Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 1/15 kur. 4-5
  • Unaweza Kuwa na Uhakika Kadiri Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Unaweza Kuwa na Uhakika Kadiri Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Habari Zinazolingana
  • Kutafuta Maisha Yenye Usalama
    Amkeni!—1998
  • Ni Kitulizo Gani Kinachoweza Kupatikana Sasa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Je! Wanadamu Wanaweza Kuleta Amani na Usalama Wenye Kudumu?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Pigo la Ukosefu wa Kazi ya Kuajiriwa
    Amkeni!—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 1/15 kur. 4-5

Je! Unaona Utakuwa Salama?

Unaweza Kuwa na Uhakika Kadiri Gani?

JE! WEWE umejaribu kufanya mtihani wetu katika ukurasa wa 3? Ni majibu gani ambayo umejibu Ndivyo? Ikiwa umejibu “Ndivyo” ulizo moja au zaidi, si wewe peke yako unayeona wasiwasi wa kukosa usalama. Watu wengi sana wa dunia wanaishi sasa katika hali ya wasiwasi na wana mashaka sana juu ya wakati ujao.

Huenda maelezo mafupi yanayofuata yakakusaidia uelewe ni kwa kadiri gani matatizo haya yanavyopata watu ulimwenguni pote.

KUKOSA KAZI YA KUAJIRIWA: Sehemu kubwa ya Ulaya ina pigo la watu wengi sana kukosa kuajiriwa kazi, na hiyo inaletea mamilioni ya jamaa wasiwasi wa kukosa usalama. Ndivyo ilivyo katika United States (Amerika), ambako watu zaidi ya milioni tisa hawako kazini. Kuhusu ongezeko linaloendelea kuwapo katika hali ya kukosa kazi, Ivor Richard, kamishina wa Ulaya wa mambo ya kiujamii, alionya hivi: “Pasipo shaka jambo hili litaleta mikazo mikubwa sana juu ya jamii za watu wetu. . . . [Linaweza] kuelekea kuiharibu misingi ya jamii zetu za kidemokrasi na zile zilizo huru.” Je! wewe unaweza kujiona salama ikiwa huna kazi?

INFULESHONI: Je! pesa zako zinanunua vitu vichache sana kuliko miaka kumi iliyopita? Ukosefu wa mafuta ya matumizi muda wa miaka zaidi ya kumi iliyopita ulionyesha wazi kabisa kwamba karibu kila nchi ingepatwa na infuleshoni. Kwa mfano, katika Uingereza bidhaa ambazo zingeweza kununuliwa kwa paundi 1 (£1) mwaka wa 1961 zinagharimu sasa karibu paundi 6. Nchi nyingi zina infuleshoni kubwa sana kuliko hiyo. Labda nchi yako ni moja kati ya hizo. Ikiwa pesa zako zinaendelea kupungukiwa na uwezo wa kununua vitu, je! unaweza kujiona una uhakika juu ya wakati ujao?

UHALIFU: Ni nani asiyetembea akiwa na woga wa kutendwa uhalifu? Uhalifu ni pigo la mataifa yote. Vichwa vya hivi majuzi vya magazeti ya Kijapani vinakazia tatizo la nchi hiyo: “Uhalifu wa Watoto Unatia Serikali Wasiwasi,” “Kuhusika kwa Watoto Wadogo Katika Uhalifu Kunaweka Rekodi.” Mahakimu wenye kuachilia makosa na hukumu zenye kutegemea rushwa zimefanya wahalifu warudie upesi matendo yao wakiwa huru katika nchi nyingi. Makala moja ya mhariri ya gazeti la Kispania ilitokeza ulizo hili lenye kuumiza mioyo, “Je! kwani sheria za hukumu zimeondolewa zikaisha?”

MAKAO YA HALI YA CHINI: Mamilioni ya jamaa kote kote ulimwenguni yangali yakiishi katika makao yenye kujawa na panya. Komba-mwiko wanamiminika kweli kweli katika makao hayo na hayana maji ya mifereji. Tunaposema hivyo hatutaji tu zile hali za watu wanaolala kwenye barabara za Bombay, India, au kwenye makaburi ya Cairo, Misri, ili kujaribu kutumia mifano hiyo kwa werevu kama njia ya kuthibitisha ndivyo ulimwengu wote ulivyo. Namna gani ile mitaa ya vitongojini na makao machafu-machafu ya umaskini yaliyo katika miji mingi mikubwa ya mataifa yanayosemwa ‘yana maendeleo’ katika nchi za Wazungu? Ripoti moja kutoka kwenye makao ya Cabrini-Green katika Chicago, USA, inasema: “Wakiisha kuingia katika nyumba, wakaaji wanakutana na mapanya wakubwa sana na komba-mwiko wengi walioko kwa wingi katika mengi ya majengo ya Cabrini-Green.” Maskini walio wengi hawana la kufanya. Wakati ujao hauna matumaini mazuri kwao.

