Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 3/15 kur. 21-24
  • Udhaifu Huo Unaweza Kushindwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Udhaifu Huo Unaweza Kushindwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Misaada Iliyotolewa kwa Njia ya Kimungu
  • Sababu Gani Wana Ugumu Zaidi?
  • Kushinda Matumizi Mabaya ya Pombe
  • Kuliacha Zoea la Kuvuta Tumbaku
  • Kushindana na Kupiga Punyeto
  • Shikilia Viwango vya Biblia
  • Kubali Msaada wa Mungu Ushinde Makosa ya Siri
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Ninaweza Kushinda Jinsi Gani Mazoea ya Kupiga Punyeto?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
  • Kuacha Kupiga Punyeto—Kwa Sababu Gani? kwa Njia Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Punyeto na Ngono za Wanaume kwa Wanaume na Wanawake kwa Wanawake
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 3/15 kur. 21-24

Udhaifu Huo Unaweza Kushindwa

MATATIZO matatu yanaelekea kusumbua vijana wa kisasa na pia watu wazima wengi, zaidi ya vile wanavyosumbuliwa na mengine. Ni matatizo gani? Uzoevu wa kunywa pombe, uvutaji wa sigareti na kupiga punyeto (ambako kunaitwa pia kujichua au mahaba ya kibinafsi ya ngono).

Mazoea hayo yanavutia udhaifu wa mwili, na mazingira ya kisasa yanafanya iwe vigumu sana kuyashinda. Kwa mfano, pombe na sigareti zinatangazwa sana ili kuvuta watu. Maelekeo ya kufanya mahaba yanaamshwa na ongezeko kubwa la vitabu vya umalaya, sinema na programu za televisheni. Lakini hiyo haimaanishi kwamba matatizo au udhaifu huo mbalimbali hauwezi kushindwa.

Misaada Iliyotolewa kwa Njia ya Kimungu

Katika habari hii inasaidia kufikiria mfano wa mtume Paulo. Ingawa yeye alikuwa mtume Mkristo, aliungama kwamba alishindwa kufanya mambo aliyotaka naye akafanya mambo asiyotaka kufanya. (Warumi 7: 14-25) Lakini, alisema hivi pia: “Mimi naupiga-piga ngumi mwili wangu na kuufanya kama mtumwa, ili, nikiisha kuhubiria wengine, mimi mwenyewe nisije nikakataliwa kwa njia fulani.” (1 Wakorintho 9:27, NW ) Kwa kweli, aliweza kuwaambia hivi Wayahudi wenzake: “Ndugu zangu, mimi kwa dhamiri safi kabisa nimeishi mbele za Mungu hata leo hivi.”—Matendo 23:1; 22:3.

Kuna misaada gani iliyotolewa kwa njia ya kimungu kutusaidia ‘kupiga-piga miili yetu’? Tunaweza kusaidiwaje tuenende ‘kwa dhamiri safi kabisa’ kwa habari ya udhaifu kama uzoevu wa kunywa pombe, mazoea ya kutumia tumbaku na kupiga punyeto?

Neno la Mungu, Biblia Takatifu, ni msaada mmoja usioondoleka. Kuisoma kwa kawaida, ndiyo, kila siku, na hasa vile visehemu kama Zaburi, kitabu cha Mithali na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kunaweza kusaidia sana. Ni kweli kwamba ‘mtu haishi kwa mkate tu ila kwa kutegemea kweli zinazotoka katika kinywa cha Mungu’ na zinazopatikana katika Neno Lake, Maandiko Matakatifu.—Mathayo 4:4.

Tunapata nguvu za kiroho kwa kusoma Neno la Mungu na vichapo vya Kikristo vinavyotusaidia tulielewe na kulitumia. Vitu hivyo vinatupa maoni mazuri zaidi juu ya mambo yanayopendeza Muumba wetu, Yehova Mungu. Zaidi ya hilo, tunapata msukumo mzuri kutokana na maagizo ya uadilifu na mifano ya kuonya iliyoandikwa katika Neno la Mungu. Hivyo tunasaidiwa kupenda —na kufanya—yaliyo mema na yanayofaa, huku tukichukia, ndiyo, tukikirihi, yaliyo mabaya, au maovu.—Zaburi 97:10; Warumi 12:9.

