Je! Unaona Utakuwa Salama?
Wakati Ujao Salama Unaonekana!
“USIWEKE tumaini lako katika wanadamu walio katika mamlaka, wala katika mwanadamu ye yote anayeweza kufa—yeye hawezi kuokoa.” (Zaburi 146:3, The Jerusalem Bible) Shauri hilo la wazi lililotolewa miaka zaidi ya elfu mbili iliyopita linafaa zaidi sana leo wakati ambao wanasiasa, wanasayansi, viongozi wa kidini na wa kijeshi wanajaribu masuluhisho ya namna zote kwa matatizo ya wanadamu.
Kwa sababu gani tusiwatumainie “wanadamu walio katika mamlaka”? Kwa sababu si juu yao kuamua ni hali gani itakayoipata dunia na wanadamu mwishowe, hata ingawa huenda wasiamini hivyo. Biblia inataja hivi waziwazi: “Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya [Yehova], dunia na wote wakaao ndani yake.” (Zaburi 24:1) Ndiyo, dunia ni mali ya Yehova, ni kibago (kiti) cha nyayo zake, lakini amewapa wanadamu waitumie kwa kuithamini.—Mwanzo 1:28; Isaya 66:1.
Je! mwanadamu ameitunza ifaavyo mali ambayo amekabidhiwa? Je! amejionyesha kuwa anastahili kuendelea kuwa mpangaji katika makao haya mazuri kama almasi katika ulimwengu wote? Uchafuzi mwingi sana ambao mwanadamu ameeneza kote kote duniani ni ushuhuda mwingi wa kuonyesha ameshindwa. Takataka na uchafu unaoachwa katika barabara za mji, zinazomwagwa ndani ya mito na kuenea katika fuo za bahari kuu ni ushuhuda unaoonekana wazi kwamba wengi wa wakaaji wa dunia ni wapangaji wasiofaa. Matendo yao ya kichoyo yanaelekea kuharibu wakati ujao na usalama wa wale wanaotaka kupata uzima juu ya dunia safi.
Ni hatua gani zinazochukuliwa na mamlaka za kibinadamu wakati mali inapokosa kuheshimiwa kisha watu wanakosa kulipia nyumba kodi? Hatua ya kisheria inachukuliwa ili wakosaji waondoshwe katika nyumba wanamokaa. Je! Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hana haki ya kuwaondosha wale wanaoelekea kuharibu usalama wa dunia wa wakati ujao? Ndiyo, hakika anayo, kwa kuwa “ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya . . . hakuiumba ukiwa.”—Isaya 45:18.
Je! Kuna Mfano wa Zamani wa Jambo Hili?
Wakati Yehova Alipoondoa haki za kuikaa Nchi ya Ahadi kutoka kwa wakaaji wa kwanza kisha akawapa Israeli haki hizo miaka 3,500 iliyopita, aliwawekea pia miongozo ya wazi: “Hamtaitia unajisi nchi ambayo mwaiketi; kwa kuwa damu huitia nchi unajisi . . . Kwa hiyo msiitie unajisi nchi muiketiyo.” (Hesabu 35:33, 34) Baada ya wakati wa Israeli, historia ya kibinadamu imeshindwa kupata mafanikio katika jambo hilo. Muda wa karne zote dunia imechafuliwa kwa damu na mamilioni ya watu wenye kuuawa katika vita na mauaji ya kisiasa au ya kidini. Kisha upeo umefikiwa katika hesabu ya vifo vya karne yetu ya 20 vyenye kuletwa na uhalifu na kuharibiwa kwa mimba.
Mwishowe Israeli wa kale walipuza sheria za Yehova nao wakakiona—walifukuzwa wakaondoka nje ya mipaka ya nchi hiyo. Taifa la Yuda lenye makabila mawili lilifuata njia iyo hiyo kisha likajipatia kemeo linalofuata: “Dunia imetiwa unajisi kwa watu wanaoikaa; kwa maana wameziasi sheria, wameibadili amri, wamelivunja agano la milele.” (Isaya 24:5) Kwa sababu hiyo, walipelekwa uhamishoni muda wa miaka 70. Kwa mfano uo huo Yehova atachukua hatua katika hiki kizazi kinachopita mbio sana.—Luka 21:25-36.
Yehova atachukua hatua gani? Biblia inatoa unabii wa kwamba ulimwengu wote unakaribia kusafishwa kila mahali kwa agizo la Mungu. Hatua hiyo ya kusafisha ni ile vita ya Har–Magedoni iliyotabiriwa tangu zamani. Hilo halitakuwa pigano kati ya nchi za ubepari na za Ukomunisti. Suala kuu kupita masuala yote kulingana na maoni ya Mungu linazizidi kwa mbali siasa ovyo za kibinadamu. Suala hilo linahusu matumizi ya Yehova yenye uadilifu ya enzi kuu juu ya dunia. Wapinzani wake, “majeshi ya pepo wabaya” na washirikiani wao wa kibinadamu, wanafikiri wanaweza kuikaa dunia mpaka milele na kukataa kukubaliana na hatua yo yote ya kimungu. (Waefeso 6:12; Zaburi 14:1-3) Har–Magedoni, ambayo ni hukumu ya Yehova ya kuondoa wasiostahili, itaondolea dunia wachafuaji wote wa kibinadamu wanaoleta uchafu kwenye sayari hii yenye thamani kubwa. Utendaji wa Yehova wa kusafisha dunia utaondoa pia na kuyamaliza nguvu “majeshi ya pepo wabaya” ambayo kwa muda mrefu yameongoza wanadamu wachoyo, wenye kutaka sana mamlaka ya kutawala watu.—Ufunuo 16:14, 16; 20:1-3.
Ni jambo gani litakalofuata mauaji ya wabaya kwenye Har–Magedoni? Yehova ameahidi hivi: “Tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya.” Ingawa ahadi hiyo ilitimizwa kwa kadiri ndogo wakati Wayahudi waliporudia Yerusalemu mwaka wa 537 kwa kutoka utumwani Babeli, utimizo wa mwisho ulio kamili bado haujatokea. Petro mtume Mkristo alilikazia tumaini hili hakika kwa wakati ujao alipoandika hivi: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.” Huo mfumo mpya ulioagizwa na Mungu utahakikisha kabisa kwamba duniani kutakuwa na wakati ujao salama kwa ajili ya wanadamu washikamanifu na watiifu.—Isaya 65:17; 2 Petro 3:13, NW; Tito 1:2.
Ikiwa ungependa kupata habari zaidi juu ya huu wakati ujao salama utakaokuwa chini ya utawala wa ufalme wa Mungu kupitia Kristo, tafadhali usisitesite kuendea Mashahidi wa Yehova katika ujirani wako au uandikie watangazaji wa gazeti hili.