Jinsi Ufalme huo ‘Unakuja’
JUU ya kipindi cha wakati kinachobaki kabla “dhiki kubwa” haijatokea sisi hatujui. “Siku za mwisho” za taratibu ya mambo ya Kiyahudi zilikuwa kuanzia mwaka wa 29 mpaka 70 W.K., hiyo ikiwa ni jumla ya miaka 41. Lakini sasa taratibu iliyo kubwa zaidi inaelekeana na kufikilizwa kwa hukumu ya Mungu. Hiyo ndiyo taratibu nzima ya ulimwengu wa Ibilisi, na katika taratibu hiyo milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, hasa Ukristo wa bandia wa Jumuiya ya Wakristo, ndiyo sehemu yenye kulaumika zaidi. Kwa hiyo si ajabu kwamba “siku za mwisho” za taratibu hii ya ulimwengu zimeendelea kusonga kwa miaka 68 mpaka sasa, tangu 1914 mpaka 1982. Jambo hilo limetukia kwa kusudi fulani. Kusudi gani?
2. Ni kwa njia gani Wakristo wa karne ya kwanza walivyokuwa mfano kwetu leo?
2 Haya basi, Wakristo wa karne ya kwanza walifanya nini wakati wa “siku za mwisho” za taratibu ya Kiyahudi? Wao walihubiri. Wao walisikizisha onyo. Na kwa hiyo, baada ya makumi machache tu ya miaka mtume Paulo angeweza kuandika hivi: ‘Tumaini la Injili mliyosikia habari zake, lilihubiriwa katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu.’—Wakolosai 1:23.
3, 4. Roho ya Yehova imetia nani nguvu watoe ushuhuda wa kisasa, na matokeo yakawa nini?
3 Sasa, leo, shamba ni pana zaidi. Shamba hilo ndio ulimwengu, ulimwengu wote! Lakini tena, wakiwa chini ya nguvu kubwa yenye kutia uwezo ya roho ya Mungu, mashahidi wa Yehova wa Kikristo wamekwenda kwenye miisho ya dunia. Wameihubiri kweli katika lugha zaidi ya 160 mbalimbali. Wamekusanya pamoja watu wenye mfano wa kondoo kutoka mataifa yote, kufikia watu 5,980,000 waliohudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu mwaka wa 1981. Akiwa jamii ya mlinzi, “mtumwa mwaminifu mwenye akili” amehubiri siku ya kisasi cha Yehova, na wakati ule ule akawa akiwafariji wote wanaoomboleza. (Isaya 21:11,12; 61:1, 2) Kuhusiana na kazi yao ya kuhubiri kwa muda wa karne moja iliyopita, Mashahidi wa Yehova wamegawa Biblia na vitabu vizuri kufikia hesabu ya milioni 460, nayo magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yakafikia hesabu ya bilioni 4 na milioni 767. Wewe hukubali kwamba huu umekuwa ushuhuda mkubwa ajabu kwa jina na ufalme wa Yehova?
4 Mahubiri haya ya habari njema za Ufalme sasa yanakaribia upeo wayo! Wakiwa wameungana duniani pote, misionari waaminifu, mapainia na wahubiri wa makundi wametimiza kazi kubwa ajabu —“si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu,” asema Yehova wa majeshi. (Zekaria 4:6) Kwa sababu hiyo, mamilioni ya wanadamu wamejitokeza kujiunga na “mtumwa mwaminifu,” wakisema: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.”—Zekaria 8:23.