Sala kwa Mungu ni msaada mwingine mkubwa. Mara nyingi Wakristo wameshuhudia wakisema kwamba sala inasaidia sana katika kushindana na udhaifu wetu mbali-mbali. Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya mwanamke mmoja Mkristo aliyekuwa na tatizo la kuacha zoea la kuvuta sigareti. Aliposikia hotuba nzuri ya Biblia juu ya habari ya sala, alienda nyumbani, akampelekea Yehova Mungu sala kwa bidii ili amsaidie kushinda zoea hilo, na kuanzia hapo yeye hakuwa tena na tatizo hilo. (Wafilipi 4: 6, 7) Wakati tunapoomba kwa weupe wote wa moyo ili Mungu atusamehe kwa sababu tumekosa katika jambo fulani, tunajisikia kwa njia fulani tukiwa tumetulia na tunasaidiwa kufanya mwanzo mpya katika jitihada yetu.

Roho takatifu ya Mungu, au kani ya utendaji, ni msaada pia. Inapatikana kwetu tukisali tupewe. Yesu alisema: “Ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi nzuri, lo! jinsi Baba aliye katika mbingu atakavyowapa roho takatifu kwa wingi zaidi wale wanaomwomba.” Roho takatifu hiyo ni kani yenye nguvu nyingi. (Luka 11:13, NW; Zekaria 4:6) Tukijiacha tuongozwe na mavutano yake, tutasaidiwa, kwa maana tunda la roho linatia ndani kujiweza, ambako kunahitajiwa sana ili kupambana na matatizo yanayopiga watu kwa wingi.—Wagalatia 5:22, 23, NW.

Wakristo waliokomaa pia wanaweza kuwa chanzo cha msaada. Hasa ndivyo ilivyo kuhusu wale walio na sifa za kiroho, kama vile wazee wa kundi. Kwa kuendea mzee na kumweleza mambo ya siri, tunaweza kusaidiwa sana katika jitihada yetu. Lakini wengine pia wanaweza kusaidia. Huenda “wanawake wazee” wakaweza kusaidia wanawake vijana. (Tito 2:3-5, NW ) Kwa mfano, mkunga mmoja wa kike aliyestaafu kazi ambaye alikuwa amevuta sana sigareti muda wa maisha yake yote alikaza nia aache kuvuta ili astahili kubatizwa. Alijiwekea tarehe fulani kisha akaambia washirika wenzake wa karibu walio Wakristo juu ya nia yake. Kila siku mmoja wa waamini wenzake hao ama alimpigia simu au akamtembelea ili kumwunga mkono kwa hali. Matokeo yakawa kwamba mwishoni mwa juma yeye alikuwa ameshinda kabisa tamaa yake ya sigareti.

Basi, tumeona njia nne kubwa za kupata msaada: (1) kusoma na kujifunza Neno la Mungu, pamoja na vitabu vya Kikristo; (2) kudumu katika sala; (3) kujiacha tuongozwe na mavutano ya roho takatifu ya Mungu; na (4) kuomba msaada wa Wakristo waliokomaa. Kwa njia hizo, watu wengi sana wamesaidiwa katika jitihada yao ya kushinda udhaifu mbalimbali. Hata hivyo, wengine wanatatizika zaidi ya wengine katika kushinda udhaifu mbalimbali. Je! bado kuna misaada mingine ambayo wangeweza kutumia kwa matokeo mazuri?

Sababu Gani Wana Ugumu Zaidi?

Kwa sababu gani wengine wana ugumu mkubwa zaidi ya wengine katika kushinda udhaifu mbalimbali? Bila shaka, kutokukomaa kiroho kunahusika. Mtu ye yote anayeshindwa kutumia misaada iliyotangulia kutajwa, au anayeitumia kama wajibu tu, atatatizika zaidi katika kushinda udhaifu wake mbalimbali.

Kurithi tabia katika ukoo wa mtu kunahusika pia. Wengine inaonekana wamepata udhaifu fulani wa namna mbalimbali kutokana na wazazi wao, au hata mababu na nyanya zao, kwa njia ile ile ambayo mtu anaweza kuelekea kupatwa na ugonjwa, kama ule wa sukari. Kwa hiyo kwa habari ya udhaifu mbalimbali inaonekana kwamba ‘akina baba wamekula zabibu mbichi, nao watoto wakatiwa ganzi la meno.’—Ezekieli 18:2.

Pia inategemea ni kwa kadiri gani au ni mara nyingi namna gani mtu amefuatia mwendo wenye kutilika mashaka. Jambo hilo linaamua sana kiasi ambacho amelizoea. Kwa mfano: Mtu anayevuta nusu tu ya kifurushi cha sigareti kwa siku inaelekea kuwa hatatiziki sana kuacha zoea hilo kama yule anayevuta vifurushi vitatu kwa siku, mvutaji wa mfululizo.

Huenda mazingira pia yakahusika katika tatizo hilo. Kwa mfano, huenda mke akataka kuacha kuvuta sigareti, lakini mume wake na watoto matineja wawe wote wanavuta. Ingekuwa vigumu sana kwake kuacha zoea hilo kuliko vile ingekuwa kwa mwanamke ambaye jamaa yake haitumii tumbaku. Vivyo hivyo, ikiwa kabla ya kupata maarifa ya Kimaandiko mtu alikuwa na zoea la kufikiria saa zote mawazo machafu, ingekuwa vigumu zaidi kwake kutii amri iliyo kwenye Wafilipi 4:8 juu ya kufikiria mawazo safi, na hasa ndivyo ingekuwa kama angelazimika kufanya kazi ya kimwili kati ya watu wenye maongezi ya kutaka mambo machafu.

Kushinda Matumizi Mabaya ya Pombe

Ni njia gani nyingine inayoweza kufuatwa na mtu anayeelekea kuwa na tatizo ambalo ni kama halishindiki kuhusiana na udhaifu wake? Kuna njia ile inayohusu mwili. Inaweza kuitwa kanuni ya uhusiano wa mwili na maoni ya moyoni (psychosomatic principle) kwa kinyume. Kanuni hiyo ya uhusiano wa mwili na maoni ya moyoni ni ya kwamba mwili na akili ni kitu kimoja na kwa hiyo akili na maoni ya moyoni (psyche) yanaletea mwili (soma) matokeo fulani. Lakini kinyume cha hivyo pia kinafanya kazi; hali ya mwili inapelekea akili matokeo fulani pia. Hivyo wagonjwa wanaougua kansa wanapatwa mara nyingi na hali ya kushuka moyo kuhusiana na akili. Kwa hiyo, watu fulani wenye ujuzi wa kushughulika na ulishaji unaofaa wa mwili wanashikilia kwamba kwa kujenga afya ya kimwili kupitia mazoea mazuri ya kula mtu angekuwa katika hali bora ya kushinda tamaa ya pombe.

Katika jaribio moja la uchunguzi, panya walipewa maji yasiyochanganywa na kitu kingine na pia maji yenye pombe. Panya wengine walikunywa sana maji yenye pombe, wengine wakanywa kiasi kidogo kikilinganishwa na cha wale wengine na panya mmoja hakuyanywa. Wakati panya hao walipolishwa chakula chenye vitamini na madini nyingi, wengi wao walipunguza sana unywaji wa maji yenye pombe. Lakini walipopewa chakula chenye kukosa sana vitu vinavyohitajiwa mwilini, panya wote walianza kunywa kiasi kingi cha maji yenye pombe. Wenye kufanya jaribio hilo la uchunguzi, ambao wengine wao walikuwa ni wachunguzi wakuu wa mambo ya tiba, walifikia kukata shauri kwamba bila shaka pana uhusiano kati ya maelekeo ya kuzoea unywaji wa pombe na ulaji wa vitu visivyotosha katika mwili; pia kwamba tofauti za urithi zilisababisha kiasi chenye kutofautiana cha maji yenye pombe kilichonywewa na panya hao.