NJAA: Chanzo fulani cha habari kinasema kwamba sehemu mbili kwa tatu za watu wenye njaa ulimwenguni ziko katika nchi tisa zilizo na asilimia 27 za idadi ya watu ulimwenguni. Gazeti Financial Times la London lilieleza hivi chini ya kichwa “Maskini zaidi sana wazidi kuwa maskini”: “Labda jambo lililo hatari kuliko yote ni kwamba Afrika imeshindwa kwa muda mrefu kulisha watu wake wanaoendelea kuongezeka ajabu, na hali hiyo ya kushindwa inaendelea kuongezeka.” Hata katika mataifa yenye maendeleo kutokupata mapato yanayolingana na kuwa na umaskini ni mambo yanayoharakisha njaa sehemu ambazo zinaonekana kuwa na wingi wa vitu. Je! kila siku unahangaikia pia chakula chako cha siku hiyo?

MAGOMBANO NYUMBANI: Inaripotiwa kwamba asilimia zaidi ya 40 za ndoa katika United States (Amerika) zinavunjika. Katika nchi iyo hiyo watoto wapatao milioni kumi na mbili wa chini ya miaka kumi na minane ni wa wazazi waliopeana talaka. Katika sehemu nyingi za ulimwengu mamilioni ya watu wazima wanaoishi pamoja hawajapata kuoa au kuolewa hata siku moja. Huko kuvunjika-vunjika kwa jamaa kunakuwa katika hesabu ya wanawake walioachwa wa ndoa za kimila na watoto wa haramu. Je! watu wazima na watoto wanaweza kujiona salama ikiwa mwungano wa jamaa unavunjwa na kutenganishwa?

KUHANGAIKIA WATOTO: Jeuri katika shule inazidi kusumbua sana. Mwaka wa 1981 Mji wa New York uliweka kwa mara ya kwanza walinzi wa shule 420 katika shule zake za masomo ya chini kujaribu kupunguza hesabu ya mashambulio yanayofanywa kwa waalimu na wanafunzi. Shule katika Uingereza na Japan pia zinapatwa na jeuri nyingi. Hali ya kukosa nidhamu ikiwa kubwa hivyo, je! wewe unaweza kuwa na maoni ya kwamba elimu ya mtoto wako ina usalama?

KUSHUKA MOYO: Gazeti Toronto Star la Canada lilisema: “Mamilioni ya watu wa Amerika ya Kaskazini wanavumilia kwa unyamavu maumivu yanayoleta sana hasara katika kazi​—na maisha za watu. . . . Kushuka moyo ni hali inayopata watu wengi sana na kunaleta hasara kubwa sana katika jamii ya watu.” Gazeti ilo hilo lilimtaja daktari wa akili Emmanuel Persad kuwa alisema: “Wachunguzi wengi wanaamini hali ya kushuka moyo imeenea zaidi miaka ya majuzi kwa sababu ya anguko kubwa la ghafula katika hali ya uchumi, kwa sababu ya jamaa kuvunjika-vunjika, na watu kujitenga na wenzao.” Je! hali ya kushuka moyo iliyoenea kote haionyeshi kuna tatizo kubwa la watu kutokutumainiana?

DAWA ZA KULEVYA: Mamilioni ya watu wanategemea sana mazoea ya dawa za kulevya. Mali nyingi sana zinaharibiwa kila siku kununua tumbako na kutumia vibaya pombe na dawa za kulevya. Je! hiyo inampa mtu maoni ya kujisikia salama?

VITA VIKUBWA VINGINE—VINA UWEZEKANO WA KUTOKEA, HUENDA VIKAKOSA KUTOKEA AU HAVIWEZI KUEPUKWA? Viongozi fulani wa ulimwengu wanaendelea kufuata maoni ya kwamba vita vya nyukilia vinaweza kupiganwa na ushindi upatikane, badala ya kukaa kama hapo zamani wakiwa wameshindwa na la kufanya kwa sababu ya lile kisio walilokuwa nalo la kusema pande zote mbili zitaangamizana vita ikitokea. Je! wewe una uhakika hakutakuwa na vita vikuu vingine?

Badiliko baya hilo la maoni linaonyesha nini? Je! kweli unaweza kujisikia ukiwa na wakati ujao salama wako na wa jamaa yako? Je! tuna uchaguzi mwingine isipokuwa kuwatumainia viongozi wa kisiasa na kijeshi na viongozi-wafariji wa kidini? Je! kuna njia hakika ya kupitia ili tupate usalama? Makala zinazofuata zitatoa jibu la Biblia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki