Yatii ‘Maonyo Yaliyowekwa Mbele Yetu’!
1, 2. Ile barua ya Yuda inatoa nini kwa namna ya agizo?
YEHOVA ni Mungu wa onyo. (2 Wafalme 17:12-15; Ezekieli 3:17-21) Watu wake wanajua kwamba yeye hataki kuona mtu ye yote akipotea kwa sababu ya kufuatia mwendo unaoongoza kwenye uharibifu. (Ezekieli 18:23, 32) Na bila shaka Mashahidi wa Yehova wanashukuru kwa vile Baba yao wa kimbingu anaonya, anaelekeza na kuokoa wale wanaompenda.
2 Barua ya Yuda iliyoongozwa na Mungu inatoa onyo pamoja na mwelekezo. Katika makala iliyotangulia tulijifunza sababu gani Yuda alisihi waamini wenzake ‘waishindanie imani.’ Sasa na tuyafikirie kwa sala maonyo yake ya kutoka zamani.—Warumi 15:4.
Jihadhari na Ukosefu wa Imani
3. Yuda ‘alipenda kuwakumbusha’ waamini wenzake juu ya nini?
3 Yuda anaendelea na onyo linalohusu imani, akisema:
“Tena napenda kuwakumbusha, ijapokuwa mmekwisha kujua haya yote, ya kwamba [Yehova], akiisha kuwaokoa watu katika nchi ya Misri, aliwaangamiza baadaye wale wasioamini.” (Yuda 5)
Wakristo ‘wasipoishindania imani,’ wanaweza kupoteza msimamo uliokubaliwa mbele za Yehova Mungu. Ili kuzuia hilo, Yuda ‘alipenda kuwakumbusha’ waamini wenzake waliohatirishwa juu ya mambo waliyokuwa wamejifunza wakati mmoja na jinsi Mungu alivyoshughulika na wale wasioaminika katika nyakati za zamani.
4. Yehova ‘aliokoa’ Waisraeli waliotumikishwa namna gani na kwa sababu gani?
4 Katika mstari wa tano kwanza Yuda anaeleza kwamba Yehova Mungu ‘aliokoa,’ au aliwakomboa Waisraeli waliotumikishwa kutoka utumwa wa Misri. Mungu alifanya hivyo walipokwisha kuadhimisha kwa utiifu ile Sikukuu ya Kupitwa ya kwanza. Ukombozi huo wa kimwujiza kutoka Misri ulifanyizwa na Yehova kwa sababu watu hao ambao wakati mmoja walikuwa watumwa walitenda katika imani.—Kutoka 12:1-14, 31.
5. (a) Misri ya mfano ni nini, na ni juu ya msingi gani Yehova anaokoa watu wake kutoka huko? (b) Ili wapate wokovu wa mwisho, ni lazima mashahidi walio wakf wa Yehova wafanye nini?
5 Kwa kulinganisha, Yehova anaokoa watu kutoka Misri ya mfano, ule ulimwengu wa wanadamu waliotengwa naye. (Ufunuo 11:8) Anafanya hivyo kwa sababu katika imani wanamkubali yeye kuwa Mungu wa wokovu wao na Yesu Kristo kuwa Mwana-Kondoo wa mfano wa kupitwa ambaye damu yake inawanunua katika ulimwengu huu. (1 Wakorintho 5:7) Lakini ili kushiriki wokovu, kwamba ni mbinguni ama duniani, shahidi wa Yehova aliyejiweka wakf lazima aendelee kuwa mshikamanifu kwake Yeye na asiasi imani kamwe na kurudi kwenye ulimwengu huu mbovu na utumwa wake wenye dhambi, kama vile Waisraeli waliokombolewa hawakurudi Misri. (Kumbukumbu la Torati 17:16; Mathayo 24:13) Imani isiyokoma ni ya lazima, kwa maana ijapokuwa alikwisha “kuwaokoa” watu katika Misri, Yehova “aliwaangamiza baadaye wale wasioamini,” wale waliotaka kurudi Misri au kurudia njia za Kimisri. (Linganisha 1 Wakorintho 10:1-12; Kutoka 32:4-6; Hesabu 25:1-18; 21:4-9; 14:35-38.) Basi, bila shaka ili kupata wokovu wa mwisho mashahidi wa Yehova waliojiweka wakf leo lazima wadumishe imani yao.—Waebrania 3:12, 13.
Matokeo Yenye Hatari ya Kukosa Adili
6. (a) Ilikuwa “enzi” gani ya kwanza ya wale malaika, na “makao yao yaliyowahusu” yalikuwa nini? (b) Malaika fulani walifanya dhambi ya namna gani? (c) Ule mwendo wenye dhambi wa malaika waasi ulilinganaje na ule wa “makafiri” wanaotajwa na Yuda?
6 Akitoa mfano wa pili wa kuonya, Yuda aliandika:
“Na malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu, amewaweka katika vifungo vya milele chini ya giza kwa hukumu ya siku kuu.” (Yuda 6)
Malaika waliumbwa wawe viumbe vya kiroho, wakiwa na taraja la uzima wa milele katika mbingu. (Zaburi 103:20; 104:4; Waebrania 1:7) Huo ulikuwa ndio mwanzo wao, “enzi yao.” “Makao yao yaliyowahusu,” au makao waliyokusudiwa, yalikuwa katika mbingu zisizoonekana. Lakini malaika fulani kwa kimbelembele waliacha makao yao yanayofaa ya kimbingu. Mtume Petro alisema kwamba ‘walikosa,’ na mara baada ya hapo alitaja matukio ya siku za Noa. (2 Petro 2:4, 5) Jambo hilo linavuta fikira kwenye wakati ule wa kabla ya gharika, kwa wazi “wana [Hati ya Elexandrine ya karne ya tano ya Septuagint Version inasema “malaika”] wa Mungu,” kwa kujivika miili yenye nyama, walipowatwaa kwa kutokutii wanawake wenye sura nzuri wawe wake zao. (Mwanzo 6:1, 2) Kwa vile kukaa kinyumba pamoja na wanawake kulivyokuwa jambo lisilo asili ya viumbe wa roho, malaika hao walifanya dhambi kwa kufuata ile ambayo kwao ilikuwa tamaa mbaya sana. (Yakobo 1:13-15) Hali moja na hayo, wale “makafiri” ambao Yuda alinena juu yao walitamani kufanya uasherati na watu wasio wa aina yao.
7, 8. (a) Ni jambo gani limewapata wale malaika wasiotii? (b) Kwa hiyo, ni lazima tufanye nini ili tuendelee kuwa katika hali ya kuokolewa?
7 Yaliyowapata malaika hao wasiotii yalitumika kuwa onyo kwa Wakristo wa siku za Yuda, nayo yanatumika kuwa onyo kwa Mashahidi wa Yehova wa nyakati za kisasa. Ijapokuwa malaika hao waliweza kuepuka kufa katika gharika kwa kuivua miili, walizuiwa wasiirudie “enzi yao” (cheo chao cha kwanza) wakiwa viumbe vitakatifu vya kiroho vyenye kufurahia ile nuru ya shauri na kibali ya Mungu. Badala yake, wamewekwa akiba wakiwa katika “vifungo vya milele,” kwa nguvu za Mungu zenye uzuifu, mpaka “hukumu ya siku ile kuu” ya kimungu ya uharibifu wao. Kwa sasa, hakuna cho chote kinachoonyesha kwamba wanaweza kuvaa miili yenye nyama, nao wanaendelea kuzuiwa kuwa katika utumishi wa Yehova, wakiwa katika giza zito la kiroho, katika mahali panapoitwa Tartaro.—2 Petro 2:4, NW.
8 Kwa kuwa malaika wasiotii hawatakosa kupata uharibifu wao, Mashahidi wa Yehova leo wanafahamu kwamba wanaweza kuendelea kuwa katika hali ya kuokolewa kwa ‘kuishindania imani’ tu. Kweli kweli, ni lazima tuwapinge wanadamu wo wote ambao wangeivuka mipaka iliyotolewa na Mungu na kutaka kunajisi mwili.
9, 10. (a) Wakaaji wa Sodoma na miji ya karibu-karibu walikuwa na hatia ya dhambi gani za kiadili? (b) Ni mfano gani wa kuonya uliotolewa na Sodoma, Gomora na miji iliyozunguka?
9 Akitoa mfano wa tatu wa kuonya, Yuda anasema:
“Kama vile Sodoma na Gomora, na miji iliyokuwa kando-kando, waliofuata uasherati kwa jinsi moja na hao, wakaenda kufuata mambo ya mwili yasiyo ya asili, imewekwa [mbele yetu kuwa mfano wa kuonya] wakiadhibiwa katika moto wa milele.” (Yuda 7)
Kwa wazi “Sodoma na Gomora, na miji iliyokuwa kando-kando” illitia ndani Adma na Seboimu na labda miji mingine katika Wilaya hiyo. Kwa sababu ya uovu wa wakaaji wayo, kwa mvua ya kiberiti na moto kutoka mbinguni Yehova aliiangusha n yote hiyo isipokuwa Soari ambako “Loti mwadilifu” na binti zake walikimbia. (2 Petro 2:6-10, NW; Mwanzo 14:2; 19:18-29; Kumbukumbu la Torati 29:22, 23) Kwa kutumia maneno yanayotafsiriwa “kama vile,” kwa wazi Yuda alishirikisha yale yaliyoipata miji hiyo na yale yaliyotukia kuhusiana na wale malaika wasiotii, waliokuwa wametenda jambo fulani lisilo asili ya viumbe vya roho kwa kuwatwaa wanawake kuwa wake zao. Hapa The Jerusalem Bible inasomwa hivi: “Ule uasherati wa Sodoma na Gomora na miji mingine ya karibu-karibu ulikuwa usio wa asili kwa kulingana.” Wakaaji wayo hawakufanya tu uasherati pamoja na wanawake bali walitosheleza tamaa yao mbaya ya kwa kulala na wanaume na labda hata na wanyama. (Linganisha Mambo ya Walawi 18:22-25.) Kikundi cha watu wenye ghasia pamoja na wavulana katika Sodoma kilitamani sana kufanya ngono pamoja na wageni wa Loti ambao kikundi hicho cha wafanya ghasia kiliwadhania kuwa wanaume, lakini kikashindwa wakati malaika hao wawili wageni walipokipofusha, kisha wakamwokoa Loti katika mji huo ulio-kusudiwa kuangamizwa.—Mwanzo 19:1-17.
10 Sodoma, Gomora na miji iliyozunguka ilitoa mfano wenye kuonya kwa ‘kuadhibiwa [na Yehova Mungu] katika moto wa milele,’ uharibifu wa milele. Magofu yenye kuteketea kuwa makaa ya Sodoma, Gomora, Adma na Seboimu yanafikiriwa kuwa yako chini ya maji ya ile sehemu ya kusini ya Bahari ya Chumvi au katika mkoa huo. Hivyo wala miji hiyo wala wakaaji wayo hawaendelei kuchomeka. Kwa wazi miji hiyo yenyewe, badala ya wakaaji wayo wote, iliharibiwa milele, kwa maana inaonekana kwamba angalau watu fulani mmoja mmoja ambao wakati mmoja walikuwa wakikaa huko watafufuliwa. (Mathayo 10:15; 11:24; Ufunuo 20:12, 13) Lakini jambo lililoipata miji hiyo yenye ufasiki ni onyo kubwa juu ya mwenendo usio wa adili, onyo ambalo Mashahidi wa Yehova leo wanapaswa walitii.
Usidharau Mamlaka Iliyotolewa na Mungu
11. Wale “makufiri” waliokuwa wamejiingiza kwa siri miongoni mwa watu wa Mungu walilinganaje na watu wafasiki wa Sodoma na miji iliyozunguka?
11 Kisha Yuda aliwataja wale “makafiri” na kusema:
“Kadhalika na hawa, katika kuota kwao, huutia mwili uchafu, hukataa kutawaliwa, na kuyatukana matukufu.” (Yuda 8)
“Kadhalika,” au, kwa wazi, katika njia iyo hiyo ambayo watu wenye ufasiki wa Sodoma na miji iliyozunguka walichafua mwili wao kwa ngono za upotovu na zisizo za asili, vivyo hivyo watu wenye nia mbaya waliojiingiza kwa siri miongoni mwa watu wa Mungu waliuchafua mwili. Hawakujali shauri la mitume la ‘kuikimbia zinaa.’—1 Wakorintho 6:18-20.
12. (a) Wale wadukizi wasiomcha Mungu walikuwa ‘wakiotaje ndoto’? (b) Ni nini kinachongojea wazoevu wa ufisadi wasiotubu?
12 Wadukizi hao vilevile ‘walikuwa wakiota ndoto,’ labda kwa sababu walitaka kutegemeza maoni yao kwa ndoto za kiunabii za uongo. (Linganisha 2 Petro 2:1; Kumbukumbu la Torati 13:1-5.) Kwa sababu hiyo, ndoto zao labda zilihusu mawazo-mawazo machafu ya ngono, au labda usemi huo unamaanisha kwamba mafundisho yao yalikuwa “madanganyo” tu. (JB) Kwa vyo vyote, “makafiri” hao walitafuta njia za kuendeleza nafasi zao za kufanya ngono nao walidhani wangeweza kuendelea na mwenendo mchafu bila kuadhibiwa. Ye yote wa Mashahidi wa Yehova leo asijiache aangukie mtego huo! Pasipo shaka yule Hakimu Mkuu anatekeleza hukumu juu ya wazoevu wa ufisadi wasiotubu.—Mwanzo 18:25.
13. ‘Waotaji ndoto’ hao wafisadi walikuwa na maoni gani kuelekea mamlaka iliyowekwa kimungu?
13 ‘Waotaji ndoto’ hao wenye ufisadi vilevile ‘walikataa kutawaliwa na kuyatukana matukufu.’ Kwa majivuno walidharau mamlaka iliyowekwa kimungu. (Mithali 21:4; 2 Petro 2:10) Kama wale malaika wasiotii, watu hao walikuwa na roho ya uasi nao walistahili hukumu kali kwa sababu kwa hakika hawakuwa na heshima yo yote kwa yule Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Mzima na Mwanaye mpendwa.
14. Ni nani waliokuwa “matukufu” (wenye utukufu)?
14 Watu hao makafiri vilevile waliwatukana “matukufu” (kwa halisi, “wenye utukufu”), kwa wazi wale waliokuwa na utukufu fulani ambao walipewa na Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Yohana 17:22; 1 Petro 4:12-14) Bila shaka, kwa kuwa utukufu huo, au heshima, ilitoka kwa Mungu, hakuna sifa ya moja kwa moja iliyopasa itolewe kwa watu hao waliopendelewa duniani walioifurahia. Walakini, wote walio wa Mashahidi wa Yehova wamepaswa waheshimu “utukufu” huo na kusema juu yake kwa kulingana, wakiwa na heshima kuu kwa Yehova Mungu.—1 Samweli 2:30.
15. (a) ‘Waotaji ndoto’ hao wenye kuchafua mwili walisemaje juu ya “matukufu”? (b) Imetupasa tufanye nini iwapo tuna maelekeo ya kudharau mamlaka iliyotolewa na Mungu?
15 Bila shaka, wale walio wa wafuasi wapakwa mafuta wa Kristo wanaotumikia kwa uaminifu wakiwa waangalizi wa Kikristo waliowekwa wamekuwa na utukufu, au heshima, waliyopewa. Mashahidi wenzao wamepaswa washirikiane nao na kuwaunga mkono katika utumishi wa Mungu. Sisi tusiwe kama wale ‘waotaji ndoto’ wenye kuchafua mwili wa siku za Yuda waliodharau utawala wa Yehova nao hawakuheshimu matukufu kutoka kwake, bali wakawatukana wale waliovikwa utukufu huo. (Linganisha 3 Yohana 9, 10.) Hivyo, ikiwa tunayo hata maelekeo ya kudharau mamlaka iliyotolewa na Mungu, na tutafute kwa sala msaada wa Yehova ili turekebishe maoni yetu.
Mfano Bora wa Mikaeli
16. Kulikuwa na tofauti gani kati ya Mikaeli yule malaika mkuu na ‘waotaji ndoto’ wasio na heshima?
16 Kwa faida yetu, Yuda anataja mfano bora, akisema:
“Lakini Mikaeli, malaika mkuu, aliposhindana na Ibilisi, na kuhojiana naye kwa ajili ya mwili wa Musa, hakuthubutu kumshitaki kwa kumlaumu, bali alisema, [Yehova] na akukemee.” (Yuda 9)
Lo! kulikuwako tofauti kama nini kati ya wale ‘waotaji ndoto’ wasio na heshima na Mikaeli yule malaika mkuu ambaye akawa Bwana yetu Yesu Kristo! (Linganisha Mithali 8:22-31; Yohana 6:62; Wafilipi 2:5-11; 1 Wathesalonike 4:15, 16.) Katika kuwatukana watumishi wa Mungu, ‘waotaji ndoto’ hao makafiri walichukua mwendo usio wa heshima ambao hata Mwana wa Yehova hakuchukua alipokuwa akibishana na Shetani juu ya mwili wa Musa yule nabii Mwebrania. Hakuna maandishi ya Kimaandiko yaliyotangulia yanayoonyesha mabishano hayo. Lakini kwa jinsi fulani isiyofunuliwa Yuda alipokea taarifa hiyo naye akaiandika kwa faida yetu.
17. (a) Katika kubishania mwili wa Musa, Mikaeli hakufanya nini, na kwa sababu gani? (b) Mikaeli aliwekeaje watu wa Yehova mfano wa kuheshimu mamlaka ya kimungu?
17 Labda, Ibilisi alitaka mwili mfu wa Musa ili aanzishe madhehebu ya kidini juu yake na kwa njia hiyo awapotoe watu wa Yehova. Lakini Mikaeli hakutaka kuleta hukumu dhidi ya yule Ibilisi kwa njia ya matusi. Mikaeli “hakuthubutu” kufanya hivyo kwa sababu ya kumwogopa Yehova kwa kufaa. Wala yeye hakutangulia wakati wa Yehova alioweka kushughulika na Shetani. (Ufunuo 12:7-9; 20:1-3, 7-10) Badala yake, Mwana mpendwa wa Mungu alionyesha heshima kwa yule Hakimu Mkuu na akampa ile haki ya kumkemea Ibilisi. Kwa hiyo, Mikaeli alimwambia Shetani hivi: “[Yehova] na akukemee.” Ijapokuwa maneno ya Mikaeli hayakuwa makali-makali, alionyesha uwezo kwa kuzuia mwili wa Musa, naye Yehova akamzika nabii huyo katika kaburi lisilotiwa alama. (Kumbukumbu la Torati 34:1-6) Bila shaka, katika yote hayo Mwana wa Mungu aliwekea watu wa Yehova mfano bora wa kuheshimu mamlaka ya kimungu. Na tuufuate.
18. Sababu gani inaweza kusemwa kwamba wale waliotaka kuchafua mwili walikosa hali ya kiroho?
18 Kwa njia ya kutofautisha, kisha Yuda akasema:
“Lakini watu hawa huyatukana mambo wasiyoyajua, na mambo wayatambuayo kwa asili wajiharibu kwayo kama wanyama wasio na akili.” (Yuda 10)
Ijapokuwa wale waliotaka kuchafua mwili walikuwa wadogo kwa Mikaeli, ambaye hakutaka kuleta hukumu juu ya Shetani kwa njia ya matusi, waliyatukana si “matukufu” pekee yao bali vilevile “mambo [ya kiroho] wasiyoyajua” au kufahamu. ‘Kwa kutokuwa na hali ya kiroho’ (Yuda 19, NW), hawakuweza kufahamu mambo ya kiroho. (1 Wakorintho 2:6-16) Mawazo ya Yehova, njia, shughuli na matendo yake yalikuwa ya kigeni kwa “makafiri” hao.
19. “Makafiri” hao walikuwaje kama “wanyama wasio na akili”?
19 Kwa kumheshimu Yehova Mungu, wala Mikaeli yule malaika mkuu wala malaika wengine waadilifu hawawatukani wale ambao Mungu ameweka utukufu fulani juu yao. Lakini “makafiri” hao walifanya hivyo kwa sababu walikuwa wamefuata kabisa tamaa za unyama. Hawakufahamu mambo ya kiroho ila tu yale yaliyopendeza tamaa zao za kimwili. Hivyo, kama wanyama wanaofikiria tu ya mwili, walitaka raha ya mwili wenye dhambi. Watu hao, wenye kusudi la kutosheleza tamaa zao mbaya zenye anasa, ‘walijiharibu wenyewe’ katika dhambi za kimwili. Hivyo walijionyesha wenyewe kuwa si bora kuliko “wanyama wasio na akili, ambao walizaliwa kama wanyama tu wa kukamatwa na kupotezwa” bila tumaini lo lote la kufufuliwa.—2 Petro 2:9-13.
20. Kulingana na maneno ya Yuda ambayo tumezungumza mpaka hapa, ni mwendo ni mwendo gani ambao mashahidi washikamanifu wote was Yehova wamepaswa kufuatia?
20 Ni jambo la maana kama nini kwamba ni lazima Mashahidi wa Yehova wa leo wapinge kabisa walimu wa uongo, wanaotaka kuchafua mwili na wale wasioheshimu mamlaka iliyowekwa kimungu! Hata hivyo, ikiwa lile shauri ambalo limechunguzwa mpaka hapa katika barua ya Yuda linafunua kadiri fulani ya kosa katika maoni yetu mmoja mmoja au njia zetu, na tufanye haraka kuubadili mwendo wetu, tukitafuta kwa sala msaada wa Baba yetu wa kimbingu. Na tuendelee kufaidika kiroho kwa sababu ya kuyatii ‘maonyo yaliyowekwa mbele yetu.’—Kutoka The Watchtower la Agosti 15, 1982.
(Mazungumzo yetu ya barua ya Yuda yatamalizika katika toleo litakalofuata la Mnara wa Mlinzi.)
Unaweza kuyakumbuka mambo haya?
□Yaliyowapata Waisraeli wa kale yanathibitishaje kwamba ni lazima tuwe na imani isiyokoma ili tupate wokovu?
□Wale malaika wasiotii wanatupatia mfano gani wa kuonya?
□Sodoma, Gomora, na miji iliyozunguka inatoa onyo gani kwa Wakristo?
□Sababu gani haitupasi kudharau mamlaka iliyowekwa kimungu?
□ Mikaeli malaika yule mkuu aliweka mfano gani wa kuheshimu mamlaka, na hivyo tutendeje?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Hata kama vile Mungu ‘alivyookoa watu katika Misri,’ Wakristo wameokolewa katika ulimwengu huu mbovu. Lakini imani isiyokoma inatakwa ili kupata wokovu wa mwisho
[Picha katika ukurasa wa 17]
Yaliyoipata Sodoma na miji iliyoizunguka ni onyo dhidi ya mwenendo usio wa adili