Matokeo hayo yametumiwa vizuri na washiriki fulani wa kikundi hicho cha uchunguzi wa mambo ya tiba katika kushughulika na watu wenye uzoevu wa kunywa pombe. Lakini, matabibu wanakazia kwamba ili njia hiyo ya ulishaji iwe na matokeo, ni lazima mtu awe na tamaa ya weupe wa moyo ya kutaka kushinda mazoea ya kutumia pombe, kwa maana lingekuwa kosa kupuuza ule upande wa kiadili unaohusu uzoevu wa kunywa pombe. Hawakubaliani na wale wanaotaka tuamini kwamba uzoevu wa kunywa pombe ni tatizo linalohusu kuwa na hali ya ugonjwa tu. Wala hawakosi kufikiria uhakika wa kwamba kulikuwa ama na hali ya kupuuza mambo au ya kutokujali upande wa wale ambao walikuja kuzoea kunywa pombe, ingawa huenda urithi na ulaji mbaya ukawa ulihusika sana.

Wale wanaotaka kuishi maisha za kimungu wanafikiria zaidi maoni ya Mungu juu ya matumizi mabaya ya pombe. Neno lake takatifu linasema pasipo shaka kwamba matumizi yasiyo ya kiasi ya vileo yanapasa kuepukwa na wale wanaotaka upendeleo wa kimungu. (Mithali 23:29-35; 1 Wakorintho 6:9,10) Jambo hilo linatoa msukumo usio na ulinganifu katika kushinda udhaifu wa namna hiyo.

Kuliacha Zoea la Kuvuta Tumbaku

Tabibu fulani alikuwa na mazoea ya kuvuta tumbako na alijaribu mara nyingi kuacha kuitumia. Lakini hakupata matokeo mazuri mpaka alipoamua kuwa Mkristo. Halikuwa jambo jepesi kuacha kuvuta sigareti, lakini haikuwa vigumu mno. (2 Wakorintho 7:1) Lakini, tabibu mwingine, ambaye ni ndugu ya kimwili ya daktari huyo, alikabiliwa na tatizo ilo hilo. Kwa habari yake, ilimchukua jitihada kubwa sana kushinda zoea hilo, kwa maana alikuwa mvuta-sigareti wa mfululizo. Ingawa mwishowe alipata matokeo mazuri, alisema kwamba kuvunja zoea hilo karibu kumfanye ajiue.

Watu fulani wenye ujuzi wa ulishaji unaohitajiwa mwilini watasaidia mtu aache zoea la kutumia tumbaku. Wanaamini kwamba mara nyingi wale walio na mazoea ya kutumia tumbaku wana neva mbaya, mzunguko usiofaa wa damu au wana uzito unaopita kiasi na kwamba kwa kuondoa matatizo hayo kuna nafasi nzuri zaidi ya kushinda mazoea hayo.

Njia nyingine inayohusu mwili (inayoitwa “Hatua Moja Moja”) ni ya kuvuta sigareti zenye vichungi fulani. Kwanza, mvutaji anatumia kichungi kinachoondoa asilimia 25 ya sumu ya tumbaku. Halafu kwa majuma mawili anatumia kingine kinachochunga asilimia 50; kisha, kingine kinachoondoa asilimia 75; na, mwishowe, kichungi kinachochunga asilimia 90. Inadaiwa kwamba baada ya hapo mtu hapaswi kuwa na ugumu wo wote wa kuacha kabisa.

Kushindana na Kupiga Punyeto

Tatizo jingine linalosumbua mawazo ya wengi, hasa vijana, ni kupiga punyeto, kujichua au mahaba ya kibinafsi ya ngono. Ni kweli Biblia haitaji kupiga punyeto kwa jina. Lakini, kwa kuwa kwa kawaida kunashirikishwa na mawazo ya kusisimukia ngono, kwa uhakika inakatazwa na maandiko yote yanayokataza mawazo na matendo ya namna hiyo. Kwa mfano, fikiria Warumi 13:14; Wagalatia 5:19, 24; Waefeso 5:3-5; 1 Wathesalonike 4:3-5; 1 Petro 2:11.

