Je! Kuna Wakati Ambao Wewe Utaishi Katika Ulimwengu Wenye Furaha?
WALE wanaothibitika kuwa wapenda Mungu—“watu wake”—wana sababu nzuri za kupanga kuishi katika ulimwengu wenye furaha. (Warumi 15:10) Ingawa wakati ujao wa hapa karibu unaelekea kuwa usio na matumaini mazuri kwa ulimwengu wa wanadamu, Mungu wa mbingu anatangazisha duniani pote ‘habari njema zake tukufu,’ nazo ni ujumbe wenye kuwatia watu moyo kweli kweli. (1 Timotheo 1:11, NW) Ni muda mfupi ambao sasa umebaki ndipo Ufalme wa kimbingu wa Mfalme wa Kimasihi Yesu Kristo ambao umengojewa muda mrefu ugeuze mambo yanayoonyesha dalili za maafa ambayo yanaonekana wazi sana duniani leo. Kisha utayamaliza matatizo yanayowapiga wanadamu sasa. Ufalme huo uko karibu kuleta upesi ulimwengu wenye furaha.
Mambo Ambayo Ufalme Utafanya
Je! kuna hangaiko juu ya kujaza dunia watu wengi mno? Kuzuia jambo hilo hakutamshinda wala Yehova Mungu wala Mfalme Yesu Kristo. Mwanzoni kabisa Mungu alikusudia wanadamu ‘wajaze dunia,’ si waijaze kupita kiasi. Hata iwe ni njia gani itakayotumiwa kuzuia dunia isijae watu wengi mno, tunaweza kuwa na uhakika kwamba mapenzi ya kimungu katika jambo hili yatatimia duniani.—Mwanzo 1:27, 28; Isaya 45:18.
Chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, je! kutakuwako pengo lenye kusumbua sana mioyo ya watu lililo kati ya matajiri na maskini? La, hasha! Bali, ilitabiriwa katika Maandiko kwa njia yenye kutegemeka kwamba Mfalme mkarimu wa Mungu “atamwokoa mhitaji aliapo.”—Zaburi 72:1, 12, 13.
Je! kuna sababu za kukatishwa tamaa na upungufu wa mali za asili na kupoteza kwa mazingira “nguvu kuu za namna mbalimbali zinazosaidia kuendeleza uhai”? Je! tuna uhitaji wa kukata tamaa kwa sababu bei za vitu zinapanda sana kwa kiasi kisichoweza kufikiwa na watu wa kawaida? Ingawa wakati ujao wa hapa tu mbele yetu hauonyeshi matumaini mazuri katika jambo hilo, Neno la Mungu, Biblia, linaahidi hivi: “Kutakuja kuwa na nafaka tele juu ya dunia; juu ya kilele cha milima kutakuwa na mfuriko.” (Zaburi 72:16, NW) Je! maneno hayo yanaonyesha dunia wakati huo itakuwa haina mali za asili, kwamba mazingira yake hayatakuwa na “nguvu kuu za namna mbalimbali zinazosaidia kuendeleza uhai”? Au ahadi hiyo ya Kimaandiko inaonyesha kwamba mahitaji ya maisha yatakosekana sana hata iwe haiwezekani kuwa na maisha yenye kuridhisha duniani? Hakika haionyeshi hivyo.
Chini ya utawala wa Ufalme, je! Ulimwengu “utakuwa zaidi na maelekeo ya kupatwa na maafa yanayosababishwa na nguvu za asili na kuletewa misukosuko ya ghafula na wanadamu”? Hapana, kwa maana karibuni Mungu ‘atavikomesha vita’ milele. Kuongezea hilo, chini ya usimamizi wa Ufalme majangwa yatachanua, na vitu vyenye madhara havitaelekea tena kuharibu afya na uhai. Furaha isiyo na mipaka itakuja ichukue mahali pa magumu na kihoro (huzuni).—Linganisha Zaburi 46:1, 9; Isaya 35:1-10; 65:25.
Kitu Kipya Kwenye Upeo wa Macho
Kati ya unabii mwingi wenye kutia moyo na kutabiri baraka nzuri ajabu watakazopata wanadamu ni ule ulioandikwa na mtume Mkristo Yohana akisema hivi:
“Nikaona mbingu mpya na nchi mpya; kwa maana mbingu za kwanza na nchi ya kwanza zimekwisha kupita, wala bahari tena. Nami nikauona mji ule mtakatifu, Yerusalemu mpya, ukishuka kutoka mbinguni kwa Mungu, umewekwa tayari, kama bibi-arusi aliyekwisha kupambwa kwa mumewe. Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha enzi ikiseme, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:1-4.
Hapa semi nyingine zimetumiwa sana kwa njia ya mfano, lakini ni wazi kwamba baraka zitakuwa kubwa. “Mbingu mpya” ndizo ufalme wa kimbingu wa Yesu Kristo na wafalme na makuhani wenzake 144,000. (Warumi 8:16, 17; Ufunuo 14:1-4; 20:4) “Nchi mpya” si dunia iliyo sayari mpya, bali ni jamii mpya ya watu watakaokuwa juu ya dunia ii hii, wote wakiwa wamejitiisha kabisa kwa ufalme wa Kristo bila kuwa na migawanyiko ya kikabila, kitaifa wala ya kilugha. (Linganisha Zaburi 96:1.) Jamii hiyo itakuwako baada ya uharibifu wa “mbingu” na “nchi” za sasa zilizo za mfano. Jamii mpya ya kidunia iliyoahidiwa itakuwa yenye uadilifu kwa sababu “bahari” ya mfano ambayo ni watu wenye fujo, waasi na wasiomcha Mungu hawatakuwapo tena, ingawa bahari halisi zitabaki. Watawala wa kimbingu walio washirika wa Kristo ndio watakaokuwa “Yerusalemu mpya,” tengenezo kuu lililowekwa kufaidi jamii ya wanadamu wenye uadilifu. Mungu atapiga hema yake pamoja na watu hao duniani kwa njia ya kuwakilishwa mpaka watakapokuwa wamepatanishwa naye kabisa kupitia Kristo, “Mwana-kondoo wa Mungu,” baada ya siku ya hukumu ya miaka elfu moja.—Yohana 1:29, 36; Ufunuo 20:6.
Chini ya utawala wa Ufalme, kutakuwako sababu nyingi za kufurahi. Maombolezo, kilio na maumivu yanayoletwa na mambo mbalimbali yataondolewa. Kifo kilichoenea kutokana na Adamu mwenye dhambi, yule mtu wa kwanza, hakitakuwapo tena. (Warumi 5:12) Chanzo kikubwa sana chenye kuleta machozi ulimwenguni pote kitakuwa kimetoweka! Na lo! kutakuwako sababu za kufurahi kama nini wakati kutakapotokea visa vya ufufuo badala ya visa vya kufa kwa sababu ya Adamu, wakati wazao wake watakuwa wameokolewa kutokana na matokeo ya dhambi yake, na wakati afya nzuri kabisa ya kibinadamu itakuwa imekuja badala ya magonjwa mengi yanayowapiga wanadamu sasa! Hakika hapo ndipo ‘mambo ya kwanza yatakapokuwa yamekwisha kupita.’
‘Wapi, hizo ni ndoto tu!’ huenda mtu akapaza sauti. Hapana, si ndoto, kwa maana baada ya mtume Yohana kuona “mbingu mpya” na “nchi mpya” zitakazoletea wanadamu baraka kubwa-kubwa, aliongeza kusema: “Na yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi [Yehova Mungu] akasema, Tazama, nayafanya yote kuwa mapya. Akaniambia, Andika ya kwamba maneno hayo ni amini na kweli.” (Ufunuo 21:5) Ndiyo, tunaweza kuyaamini.
Kwa kweli, ulimwengu tofauti uko kwenye upeo wa macho. Kuwako kwake hakutategemea mabadiliko ya kibinadamu katika “njia ya kuendesha mambo ya watu wote” yenye kusudi la kuokoa wanadamu katika matokeo mabaya sana yaliyotokana na “kukosa kutumia vizuri hali ambazo zingaliweza kuleta mafaa.” Hapana, bali mambo mazuri yote yaliyoahidiwa katika Maandiko yanategemea kutimizwa kwa mapenzi ya kimungu yasiyoweza kuzuiwa, yenye kufanikiwa nyakati zote.
Furaha Ambayo Wewe Unaweza Kupata
Ni nani atakayefurahia baraka zote hizi zitakazotoka kwa Mungu? Ni akina nani watakaokuwa na sababu ya kufurahi daima dawamu? Ni wote wanaoutumia vizuri mpango wa Mungu wa kupata uzima wa milele! Baraka hiyo iliyo nzuri ajabu imefanywa na Yehova iweze kupatikana, yule ‘Mungu wa upendo,’ kupitia Mwanaye, Yesu Kristo.—1 Yohana 4:8, 9; Yohana 3:16.
“Habari njema” za mambo makubwa hayo ndizo Mashahidi wa Yehova wanajaribu kueleza watu wenye mioyo minyofu. Hiyo ndiyo sababu wanatoa ushuhuda nyumba kwa nyumba kwa kufuata njia iliyotumiwa na mitume wa Yesu na wanafunzi wake wengine. (Matendo 5:42; 2:20) Bila shaka wewe unaweza kufahamu ni kwa sababu gani Mashahidi wanavutwa na mioyo yao wautangaze ujumbe wenye furaha wa Ufalme kwa juhudi na furaha ya moyoni. Hizo ni habari njema kweli kweli! Lakini utafanya nini na habari hizo zenye kutia moyo? Inawezekana ufurahie uzima usio na mwisho katika furaha ukiwa juu ya dunia ya paradiso chini ya utawala wa Ufalme. Walakini, ili uufurahi unatakwa uwe na maarifa sahihi ya Biblia. Kwa hiyo, ingefaa utumie kwa njia yenye faida nafasi ulizo nazo za kuyazungumza Maandiko pamoja na Mashahidi wa Yehova, ikiwa hujafanya hivyo bado. Yesu alisema kwamba kutwaa maarifa sahihi ya kumjua Baba yake wa kimbingu na yeye mwenyewe ‘kunamaanisha uzima wa milele.’—Yohana 17:3, NW.
Ulimwengu wenye furaha uko hapa mbele tu. Lakini sasa hivi wewe unaweza kuwa na sababu nzuri za kufurahi. Si baraka zote kutoka kwa Mungu wala si sababu zote zenye kuleta furaha zitakazopatikana wakati ujao tu. Kwa sasa inawezekana kumtumikia Yehova kwa moyo wenye kujaa furaha, nasi tukimpendeza Mungu hakuna shaka kwamba tunaweza kushangilia wakati wa siku zetu zote.