5. Danieli sura ya pili inaonyeshaje ‘kuja’ kwa Ufalme huo?
5 Kwa hiyo sasa kilichobaki ni ufalme wa Mungu “uje”! Uje kwa njia gani? Naam, katika njia ile ambayo nabii Danieli aliitabiri katika sura ya pili ya unabii wake. Aliusimulia ufalme wa Kimasihi, kama “jiwe” lililokatwa kutoka “mlima” wa mfano wa enzi kuu ya Yehova inayodumu daima dawamu. Kama vile mzinga, ufalme huo unakwenda mbio, naam, ‘unakuja,’ ulipige chini kwa dharuba lile umbo la serikali zilizotengenezwa na wanadamu, na kuzisaga-saga tikitiki ziwe unga-unga. Baada ya hayo “jiwe” hilo lililo Ufalme linakuwa “mlima,” likiijaa dunia, kisha Yehova anapata sifa na utukufu.— Danieli 2:34, 35, 44, 45.
Kumfanya Ukiwa Yule “Kahaba”
6. (a) Kwa sababu gani haipasi kushangaza kwamba Yehova atatumia mashirika ya kibinadamu yenye kutaka mapinduzi ili kufikiliza hukumu? (b) Yerusalemu una mfano gani wa kisasa, nayo pia ni sehemu ya milki gani?
6 Walakini, kuna mambo fulani yatakayotangulia kupondwa-pondwa kwa mwisho kwa utawala wa mwanadamu katika dunia. Kitabu chenye unabii cha Ufunuo kinaonyesha kwamba kwanza Yehova atatumia mamlaka zenye kutaka mapinduzi kutokana na Umoja wa Mataifa ziwe kama nyundo ya uharibifu. Jambo hilo halipasi liwe la kushangaza, kwa maana nyakati za kale Yehova aliitumia mamlaka ya ulimwengu ya Babeli kama “nyundo ya dunia yote” katika kufikiliza hukumu yake juu ya mataifa, na juu ya Yerusalemu hasa wenye kuasi imani. (Yeremia 50:23) Yerusalemu wa zamani unafananishwa siku hizi na dini za Jumuiya ya Wakristo. Dini hizo zinasema zinamwabudu yule Mungu wa Biblia, lakini badala ya kufanya hivyo zimejifanya sehemu ya milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Unabii huo unaitambulisha milki hii kuwa ‘Babeli Mkuu, mama wa makahaba na machukizo ya nchi.’—Ufunuo 17:5.
7. (a) Dini ya uongo imefanya uchaguzi gani? (b) Wanenaji wayo wanaonyeshaje tumaini lao? (c) Lakini Maandiko yanaonyesha tumaini la wanadamu kuwa nini?
7 Milki hiyo ya ulimwengu ya dini ya uongo imejifanyia uchaguzi. Imeukataa ufalme wa Mungu unaokuja ukiwa mikononi mwa Masihi wake ikapendelea mashirika mengine yaliyotengenezwa na wanadamu. Leo, viongozi wa dini za ulimwengu wanauunga Umoja wa Mataifa mkono kwa mioyo yao yote. Kulingana na maneno ya rabi mmoja wa Kiyahudi, Umoja wa Mataifa “ndilo tumaini pekee la amani yenye kudumu katika ulimwengu ambao unategemea shirika hilo ndipo uweze kuokoka.” Naye Papa John Paul wa Pili analieleza shirika hilo kuwa “ndipo mahali pakuu pa amani na haki ya hukumu.” Lakini je! Umoja wa Mataifa umeiletea dunia yetu amani na haki ya hukumu? Je! kweli Umoja wa Mataifa “ndilo tumaini pekee” la wanadamu? Au tumaini hilo ni ufalme wa Mungu? Kusema kweli, tumaini hilo linategemea ‘kuja’ kwa ufalme wa Masihi kupitia Masihi!—Mathayo 12:18, 21.
8. Ni usemi gani wa Katiba ya Umoja wa Mataifa unaotukumbusha juu ya 1 Wathesalonike 5:3, na kwa sababu gani jambo hilo lapasa kutupendeza?
8 Katika Katiba yake, Umoja wa Mataifa unasema kusudi lake la kwanza ni “kudumisha amani na usalama wa mataifa yote.” Je! sisi kama Mashahidi wa Yehova, hatusikii maneno hayo yakionyesha jambo tunalolijua sana? Ndiyo! Kwa maana mtume Paulo alisema: “Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa.” (1 Wathesalonike 5:3) Kwa hiyo, tunaposonga mbele kuielekea hatua ya mwisho ya hizi “siku za mwisho “hatutaki tupotezwe na ahadi za kibinadamu na sauti zenye kupotosha zinazopazwa zikisema “Amani na salama!” Hilo litakapopazwa na mataifa, ni nini kitakachofuata? Unabii huo unatuambia: ‘Uharibifu wa ghafula, uharibifu wa kushtukiwa upesi usioweza kuepukwa’!
9. (a) Dini ya uongo inangojea mwisho gani wenye msiba? (b) Viongozi wa siasa na wa biashara kubwa-kubwa watalionaje jambo hilo, na kwa sababu gani?
9 “Mapenzi” ya haramu yanayofanywa kati ya dini na Umoja wa Mataifa yatafikia kikomo chenye msiba mkubwa sana! Katika “saa moja” mambo yote yatakuwa kwisha! Zile “pembe kumi” za “mnyama” ambaye ni Umoja wa Mataifa zitamgeuka Babeli Mkuu. Sehemu za kijeshi zenye kutaka mapinduzi zilizomo katika shirika hilo la ulimwengu mzima zitamrarua-rarua, zimfanye mkiwa, zimvue mavazi yake ya anasa nyingi kisha zimteketeze awe majivu. Wanasiasa waliotumia dini ya uongo ili wadumishe cheo chao pamoja na waendeshaji wa biashara kubwa-kubwa ambao wamemtumia awe mahali pao pa kujificha wanapoendesha magendo yao ya kuuza silaha za vita kwa siri na kujipatia faida kubwa-kubwa kwa kupandisha sana bei, watamlilia kwa sauti za masikitiko wakiwa mbali. Wataomboleza, wakisema: “Ole! Ole kwako Babuloni, mji maarufu na wenye nguvu! Kwa muda wa saa moja tu adhabu yako imekupata. . . . kwa saa moja tu utajiri wako umetoweka!”—Ufunuo 18:10, 17, HNWW.
Har—Magedoni—Na Baada
10. Kwa sababu gani Har–Magedoni itafuata upesi, na matokeo yawe nini?
10 Mambo yatakwenda mbio-mbio yamalizike upesi. “Pembe” zile zile za kisiasa zitakazomharibu yule “kahaba” mkuu ndizo zitakazowageuka Mashahidi wa Yehova wenye kuonekana kana kwamba hawana mtu wa kuwalinda. Lakini hapo sasa watajikuta wakipigana na yule ambaye si mwingine ila ni ‘Mfalme wa wafalme, na Bwana wa mabwana’ aliyetokezwa na Yehova. Watakuwa wamejileta kwenye Har–Magedoni. Hapo ndipo ufalme wa Yehova ulio mikononi mwa Masihi ‘utakapokuja’ ulitende tendo lake lililo kubwa zaidi ya yote katika kuondolea lawama enzi kuu ya Yehova na watumishi wake waaminifu. Pigano hilo litaonyesha mambo wazi na kukata maneno kabisa. Utawala wa Shetani ambao umeitawala dunia kijeshi na kisiasa utafutiliwa mbali, naye Shetani mwenyewe atafungwa na kuvurumishwa kwa nguvu nyingi ndani ya lile shimo kubwa sana kwa miaka 1,000, “asipate kuwadanganya mataifa tena.”—Ufunuo 16:14; 17:14; 19:11-21; 20:2, 3.
11. (a) Halafu ‘kuja’ kwa Ufalme huo kutawabarikije wanadamu wote? (b) Ni uhamisho gani utakaofuata miaka 1,000 imalizikapo, na kukiwa na taraja gani lenye furaha?
11 Halafu? Naam, ndipo ufalme wa mileani utakapokuwa umetufikia hapa! Weee, jamani! waokokaji wa Har–Magedoni watafurahi furaha iliyoje! Looo, dunia yote itajawa na upendo, furaha na amani kama nini! Hm-m-m-m! itakuwa ajabu kama nini ufufuo utakapowaunganisha tena wapendwa kote kote ulimwenguni! Ai! utaratibu uliopangwa kuwaponya watu utaleta msisimuko ulioje wakati Yesu na wafalme-makuhani wenzake wazitumiapo faida zenye kuponya za dhabihu yake ya ukombozi, wakiwafanya mabilioni ya wanadamu wakifikie kipimo cha ukamilifu! Tena wote watakaoliokoka jaribu la mwisho la Shetani kisha waache kuwa katika milki ya ufalme wa Kristo wa miaka 1,000 na kuingia katika milki ya enzi kuu ya Yehova ya milele watakuwa na shangwe nyingi kama nini kwa kuweza kuishi milele wakati mambo mazuri ajabu yatakapoendelea kutokea mpaka umilele!—Ufunuo 20:7-9; 21:3, 4.
12. Ni nini kinachowezesha mambo hayo mazuri ajabu, kwa hiyo sasa tunapaswa kuchochewa tufanye nini?
12 ‘Kuja’ kwa ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Masihi ndiko kunakofanya mambo yote hayo yaliyo mazuri sana yawezekane. Wakati wa hizi siku za mwisho-mwisho kabisa za taratibu ya Shetani, je! mambo hayo hayavuti mioyo yetu tutake kuwaeleza wengine habari za ‘Mfalme wa wafalme’ aliyemtokeza na habari za ufalme wa Kimasihi? (Zaburi 145:11; Matendo 2:11; Waebrania 12:28) Je! hatuvutwi tusali tukiwa na mioyo yenye kuwaka shauku kumwambia Baba yetu wa kimbinguni, “Ufalme wako uje”?—Mathayo 6:9,10.
13. Kwa sababu gani tunapaswa kusali kwa moyo wote ili Ufalme huo “UJE”?
13 Ndiyo, “UJE,” ufalme wa Mungu uziharibu kazi za Shetani na tengenezo lake, uziondoe duniani! Ndiyo, “UJE,” uwape wanadamu wote serikali ya namna ifaayo! Ndiyo, “UJE,” uulete utawala wa mileani wenye mambo matukufu, ili Paradiso irudishwe, ili wafu wafufuliwe kisha wanadamu wote wainuliwe wafikie kipimo cha ukamilifu wa kibinadamu! Ndiyo, “UJE,” Ee ufalme wa Masihi ili utakase kwa umilele wote jina la Bwana Mwenye Enzi Kuu YEHOVA!
—Kutoka The Watchtower, May 1, 1982.
UFALME HUO KATIKA KUSUDI LA MUNGU
□ Manabii wa Yehova waliutabiri
□ Ulifananishwa na ufalme wa Daudi
□ Wanafunzi wa Yesu waliuhubiri
□ Ulisimamishwa mbinguni, 1914
□ Ulihubiriwa uwe ushuhuda kwa mataifa yote, tangu 1919
□ Sasa “mkutano mkubwa” unakusanywa kwa ajili ya wokovu
□ Mwisho unakuja—Kilio cha “Amani na Salama” kikitolewa! ‘Babeli Mkuu’ yaharibiwa Ufalme wafanya ukiwa watawala wa wa kisiasa, majeshi, wenye kuunga mkono
□ Ufalme huo waijaza dunia kwa furaha, amani, sifa kwa Yehova
1. Ni kwa sababu gani haishangazi kwamba “siku za mwisho” za dunia zimeendelea kufika 1982?
[Picha katika ukurasa wa 21]
Jiwe hilo la Ufalme lenyewe linakuwa “mlima” unaoijaza dunia