Kusudi letu hapa si kuzungumza habari inayoleta sana ubishi juu ya namna hasa kupiga punyeto kunavyoweza kudhuru mwili. Hata hivyo, ingefaa kuangalia kwamba Alexis Carrel ambaye amekwisha kufa, aliyekuwa mwanabayolojia mashuhuri na mshindi wa zawadi ya Nobel, alisema hivi katika kitabu chake Man, the Unknown: “Inajulikana sana kwamba mazoea ya kupita kiasi katika ngono yanazuia utendaji wa akili,” na kwamba kujiweza kunahitajiwa sana ili mtu aweze kutumia kwa ukamili nguvu zake za akili. Ni njia gani inayohusu mwili inayoweza kufuatwa isaidie?

Mara nyingi wale wanaopiga punyeto muda baada ya muda wanasumbuka katika neva na wanatatizwa na hali ya kukosa usingizi. Kwa kadiri ambayo wanaweza kufanyia maendeleo afya yao ya kimwili, kutia neva zao nguvu na kuletea maendeleo usingizi wao, watasaidiwa pia kujizuia katika jambo hilo.

Kula kwa kiasi ni msaada mwingine mkubwa. Kitabu Encyclopaedia Britannica (chapa ya mwaka wa 1959) kinasema yafuatayo chini ya kichwa “Viamsha Nyege”: “Ni jambo la maana kuepuka chakula chenye nyama nyingi na vikolezo, na hasa vileo.” Huenda ikawa kwamba wengine hawatakubaliana na maneno hayo. Lakini, hata mtu atoe sababu gani za ubishi, huenda akapata msaada kwa kujaribu njia hiyo inayohusu mwili.

Shikilia Viwango vya Biblia

Leo, zaidi ya nyakati zote zilizotangulia, washiriki wa jamii ya kibinadamu wanatatizwa wanapojaribu kuishi kulingana na viwango vya uadilifu vinavyopatikana katika Biblia. Bila shaka, kati ya mambo yanayosababisha jambo hilo ni urithi na pia malezi ya mtu na mazingira. Tena usiopasa kusahauliwa ni uhakika wa kwamba Shetani Ibilisi na mashetani wake wamejikaza waingize jamii ya kibinadamu katika tabia zilizoshuka. (Ufunuo 12:12) Lakini, kwa msaada wa Mungu na kwa kushikilia viwango vya Biblia, mtu anaweza kupata matokeo mazuri ampinge Adui huyo.—Yakobo 4:7.

Nyakati nyingine ile njia inayohusu mwili imesaidia katika kushughulika na matatizo ya uzoevu wa kunywa pombe, mazoea ya kutumia tumbaku na kupiga punyeto. Hata hivyo, dawa zilizo kuu ni misaada ya kiroho, kutia ndani kujifunza Neno la Mungu na vichapo vya Kikristo, kudumu katika sala, kujiacha tuongozwe na mavutano ya roho takatifu ya Yehova na kupokea msaada wa Wakristo waliokomaa. Kwa kuwa na msaada huo, udhaifu mbalimbali wenye kusumbua sana unaweza kushindwa kikweli.

[Sanduku katika ukurasa wa 24]

Wewe Unajitahidi?

Inakupasa ufanye nini ukitambua kwamba unahitaji kushinda matumizi mabaya ya pombe, zoea la kutumia tumbaku au kupiga punyeto? Ona kama unaweza kupata nguvu nyingi zaidi katika mmoja au mingi kati ya misaada hii iliyotolewa kwa njia ya kimungu:

1. Soma Neno la Mungu kwa ukawaida, ukijipatia nguvu kutokana nalo.

2. Mpelekee Mungu sala kila siku, ukitafuta faraja na msaada wake.

3. Omba Mungu roho takatifu yake, au kani ya utendaji.

4. Jipatie nguvu kutokana na msaada unaopatikana kwa Wakristo waliokomaa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki