Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 10/15 kur. 25-30
  • Kubali Msaada wa Mungu Ushinde Makosa ya Siri

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kubali Msaada wa Mungu Ushinde Makosa ya Siri
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kosa la Siri Linalohusu Tamaa ya Ngono
  • Kuacha Kosa Hilo la Siri
  • Kushindana na Matumizi Mabaya ya Kileo
  • Mungu Anathawabisha Vitendo vya Faragha
  • Kuacha Kupiga Punyeto—Kwa Sababu Gani? kwa Njia Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Ninaweza Kushinda Jinsi Gani Mazoea ya Kupiga Punyeto?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
  • Punyeto na Ngono za Wanaume kwa Wanaume na Wanawake kwa Wanawake
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Kuendelea Kuwa na Maoni ya Mungu Juu ya Ngono
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 10/15 kur. 25-30

Kubali Msaada wa Mungu Ushinde Makosa ya Siri

“Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.”​—WAFILIPI 4:13.

1. Baba mmoja mwenye kuhangaika alitoa ombi gani?

MVULANA huyo alikuwa mwenye kifafa.a Alitokwa na povu kinywani, mwili ulitetemeka-tetemeka, na nyakati nyingi alianguka ndani ya maji au moto. Baba yake mwenye wasiwasi akamtafuta mtu aliyejulikana kwa kuponyesha wagonjwa. Ilipoonekana kwamba baba huyo hakuwa na uhakika kwamba mtu huyo alikuwa mwenye uwezo, baba alilia hivi: “Nina imani! Nisaidie pale nilipo na uhitaji wa imani!” (NW)

2. Tunaweza kuwaje na uhakika kwamba Mungu anataka kutusaidia tuache makosa?

2 Tunaweza kujifunza jambo fulani kutokana na baba huyu aliyetaka msaada wa Yesu. Mtu huyo alikubali kwamba imani yake labda ilikuwa na kasoro; pia alikuwa na uhakika kwamba Yesu alitaka kusaidia. Inaweza kuwa hivyo kwetu, tunapokabili makosa yetu wenyewe​—hata yale ya siri​—na kujitahidi kuyashinda. Tunaweza kutumaini kwamba Yehova Mungu anataka kutusaidia, kama ambavyo amesaidia wengine wakati uliopita. (Linganisha Marko 1:40-42.) Kwa mfano, yeye alisaidia mtume Paulo akabiliane na makosa yanayoweza kuletwa na kuwa na vitu vingi au kuwa na uhitaji. Huenda maskini akatamani sana utajiri; kasoro ya tajiri yaweza kuwa tumaini lake la kujivunia mafanikio na kudharau wale wenye vitu vichache. (Ayubu 31:24, 25, 28) Paulo alishindaje au aliepukaje makosa hayo? Anasema: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.”​—Wafilipi 4:11-13.

3. Kwa sababu gani ni jambo la hekima tujaribu kushinda udhaifu wetu?

3 Tukitumia nguvu za Mungu, tunakuwa wenye hekima tukijitahidi kushinda makosa yetu, wala si kuyapuuza tu kwa sababu kwa wakati huu ni ya siri. Mtunga zaburi alisema hivi juu ya Yehova: “Ndiye azijuaye siri za moyo.” (Zaburi 44:21) Tusiposhinda makosa yetu, huenda yakatokea nje na kuleta madhara makubwa. Kanuni hii inahusika: “Dhambi za watu wengine zi dhahiri, zatangulia kwenda hukumuni; wengine dhambi zao zawafuata.” (1 Timotheo 5:24) Na tuchunguze makosa mawili ambayo ni ya kawaida yanayostahili kuangaliwa na Wakristo wanaotaka kumpendeza Yehova.

Kosa la Siri Linalohusu Tamaa ya Ngono

4, 5. (a) Biblia inatoa maoni gani yaliyosawazika juu ya tamaa za ngono? (b) Ni maonyo gani tunayopata katika Maandiko kuhusu nyege?

