Je! Tunaweza Kuipata Ile ya Haki?
TUNAPOJUA mahali dini hizo nyingi zilipoanza, inakuwa rahisi zaidi kujibu ulizo hili: Dini ya haki ni gani? Kwa wazi, dini ya kweli ni ile ambayo haiwezi kufuatishwa mpaka kwenye uasi huo wa kale juu ya Asili ya kweli ya uhai.
Kitabu Encyclopedia of World Religions kinatoa maelezo yenye kupendeza yanayoweza kutusaidia sisi hapa. Kinasema hivi: “Dini za ulimwengu kwa ujumla zinaweza kugawanywa kuwa za aina mbili— zile za kiunabii na zile za mafumbo. . . . zile za kiunabii [hatimaye zinatokana na] Wayahudi.”
Kulingana na maandishi ya Kibiblia, mababu waliokufa wa Wayahudi hawakujiunga na uasi katika Babeli uliofanywa juu ya Asili ya kweli ya uhai. Nasaba yao ya mababu waliokufa inatia wanaume kama Shemu, Ibrahimu, Isaka na Yakobo, ambao walijulikana kwa ajili ya kushikamana na ibada safi ya Mungu. Kwa kweli, Ibrahimu anaitwa “rafiki wa [Yehova].” “Yehova” ni jina la Mungu wa kweli, kama inavyosemwa waziwazi katika Biblia. (Kutoka 6:3; Zaburi 83:18; Yakobo 2:23) Je! kuna watu wo wote wanaomwabudu Yehova katika njia ambayo Ibrahimu alimwabudu?
Nasaba ya Waabudu wa Kweli
Kwa sababu ya uaminifu wa Ibrahimu, Yehova Mungu aliahidi kwamba hatimaye wazao wake wangekuwa taifa la pekee machoni Pake. Ahadi hiyo ilitimizwa kwa Waisraeli wa kale. Wao walimsikia Mungu akisema hivi: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu.”—Kutoka 19:5.
Kwa miaka mingi ibada ya Yehova iliendelezwa duniani kupitia kwa Wayahudi, ingawa mara nyingi waliangukia dhambi na uasi wa imani. Hata hivyo, kwa kurudia-rudia Yehova aliwaambia kwamba yeye alikuwa akimpeleka mjumbe wa pekee ambaye angeletea wanadamu wokovu. Baada ya miaka 1,500 mjumbe huyo alitokea. Yeye alikuwa Yesu Kristo.
Kwa kusikitisha, mpaka wakati Yesu alipofika, Wayahudi walikuwa wamekengeuka sana kutoka kwa Yehova. Wao bado walidai kwamba walikuwa wakimwabudu, lakini, kama Yesu alivyowaambia viongozi fulani wao wa kidini: ‘Mmelitangua neno la Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu.’ (Mathayo 15:1, 6) Kwa sababu Wayahudi walimpinga Yesu, walikataliwa na Mungu. Yesu aliwaonya hivi: “Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu, nao watapewa taifa lingine lenye kuzaa matunda yake.”—Mathayo 21:43.
Ukristo
“Taifa” hilo lilipata kuwa ndilo kundi la Kikristo. Hao ni wale waliomkubali Yesu Kristo wakati Wayahudi, kwa ujumla, walipomkataa, na Mungu aliwabariki washikamanifu hao kwa ajili ya imani yao. Muda mfupi baada ya kifo cha Yesu, kwa njia ya kimwujiza Mungu aliwatia nguvu wafuasi wa kweli wa Yesu wazungumze katika lugha za kigeni—si kupayuka-payuka upuzi, bali wakazungumza katika lugha halisi ambazo wengine wangeweza kuzifahamu. Maponesho, ufufuo na miujiza mingine ilithibitisha uhakika wa kwamba, kweli kweli, hilo lilikuwa “taifa” ambalo Mungu alikuwa akitumia.—Waebrania 2:4; linganisha Matendo 2:1-4; 3:1-10; 9:32-41; 20:7-12.
‘Lakini kwa hakika,’ huenda ukasema, ‘Ukristo una mvurugo leo sawa na dini nyinginezo za ulimwengu. Mamia ya vikundi vinajiita kuwa vya Kikristo, hali vyote vinatofautiana na kupingana. Hilo lilitokeaje?’
Historia inaonyesha kwamba Wakristo wengi walifanya sawa kabisa na walivyofanya Wayahudi. Waliiasi imani. Waliuchanganya ujumbe wa Yesu na mafundisho, kutoka kwa dini nyingine. Kwa njia hiyo wakaanza kufundisha mafundisho, kama nafsi tatu katika mungu mmoja (Utatu wa miungu), na jambo hilo asili ni vyanzo visivyo vya Kikristo na visivyo vya Kiyahudi.
Kwa kweli, mafundisho hayo yalitoka wapi? Kuhusu Utatu wa miungu, mwanachuo mmoja aliandika hivi: “Neno ‘Utatu wa miungu’ halionekani po pote katika Agano Jipya. Wazo hilo lilichukuliwa tu na Kanisa miaka mia tatu baada ya kifo cha Bwana yetu; na asili ya wazo hilo ni ya kipagani kabisa.” (The Paganism in Our Christianity, cha Arthur Weigall) Hayo hayo yanaweza kusemwa juu ya fundisho la nafsi isiyokufa, matumizi yaliyoenea ya sanamu, kupendwa kwa unajimu na watu wengi na mafundisho mengine mengi pamoja na mazoea ya Jumuiya ya Wakristo yenye kufahamika. Yanafuatishwa mpaka kwenye ule uasi wa kidini wa kale katika Mesopotamia wala si kwenye Asili ya kweli ya uhai.
Hata hivyo, si Wakristo wote waliopotoshwa. Yesu mwenyewe alionya juu ya uasi imani huo, lakini akaahidi kwamba dini ya kweli ingeendelea kuwapo mpaka mwisho. (Mathayo 13:18-30) Basi, tunawezaje kuipata leo?
Kuipata Dini ya Kweli
Yesu alitoa amri ya kuitambua dini ya kweli. Yeye alisema hivi: “Kila mti mwema huzaa matunda mazuri.” Matunda mabaya yangetambulisha dini ya uongo, na matunda mazuri yangeonyesha wazi iliyo ya kweli.—Mathayo 7:15-20.
Ni nini matunda ambayo dini ya kweli itazaa? Kisanduku kilichopo hapa kinaonyesha baadhi ya matunda hayo, kama tunavyoambiwa katika Biblia. Ukilinganisha orodha hiyo na dini zote unazofahamiana nazo, tuna uhakika utatambua kwa haraka ile yenye kweli na ile isiyo na kweli.
Hata hivyo, utahitaji kuchunguza orodha hiyo kwa uangalifu. Kwa mfano, unaona kwamba alama moja ya dini ya kweli ni ‘kuwa na upendo wa kweli.’ Dini nyingi zinasema zina upendo huo. Lakini ikiwa kudanganya katika biashara, mwenendo mchafu, au choyo ni mambo ambayo yameenea kati ya washiriki wa dini fulani, je! kweli kweli wanapendana? Na ikiwa wako tayari kuuana katika mapinduzi au vita, upendo wao ni wa kweli kadiri gani? Vivyo hivyo, alama nyingine ni ile ya kwamba “msingi wa imani zao zote ni Biblia.” Bila shaka, washiriki wa makanisa mengi katika Jumuiya ya Wakristo wanadhani ndivyo ilivyo kwa zao. Lakini je! unaijua dini ambayo washiriki wote wanajisumbua kufungua Biblia waone kama ndivyo imani zao zilivyo?
Ukiwa na matatizo yo yote katika utafutaji wako, Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia.
Kweli kweli, jitihada ya kutafuta dini ya kweli inastahili. Kwa silika wanadamu wanaona uhitaji wa maisha bora zaidi ya yale wanayofurahia sasa. Dini ya kweli inaweza kuelekeza kwenye maisha hayo. Kama ilivyo tunauliza maulizo kama: “Kwa sababu gani tupo hapa?” “Kusudi la maisha ni nini?” Dini ya kweli inaweza kutuhusianisha na aliye Asili ya uhai wote, Yehova Mungu, ambaye atatujibu maulizo hayo. Pamoja na hayo, nyakati nyingine sisi sote tunahitaji sana uongozi katika kutatua matatizo yaliyo mbele yetu siku baada ya siku. Dini ya kweli inaweza kutupa uongozi huo.
Ndiyo, iko dini ya kweli, na tunaweza kuipata. Tukifanya hivyo tutapata baraka za milele, kwa maana Biblia inatuahidi hivi: “Wamtafutao [Yehova] hawatahitaji kitu cho chote kilicho chema.”—Zaburi 34:10.
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
ALAMA ZA KUTAMBULISHA DINI YA KWELI
◻ Wale wanaoizoea wana upendo wa kweli kati yao,—Yohana 13:35.
◻ Msingi wa imani zao zote ni Biblia.—Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:16, 17.
◻ Wanamwomba Mungu alitakase jina lake.—Mathayo 6:9; Zaburi 83:18.
◻ Wanatangaza ufalme wa Mungu katika dunia yote,—Mathayo 24:14.
◻ Wanajiepusha na mambo ya ulimwengu.—Yakobo 1:27; Yohana 17:14.
◻ Wanaweka ufalme wa Mungu na haki yake kwanza maishani-Mathayo 6:33.
◻ Wanasitawisha matunda ya roho ya Mungu.—Wagalatia 5:22, 23.
◻ Wanatii sheria zote za kibinadamu zisizopingana na sheria ya Mungu.—Warumi 13:1-7.