali yenye mvurugo ya leo ilitokeaje?
Kulingana na Biblia, chanzo chake kilikuwa uasi juu ya Asili hiyo ya kwanza. Katika hati yenye umri wa miaka zaidi ya 3,000, mtu anayeitwa Nimrodi alipata kuwa mjenzi wa mji, akajenga miji katika eneo la kale linaloitwa Mesopotamia. Leo eneo hilo ni sehemu ya Iraq. Baadhi ya miji iliyojengwa iliitwa Babeli, Ereki, Akadi na Kalne.—Mwanzo 10:10-12.
Dakt. Robert M. Adams, akiandika katika gazeti Scientific American, aliuita ujenzi huo wa miji “‘Badiliko’ la pili kuu katika utamaduni wa kibinadamu.” Kwa kuwa miji ambayo Nimrodi alijenga ndiyo iliyokuwa kati ya ile ya mapema zaidi ambayo imeandikwa katika Biblia, twaweza kuwazia namna mtu huyo alivyokuwa na uvutano mwingi.
Juu ya ule ambao hatimaye ulipata kuwa mji mkuu zaidi kati ya hiyo miji ya kale, Babeli (au, Babiloni), Biblia inasimulia juu ya jitihada ya kuzuia mapenzi yaliyotamkwa ya Mungu kwamba wanadamu wasambae duniani pote na kuijaza. Watu hao walisema hivi: “Haya, na tujijengee mji, na mnara, na kilele chake kifike mbinguni, tujifanyie jina; ili tusipate kutawanyika usoni pa nchi yote.” (Mwanzo 11:4) Hata hivyo, kwa sababu ya Mungu kujiingiza walishindwa kutimiza kusudi lao na polepole wakatawanyika kwenye sehemu mbalimbali za dunia. Kwa kufanya hivyo, walikwenda pamoja na mawazo yao ya uasi wa kidini.
Jambo hilo linalinganaje na mawazo ya wakati huu ya wanachuo?
Kwanza: Kitabu Encyclopedia Americana kinasema hivi: “Karibu wanachuo wote wanakubali kwamba ustaarabu wa mapema zaidi tunaojua ulianza kati ya Wasumeri katika Mesopotamia.” Dakt. Gideon Sjoborg, akiandika katika makala fulani katika Scientific American, anakubali hivi, kwa kusema: “Kama inavyojulikana, miji ya kwanza ya ulimwengu ilisitawi . . . katika Nusu-Duara Yenye Rutuba, kisehemu cha upande wa mashariki kinachotia Mesopotamia.” Kwa hiyo, wanasayansi wana maoni ya kwamba wanadamu walianza kujenga miji mikubwa-mikubwa karibu na eneo lile lile ambalo Biblia inalitaja.
Pili: Wabukuzi wa mambo ya kale wanayafahamu sana majina na sehemu ilikokuwa miji mingi ambayo Biblia inasema ilijengwa na Nimrodi.
Tatu: Wakaaji wa Mesopotamia walijulikana kuwa wajenzi wa minara mikubwa sana kwa makusudi ya kidini. Walikuwa wakiiita zigurati. Bila shaka, mnara ule unaotajwa katika Mwanzo sura ya 11 haukukamilishwa. Walakini wabukuzi wa mambo ya kale wamebukua minara mingi iliyokamilishwa ambayo inaelekea ilifanana na huo.
Nne: Jina “Nimrodi” halijagunduliwa isipokuwa ndani ya Biblia yenyewe, walakini vitabu fulani vyenye kutoa maarifa mengi vinalishirikisha na jina la mungu mkuu wa Wababeli, Marduki. Herufi “MRD,” ambazo zinaonekana katika majina hayo mawili, zaelekea kuwa ndicho chanzo, au sehemu yenye kutoa maana, kwa maneno hayo mawili. Ikiwa ni sahihi kushirikisha kwa njia hiyo, basi hatimaye Nimrodi aliabudiwa kama mungu fulani sawa na Makaisari wa Roma na Mafarao wa Misri walivyoabudiwa kama miungu, katika miaka ya baadaye.
Bila shaka, wabukuzi wa mambo ya kale hawana uwezo wote wa kugundua mambo yaliyotokea muda mrefu sana uliopita. Mengi ya magofu wanayochimbua yameharibika sana, na ni vigumu kuyafasiri kwa njia iliyo sahihi. Bila shaka ushuhuda mwingi wa maana umepotea milele.a Kwa hiyo, mwanafunzi wa Biblia hategemei ubukuzi wa mambo ya kale uthibitishe ukweli wa maandishi ya Biblia.
Vilevile ni jambo linalostahili kuangalia kwamba historia hiyo ya kale inatusaidia tufahamu sehemu fulani juu ya tamasha ya kidini ya ulimwengu wa leo. Jinsi gani? Kwa kuwa wakaaji wa Mesopotamia walikuwa wenye kufuata dini sana baada ya uasi ule wa kwanza. Wao waliamini kwamba mwanadamu alikuwa na sehemu ya roho iliyoendelea kuishi baada ya kifo. Walikuwa na imani yenye nguvu sana katika mashetani. Walitumia sanamu. Walipiga bao na kufanya unajimu, na hata walikuwa na miungu ya utatu. Hizo ni baadhi ya imani ambazo kwa kufanana wengi wanazo leo.
Je! hiyo maana yake ni kwamba dini ya Mesopotamia ya kale ilisambaa na kuwa na uvutano juu ya dini ulimwenguni pote? Wanachuo wengi wamekata maneno hivyo Katika kitabu Handbooks of the History of Religions, Prof. Morris Jastrow alizungumza juu ya “tokeo lililo wazi sana lililoupata ulimwengu wa kale kupitia vionyesho vya wazi sana vya wazo la kidini katika Babilonia.”
Katika kitabu The Worship of the Dead, Kanali J. Garnier aliandika hivi: “Si Wamisri, Wakaldayo, Wafoinike, Wagiriki na Waroma tu, bali pia Wahindu, Wabuddha, . . . Wajeremani wa Kale, Waingereza wa Kale, Makasisi wao, Wameksiko na Waperu . . . lazima wote wawe waliyapata mawazo yao ya kidini kutokana na asili ile ile na mahali pale pale. Kila mahali tunaona sherehe zenye kufanana kwa ajabu, mila, mapokeo, na katika majina na uhusiano kati ya miungu yao ya kiume na ya kike.” Kwa wazi, wakati Wababeli hao wa kwanza walipolazimishwa wahamie kwenye sehemu zote za dunia, walikwenda pamoja na mawazo yao ya kidini kwenye makao yao mapya.
Walakini je! habari hiyo inaweza kutusaidia tuitambue dini ya haki leo?
[Maelezo ya Chini]
a Kwa sababu zaidi zilizo thabiti za kuikubali Biblia kuwa kweli, tazama kitabu Is the Bible Really the Word of God?, kilichochapishwa na Sosaiti.
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Utatu wa miungu. Matumizi ya sanamu. Unajimu. Kuwapo kwa roho zisizoonekana. Sehemu ya kiroho ya mwanadamu inayoendelea kuishi baada ya kifo. Imani hizo zinafanana katika dini katika nchi nyingi
[Picha katika ukurasa wa 4]
BABELI YA KALE
Piramidi ya Maya
Utatu wa miungu wa Wahindu
Utatu wa miungu wa Jumuiya ya Wakristo
Ibada ya Maria
Ibada ya Mababu Waliokufa