Yesu Alizaliwa Desemba 25?
LABDA watu walio wengi wanaamini alizaliwa tarehe hiyo. Ushuhuda unaonyesha nini?
Kwa sababu gani usichunguze habari ya “Krismasi” (Christmas) katika kitabu cha ensaiklopedia? Inaelekea kuwa kitaonyesha chanzo cha Krismasi, na namna tarehe ya Desemba 25 ilivyochaguliwa kuwa ndiyo siku ya kuzaliwa kwa Yesu. Kila mwaka vichapo vingi vinakuwa na habari za kueleza jambo hilo. Maelezo yanayofuata ni ya kutoka katika magazeti yaliyochapishwa mwezi Desemba wa mwaka juzi tu.
Frontier, ambacho ni kichapo cha Shirika la Ndege la Frontier, kilisema hivi: “Kwa Wakristo wa kwanza, sikukuu za kuzaliwa zilikuwa desturi ya kipagani. Lilikuwa jambo lisilowazika kusherehekea siku ya kuzaliwa kwa mtu mwenyewe, achia mbali siku ya kuzaliwa kwa Kristo. Lilionekana kuwa jambo la kumchukiza Mungu hata kutoa wazo la kwamba Mtu wa Kimungu fulani alikuwa amekuwa na siku ya kuzaliwa.
“Katika miaka 300 iliyofuata maoni hayo yalianza kubadilika, na katika mwaka wa 354 A.D., Askofu wa Roma alitangaza Desemba 25 kuwa siku ya kukumbuka kuzaliwa kwa Kristo.”
These Times, ambacho ni kichapo cha Waadventisti, kilisema hivi: “Kwa muda fulani kabla ya kuja kwa Ukristo, Desemba 25 ilikuwa imekuwa ni wakati wa sherehe ya kipagani . . . Mfalme Aurelian (A.D. 270-275) alifanya haraka ya kutumia kwa faida yake mwenyewe ile ibada ya wapagani ya kuabudu jua, halafu, katika mwaka A.D. 274, akatangaza rasmi tarehe ya Desemba 25 kuwa ndiyo siku ya kuzaliwa kwa Jua Lisiloshindika . . . Katika A.D. 354, miaka miwili baada ya mwisho wa utawala wa Mtakatifu Yulio, Liberio, askofu mpya Mroma, aliagiza watu wake wote washerehekee Desemba 25 kuwa siku iliyo sahihi ya kuzaliwa kwa Kristo.”
Ndiyo, Desemba 25 ilichaguliwa kuwa siku ya kuzaliwa kwa Yesu kutokana na sherehe za kipagani, kama vile kichapo U.S. Catholic kinavyoeleza: “Sherehe iliyopendwa zaidi na Waroma ilikuwa Saturnalia, ambayo ilianza Desemba 17 na kumalizika wakati wa ‘siku ya kuzaliwa kwa jua lisiloshindika’ (Natalis solis invicti) katika Desemba 25. Wakati fulani katika robo ya pili ya karne ya nne, maafisa wajanja wa kanisa la Roma wakaamua kwamba tarehe ya Desemba 25 ingekuwa siku nzuri kabisa ya kusherehekea siku ya kuzaliwa kwa ‘jua la uadilifu.’ Ndivyo Krismasi ikazaliwa.” Kichapo hicho kinaendelea kusema: “Haiwezekani kutenganisha Krismasi na vyanzo vyake vya kipagani.”
Wakati wanapojua mambo hayo ya uhakika juu ya Krismasi, watu wengine wamepatwa na matokeo gani? The World Book Encyclopedia kilisema hivi chini ya kichwa kinachosema “Krismasi”: “Wakati wa miaka ya 1600, kwa sababu ya maoni hayo, Krismasi ilipigwa marufuku katika Uingereza na katika sehemu za makoloni ya Uingereza katika Amerika.”
Basi, lisiwe jambo la kushangaza kwamba Wakristo wanaojua mambo hawasherehekei Krismasi leo.