4 Moja ya zawadi nzuri za Mungu ni ndoa, pamoja na uwezo na tamaa ya kuzaa. (Mwanzo 1:28) Tamaa ya ngono inayoonyeshwa wakati wa ngono ni jambo la asili na ni safi. Biblia inasifu kufurahia ngono na mwenzi wako mwenyewe. (Mithali 5:15-19) Lakini, tamaa ya ngono inapasa kuwekewa vizuizi. Kwa kulinganisha, fikiria tamaa yetu ya chakula. Kwa sababu hamu yetu ya chakula inarudi-rudi haimaanishi kwamba tunapaswa kusitawisha tamaa isiyofaa ya chakula, au kwamba hatuhitaji kuweka mipaka ya ni wakati gani, ni wapi, na jinsi gani tutakula.​—Mithali 25:16, 27.

5 Huenda ikawa wakati mmoja Paulo alikuwa ameoa, na alijua kwamba mawonyeshano ya kawaida ya ngono kati ya wenzi yalifaa. (1 Wakorintho 7:1-5) Kwa hiyo lazima awe alikuwa akimaanisha juu ya jambo jingine alipoandika hivi: “Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya [za ngono], mawazo mabaya, na kutamani.” (Wakolosai 3:5) Lazima awe alikuwa akimaanisha mawonyesho ya ngono yanayopita mpaka wa ndoa unaofaa na namna ya kuyatosheleza. Mtume huyo pia alisema: “Kila mmoja wenu anapaswa kujua namna ya kumiliki chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima; si katika hali ya tamaa mbaya [ya ngono].” (1 Wathesalonike 4:4, 5) Shauri hilo la waziwazi, lililoongozwa kwa roho ya Mungu lina faida kwa Wakristo waliofunga ndoa na walio waseja.

6. Ni kwa sababu gani kwa kufaa Wakristo wanaepuka kupiga punyeto?

6 Njia moja ambayo hiyo “tamaa kali ya mwili” (1 Wathesalonike 4:5, The New Testament for English Readers, ya Henry Alford) inaonyeshwa mara nyingi ni kwa mtu kusisimua viungo vyake vya ngono kwa ajili ya raha inayohusika. Jambo hilo linaitwa kupiga punyeto, au kujichua. Ni jambo la kawaida sana kati ya watu wa kiume na kike walio waseja. Lakini pia wengi ambao wamefunga ndoa wanashiriki zoea hilo. Kwa kuwa ni la kawaida, linafanya madaktari wengi wadai kwamba ni jambo linalofaa tena lenye faida. Lakini, zoea hilo linapingana na shauri la Mungu linalokataza ‘tamaa mbaya ya ngono.’ Tunaweza kuthamini zaidi ni kwa sababu gani ndivyo ilivyo, na kwa sababu gani Wakristo wanapaswa kushinda zoea hilo, kwa kufikiria mashauri fulani aliyotoa Yesu.

7. Andiko la Mathayo 5:28 linatoaje sababu ya ziada ya kujiepusha na kupiga punyeto?

7 Yesu alisema: “Kila mtu atazamaye [“anayeendelea kumtazama,” NW] mwanamke kwa kumtamani [“hata awe na nyege kwa ajili yake,” NW], amekwisha kuzini naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28) Yeye alijua kwamba mara nyingi mawazo ya kuzini yenye kuongozwa na nyege yanatangulia vitendo vya kukosa adili. Na hata wale wanaosema kupiga punyeto si kosa wanakubali kwamba kwa kawaida kunaleta mawazo ya ngono. Baada ya kuzungumza juu ya vijana “kutambua raha ambayo kupiga punyeto kunaweza kuleta,” kitabu Talking With Your Teenager kinaongeza kusema hivi: “Huenda wakajiwaza katika hali za kufanya ngono za maajabu au na wenzi wa jinsia ile ile au na watu ambao ni wakubwa kwa umri kama walimu, watu wa ukoo, hata [wazazi]. Huenda wakawa na mawazo juu ya jeuri ya ngono. Yote hayo ni mambo yanayofaa kabisa.” Lakini yanafaa kweli? Wakristo wangewezaje kuyaona mawazo hayo na kupiga punyeto kuwa ni “mambo yanayofaa” kwa kukamatana na onyo la Yesu juu ya ‘kuzini moyoni’ au shauri la Paulo dhidi ya ‘tamaa mbaya ya ngono’ (“nyege,” NW)? Hapana, mawazo hayo na kupiga punyeto​—kuwe kunafanywa na kijana au mtu mzima, na mseja au mtu aliyefunga ndoa​—yanahitaji kuachwa.

Kuacha Kosa Hilo la Siri

8, 9. Ni kuthamini mambo gani ya uhakika kunakoweza kumsaidia mtu avunje tabia ya kupiga punyeto?

8 Ikiwa Mkristo alikuwa na kosa hilo la siri, angeweza kufanya nini ili aliache, “ajue kuuweza mwili wake katika utakatifu na heshima”? (1 Wathesalonike 4:4) Kupitia Neno lake, Mungu anatoa msaada wenye thamani sana.

9 Kwanza ni jambo la maana kutambua kwamba Yehova ana viwango. Anaonyesha wazi kosa la kufanya ngono nje ya ndoa, uasherati na uzinzi pia. (Waebrania 13:4) Kwa hiyo, ikiwa tunasadiki kwamba njia zake ndizo bora, tutatafuta thawabu za kuridhisha za wonyesho wa nyege katika ndoa tu. (Zaburi 25:4, 5) Kitabu Adolescence, cha E. Atwater, kinataja kwamba kuhusu kupiga punyeto, kwa kawaida vijana wanaonyesha ‘kuficha maoni yao, kuona aibu na kujitilia mashaka.’ Sababu moja inayotolewa ni kwamba ‘ukaribu wa uhusiano wa upendo unaoambatana na ngono unakosekana katika kupiga punyeto.’ Ndiyo, kuna faida ya kuzuia nyege mpaka ziweze kuonyeshwa katika uhusiano wa upendo katika ndoa.

10. Ni hatua gani kati ya zile ambazo mtu anaweza kuchukua ili aache zoea hilo ni gani?

10 Neno la Mungu linatoa msaada zaidi kwa kushauri hivi: ‘Mambo yo yote yaliyo ya kweli, mambo yo yote yanayohusu kwa uzito, mambo yo yote yaliyo ya uadilifu, mambo yo yote yaliyo safi, mambo yo yote yenye kusemewa vizuri na wema wo wote uliopo, endeleeni kufikiria mambo hayo.’ (Wafilipi 4:8, NW) Kwa wazi, picha za kuamsha nyege na vitabu vya hadithi zisizo za adili si ‘safi na havisemewi vizuri.’ Na mambo hayo mara nyingi ndiyo kawaida ya wenye kupiga punyeto. Mtu ye yote aliyeazimia kushinda kosa hilo, basi, lazima aepuke kabisa vitu hivyo vyenye kuamsha nyege. Mambo yaliyoonwa yamethibitisha kwamba kama tamaa za mtu zinaanza kuvutwa kuelekea vitu vya kuamsha nyege kwa njia ambayo hapo kwanza ilisababisha kupiga punyeto, azimio la kukaza fikira juu ya yaliyo ya uadilifu na yaliyo safi laweza kutuliza tamaa hizo. Jambo hilo ni la maana hasa ikiwa mtu yuko peke yake au gizani, wakati ambapo kosa la siri la kupiga punyeto linakuwa la kawaida zaidi.b​—Warumi 13:12-14.

11. Simulia mambo zaidi ambayo yamekuwa yenye faida katika kupambana na kosa hilo.

11 Msaada unaohusiana na huo ni kujishughulisha, kwa kupatana na onyo la upole hili: “Endeleeni kulinda kwa uangalifu sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama wasio na hekima bali kama watu walio na hekima, kununua kabisa wakati unaofaa kwa ajili yenu wenyewe, kwa sababu siku ni zenye uovu.” (Waefeso 5:15, NW) Muulize Mkristo aliyekomaa ambaye unaweza kumweleza siri zako akupe mapendekezo juu ya mambo yanayofaa unayoweza kufanya. (Isaya 32:2) Wengi ambao wameacha kosa hilo wanakubali kwamba kujua kwao kwamba Mkristo anayewahangaikia angewauliza maendeleo waliyofanya kuliwasaidia wasitawishe kujiweza. Bila shaka, Yule anayepaswa kuwa msiri wetu wa karibu zaidi ni Yehova. Kwa hiyo ni jambo la maana sana kumwendea yeye katika sala, na kutafuta msaada wake. (Wafilipi 4:6, 7) Mtu ambaye ameshindana na kosa hili kwa muda ‘akijikwaa,’ anaweza kumwomba Mungu nguvu, halafu anaweza kutia jitihada mpya na inaelekea atafaulu tena, kwa kipindi kirefu hata zaidi.​—Waebrania 12:12, 13; Zaburi 103:13, 14.

Kushindana na Matumizi Mabaya ya Kileo

12. Maoni ya Kikristo juu ya vileo ni nini?

12 ‘Divai humfurahisha Mungu na wanadamu,’ ndivyo unavyosema mstari mmoja wa Biblia. (Waamuzi 9:13) Huenda ukakubaliana nao, kwa maana vileo vimekuwa msaada wa kustarehesha na chanzo cha furaha nyingi kwa wengi. (Zaburi 104:15) Lakini, ni wachache ambao wangekana kwamba kutumia kileo kunaweza kutokeza hatari za kimwili na za kiadili. Tatizo kubwa ni ulevi wa kabisa. Kosa hilo ni zito sana hata kwamba Mungu anaonya kwamba walevi wanaweza kufukuzwa kutoka kwenye kundi na kuzuiwa wasiingie katika Ufalme. (1 Wakorintho 5:11-13; Wagalatia 5:19-21) Wakristo wanatambua hilo na wangekubali kwamba ni lazima waepuke kulewa. Lakini, licha ya ulevi, matumizi ya kileo yangewezaje kuwa kosa la siri?

13. Onyesha jinsi kutegemea kileo kunaweza kusitawi.

13 Huenda Mkristo akanywa kwa kiasi, lakini bado awe na kosa zito. Fikiria jambo lililoonwa na mtu ambaye tutamwita Juma.

Yeye, na mkeye, na watoto walikuwa Wakristo wa kweli na walikuwa wenye kutenda sana katika kundi la kwao. Muda si muda Juma aliwekwa awe mzee akaja kuonwa ni ‘nguzo’ kati ya makundi ya mji huo. (Wagalatia 2:9) Ni jambo la kueleweka kwamba alikabili mikazo ya kulea jamaa yake na mahangaiko mengine katika kutunza kundi. (2 Wakorintho 11:28) Lakini, kazi yake ilimletea mkazo mwingi kwa sababu shirika alilokuwa akifanyia kazi lilikuwa linakua, na tajiri wake alitaka ashughulike na matatizo na maamuzi mengi.

Jioni nyingi Juma alikuwa mwenye wasiwasi sana. Akakuta kwamba bilauri moja au mbili zingemsaidia kustarehe. Kwa wazi, akiwa Mkristo aliyekomaa aliepuka kwa uangalifu kunywa kupita kiasi au kulewa. Ingawa alikunywa vinywaji fulani ili astarehe jioni, yeye hakuhitaji kileo mchana, na wakati mwingi hata hakuwa akinywa alipokuwa akila chakula. Yeye hakujulikana kuwa ‘mwenye kujipa kwa divai nyingi.’​—1 Timotheo 3:8, NW.

Bila kutazamiwa Juma alipelekwa hospitali afanyiwe upasuaji wa kawaida. Dalili fulani zisizo za kawaida zikatokea. Zilisababishwa na nini? Haikuwachukua muda mrefu wafanyi kazi wa hospitali kutambua kwamba Juma alikuwa akitatizwa na dalili za zoea alilokuwa ameliacha. Ndiyo, mwili wake ulikuwa umekuwa wenye kutegemea kileo. Jambo hilo liliishangaza jamaa, lakini walimuunga mkono na kutegemeza azimio lake la kuacha kabisa kileo.

14. Ni mambo gani ambayo yanaweza kumwongoza mtu adhihakiwe na vileo?

14 Wengine wanahisi kwamba kileo kimekuwa na mahali pasipo pa kawaida maishani mwao, kwa hiyo wanajaribu kuficha unywaji wao, wasitake jamaa na marafiki watambue wanakunywa kiasi gani au ni mara ngapi wanakunywa. Huenda wengine wasihisi wanategemea kileo, na bado kunywa kumekuwa jambo kubwa kila siku. Walio katika yo yote ya hali hizo wako katika hatari kubwa ya kunywa kupita kiasi pindi fulani au ya kuwa wazoelevu wa kileo wa siri. Fikiria mithali hii: “Mvinyo hudhihaki, kileo huleta ugomvi; na akosaye kwa vitu hivyo hana hekima.” (Mithali 20:1) Jambo kubwa ni kwamba kunywa kupita kiasi kunaweza kumfanya mtu achangamke kupita kiasi na kutenda kipumbavu. Hata hivyo, divai inaweza kumdhihaki mtu kwa njia nyingine. Mtu anastahili dhihaka ikiwa anafikiri kwamba kunywa kwake ni siri kwa Mungu.

15. Maneno ya Paulo katika 1 Wakorintho 9:24-27 yanahusuje matumizi ya Mkristo ya kileo?

15 Moja la matunda ya roho ya Mungu ni kujiweza, nasi tunahitaji tunda hilo katika sehemu zote za maisha. (Wagalatia 5:22, 23) Paulo alimfananisha Mkristo na mwanariadha. Katika mbio za kawaida mwanariadha “anazoea kujiweza katika mambo yote” ili apate tu “taji lenye kuharibika.” Hali moja na hiyo, Mkristo anahitaji kuonyesha “kujiweza katika mambo yote” ili apate thawabu ya thamani kubwa zaidi​—UZIMA. Paulo alikazia kwamba ni lazima ‘tuongoze mwili wetu kama mtumwa’ ili tuwe na uhakika ‘kwamba baada ya kuhubiria wengine hatutakataliwa kwa vyo vyote,’ kama kwa kosa la siri linalohusu kileo.​—1 Wakorintho 9:24-27, NW

16. Mtu anaweza kuamuaje kama kileo kimekuwa kosa katika kisa chake?

16 Ni nini kinachoweza kumsaidia Mkristo apambane na kosa hilo? Inasaidia kujua kwamba ingawa mnywaji huenda akaficha wanadamu wengine kielelezo chake, hawezi kumficha Mungu. (1 Wakorintho 4:5) Kwa hiyo, kwa unyofu​—machoni pa Mungu​—mtu anapaswa kufikiria juu ya tabia zake za unywaji. (Tunamaanisha kunywa kwa ajili ya raha au ili mtu ajisikie vingine, si kiasi kidogo kama kileo cha kawaida pamoja na chakula.) Lakini, wengine huenda wakasema, ‘Lakini si lazima ninywe. Ninakifurahia tu; kinanistarehesha. Kama ningetaka naweza kujiepusha nacho.’ Kwa sababu ya hatari zinazoweza kuwapo za kunywa kupita kiasi au kutegemea kileo, sababu gani usiache kwa mwezi mmoja au miwili? Au, kwa kuwa kuna mwelekeo wenye nguvu wa kukana kwamba hakuna tatizo, azimia kwa mwezi mmoja kuacha nyakati zote ambazo kunywa kungekuwa ni kawaida. Kwa mfano, mtu ambaye kwa kawaida anakunywa baada ya kazi, kabla ya kwenda kulala, au kwenye mkusanyiko wa kirafiki angeweza kuepuka kufanya hivyo. Kwa njia hiyo anaweza kupima anavyojisikia. Ikiwa ni vigumu, au ‘anashindwa kustarehe,’ ana kasoro kubwa.

17. Ni kwa sababu gani Mkristo mwenye kosa la siri linalohusu kileo anapaswa kujitahidi kulishinda?

17 Mara Mkristo mwenye moyo mweupe akiisha kutambua mbele za Mungu kwamba ana kosa linalohusu kileo, itakuwa rahisi kuliacha. Huenda akawa anajua tayari kwamba Biblia inasema “mjinga” ndiye anayewaza kwamba “maji yaliyoibiwa ni matamu, na mkate [au kileo] ulioliwa kwa siri hupendeza.” Hata hivyo, Mithali hiyo inasema, watu wa namna hiyo wataishia katika kifo wakiwa wasiojiweza. Tofauti yake, mwenye hekima hupenda karipio, na kwa furaha ‘anaacha wajinga na kuendelea kuishi kwa kutembea katika njia ya ufahamu.’ (Mithali 9:1, 6, 8, 13-18) Ndiyo, Mungu anatoa msaada zaidi wa kuacha makosa ya siri kwa kutujulisha yaliyo mbele, yatakayokuwa matokeo ya mwisho.

Mungu Anathawabisha Vitendo vya Faragha

18. Tunapoacha makosa yetu ya siri, tunaweza kuwa na uhakika wa nini? (Mithali 24:12; 2 Samweli 22:25-27)

18 Watu wengine wanaishi wakiogopa kwamba njia zao mbaya zitajulikana, na wanadamu au na Mungu. Na isiwe hivyo kwetu. Badala yake, na tuishi tukitambua kwamba hatuwezi kumficha mambo Yeye, “kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.” (Mhubiri 12:14) Na tukubali msaada wa Yehova wa kutuachisha makosa yetu, hata yale yaliyofichwa. Halafu tunaweza kutazamia wakati ambapo “yaliyositirika ya giza” yataangazwa na “mashauri ya mioyo” yatakapoonyeshwa wazi. “Ndipo kila mtu atakapoipata sifa yake kwa Mungu.”​—1 Wakorintho 4:5; Warumi 2:6, 7, 16.

[Maelezo ya Chini]

a Maandiko ya Mathayo 17:14-18, Marko 9:17-24, na Luka 9:38-43 yanaonyesha kwamba kupagawa na mashetani kulisababisha hali yake. Biblia inatofautisha kifafa hicho na kile kinachosababishwa na mambo ya asili.​—Mathayo 4:24.

b Nyakati nyingine wakati wa usingizi mwili unatoa shahawa bila mtu kutaka. Tukio hilo la asili si sawa na kupiga punyeto kwa makusudi.

Je! Unakumbuka?

◻ Mungu anaonaje makosa ya siri ambayo huenda tukawa tunajitahidi kuyaacha?

◻ Ni mashauri gani ya Kimaandiko yanayoonyesha kwamba kupiga punyeto kunapasa kuepukwa?

◻ Mkristo anaweza kuachaje tabia ya kupiga punyeto?

◻ Kwa kuwa Biblia hailaani kileo, kukitumia kunaweza kuwaje kosa la siri?

◻ Ni hatua gani za hekima zinazoweza kuchukuliwa katika kupambana na kosa la kibinafsi linalohusu vileo?

[Sanduku katika ukurasa wa 26]

Aliacha Kupiga Punyeto

AKIWA KIJANA MWANAMUME, C———alikuwa na nyege zilizo za kawaida, lakini pia alikuwa na tatizo. Tangu umri wa miaka 13 alikuwa na tabia ya kupiga punyeto, kwa kawaida akiwa katika siri kwenye chumba chake cha kulala. Alionea jambo hilo aibu kidogo, lakini alikuwa na maoni kwamba halikumuumiza mtu mwingine ye yote.

Kufikia alipokuwa mwenye miaka 19, zoea hilo lilikuwa limetia mizizi Pindi fulani C——alikiri jambo hilo kwa kasisi wake, lakini aliambiwa ingawa lilikuwa kosa halikuwa kosa zito sana.Wakati C———alipojiunga na jeshi, hakuwa na wakati mwingi wa kuwa katika siri Kwa hiyo, ni mara chache alipopiga punyeto, jambo ambalo, kama ilivyo, linaonyesha kwamba tabia yake ya kwanza haikuwa matokeo ya nyege zisizozuilika.

Alipotoka jeshini, C———alirudi nyumbani. Alianza kununua magazeti yenye kuonyesha ngono kwa njia chafu na, kwa kuamshwa nayo, upesi akarudia njia zake za kwanza Alipoanza kuishi peke yake, ilikuwa rahisi kuwa na vitabu vya kusisimua nyege Mara nyingi alipiga punyeto mara kadha kwa siku

Halafu akaanza kujifunza Biblia pamoja na mhudumu wa Mashahidi wa Yehova. Alipojua maoni ya Mungu juu ya mwenendo usio wa adili,C———aliona aibu kununua vitabu vyenye kuonyesha ngono kwa njia chafu, naye alitaka kuvunja tabia ya kupiga punyeto. Alijaribu Lakini baada ya juma moja au mbili angehisi nyege zimemkaza, angesimama kando ya meza ya magazeti, na angeamshwa na vitabu hivyo vya mwenendo usio wa adili. Akiisha kurudi nyumbani, angekuwa na maoni kwamba kwa kuwa tayari alikuwa ameshindwa, ni sawa tu akichukua hatua nyingine. Baadaye, angesikitika. Je! kwani hangeweza kamwe kuvunja tabia hiyo mbaya?

Mwishowe C———akazungumza na mzee wa kiroho kwenye kundi. Mhudumu huyo alikuwa mwenye ufahamu naye akamsaidia asome vitabu vyenye kutegemea Biblia ambavyo vingemsaidia afanye kujiweza kwake kuwe bora Mhudumu huyo pia akaeleza:

‘Wazia tamaa ya kuwa kama mnyororo. Kiunganishi cha kwanza ni kidogo na dhaifu. Lakini kila kiunganishi kinachofuata mfululizo huo kinakuwa kikubwa zaidi na kigumu zaidi. Ndivyo vilivyo vishawishi vinavyoongoza kwenye kupiga punyeto. Kwa hiyo unahitaji kuacha nyege upesi iwezekanavyo. Zinavyoendelea zaidi, ndivyo tamaa yako inavyoongezeka zaidi. Mwishowe zitakuwa karibu zisizozuilika. Ndiyo, jaribu kuvunja mnyororo kwenye kiunganishi cha kwanza. Unapohisi nyege ikija, CHUKUA HATUA! Simama ubadili kikao chako, piga rangi viatu vyako, katupe taka-taka zilizo ndani ya nyumba​—fanya jambo lo lote uvunje kiunganishi hicho .Huenda ukaanza kusoma kitu fulani kwa sauti kubwa, kama vile Biblia au kichapo cha Kikristo kitakachoelekeza fikira zako katika njia safi.’

Mhudumu huyo akawa akimuuliza C———kwenye mikutano mambo yalivyokuwa yakiendelea, kwa ukawaida akimsifu na kumtia moyo azimio lake. Kwa majuma saba C———alifaulu. Halafu, alipokuwa amevurugika akili na kuvunjwa moyo na tatizo jingine, akaanguka tena, akanunua vitabu vyenye kuamsha nyege. Kufanya hivyo kukamrudisha katika hali ya kwanza. Matukio kama hayo yalikuwa vikwazo, lakini mhudumu huyo alimtia moyo aendelee kung’ang’ana. Polepole vipindi vya kuacha vikarefuka vikawa majuma 9, kisha majuma 17, halafu hata virefu zaidi. Polepole uhakika wake ukaongezeka kwamba angeweza kushinda tatizo hilo la siri.

Mwishowe C———akaufahamu vizuri uhakika wa kwamba Yehova alijua yote aliyokuwa akifanya. Kwa hiyo, kama alitaka kumtumikia Mungu kwa dhamiri safi, angepaswa kuondoa kabisa zoea hilo maishani mwake. Alifanya hivyo! Sasa hata hawezi kukumbuka ni muda gani umepita. Akiwa Mkristo aliye mfano mwema, C———amepewa daraka kundini, na anafanya mipango ya kuongeza utumishi wake iwe kwa sifa ya Mungu Yeye ni mtu tofauti.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki