Kinachokaziwa Ni Imani Yako—Katika Warumi
NI JAMBO gani linalohitajiwa kabisa ili umpendeze Mungu?
Huenda ukatoa majibu mbalimbali: Kuishi maisha mema. Kutokutenda wenzako madhara. Kujinyima mambo fulani-fulani kwa ajili ya Mungu. Kutii sheria zake. Kutenda mema. Kumkubali Kristo na kuwa mnyofu katika ibada yako.
Majibu hayo yanafaa, kwa maana yanagusa mambo ambayo unahitajiwa kufanya ili upate kibali ya Mungu. Lakini kuna jambo jingine la maana sana ambalo likikosekana yote yaliyotangulia kutajwa yangekuwa hayana kazi. Jambo hilo ni IMANI.
Labda wewe una maoni ya kusema, ‘Mimi nina imani, tena najua kwamba imani ni ya maana.’ Hata hivyo, ingetupasa sisi sote tufikirie wazo linalotufikilia mara nyingi kutokana na kitabu cha Warumi. Utakiona kichwa hicho kinachohusiana na imani katika Warumi 1:16, 17 (NW). Hapo mtume Paulo anatuambia kwamba ‘habari njema ndizo uwezo wa Mungu wenye kuleta wokovu’ na kwamba ‘aliye mwadilifu ataishi kupitia imani.’ Je! ndiyo kusema kila mtu anaweza kupata wokovu akiwa na imani? Je! imani inafanya kazi za Kikristo ziwe hazihitajiwi sana? Barua ambayo Paulo aliandikia Warumi inajibu.
Je! wewe binafsi umepata kukisoma kitabu cha Warumi? Au, je! umekisoma kwa kukirudia-rudia? Hili la pili ni ulizo zuri zaidi, kwa maana imesemwa kwamba katika Warumi ndipo tunapopata maelezo marefu zaidi yenye kumwonyesha Paulo akizihubiri habari njema. Kwa hiyo kitabu cha Warumi kinastahili kusomwa-somwa mara nyingi; kadiri unavyozidi ‘kukitafuna’ ndivyo kinavyozidi ‘kukukuza.’
Wokovu kwa Wote Wenye Imani
Kulikuwako suala la kuhangaisha Wakristo wa karne ya kwanza: Je! Wayahudi na Mataifa pia wangeweza kupata kibali ya Mungu na kutangazwa naye kuwa waadilifu? Mungu alimwongoza Paulo aandike habari zilizohusu jambo hili la maana katika kitabu cha Warumi. Aliyoyaandika yanaweza kuwa na ubora mkubwa kwa maisha zetu tunapoonyesha imani na kutafuta wokovu. Yaliyoandikwa yana somo lenye thamani kubwa kwetu pia ikiwa kwa njia yo yote tuna maelekeo ya kufikiri kwamba kabila fulani au taifa fulani ndilo bora kuliko jingine.
Ili tuweze kufahamu vizuri zaidi hoja ambazo Paulo aliendelea kutokeza, acha turudie kujikumbusha kwa muhtasari mambo mengi ya kitabu hicho. Unaposoma warumi ukiwa na muhtasari huo mkononi utakuwa na tazamio la ujumla litakalokuwezesha uone njia zilizotumiwa kutoa hoja. Hivyo hutakosa kuifahamu hali yote kwa ujumla inayohusika, hilo likiwa ni jambo linaloweza kutukia unaposoma hivi hivi tu, mstari baada ya mstari.
Baada ya utangulizi wake na akiisha kutaja anatamani kutembelea kundi katika Rumi, Paulo anaeleza moja kwa moja kichwa hiki kikuu cha habari: Mungu hana upendeleo naye anamtolea “kila aaminiye” uwezekano wa kupata wokovu—awe ni Myahudi au awe ni Mtaifa. Ingawa suala la Mungu ana maoni gani juu ya Myahudi au Mtaifa halitokezwi-tokezwi kwa mkazo mwingi siku hizi kama zamani hizo, maelezo ya Paulo yanakazia imani yetu. Kwa sababu gani kila mtu anahitajiwa sana awe na imani?—Warumi 1:1-17.
Kwa kweli, wanadamu wote ni watenda dhambi wanaostahili kuonyeshwa ghadhabu na Mungu. Huenda ikawa vyepesi kuona jambo hilo kwa habari ya watu wasio Wayahudi wanaokosa kuona ushuhuda wa kwamba kuna Mungu wa kweli, kwa sababu hawajali. Mara nyingi wanaabudu vitu vilivyoumbwa na (kwa sababu wana maoni yasiyo ya kweli juu ya Mungu) wanakubali mazoea mapotovu yawashinde nguvu. (Warumi 1:18-32) Lakini kwa kweli ndivyo pia ilivyo kwa watu kama Wayahudi, ambao huenda wakawahukumu au kuwalaumu Mataifa wenye kutenda dhambi. Makundi yote mawili yako katika hali ya kuweza kuhukumiwa. Kwa sababu gani? Wayahudi wana sheria ya Mungu na wanajisema kuwa wanaifundisha. Mataifa yana dhamiri inayowachokoa-chokoa wafanye mambo yanayofaa, kwa hiyo dhamiri hiyo inawafanya wastahili kutoa jibu kwa mabaya wanayotenda. Basi, jambo kuu si kutahiriwa mwili wala kutokutahiriwa.—Warumi 2:1-29.
Kama wewe ungalikuwa u Mkristo Myahudi zamani hizo, inaelekea ungeyathamini maneno ya Paulo ya kukubali kwamba Wayahudi walikuwa wamekabidhiwa Neno la Mungu. Hata hivyo hungaliweza kuiepuka kweli ya mambo, inayoonyeshwa wazi katika Maandiko, kwamba watu wote ni wenye dhambi. Kwa hiyo njia fulani inahitajiwa sana ili wanadamu waweze kuwa waadilifu. Mungu ametimiza uhitaji huo kwa njia mpya ya kufikia uadilifu—kuwa na imani katika Yesu. Je! ungependa uthibitisho wa kwamba imani ni bora kuliko kazi za sheria? Fikiria mfano wa Abrahamu, ambaye Mungu alimhesabu kuwa mwadilifu kwa kutegemea msingi wa imani hata kabla mtu huyo hajatahiriwa au kabla Israeli hawajapewa sheria. Tena hatuwezi kuupuza uhakika wa kwamba ahadi aliyopewa Abrahamu kwa sababu hiyo ingeletea wote baraka, hata wawe ni wa taifa gani.—Warumi 3:1–4:25.
Je! basi wewe unaona namna imani ilivyo ya maana kwa Wakristo? Kwa habari ya wale waliokusudiwa kuishi mbinguni, wanapaswa kuwa na imani kwanza kabla hawajatangazwa kuwa waadilifu na kupokea utiwa-mafuta wao kwa roho takatifu. Hata hivyo sisi sote tunaweza kupiga asante kubwa kwa sababu ya uwezekano wa kupata kibali ya Mungu kupitia imani yetu! Wanadamu walioishi kabla sheria haijatokezwa walikuwa watenda dhambi na basi walikufa. Musa alipokwisha kuipokea sheria, dhambi ikaonekana wazi zaidi. Ni kitu gani kingeweza kuzuia matokeo ya dhambi ya Adamu iliyotupitishia sisi hali ya kutokamilika? Ni mwendo wa Yesu wa uaminifu na uwezo wenye kulipia dhambi wa kifo chake cha kujitoa kama dhabihu. Tukiwa na imani katika jambo hilo tunaweza kuwa na “uzima wa milele katika tazamio.”—Warumi 5:1-21, NW.
Kuishi Kulingana na Imani
Unapoendelea kusoma katika Warumi utaona kwamba Paulo anarekebisha uamuzi mbaya ambao huenda wengine wakafanya kutokana na semi zake. Namna gani? Huenda mtu fulani akawaza kwamba kwa kuwa Mungu anaweza kuonyesha fadhili zisizostahilika kuhusiana na dhambi, mtu anaweza kujisukumiza mbele atende dhambi atakavyo. Lingekuwa kosa kubwa namna gani! Paulo anaeleza kwamba Wakristo waliosamehewa dhambi zao hawapaswi tangu wakati huo na kuendelea kuacha dhambi iwatawale. Ni kama kwamba dhambi ilikuwa hapo kwanza mwenyeji wetu sisi tukiwa watumwa wake, tukawa tukiitii; lakini sasa ni kama kwamba huyo aliyekuwa bwana-mkubwa amekufa na maagizo yake yanaweza kupuzwa. Sisi tuna bwana-mkubwa mwingine—Mungu. Tukiwa na imani inatupasa tuwe “watumwa wa uadilifu,” tukiwa na “tunda katika njia ya utakatifu, na mwisho wake ni uzima wa milele.”—Warumi 6:1-23, NW.
Jitihada inahitajiwa ili mtu aishi kama Mkristo kulingana na imani. Jitihada hiyo haihusu kujaribu kushika orodha fulani ya sheria tu, kwa maana wale ambao hapo kwanza walikuwa chini ya sheria walishindwa kuishika kikamilifu na sasa wamefunguliwa katika hiyo sawa na vile mke anavyofunguliwa katika sheria ya mumewe wakati anapokufa. Lakini tunaweza kupata kitia-moyo kutokana na ungamo la Paulo la waziwazi: Yeye aliungama (alikubali) wazi kwamba hakuweza kuepuka dhambi, kwa kadiri aliyotaka kuiepuka. Hata hivyo alijisikia akiokolewa na Yesu. Sisi pia tunaweza kuokolewa ivyo hivyo katika hali hiyo yenye kutatiza.—Warumi 7:1-25.
Wale ambao Mungu amewachukua wawe wana wake wa kiroho wa kulelewa watatawala pamoja na Yesu Kristo mbinguni. Jambo hilo linawapa tumaini, na linapasa lihakikishie Wakristo wote waaminifu kwamba Mungu atasaidia wale wanaomtegemea yeye. Kwa kweli, ikiwa sisi ni waaminifu kwake, hakuna kinachoweza kututenganisha na upendo wake kupitia Yesu. (Warumi 8:1-39) Hatuna haja ya kutilia shaka juu ya kutimiza kwa Mungu yaliyo mema. Yeye ana haki na pia uwezo wa kuamua mambo namna anavyotaka, kama alivyoonyesha kwa kumchagua Yakobo na katika njia yake ya kushughulika na Farao. Kwa kuwa walio wengi kati ya Wayahudi walikwazika na hawakumkubali Masihi, Mungu aliamua kwamba mtu ye yote mwenye kuonyesha imani angeweza kuokolewa. Hakika hizo ni habari njema! Hata hivyo, uwezekano huo unaleta juu yetu daraka la kuonyesha imani kwa kuzitangaza habari njema ili watu wa mataifa yote wapate kusikia na kupata imani.—Warumi 9:1–10:15.
Inatupasa tulifahamu somo lililo katika njia iliyotumika kutimiza jambo hilo. Ingawa Wayahudi wa asili walikuwa katika cheo chenye kupendelewa na Mungu na ndio waliokuwa wa kwanza katika mstari wa wenye kwenda kupata uzima wa kimbingu wakiwa “Israeli wa Mungu,” wao hawakubaki katika cheo chao. Walikatwa kama matawi ya asili yaliyo katika mzeituni uliopandwa na kupaliliwa, ikapatikana nafasi ya Mataifa (wanaofananishwa na matawi ya mzeituni-mwitu) ambao walimkubali Kristo. Bila shaka, wote ambao wamepokea rehema ya Mungu kwa njia hiyo au nyingineyo yote wanapaswa kuendelea kuonyesha imani kwa kuthamini mambo ili wapate wokovu.—Wagalatia 6:16; Warumi 10:16–11:36.
Ni kwa njia gani mbalimbali unavyoweza kudhihirisha imani yako, ufanye mengi yanayozidi kutoa tu tangazo la waziwazi kwa ajili ya wokovu na hivyo usaidie wengine wazijue habari njema? Utapata majibu fulani katika Warumi 12:1–13:14. Wewe kama Mkristo unaweza kuepuka kufuata kielelezo cha mfumo huu mbovu; unaweza kusitawisha hali ya kujiona mdogo, kuonyesha ukaribishaji na kushinda uovu kwa kutenda wema. Bila shaka, unaposoma kifungu hicho cha maneno utakuta mapendekezo mengine yaliyo bora kabisa, kutia ndani mengine yanayohusu utii wako wa kiasi kwa “mamlaka zilizo kuu” (NW) ambazo ni serikali.
Wajibu mwingine wa Kikristo ni kuwafikiria kwa huruma watu wenye dhamiri dhaifu, kuwa na nia ya kujinyima mambo yanayoruhusika ili tusiwakwaze hawa. Tunapochukua hivyo udhaifu mbalimbali wa wale wasio na nguvu badala ya kujipendeza wenyewe, tunaiga kielelezo ambacho Kristo aliweka. Vilevile tunaendeleza amani na umoja.—Warumi 14:1–15:16.
Unaposoma sura mbili za kumalizia za Warumi utaona kwamba kwa uhakika Paulo aliishi kulingana na imani yake. Alikuwa na huduma ya kufanya hasa kwa watu wa mataifa yasiyo ya Kiyahudi, naye alijishughulisha kweli kweli kuitimiza huduma hiyo. Zaidi ya kulitembelea kundi katika Rumi, Paulo alitumainia kusafiri mpaka Spania. Hilo lilikuwa eneo kuu la mbali la Milki ya Rumi upande wa magharibi, na kulingana na maoni ya Paulo halikuwa limehubiriwa. Salamu nyingi za kibinafsi ambazo Paulo alipelekea Wakristo katika Rumi ni ushuhuda mwingine wenye kuonyesha alikuwa na imani yenye uhai na matendo.
Kwa wazi, kitabu cha Warumi kinatusaidia tuthamini ubora wa imani unaozidi kazi za sheria. Kinaonyesha wazi kabisa kwa kuwa Mungu hana upendeleo ana nia ya kuwakubali wote wanaoonyesha imani, akiwapa taraja la kuwa waadilifu na kupata uzima usiokwisha. Basi, acheni tuuone sikuzote uhitaji wetu wa kuwa na imani yenye nguvu na kuishi kulingana nayo.