Heshimuni Ndoa ya Kimungu!
MAONI ya Yehova juu ya ndoa ya kibinadamu yametajwa waziwazi katika maandiko kadha, kama lile linalosema, “Alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe,” na, “Yeye [Yehova] amechukia talaka.” (Marko 10:9; Malaki 2:16, NW) Kwa upande mwingine, yule mpinzani mkuu, Shetani Ibilisi, anapinga kila jambo safi na la uadilifu. Katika hizi “siku za mwisho,” ambapo “watu wabaya . . . [wanaendelea], na kuzidi kuwa waovu,” Shetani anajaribu kutupa mashutumu juu ya mipango yote ya Yehova yenye upendo, kutia ndani ndoa aliyoianzisha. (2 Timotheo 3:1-5, 13; Ufunuo 12:9, 12) Kulingana na vile nyakati hizi zilivyo, inawapasa Mashahidi wa Yehova wakaze zaidi nia yao wauunge mkono mpango wa Mungu wa ndoa na kuiendeleza ndoa ikiwa katika hali safi kwa ushikamanifu.—Mwanzo 2:24; Mithali 27:11; Waebrania 13:4.
Matatizo Katika Ndoa
Ni jambo la uhakika kwamba kwa muda ambao wanadamu wataendelea kuwa si wakamilifu, matatizo yatatokea katika ndoa. (1 Wakorintho 7:28-34) Lakini, ikiwa wenzi wote wawili ni waamini, kuna msingi mzuri wa kifungo cha ndoa kuwa chenye nguvu kwa sababu Yehova anahesabiwa ndani. Ndoa ya Kikristo inakuwa “kamba ya nyuzi tatu [ambayo] haikatiki upesi.” (Mhubiri 4:12) Ikiwa kuna haji ya kutokupatana, au tatizo lo lote jingine, wenzi waliooana wa Kikristo wanaweza kulizungumza kwa kumpelekea Yehova sala, wakiwa na uhakika watapata msaada wake. Mara nyingi, utatuzi unaweza kupatikana kwa kurudia kuzungumza namna mambo yalivyotendeka, kwa msaada wa maandiko kama 1 Wakorintho 13:4-8, Waefeso 5:21-33 na Wakolosai 3:12-14, 18, 19. Hivyo, wakati shauri la Biblia la ‘kuoa katika Bwana’ limefuatwa, kunakuwa na msingi mzuri wa kutatulia matatizo kwa msaada wa Maandiko.—1 Wakorintho 7:39.
Ikiwa jambo linalohusika halikumalizwa faraghani kwa kiasi chenye kuridhisha, watu hao wawili waliooana wanaweza kuomba mashauri ya mzee fulani katika kundi la Kikristo. Kwa kupata maoni ya Yehova, bila shaka wataweza kuendeleza ndoa yao katika hali ya kutokuharibika kisha wasitawishe umoja na upendo pia ambao Mungu alikusudia hapo mwanzo uwe kati ya wenzi wa ndoa.—Mwanzo 2:24; Mithali 31:10-12, 28, 30; Mathayo 19:4-6.
Ukiwa na Mwenzi Asiyeamini
Huenda hali ikawa tofauti wakati mtu anapokuwa mwamini na mwenzi wake asiuitikie ujumbe wa Ufalme. Hata iwe hivyo, kunaweza kuwa na ndoa nzuri sana, ikiwa mume na mke wake wataonyeshana upendo. Na, kama vile mtume Petro alivyosema, ‘mwenendo safi wa mke pamoja na heshima nyingi’ huenda baadaye ukafanya mume asiyeamini awe mwamini. Vivyo hivyo, huenda mume ambaye amegeuka majuzi akawa mwamini akafanya mke wake aamini. (1 Petro 3:1-7, NW)| Ikiwa kuna matatizo makubwa zaidi, mwamini atahitajiwa ayashughulikie kwa busara na kwa uvumilivu wenye subira, sikuzote akionyesha ‘tunda la roho.’—Wagalatia 5:22, 23.
Katika visa fulani huenda mwenzi wa ndoa aliye Mkristo akatukanwa na kuvu-njiwa heshima kimwili, kufanyiwa matisho na kupigwa-pigwa. Lakini je! hiyo inamaanisha kwamba mwenzi huyo amwache mwenzake asiyeamini? Mtume Paulo anashauri hivi: “Mke asiachane na mumewe; lakini, ikiwa ameachana naye [ameondoka, NW], na akae asiolewe, au apatane na mumewe; tena mume asimwache mkewe.” Kama Paulo anavyoonyesha, kuhifadhi ndoa kutaleta faida kwa watoto wo wote wanaoweza kuwa nao. Pia, kunaweza kuleta faida za kimwili kwa mzazi anayeamini pamoja na watoto wake. Hata hivyo mwenzi anayeamini akitendwa mabaya yanayokuja kuwa yasiyovumilika, au uhai wake uwe katika hali ya hatari, anaweza kuchagua ‘kuondoka.’ Lakini hatua hiyo inapasa iwe na lengo la ‘kupatana’ tena na mwenzi wake baadaye. (1 Wakorintho 7:10-16) Lakini, ‘kuondoka’ kwenyewe si msingi unaopatana na Maandiko wa talaka wala wa kuoa au kuolewa na mtu mwingine; hata hivyo, talaka ya kisheria au mtengano wa kisheria huenda vikampa mwenzi. ulinzi wa kiasi fulani asiendelee kutendwa mabaya.
Talaka Inayopatana na Maandiko
Je! kuna hali zo zote ambapo Mkristo anaweza kuchukua hatua zaidi na kujipatia talaka ya kumpa uhuru wa kuoa au kuolewa na mtu mwingine? Kumbuka kwamba Yesu alishauri hivi, “Alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe.” Lakini yeye akaendelea kuonyesha kwamba kungeweza kuwa na msingi unaofaa wa kujipatia talaka, kwa maana alisema hivi: “Mtu ye yote atalikiye mke wake, isipokuwa kwa sababu ya uasherati, na kuoa mwingine afanya uzinzi.”—Mathayo 19:6, 9, NW; ona pia 5:32.
Je! maana yake ni kwamba Mkristo akichoshwa na mwenzi wake wa ndoa au akijisikia anapendana na mtu mwingine, anaweza kutumia hali fulani inayohusiana na uasherati kisha amchukue huyo anapendana naye na kumwacha yule mwingine? Inasikitisha kusema kwamba, katika visa fulani ambapo wenzi wote wawili wanadai kuwa wao ni waamini, njia hiyo ya kufanya uasherati (kwa kawaida uzinzi) imetumiwa kama chombo cha kutunga hila ya kuvunja kwa makusudi vifungo vya ndoa inayopatana na Maandiko. Je! watu wenye kufanya hivyo wanataka kuwa wapumbavu sana kiasi cha kufikiri kwamba Yehova hayajui “mawazo na makusudi ya moyo”? (Waebrania 4:12, 13) Inaelekea kuwa hao wamejichukulia maoni ya kwamba wanaweza kufanya uasherati kwa makusudi, watengwe na ushirika muda wa mwaka mmoja hivi, kisha “wa-tubu” na kurudishwa katika kundi wakiwa na mwenzi tofauti wa ndoa.
Lakini, ikitukia hivyo, muda mwingi unapasa kupita kabla wazee hawajaweza hata kufikiria ombi lo lote la kurudishwa. Wazee wenye kudhamiria mambo hawatafanya haraka-haraka. Wanahitaji kuona ushuhuda ulio wazi sana wa matunda yanayoistahili toba. Hata mtenda dhambi huyo akija kurudishwa baadaye, miaka mingi inapasa ipite kabla wazee hawajaweza kumpendekeza apate mapendeleo ya pekee kundini, kama kweli kuna siku itakayofika wampendekeze. Na kwa vyo vyote hawatampendekeza kabla mwenzi yule asiye na hatia waliyemwacha hajaoa au hajaolewa tena au kama hajafa. (1 Timotheo 3:2, 12) Tunaweza kuthamini namna Yehova Mungu anavyouona kwa uzito uzinzi wa namna hiyo uliotangulia kufanyiwa mipango tukikumbuka kwamba chini ya Torati yake yenye uadilifu iliyokuwa katika Israeli wa kale, wazinzi wangaliuawa kwa kupigwa kwa mawe. (Kumbukumbu la Torati 22:22) Na leo, hata uwe ni uamuzi gani utakaofanywa na makundi, Mwamuzi wa mwisho atakuwa ni Yehova. “Waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.”—Waebrania 13:4.a
Kuihifadhi Ndoa
Ili kuwalinda watu wa Mungu, na kwa kutumaini kwamba watu wo wote walio na matatizo ya kufuata maadili (tabia njema) watalitegemea kundi la Kikristo wapate mwongozo katika kuuheshimu mpango wa ndoa ulioanzishwa na Yehova, pande fulani za tendo la uasherati zitazungumzwa hapa kwa kuzitoboa waziwazi kabisa. Hatua hiyo inachukuliwa kupatana na Maandiko, ambayo yanasema mambo waziwazi na kinagaubaga hata wakati yanapozungumza mambo yanayoonewa haya na ya usiri.—Linganisha Mambo ya Walawi 20:10-23; Kumbukumbu la Torati 31:12; Mathayo 5:27, 28; Warumi 1:26, 27; Yuda 7.
Badala ya kutafuta kisababu cha kupata talaka, inawapasa waliooana wawe wakitafuta njia za kufungamanisha ndoa. Ikiwa mwenzi anafanya ufisadi na anaonyesha toba, mwenzi asiye na hatia anaweza kuchagua kumsamehe, akiwa na shabaha ya kuuendeleza mpango wa ndoa uliofanywa na Mungu. Hivyo rehema inaweza kuonyeshwa, kwa kuiga Yehova katika sifa hiyo ambayo ni moja ya sifa zake zinazozidi nyinginezo kwa ubora.—Kutoka 34:6; linganisha Nehemia 9:17.
Lakini, namna gani ikiwa mwenzi wa ndoa hatubu, anatengwa na ushirika na hata anaendelea kufuata mwendo uliothibitishwa kuwa wa ufisadi mbaya sana? Au namna gani ikiwa afya ya kibinafsi na hali ya kiroho ya mwenzi asiye na hatia inatiwa katika hali ya hatari? Ingawa lile onyo la upole la Maandiko linalosema ndoa ihifadhiwe inapowezekana halipasi kupuzwa, maneno ya Yesu yaliyotangulia kutajwa katika Mathayo 19:9 yanaonyesha kwamba kuna msingi wa talaka—msingi ulio wa pekee wa talaka inayopatana na Maandiko—uasherati.
Kueleza Maana ya “Uasherati”
Hapo tunaelewa nini kutokana na neno “uasherati”? Neno la Kigiriki lililo katika andiko hilo ni porneia. Katika kuzungumza jambo hilo, Mnara wa Mlinzi wa Februari 15, 1975, kurasa 94-96, ulionyesha kwamba neno porneia “linatoka kwa neno la asili linalomaanisha ‘kuuza.’ “Hivyo linakamatanishwa na umalaya, kama ule uliozoewa katika mahekalu mengi ya kipagani katika karne ya kwanza na ule unaofanyika katika nyumba za makahaba leo.
Ni kweli kwamba neno porneia linatumiwa nyakati nyingine katika maana isiyotia ndani mambo mengi, kutumiwa kuhusu ngono kati ya watu wasiooa au wasioolewa (waseja). Mfano wa matumizi hayo ya ufupi ni 1 Wakorintho 6:9, ambapo “waasherati” wanatajwa kwa kutenganishwa na wale wanaojitia katika maovu mengine ya kutumia viungo vya uzazi kama uzinzi na kulalana kwa wanaume na wanaume (ulawiti). Lakini muda mfupi tu kabla ya kutaja hivyo, kwenye 1 Wakorintho 5:9-11 Paulo alitumia neno hilo hilo alipokuwa akishauri Wakristo wasichangamane na “waasherati.” Je! ni jambo la akili kufikiri kwamba hapo alimaanisha wafisadi wasiooa au wasioolewa peke yao? Haiwezi kuwa hivyo, kwa maana sura ya 6 inaonyesha namna nyingi za mazoea yasiyofaa ya kutumia viungo vya uzazi ambayo ni lazima yaepukwe, kutia ndani uzinzi na kulalana kwa watu wa maumbile mamoja ya mwili. Vivyo hivyo, haiwezi kuwa kwamba maandiko ya Yuda 7 na Ufunuo 21:8, yanayoonyesha Mungu anahukumu “waasherati” wasio-tubu kuwa wanastahili uharibifu wa milele, yanahusu wasiooa au wasioolewa peke yao ambao wanafanya ngono. Na ni lazima amri ya baraza lenye kuongoza la huko Yerusalemu iliyotolewa kwenye Matendo 15:29, ya ‘kujiepusha na uasherati,’ ieleweke kuwa na ile maana pana inayotia ndani mambo mengi.b
Basi, ni wazi kwamba katika maana iliyo pana, neno “uasherati” kama lilivyo tumiwa kwenye Mathayo 5:32 na 19:9 linamaanisha namna nyingi za ngono haramu au zisizo halali zinazofanywa nje ya ndoa. Neno porneia linatia ndani matumizi ya ufisadi mzito wa Kiungo (Viungo) cha angaa mwanadamu mmoja (yawe ni matumizi ya kiungo hicho kwa njia ya asili au kwa njia iliyopotoshwa); pia, ili lihesabiwe hivyo ni lazima kuwe kulikuwa na mwingine mwenye kuhusika katika ufisadi huo—mwanadamu, awe ni mwanamume au mwanamke, au mnyama.c Hivyo, kupiga punyeto (kusugua kwa mtu kiungo cha uzazi chake mwenyewe ili kutosheleza nyege, ambalo ni tendo la upumbavu na la hatari sana kiroho) si kufanya porneia. Lakini mpaka leo hii, neno porneia linatia ndani namna mbali-mbali za utendaji unaohusu viungo vya uzazi unaoweza kufanywa katika nyumba ya umalaya, ambako watu wananunua ngono na kuziuza. Mtu anayeendea kahaba wa kiume au wa kike akanunue ngono ya namna yo yote ya kutumia kiungo cha uzazi angekuwa na hatia ya kufanya porneia.—Linganisha 1 Wakorintho 6:18.
Wakristo Waliooana
Namna gani utendaji wa kutumia kiungo cha uzazi kati ya watu waliooana ndani ya kifungo cha ndoa? Si kazi ya wazee kuchungulia-chungulia maisha ya usiri ya Wakristo waliooana. Lakini, bila shaka Biblia inahusika kwa haki katika maisha yao. Wale wanaotaka kuendelea ‘kuenenda kwa roho’ hawapaswi kuvipuza viishara vya Kimaandiko vinavyoonyesha vile Mungu anavyofikiria mambo. Nao watapaswa kusitawisha chuki ya kila jambo lililo chafu mbele za Yehova, hiyo ikiwa ni kutia ndani mazoea ya kutumia kiungo cha uzazi ambayo kwa wazi yanafanywa kwa njia iliyopotoka. Watu waliooana wanapaswa kutenda kwa njia itakayowaacha wakiwa na dhamiri safi, huku wakifanya haraka kuelekeza fikira zao juu ya usitawishaji wa ‘tunda la roho.’—Wagalatia 5:16, 22, 23; Waefeso 5:3-5.
Lakini namna gani ikiwa mwenzi mmoja anataka au hata anadai ashiriki na mwenzi wake wa kiume au wa kike katika zoea ambalo ni wazi limepotoshwa la kutumia kiungo cha uzazi? Mambo ya uhakika ambayo yametangulia kutolewa ya-naonyesha kwamba porneia inatia ndani mwenendo haramu wa kutumia kiungo cha uzazi nje ya mpango wa ndoa. Hivyo, mwenzi wa ndoa akilazimisha mwenzake wafanye matendo yaliyopotoshwa, kama vile kuingiza uume ndani ya mdomo au mkundu wa mke, huo usingekuwa ni msingi unaopatana na Maandiko wa talaka ambayo ingeweka huru mwenzi ye yote wa hao wawili kuoa au kuolewa na mtu mwingine ikiwa tendo lenyewe limefanywa ndani ya ndoa.d Ingawa mwenzi anayeamini anafadhaika sana moyoni kwa sababu ya hali hiyo, jitihada yake ya kufuata kanuni za Kimaandiko itamletea baraka kutoka kwa Yehova. Katika visa vya namna hiyo linaweza kuwa jambo lenye msaada watu hao wawili wakilizungumza shauri lenyewe waziwazi, hasa wakikumbuka kwamba ngono zinapasa kuwa zenye kuheshimika, zenye kupendeza, ziwe wonyesho wa upendo mwororo. Hakika wonyesho huo hautatia ndani jambo lo lote linaloweza kumtia dhiki au umizo mwenzi yule mwingine katika moyo wake.—Waefeso 5:28-30; 1 Petro 3:1, 7.
Kama ilivyokwisha kutajwa, si kazi ya wazee “kufanya upolisi” wa kupeleleza mambo ya faraghani ya ndoa za watu waliooana kundini. Lakini, ikipata kujulikana kwamba mshiriki wa kundi anafanya zoea la ngono iliyopotoshwa ndani ya kifungo cha ndoa au anaambia wengine waziwazi kwamba ngono ya namna hiyo inaweza kufanywa, hakika mtu huyo asingeweza kukosa kulaumika, na kwa hiyo asingekubalika katika kupata mapendeleo ya pekee, kama vile kutumikia akiwa mzee, mtumishi wa huduma au painia. Zoea hilo na kuambia wengine kwamba tendo hilo linaweza kufanywa vingeweza hata kumfanya aondoshwe katika kundi. Kwa sababu gani?
Andiko la Wagalatia 5:19-21 (NW) linataja maovu mengi yasiyotiwa katika fungu moja la kuwa porneia, ambayo yangeweza kufanya mtu ahesabiwe hastahili kuuingia Ufalme wa Mungu. Kati ya maovu hayo kuna “uchafu” (Kigiriki, akatharsia, linalomaanisha unajisi, mwenendo mchafu, upujufu) na “mwenendo mpotovu” (Kigiriki, aselgeia, linalomaanisha utovu wa heshima, mwenendo usio na aibu). Kama vile porneia, maovu hayo yakiwa mazito yanaweza kuwa sababu za kutenga mtu na ushirika wa kundi la Kikristo, lakini hizo si sababu za kupata talaka inayopatana na Maandiko. Mtu asiyeona aibu hata kidogo anapowaambia wengine kwamba matendo mabaya na yenye kuchukiza sana ya kutumia kiungo cha uzazi ni sawa tu angekuwa na hatia ya mwenendo mpotovu. Bila shaka, mtu mwenye nia hiyo huenda hata akaharibika zaidi na kujikuta akifanya porneia; halafu hapo sasa kungekuwa na msingi wa kupata talaka inayopatana na Maandiko.e Inawapasa Wakristo wote waliojitoa sana waepuka na hata wapigane na “kazi za mwili” hizo zote’.—Wagalatia 5:24, 25.
Watu wa Yehova wote, wawe wameoana au ni waseja, wanapaswa kuepuka kila namna ya ufisadi. Inawapasa waunge mkono mipango yote ya Yehova kwa ushikamanifu, kutia ndani hata ule mpango wa ndoa aliouanzisha. (Zaburi 18:21-25) Kwa kuwa ni “mwili mmoja,” wale walio oana wanapaswa wajitahidi kumtukuza Yehova, kusitawisha upendo wa kweli na heshima ya kweli katika ndoa yao. (Mwanzo 2:23, 24; Waefeso 5:33; Wakolosai 3:18, 19) Kwa njia hiyo, kama vile katika njia zile nyingine, wanaweza kuonyesha kwamba wao “si sehemu ya ulimwengu”—ulimwengu ambao umekokotwa na Shetani ukatumbukizwa ndani ya utope-utope wa uasherati na ufisadi ambao karibuni ‘utapita pamoja na tamaa yake.’ Kwa kukumbuka kwamba “yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele,” watu wote wanapaswa wajitahidi kufanya “mapenzi” ya Mungu kuhusiana na mpango Wake wa ndoa wenye thamani kubwa.—Yohana 17:16; 1 Yohana 2:17, NW.
[Maelezo ya Chini]
a Ona w11/15/79, kurasa 31 na 32; pia, Mnara wa Mlinzi wa Desemba 15, 1983, ukurasa wa 23.
b Inastahili kuangaliwa kwamba kamusi Webster’s New Collegiate Dictionary inatanguliza maelezo yafuatayo kuwa ndiyo maana ya neno “uasherati”: “Ngono ya kibinadamu iliyo tofauti na ile inayofanywa kati ya mwanamume na mke wake.” Na katika kueleza maana ya “ngono” (kati ya mwanamume na mwana mke, ya kutumia mkundu, ya kutumia mdomo), kamusi hiyo inataja kwamba tendo linakuwa ngono linapohusu “kiungo cha uzazi cha angaa mtu mmoja.” Kwa hiyo neno la Kiingereza “fornication” (uasherati) ni tafsiri inayofaa ya neno la Kigiriki porneia.
Kwa mfano, The New International Dictionary of New Testament Theology inasema kwamba porneia ni neno lenye maana ya “unajisi, ukahaba, umalaya uasherati.” Inasema hivi pia: “Fungu la maneno yenye maana zinazokaribiana [linalohusu porneia] linaweza kumaanisha namna mbalimbali za ngono zinazofanywa nje ya ndoa kwa kuwa hazifuati kawaida zinazokubaliwa kijamii na kidini (kwa mfano, kulalana kwa watu wa jinsi moja, kufanya ngono na mtu ye yote tu bila kujali, kuwatumia watoto isivyopasa kwa kufanya ngono nao, na hasa umalaya).” Hivyo, neno porneia lingetia ndani uzinzi (Kigiriki, moikheia), na linaweza kuhusu namna nyingi zaidi za mazoea ya ufisadi yanayofanywa nje ya ndoa, kama vile kufanya ngono ya kuingiza uume ndani ya mdomo au mkundu wa mwingine na kulalana na mnyama.
Chapa ya mwaka wa 1979 ya ile kamusi inayoheshimiwa sana inayoitwa Greek-English Lexicon of the New Testament and Other Early Christian Literature (iliyotayarishwa na Bauer, Arndt na Gingrich) inaeleza maana ya porneia kuwa “umalaya, unajisi, uasherati wa kila namna ya ngono zilizo haramu.”
c Mwanamume au mwanamke anayelalwa kwa nguvu asingekuwa na hatia ya kufanya porneia.
d Haya ni maelezo ya kirefu na rekebisho katika ufahamu wa habari zinazoonekana katika Mnara wa Mlinzi wa Machi 1, 1975, kurasa 117, 118, na Novemba 1, 1978, kurasa 22-24. Wale waliochukua hatua kwa kutegemea maarifa waliyokuwa nayo wakati huo hawapaswi kulaumiwa-laumiwa. Wala hiyo isingebadili msimamo wa mtu ambaye hapo zamani aliamini kwamba mwenzi wake wa ndoa alifanya porneia kwa kuingilia ngono zilizopotoshwa ndani ya ndoa, na kwa sababu hiyo akampa talaka na sasa ameolewa na mtu mwingine.
e W9/15/73, kurasa 574-576.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Ni lazima ndoa iwekwe katika hali ya kuheshimika na itenganishwe na ufisadi wa kilimwengu