Njaa Ina Maana Gani?
INGAWA ni kweli kwamba ukulima umefanya maendeleo mengi miaka ya majuzi, ni kweli pia kwamba tangu mwaka wa 1914 wanadamu wameshuhudia upungufu wa chakula mara nyingi sana. Acha tuchunguze mara fulani-fulani tuone kama zinaweza kuwa zinatimiza unabii wa Yesu na njozi ya mtume Yohana juu ya habari hii. Ikielekea kuwa zinalingana na yanayotukia, basi tutazidi kuchunguza tuone kama kuna jambo lo lote juu ya upungufu wa chakula wa karne ya 20 linalouonyesha kuwa tofauti na ule uliowapata watu zamani katika historia ya ulimwengu.
Njaa Katikati ya Wingi wa Vitu
Huenda wengine wakawa na maoni ya kwamba kwa sababu kuna utajiri mwingi sana leo, si jambo linalopatana na akili nzuri kusema kwamba huu ndio wakati ambao yule farasi mweusi wa njaa anapita katika sehemu kubwa ya dunia. Lakini Biblia haisemi kwamba kila mtu angekuwa akifa njaa wakati huo. Kwa kweli, ile sauti katika njozi iliyotangaza bei ya juu sana kwa vyakula vinavyotumiwa zaidi katika matumizi ya kawaidaa ilisema hivi pia: “Usiyadhuru mafuta [ya mzeituni] wala divai.” (Ufunuo 6:6) Mafuta ya mzeituni na divai ni vitu vilivyotumiwa kwa anasa tu, bila kuwa mahitaji ya lazima. Kwa hiyo, Ufunuo unaonyesha kwamba watu wengine wangekuwa wakifurahia maisha ya anasa huku wengine wakiumizwa na njaa.
Ingawa Yesu pia alitabiri upungufu wa chakula, yeye alionya hivi: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo.” (Luka 21:34, 35) Ingawa wengine wangekuwa wakiumizwa na upungufu wa chakula, wengine wangekuwa katika hatari ya kula kupita kiasi. Je! hiyo ndiyo hali iliyopo leo?
Ndiyo. Kwa kweli, ripoti mbalimbali zinatuambia kwamba kuinua viwango vya maisha ya watu wengine kunafanya wengine wawe na njaa kwa kukosa chakula. “Maendeleo katika viwango vya maisha na ongezeko la wenye kudai chakula katika sehemu zote za ulimwengu yameleta mkazo katika bei za chakula [yakafanya bei ya chakula iwe ghali zaidi] na kufanya nchi zilizo maskini zaidi ziagize nchi nyingine za nje ziwaletee vyakula vinavyohitajiwa.” (Gazeti The New York Times, Agosti 16, 1981) Ndiyo kusema, “ulafi” wa wengine unafanya “upungufu wa chakula” wa wengine uzidi kuwa mwingi.
“Mahali Hapa na Mahali Hapa”
Yesu alionya kwamba kungekuwa na “upungufu wa chakula . . . mahali hapa na mahali hapa.” (Mathayo 24:7, NW) Je! jambo hilo limetukia tangu mwaka wa 1914? Ndiyo. Hii ni mifano michache: Mwaka wa 1921, njaa iliua watu karibu milioni 5 katika Urusi. Mwaka wa 1929, njaa ilisababisha vifo vinavyokadiriwa kuwa milioni 3 katika China. Miaka ya 1930, watu milioni 5 waliuawa na njaa katika Urusi. Miaka michache tu iliyopita ukame wa muda mrefu katika nchi zilizo kando-kando ya Jangwa la Sahara ulifanya hesabu kubwa sana ya watu wakimbilie nchi nyingine na uliua watu 100,000.
Ingawa hivyo, kumbuka kwamba katika njozi ya mtume Yohana yule farasi mweusi wa njaa alimfuata farasi mwekundu wa vita. Kulingana na hilo, mwingi wa upungufu wa chakula ambao umekuwako siku zetu umeletwa moja kwa moja na vita. (Ufunuo 6:3, 4) Kwa mfano, vita iliyofanywa kati ya raia za Spania iliiletea njaa nchi hiyo katika miaka ya 1930. Vita ya Ulimwengu ya Pili ilileta maafa ya njaa katika Ugiriki, Polandi, Urusi, Holandi na mahali pengine pengine. Watu zaidi ya 1,500,000 waliuawa huko Bengali, India, wakati wa miaka 1943-44 na njaa iliyosababishwa kwa kiasi fulani na vita iyo hiyo.
Siku za majuzi zaidi, katika miaka ya 1960, watu waliuawa na njaa katika Kongo (ambayo sasa ni Zaire) na Nigeria kwa sababu ya vita ya kiraia. Katika magazeti tuliwaona watoto wa Kampuchea wenye kufa njaa katika nchi hiyo wakitukodolea macho. Hivi majuzi, tulisoma kwamba wakimbizi zaidi ya miloni moja wanaelekea kuuawa na njaa katika Somalia, ambako wamekimbilia waepuke ukame na mapigano katika Ethiopia. Vyanzo vya uenezaji wa habari vinadai kwamba wakimbizi zaidi ya milioni 9 wanakaribia kufa njaa huko Thailand, Sudan, Zaire, Nicaragua, Honduras na Pakistan. Hivyo ndivyo maelezo yenye kusikitisha yanavyozidi kutolewa.
Kulingana na historia, njaa zimesababishwa na vita, ukame, kuharibiwa kwa mazao na wadudu au na maangamizi ya namna nyingine. Je! sisi tumeona upungufu wa chakula unaozidi ule wa vizazi vilivyotangulia? Hatuwezi kusema kwa uhakika kwa sababu hesabu zilizoandikwa si kamili. Lakini karne hii imepatwa na maafa ya asili na ikaumizwa zaidi na vita kuliko kizazi kinginecho chote katika historia.b Kwa hiyo, huenda ikawa kwamba kwa ujumla kumekuwa na upungufu wa chakula unaozidi ule wa wakati wo wote uliotangulia. Kwa uhakika, tumeona njaa ingawa kuna wingi wa vitu, njaa yenye kusababishwa na vita na upungufu wa chakula “mahali hapa na mahali hapa,” sawa na ilivyotabiriwa.
Hata kuna namna mpya ya upungufu wa chakula unaoendelea kuongezeka kuonyesha kwamba wakati wetu ni tofauti.
“Haina Kifani Katika Historia ya Kibinadamu”
Katika utangulizi wake wa kitabu The Dimensions of World Food Problems (Kiasi cha Mweneo wa Matatizo ya Chakula Ulimwenguni), mhariri wa kitabu hicho, E. R. Duncan, anaeleza kwamba kufikia hivi majuzi vyakula vilikuwa vimeongezeka kwa ujumla kadiri hesabu ya watu ilivyoendelea kuongezeka. Ni kweli kwamba maafa yalileta njaa huku na huku. Lakini watu walipata nafuu tena. Lakini kuanzia miaka ya 1940 jambo jipya liliingia: ongezeko lenye kupanda haraka sana la hesabu ya watu wa ulimwengu linalotatiza sana uwezo wa ulimwengu wa kuweza kujilisha kwa kipindi kirefu. “Hali hiyo,” mhariri anasema, “haina kifani katika historia ya kibinadamu.”
India ni mfano wa jambo hilo. India imepatwa na njaa kali-kali muda wote wa historia ya nchi hiyo, lakini leo mambo ni tofauti. “Ni kufikia karne hii iliyopita tu, na sana-sana kufikia karne hii ya ishirini, kwamba hali zimekuwa zisizoweza kuvumiliwa [katika India]. Uhakika huo unaonyesha wazi kabisa kwamba kusema njaa imekuwako muda wote wa historia ni maneno yaliyotiwa chumvi.” Ndivyo anavyosema Georg Borgstrom, mkuu aliye mashuhuri katika uchunguzi wa kimataifa wa ulishaji wa watu wa ulimwengu.
Yeye anaendelea kueleza hivi: “Wakati Uingereza ilipokuja kwanza kwenye nchi hii iliyo nusu-bara, karibu miaka mia mbili iliyopita, walikuwako watu karibu milioni sitini waliokuwa wakiishi katika eneo ambalo leo linaitwa India. Kati ya watu hao, karibu milioni kumi walikuwa katika kiwango cha kufa njaa. Tangu wakati huo, idadi ya watu wa huko imeongezeka mara saba na sasa hali imebadilika, ikiwa kinyume cha ile ya kwanza, kwa maana hesabu ya wale wanaopata chakula cha kuwatosha ni kama milioni kumi.”—Kitabu The Hungry Planet, kilichotayarishwa na Georg Borgstrom.
Hali inayofanana na hiyo inaendelea kuongezeka katika nchi nyingine. Ni kweli kwamba katika ulimwengu kwa ujumla kungali kuna chakula cha kutosha kinachokuzwa kulisha kila mtu, kulingana na vile mambo yanavyopasa kuwa. Lakini idadi ya watu ikiendelea kuongezeka, baada ya muda mfupi haitakuwa hivyo tena. Hata sasa, nchi nyingi zilizo maskini zilizokuwa zikikuza chakula cha kutimiza mahitaji yao hazifanyi hivyo tena, na kwa sababu ni maskini hazina uwezo wa kununua chakula cha kutosha ili zilishe watu wao. Nyakati nyingine, hata katika nchi iliyo na chakula cha kuitosha kwa ujumla, sehemu kubwa ya watu wa nchi hiyo ni maskini sana hata wasiweze kukinunua chakula chenyewe. Kwa hiyo wanaumizwa na upungufu wa chakula.
Gazeti Los Angeles Times liliripoti hivi mwaka jana: “Upungufu wa chakula katika Afrika umekuwa mbaya zaidi katika miezi sita iliyopita na nchi 28 zinaumizwa na njaa.”
Kichapo Vancouver Sun kilisema hivi: “Leo, mwishoni mwa mwaka ‘wa kikawaida,’ shirika la FAO [Tengenezo la Chakula na Ukulima Ulimwenguni] lilikadiria kwamba kuna watu milioni 450 walio na njaa kiasi cha kufa, na kuna watu kufikia bilioni moja wasio na chakula cha kuwatosha.”
Ripoti iliyotoka kwenye Hazina ya Watoto ya Umoja wa Mataifa inakadiria kwamba milioni 17 kati ya watoto wa ulimwengu waliuawa na njaa na magonjwa mwaka wa 1981. Hesabu hiyo inavizidi vifo vilivyokadiriwa kuwa vilitokea wakati wa ile njaa mbaya sana ya huko China miaka ya 1878-79.
Je! kuna utatuzi wo wote? Gazeti The New York Times linaripoti hivi: “Hesabu zilizofanywa na Banki ya Ulimwengu zinaonyesha kwamba kuwekwa kwa dola bilioni 600 katika nchi zinazoendelea ili pesa hizo zilete faida . . . kutahitajiwa muda wa miaka 10 inayokuja kwa kusudi la uzuiaji tu wa kupungua kwa vyakula ili njaa isizidi namna ilivyo. Hakuna mtu anayejua hasa pesa hizo nyingi zitatoka wapi.” Kwa hiyo, utatuzi wa kweli hauonekani.
Habari Njema
Mweneo mkubwa sana wa tatizo la njaa lililopo leo na uhakika wa kwamba tatizo hilo litaongezeka unaufanya uwe usiopata kuwa na kifani. Kuna jambo jingine lisilo la kawaida kuhusiana na mweneo wa tatizo hilo. Linafuatana na magumu mengine ambayo yanaelekea kutotatulika.
Katika njozi ya mtume Yohana, yule farasi mweusi wa njaa alifuatana na farasi mwekundu wa vita na farasi wa kijivujivu wa magonjwa. Halafu Yesu, alipotabiri kwamba upungufu wa chakula ungetokea “mahali hapa na mahali hapa,” alisema upungufu wenyewe ungetokea pamoja na matetemeko makubwa ya ardhi, magonjwa ya kipuku, vita na mambo mengine mengi yenye kutaabisha watu. (Mathayo 24:7-14; Luka 21:10-28) Uhakika wa kwamba mambo hayo yote yanatukia leo unauonyesha huu kuwa ndio wakati unaostahili kuangaliwa ambao Yesu na mtume Yohana walikuwa wakiutabiri.
Uendeshaji wa wale wapandaji wanne wa kitabu cha Ufunuo ungekuwa kionyesho cha kwamba Yesu aliyevikwa taji ya kifalme majuzi alikuwa anaenda “akishinda na kumaliza ushindi wake.” (Ufunuo 6:1-8, NW) Maelezo marefu ya matukio ya ulimwengu ambayo Yesu alitoa yalikuwa ya kulijibu ulizo hili la wafuasi wake: “Mambo hayo yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”—Mathayo 24:3, NW.
Sisi tunaishi katika siku za maana. Sasa Yesu anatawala akiwa Mfalme asiyeonekana. Karibuni yeye ‘atamaliza ushindi wake’ kwa kuwaondoa waovu na kummaliza nguvu yule msababishi mkuu wa uovu, Shetani Ibilisi. (Zaburi 37:9-11; Ufunuo 20:1-3) Hiyo ndiyo sababu Yesu aliendelea kusema hivi: “Mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.”—Luka 21:31.
Hizo ndizo habari njema za mambo yatakayofanyika baada ya maafa tunayoyasoma katika magazeti. Karibuni kukimbia kwa yule farasi mweusi wa njaa kutakoma na Ufalme wa Mungu ulete duniani serikali yenye uadilifu. (Zaburi 72:1, 16) Hilo litakuwa ndilo badiliko lenye kuleta faida kubwa zaidi katika historia yote ya wanadamu. Unaombwa wewe mwenyewe ujifunze habari hizo katika Biblia yako mwenyewe. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukupa msaada wo wote unaohitaji. Kwa njia hiyo wewe utaweza kuifahamu maana halisi ya mwendo wenye maafa wa yule farasi mweusi wa njaa.
[Maelezo ya Chini]
a “Kibaba kimoja cha unga wa ngano kwa kiasi cha fedha dinari moja, na vibaba vitatu vya shayiri kwa dinari moja” (Ufunuo 6:6, HNWW) Dinari ilikuwa mshahara wa siku moja katika wakati wa Yohana.—Mathayo 20:2.
b Ona makala inayosema “Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na Mwanzo wa Huzuni Mbalimbali,” katika gazeti Mnara wa Mlinzi, toleo la Februari 1, 1984.