“Kwa Nini Sisherehekei Krismasi”
WATU fulani husema kwamba watoto wa Mashahidi wa Yehova wamenyimwa kwa sababu hawaisherehekei Krismasi. Lakini fikiria ile insha “Kwa Nini Sisherehekei Krismasi” aliyoandika Shahidi fulani wa miaka 11 katika California, Marekani, ukiwa mgawo wa darasani:
“Kwa watu wengi, Krismasi humaanisha vitu vingi—zawadi, familia, zawadi, chakula, zawadi, kushiriki, zawadi, upendo, zawadi, Baba Krismasi, zawadi, n.k. Hata hivyo siku hizi ni nadra sana watu kufikiri Krismasi humaanisha nini ama kwa nini wao huisherehekea. Ikiwa wao hufanya, wao kwa kawaida hufikiria Krismasi kuwa siku aliyozaliwa Yesu Kristo, wakati wa familia na, kama kawaida, zawadi nyingi. Watu walio wengi huwahurumia Mashahidi wa Yehova kwa sababu wao hufikiri watoto wao wamenyimwa. Lakini, je, hakika tunakosa kitu chochote? Acheni tuchunguze kwa nini Mashahidi wa Yehova hawasherehekei sikukuu hii.
“Nikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, sisherehekei Krismasi kwa sababu nyingi. Jambo la kwanza, si siku aliyozaliwa Yesu. Biblia husema kwamba kulikuwa na wachungaji nje makondeni pamoja na kondoo zao. Katika Yerusalemu ni baridi sana katika kipupwe na kwa kawaida kuna theluji. Haielekei sana kwamba wachungaji wangekaa nje wakati wa miezi hii. . . . Hata hivyo, kuna mengi ya kufikiria.
“Si kwamba tu Krismasi haikuwa siku aliyozaliwa Yesu bali haikufuatwa kamwe na Wakristo wa karne ya kwanza. Mianzo yayo iko katika msherehekeo wa Kiroma wa kale Saturnalia, unaoanzia Des. 17 na kuishia Des. 25, kule ‘kuzaliwa kwa jua lisiloshindwa.’ Katika karne ya nne, ofisa fulani wa Kiroma aliamua kusherehekea siku aliyozaliwa Yesu Des. 25, labda ili kutakasa sikukuu yao ya kipagani.
“Haishangazi kwamba Krismasi ilipigwa marufuku kutoka kwa nchi tofauti nyingi. Leo watu fulani (kama vile Mashahidi wa Yehova) wamefuata kielelezo chao. . . .
“Nilikuwa nikisherehekea Krismasi—hadi nilipokuwa na umri wa miaka minne. . . . Kwa habari ya kunyimwa, hakika Mashahidi wa Yehova hawanyimwi. Tunapata zawadi kwa mwaka wote. Vitu pekee tunavyokosa ni sikukuu hizi za kipagani na misherehekeo yavyo ya kipagani.”
Ingawa yule mwalimu wa kike aliandika juu ya karatasi hiyo, “Sio watu wote hutazamia zawadi,” pia aliandika, “Vizuri sana,” na akampa mwanafunzi huyo “A.”