Je! Unaona Utakuwa Salama?
Ni Kitulizo Gani Kinachoweza Kupatikana Sasa?
NI KWA kadiri gani unaweza kujiona salama kwa habari ya matatizo yaliyotokezwa katika ukurasa wa 3? Daudi mshairi-mfalme anatoa jawabu la kujiona salama zaidi hata sasa. Yeye aliandika hivi: “Mimi nimeweka Yehova mbele yangu daima. Kwa sababu yeye yuko kwenye mkono wangu wa kuume, mimi sitafanywa nitikisike. . . . Mwili wangu mwenyewe utakaa katika usalama.”-—Zaburi 16:8, 9, NW.
‘Kuweka Yehova mbele yako’ kunasaidiaje katika matatizo na hofu zinazokuzunguka? Acha turudie kwa ufupi maulizo yaliyotangulia kutokezwa kisha tuone namna shauri la Yehova linavyoweza kusaidia.
Kutumia kila siku kanuni za Biblia kunaweza kukupa nafasi za kuajiriwa kazi. Kuzitumia kunaweza kufanya mtu awe mfanya kazi mwaminifu, mnyofu na mwenye bidii, kwa maana Neno la Mungu linaonya hivi kwa upole: “Mwibaji asiibe tena; bali afadhali afanye juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe.” (Waefeso 4:28) Kwa kawaida, matajiri wa kazi wenye kutumia akili wanatafuta mfanya kazi mwenye kutegemeka. Kwa hiyo ingawa kuna tatizo la kukosa kazi, tatizo lenyewe halitakuwa kubwa sana kwa mfanya kazi halisi Mkristo.
Njia ya maisha ya Kikristo inaweza hata kupunguza maumizo ya infuleshoni. Kwa sababu gani? Kwa sababu Mkristo anatumia kwa hekima mali zake chache. Hakuna sehemu ya mapato yake inayoharibiwa bure kwa kucheza kamari, kuvuta tumbako au kutumia vibaya pombe na dawa za kulevya. Yeye hanunui vitu vya bei kubwa sana ili ajionyeshe. Hiyo ni namna ya ubatili “kwa sababu kila kitu kilichomo katika ulimwengu tamaa ya mwili na tamaa ya macho na kujionyesha kwa mtu mali yake—hakitokani na Baba [Mungu], bali chatokana na ulimwengu.”—1 Yohana 2:16, 17, NW.
Maoni ya Mkristo wa kweli yanaweza kusaidiaje katika tatizo lile linalokuwako daima la uhalifu? Biblia inashauri hivi: “Usiingie katika njia ya waovu, wala usitembee katika njia ya wabaya. Jiepushe nayo, usipite karibu nayo.” (Mithali 4:14, 15) Kwa sababu ya shauri kama hilo Mkristo anajihadhari kwa hekima asiwe katika mahali na hali zenye kuelekea kuwa na uhalifu. Anaepuka kushirikiana na watu wenye maelekeo ya kufanya uhalifu.
Ingawa kwa sababu za kiuchumi Wakristo wengi wanalazimika kuishi katika makao ya hali ya chini, kanuni zao zenye kutegemea Biblia zinawaongoza kuwa na nyumba safi na za kupendeza, ambazo zina hali safi kupita za jirani wengi. Wao wanajua kwamba usafi wa kimwili ni sehemu ya ibada ya kweli ya yule Mungu mtakatifu, Yehova. Nabii Isaya alionya kwa upole hivi: “Iweni safi ninyi.”—Isaya 52:11.
Wakristo wanafundishwa kusali hivi: “Tupe leo mkate wetu kwa siku hii.” (Mathayo 6:11, NW) Ombi hilo linaonyesha kuwa na nia ya mahitaji ya chakula cha kila siku. Nia hiyo inakubali chakula kinachotosha kila siku bila kuwa na wasiwasi wa bure juu ya mahitaji ya kesho. Mwaminifu akitimiza fungu lake, hapo anajua hataachwa bila mahitaji ya kila siku ya maisha kama vile Daudi mtunga zaburi aliandika: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.”—Zaburi 37:25.
Je! inawezekana kuepuka au kupunguza magombano ya kinyumbani? Biblia ina-shauri hivi: “Asiye mwepesi wa hasira hutuliza mashindano.” (Mithali 15:18) Pia: “Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya; tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, . . . mkasameheane.” (Waefeso 4:31, 32) Je! ndoa zote zisingefaidika kwa kuonyesha roho hiyo ya Kikristo?
Wazazi wengi wanahangaika juu ya watoto wao sana na hasa juu ya vile wanavyokazwa na watoto wa rika lao shuleni wafanye uasherati. Katika jamaa za ushikamanifu kwa kanuni na kwa jamaa unapasa kukaziwa sana ili kusaidia watoto wapinge vishawishi vya kisasa. Biblia inashauri wazazi wasitawishe uenzi (urafiki) wa karibu pamoja na watoto wao, kusawazisha upendo na nidhamu (adabu). Nidhamu maana yake ni ushirika, elimu, kuzungumza kwa kutolea mtu sababu na kumsahihisha makosa.—Waefeso 6:4; Mithali 1:8.
Mkristo aliye na tumaini hakika kwa wakati ujao hataumizwa sana na zile hali zinazoleta kushuka moyo na hangaiko kubwa. Tegemeo lake la maisha ya kila siku halitakuwa ni mazoea ya kutumia dawa za kulevya ili zimsaidie kutoroka matatizo ya maisha. Ni kama vile mtunga zaburi alivyoeleza: “Katika amani nitajilaza na kupata usingizi mara, maana Wewe, [Yehova], peke yako, ndiwe unijaliaye kukaa salama.”—Zaburi 4:8.
Ingawa Wakristo wanajua kwamba kuna uwezekano wa kutokea vita nyingine kati ya mataifa, wanajua pia kwamba mwenye dunia ni Mungu, si mwanadamu. Wanajua kwamba Mungu hataruhusu mwanadamu aharibu kabisa ama dunia ama jamaa ya kibinadamu kwa kutumia vita ya ulimwengu ya nyukilia kwa sababu “ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya . . . aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:8) Ndiyo sababu ameahidi na akathibitisha kabisa kwamba atawapa wanadamu watiifu “mbingu mpya na nchi mpya.” Si sayari mpya na anga jipya bali mfumo mpya kabisa wa mambo ya kidunia unaotegemea elimu ya kiroho kwa watu wote. Hilo linapatana na unabii wa Isaya ulioongozwa na Mungu: “Maana dunia itajawa na kumjua [Yehova], kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 65:17; 11:9.
Ni namna gani na kwa sababu gani badiliko hilo litafanywa? Je! Mungu atawatumia viongozi wa ulimwengu kuleta usalama? Je! wewe utashiriki katika wakati ujao wenye uhakika? Makala ya mwisho ya mfululizo huu itajibu maulizo hayo.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Kutumia mashauri ya Biblia kunafanya nyumba ziwe safi zaidi, hata kama mazingira si mazuri