Wenye Imani Walio Hai Ambao Hawatakufa Kamwe
1, 2. Mamilioni ya wenye kumpenda Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova Mungu, hawana tamaa ya kwenda wapi wakafurahie uzima wa milele, na ni maneno gani ya Yesu Kristo juu ya kuishi bila kufa wanayoyakumbuka?
KUNA maelfu ya mamilioni ya watu wanaoishi duniani leo. Mamilioni kati yao wanajifunza sasa juu ya nafasi nzuri sana waliyo nayo ya kuendelea kuishi duniani bila ya kufa kamwe. Huenda wengi wao wakakumbuka ule wimbo wa zamani wa kidini, ‘Lazima uwe mpenda Bwana, au hutakwenda mbinguni ukifa.’ Lakini kuna mamilioni ya watu wapendao Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova Mungu, ambao wako hai na hawataki hata kidogo kwenda mbinguni. Tumaini walilopewa na Mungu ni kurudishwa kwa Paradiso kwenye dunia hii na kupanuliwa kwayo ienee dunia yote. Wao wanataka kuishi hapo muda wote, wakiwa katika ukamilifu wa kibinadamu, chini ya serikali ya kimbingu yenye uadilifu. (Luka 23:43, NW) Wanayakumbuka yale maneno mazuri ajabu ambayo Yesu Kristo alimwambia Martha, ambaye Yesu alikaribia kufufua Lazaro ndugu yake atoke kwa wafu. Hayo ndiyo maneno yanayostahili kufikiriwa kwa uzito na kila mtu anayeishi leo. Ndiyo haya:
2 “Naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele.”—Yohana 11:26.
3. Ni hotuba gani kuhusu uhai wa kibinadamu usiokatizwa iliyotolewa Februari 24, 1918, na ni matukio gani zaidi ya mwaka huo yaliyokatiza hotuba hiyo isiendelee kutolewa?
3 Wanaume na wanawake wa karne hii ya 20 waliamshwa wakaliona tumaini hilo lililo zuri ajabu siku ya Jumapili, Februari 24, 1918, katika Los Angeles, California, U.S.A. Huko kwa mara ya kwanza msimamizi wa wakati huo wa Sosaiti aliitoa hotuba ya watu yote iliyosema “Ulimwengu Umekwisha . . . Mamilioni Wanaoishi Sasa Huenda Wasife Kamwe.”a Hotuba hiyo ilitolewa wakati ule ule ambao Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, ambayo ilikuwa imehusisha ndani United States ya Amerika, ilikuwa ikikaribia upeo wake. Hotuba hiyo ya Biblia iliyoanzisha kipindi kipya ilipotaka kuendelea kutolewa ilikatizwa, hasa wakati mfupi baadaye, Mei 8, 1918, wakati msimamizi wa Sosaiti na watu saba walio washirika naye walipokamatwa huko Brooklyn, New York, kwenye makao makuu. Mapema, tarehe ya Februari 12, 1918, serikali ya Kanada ilikuwa imekipiga marufuku kitabu cha Sosaiti kilichokuwa kimetokea karibuni chenye kuitwa The Finished Mystery, na pia trakti za kutolewa bure za Sosaiti zenye kuitwa Bible Students Monthly. Siku ya Machi 14 serikali ya United States nayo ilikipiga marufuku kitabu The Finished Mystery na toleo lenye kuhusiana nacho la Bible Students Monthly. Vichapo hivyo vilikuwa na jina la msimamizi wa Sosaiti. Halafu Juni 21, baada ya majuma mengi ya kufanya kesi mahakamani, mahakama ya serikali ya United States iliwahukumu kifungo cha miaka mingi katika Gereza Kuu la Atlanta, Georgia, msimamizi wa Sosaiti, katibu-mweka-hazina, wale waandikaji wenye kushirikiana wa kitabu The Finished Mystery, washiriki wengine watatu wa wafanya kazi wa makao makuu ya Brooklyn na mtafsiri wa Sosaiti wa Kiitalia. Siku ya Julai 4, 1918, wote wanane walihamishwa Brooklyn, New York, wakapelekwa kwenye Gereza Kuu la Atlanta, Georgia, na huku Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ikiendelea kuwaka moto.
4. Kwa uneni wa kiroho, mabaki ya watu wa Yehova duniani walipataje kuwa kama wafu, na ni jambo gani lililotukia juu ya tumaini lao la kimbingu?
4 Kabla ya majira ya baridi yaliyofuata, Sosaiti iliona ni lazima ihame Brooklyn, New York, irudi Pittsburgh, Pennsylvania, kulingana na Tangazo la Kuondolewa lililopigwa chapa katika toleo la Oktoba 1, 1918 la gazeti Watch Tower, ukurasa wa 290. Katika sehemu zote za dunia washiriki vijana wa makundi ya Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote walitiwa kizuizini katika kambi za kijeshi, au hata katika magereza. Kwa usemi wa kiroho, watu wa Yehova waliojiweka wakf na kubatizwa walikuwa kama wamekufa, sana-sana kwa habari ya kuihubiri Gospeli, au habari njema. Walijisikia kama kwamba walikuwa wamefikia mwisho wa kazi yao ya maisha hapa duniani, na kwamba walikuwa karibu kupewa utukufu wa kimbingu. Lakini wapi. Mwezi wa Novemba mataifa yenye kuhusika katika vita ya ulimwengu yakatia sahihi ya kuikomesha kwa muda, kisha amani ikaingia, na jamani yalikuwako mabaki tu ya waabudu wa Yehova wakiwa hai bado katika dunia hii iliyotiwa jeraha la vita.
5. Kukosa kwao kuwa na utendaji wa kiroho kulifanana na kwa akina nani wakati wa uhamisho wa muda mrefu, lakini Neno la Mungu lilikuwa limetabiri nini juu yao?
5 Sasa iweje? Neno la Yehova la kiunabii lilikuwa limetabiri kwamba mashahidi wake wenye kuonekana kama wamekufa wangerudishwa kwenye utendaji mpya wenye uchangamfu katika utumishi wake wa kifalme hapa duniani. Wakati wa pigano la kwanza la ulimwengu hali yao ya kiroho ilikuwa imekuwa kama ile iliyowapata Waisraeli baada ya mji mkuu wao wa kitaifa, Yerusalemu, kuharibiwa na majeshi ya Babeli mwaka wa 607 K.W.K. kisha wao wakahamishwa na kupelekwa nchi ya Babeli iliyokuwa mbali, wakakae huko wakiwa na usingizi wa kiroho muda wa miaka 70.
6. Nabii Ezekieli alitumiwa namna gani kutoa mfano wa kiunabii juu ya kufufuliwa kwa taifa la Kiyahudi na kurudishwa kwao wafanye ibada katika nchi ya kwao?
6 Hali hiyo ya Israeli wa kale wakati wa miaka ya 607-537 K.W.K. ilitajwa na Ezekieli nabii wa Yehova, yeye mwenyewe akiwa mhamishwa katika Babeli. Katika moja ya njozi zake aliona bonde lenye kujaa mifupa mikavu. Akaambiwa kwamba mifupa hiyo iliyovurugika shaghala-baghala ilikuwa mfano wa nyumba yote ya Israeli katika hali yake ya uhamisho. Wakati Ezekieli alipotii amri ya Mungu akatoa unabii juu ya mifupa hiyo iliyotawanyika, ilijikusanya-kusanya ikawa magofu ya miili, nayo magofu hayo ya miili yakakisama wima juu ya miguu yao. (Ezekieli, sura ya 37) Katika utimizo wa kwanza wa mfano wa unabii huo, jambo hilo lilionyesha namna Waisraeli wangefunguliwa Babeli wakati wa anguko lake, nao wangekuwa hai tena wakiwa taifa zima, wamwabudu tena Mungu wao mwenye rehema kwenye hekalu lililojengwa upya katika mji mkuu wao uliorudishwa katika hali yake, yaani, Yerusalemu.
7. Ni tukio gani linalofanana na kufufuliwa huko kwa taifa zima kulikotabiriwa katika Ufunuo 11:3-13?
7 Karne nyingi baada ya ufufuo huo wa taifa, jambo linalofanana na hilo lilitabiriwa kwa usemi wa mfano, katika Ufunuo 11:3-13:
“Nami nitawaruhusu mashahidi wangu wawili, nao watatoa unabii siku elfu na mia mbili na sitini, hali wamevikwa magunia . . . Hata watakapoumaliza ushuhuda wao, yule mnyama atokaye katika kuzimu atafanya vita nao, naye atawashinda na kuwaua. Na mizoga yao itakuwa katika njia ya mji ule mkuu . . . Na baada ya siku hizo tatu u nusu, roho ya uhai itokayo kwa Mungu ikawaingia, wakasimama juu ya miguu yao; na hofu kuu ikawaangukia watu waliowatazama. Wakasikia sauti kuu kutoka mbinguni ikiwaambia, Pandeni hata huku. Wakapanda mbinguni katika wingu, adui zao wakiwatazama. Na katika saa ile palikuwa na tetemeko kuu la nchi.”
8, 9. (a) Katika nyakati za kisasa, ni wakati gani mwito kama huo ulipopelekwa kwa watu wa Mungu waliokuwa wafu kiroho? (b) Ni kwa uneni gani wa mfano mwito huo wa kiunabii ulitolewa katika Isaya 26:19?
8 Kulingana na hilo, mwito wa baada ya vita ulikuwa karibu kuwafikia mabaki wafu kiroho wa watu wa Yehova waliojiweka wakf, watoke wakafanye utendaji wa kuwa mashahidi wake wanaoweza kuonekana na wakaaji wa dunia yote. Katika mwaka wa kwanza ulioifuata vita, yaani 1919, walipokea mwito huo, baada ya kuamshwa kwao wafahamu kwamba Yehova Mungu alikuwa amewaacha wawe hai katika mwili hapa duniani kwa kusudi la maana sana. Wao walithamini sana jambo la kwamba wasingeweza kutimiza lo lote bila msaada wake wakati ambao wangeendelea kukaa kwa muda katikati ya ulimwengu wenye uadui. (Isaya 26:18) Baada ya wakati fulani Mungu Mweza Yote akawaondolea mashaka yao na kuwapa amri kama ilivyotabiriwa katika Isaya 26:19, ambapo maneno ya kiunabii yaliyohifadhiwa kwa faida yao yanasema hivi:
9 “Wafu wako wataishi, maiti zangu zitafufuka; amkeni, kaimbeni, ninyi mnaokaa mavumbini, kwa maana umande wako ni kama umande wa mimea, nayo ardhi itawatoa waliokufa.”
10. Yehova anatumia usemi unaoufaa wakati gani katika maneno hayo, lakini kwa sababu gani usemi uliotumiwa ulifaa?
10 Kwa kusema hivyo Yehova anatumia usemi utakaoufaa wakati wa ufufuo halisi wa wanadamu wafu waliokombolewa, watakaokuwa chini ya Ufalme wa kimbingu ulio mikononi mwa Mfalme aliyepewa kiti cha ufalme, Yesu Kristo, yule Mkombozi. Mabaki ya Waisraeli wa kiroho wa sasa walielekea kumalizwa kabisa wakati wa miaka 1914-1918, sawa na Waisraeli wa kale waliohamishwa kutoka nchi yao ya kitaifa waliyokuwa wameikaa kisha wakazikwa Babeli muda wa miaka 70, tukitumia uneni wa kiroho. Mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika mwaka wa 1918 uliwaacha mabaki wa kisasa wakiwa kama “maiti” mikononi mwa Yehova, tukitumia uneni wa kiroho.
11. (a) Ni nani pekee aliyeweza kutokeza uzaliwa wa kiroho kwa mara ya pili, na hali ingekuwa ya ubichi kama ya mmea gani? (b) Wakati ulikuwa umefika mwito gani upelekwe kwa watu wa Yehova?
11 Yehova, aliye Mpaji-Uzima Mkuu, angehakikisha kwamba “maiti” hizo zingeishi tena ziwe mashahidi wake wapakwa mafuta. Yeye angeweza kuwafufua. Kwa kuwa sasa nafasi za kipindi cha baada ya vita zilikuwa wazi, haukuwa tena wakati wao wa kuomboleza na kuwa kama wafu, kama ‘wanaokaa mavumbini.’ Ulikuwa umefika wakati wa Yehova usioweza kuahirishwa kuwaamsha kwenye uzima wa kiroho kisha wapige kelele ya furaha kwa sababu ya kuwa hai na kuwa katika utumishi wake. (Zaburi 126) Badala ya kuwa kama mizoga iliyokufa, kama wakaao katika mavumbi makavu, wangekuwa na ubichi wa uhai, kama kwamba wanasafishwa mwili kwa umande tele wa mmea wenye kutambaa chini. Yule Koreshi Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo, sasa alikuwa akitawala mbinguni, na wakati wa Yehova ulikuwa umefika wafunguliwe kutoka uhamishoni kama kwamba walikuwa katika nchi ile ya Babilonia yenye kuleta kifo. Hali yao ya uhamisho, iliyofanana na nchi ya Babilonia ambamo Waisraeli wa kale walizuiwa uhamishoni, haingewazuia tena wakiwa kama maiti zisizojiweza; ulikuwa wakati wa kuwafungua wazaliwe upya kiroho, wakiwa na ushujaa na uwezo wa kutoka katika Babeli Mkuu, ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Mwito wa Mungu uliotolewa katika wakati wenye kufaa kabisa ulisema, “Tokeni kwake, enyi watu wangu.” (Ufunuo 18:4) Walitii kwa haraka wakaacha kuendelea kujitiisha chini ya Babeli Mkuu na wafuasi wake wa kilimwengu ili wasikataliwe na Yehova.
12. (a) Watu wa Yehova wangejifichaje na maangamizi ya kimungu, na kwa muda gani? (b) Wakati huo Babeli Mkuu atafunuliwa wazi aonekane kuwa namna gani, na ni utetezi gani utakaokuwapo?
12 Isaya 26:20, 21 inaendelea kusema: “Njoni, watu wangu, ingia wewe ndani ya vyumba vyako, ukafunge mlango nyuma yako ujifiche kitambo kidogo, mpaka ghadhabu hii itakapopita. Kwa maana, tazama, [Yehova] anakuja kutoka mahali pake, ili kuwaadhibu wakaao duniani, kwa sababu ya uovu wao; ardhi nayo itafunua damu yake, wala haitawafunika tena watu wake waliouawa.” Sasa muda mwingi sana haungepita. Ungekuwa ni kama “kitambo kidogo” na baada ya hapo Yehova akomeshe Babeli Mkuu kwa kuwafanya wafuasi wake wa kilimwengu wamwangamize kabla ya wao wenyewe kuangamizwa wakati wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” kwenye uwanja wa pigano la Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Halafu damu ambayo Babeli Mkuu atakuwa na hatia ya kuimwaga itafunuliwa wazi kisha yeye alipwe kwa kumwagiwa yake. Viumbe wa kibinadamu ambao yeye ndiye amefanya wauawe ama kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja hawataendelea kuwa wamezikwa na kuachiliwa bila mtu wa kuwajali. Wao watatetewa kwa kumpa kifo mwuaji huyo. Lo! ni mashahidi wengi sana wa Yehova ambao wameuawa na Babeli Mkuu!
Wenzi Wenye Uhai wa Wale Watakaofichwa Wasipatwe na Maangamizi ya Kimungu
13. (a) Ni baraka gani za kurudishwa zilizoleta uzuri mwingi katika mwaka wa 1919 ulioifuata vita? (b) Kulingana na Isaya sura ya 35, walipitia njia gani wakirudia hali ya furaha isiyo na mwisho?
13 Mwaka wa 1919 ulijazwa wema wa kimungu. Siku ya Machi 21, kabla kazi ya kutoa ombi katika taifa zima haijamaliza kufanywa na Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote, wale wajumbe wanane wa Sosaiti walikubaliwa kuweka dhamana, na Machi 25 wakafunguliwa katika lile Gereza la Atlanta. Hawakurudi tena huko. Kwa sababu gani? Kwa sababu baadaye walisemwa hawana hatia kwa kuonekana kuwa hawakuitenda uhalifu wo wote nchi ya United States. Baadaye mwaka huo, makao makuu ya Sosaiti yalirudishwa Brooklyn, New York, mahali pale yalipokuwa zamani. Hivyo mabaki ya Waisraeli wa kiroho walifunguliwa katika utumwa wa Babeli Mkuu wakarudia makao yao ya kiroho yenye kuwafaa machoni pa Mungu waliyekuwa wakimwabudu. Kama ilivyotabiriwa katika Isaya 35:8-10, walirudia uhai wa kiroho na utendaji katika utumishi wa Yehova. Walifanya hivyo kwa kuipitia njia kuu ya mfano: “Nayo itaitwa, Njia ya utakatifu.” Unabii huo unaendelea kusema hivi: “Na hao waliokombolewa na [Yehova] watarudi, watafika Sayuni wakiimba; na furaha ya milele itakuwa juu ya vichwa vyao; nao watapata kicheko na furaha, huzuri na kuugua zitakimbia.”
14. (a) Ni kusanyiko gani lililofanywa Septemba mwaka wa 1919, na ni kichapo gani kilichotangazwa kuwa kingekuwa kikipigwa chapa? (b) Wachapishaji walirudia makao gani, na ni uchapaji gani ulioanza?
14 Siku za Septemba 1-8 za mwaka uo huo wa baada ya vita, yaani 1919, kusanyiko kuu lilifanywa huko Cedar Point, Ohio, nao wakatangaziwa huko kitu kipya cha kazi ambayo wangeifanya baada ya vita, yaani, kuchapishwa kwa gazeti lenye kurasa 32 lenye kutokea baada ya kila majuma mawili. Liliitwa The Golden Age (Kizazi cha Ufanisi), likawa msaidizi wa gazeti Mnara wa Mlinzi (la Kiingereza). Tarehe ya Oktoba 1, 1919, toleo la kwanza la hilo gazeti jipya (ambalo sasa linaitwa Amkeni!) lilitokea nalo likatimiza kusudi lake la wakati unaofaa, si la kuwajulisha wenye kumpenda Mungu juu ya Mileani (miaka elfu) nzuri ajabu iliyokuwa ikikaribia, bali pia kuifunua wazi Babeli Mkuu kuwa ilikuwa imehukumiwa maangamizi ya mapema. Baadaye, katika toleo la Desemba 15, 1919, gazeti Mnara wa Mlinzi (la Kiingereza) lilitangaza tena anwani ya wachapishaji walo kuwa ni 124 Columbia Heights, Brooklyn, New York. Nalo gazeti The Golden Age la Aprili 14, 1920 lilitangaza katika toleo la tarehe 15 kwamba sasa lilikuwa likipigwa chapa huko 35 Myrtle Avenue, katika mtaa wa Brooklyn, New York, mahali palipokuwa na kiwanda cha kwanza cha uchapaji cha Sosaiti. Leo Sosaiti na matawi yake ina viwanda vya uchapaji katika sehemu zote za dunia.
15. Kazi yote hiyo ya kurudishiwa hali inayofaa ilikuwa utimizo wa nini kilichokuwa kimetabiriwa na manabii wa Mungu, na ilikuwa sehemu ya “ishara” iliyotabiriwa na Yesu kuonyesha nini?
15 Kazi yote hiyo iliyofanywa kwa kiasi kidogo wakati huo ili kurudisha mambo kwenye hali inayofaa baada ya vita ilikuwa ndiyo mwanzo wa “zamani za kufanywa upya vitu vyote, zilizonenwa na Mungu kwa kinywa cha manabii wake watakatifu tokea mwanzo,” ili kuonyesha kwamba Yesu Kristo aliyetukuzwa alikuwa amerudi na akawapo bila kuonekana. (Matendo 3:21) Kufunguliwa wakati huo na kukusanywa kwa watu wa Yehova waliojiweka wakf kutoka Babeli iliyofananishwa kulikuwa sehemu ya “ile ishara . . . ya umalizio wa mfumo wa mambo” ambayo Yesu alitabiri katika unabii wake ulioandikwa kwenye Mathayo sura za 24, 25 (NW); Marko sura ya 13, na Luka sura ya 21.
16. Kwa kulingana na hali ya kisasa, ni nani waliorudi pamoja na Waisraeli kwenye nchi ya Yuda mwaka wa 537 K.W.K.?
16 Yote hayo yalifanya matayarisho ili kitokee kitu chenye umaana mkubwa sana. Kitu gani? Tunakumbuka kwamba wakati wahamishwa Waisraeli walipoondoka Babeli mwaka wa 537 K.W.K. kwa kuamriwa na aliyeishinda Babeli, Koreshi Mkuu, hesabu kubwa ya watu wasio Waisraeli ilirudi pamoja nao kwenye nchi ya Yuda. Kati yao walikuwako Wanethini, watumwa wa kiume na wa kike na waimbaji wa kigeni.—Ezra 2:43, 58, 64, 65, 70; 3:1; 6:21, 22; 1 Mambo ya Nyakati 9:1, 2.
17. Leo wenzi hao wasio Waisraeli wanafananisha nani, nao walifanana na nani pia?
17 Watu hao wasiokuwa Waisraeli lakini wakaambatana nao wanafananisha watu wanaosikia leo ujumbe wa Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Koreshi Mkuu wake, Yesu Kristo, kisha wakajishirikisha na mabaki ya Waisraeli wa kiroho tangu walipofunguliwa wasizuiwe na Babeli Mkuu wa kisasa na wafuasi wake walimwengu katika mwaka wa 1919, ulioifuata vita. Wanafanana pia na wale watu wasiokuwa Waisraeli, lile “kundi kubwa la watu waliochangamana nao” wakaambatana na Waisraeli wakati walipoondoka Misri wakiongozwa na Musa mwaka wa 1513 K.W.K.—Kutoka 12:37, 38; linganisha Ufunuo 7:9-17.
18. Ni wakati gani watu hao wenye mfano wa kondoo walipoelezwa juu ya pendeleo lao la “kujitakasa” (kujiweka wakf), na ni baada ya utambulishi gani zaidi wa watu hao huko Washington, D.C., mamia yao walionyesha kwamba ‘wamejitakasa’?
18 Wanalingana pia na “kondoo wengine” ambao yule Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, alisema bado angewaleta, ili mwishowe awaunganishe wawe “kundi moja” pamoja na wale kondoo wa kiroho walio katika “zizi hili” lenye warithi wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu. (Yohana 10:16)b Katika toleo la Juni 6, 1934, la gazeti The Golden Age, ukurasa wa 574, chini ya kichwa kidogo “Jamii ya Yonadabu,” hao “kondoo wengine” wa mfano walijulishwa pendeleo lao la ‘kujitakasa’ (kujiweka wakf) mbele za Yehova Mungu kupitia Kristo na kuonyesha hivyo waziwazi kwa kubatizwa katika maji. Siku ya Mei 31, 1935, msimamizi wa Sosaiti alihutubu kwenye Kusanyiko la Washington akawashirikisha “kondoo wengine” kuwa sawa na “mkutano mkubwa” uliotangulia kuonwa katika Ufunuo 7:9-17. Siku ya kusanyiko iliyofuata, watu 840 walibatizwa katika maji, na wengi kati yao walishikilia tumaini la kuishi duniani chini ya Ufalme wa Mungu.
19. (a) Kwenye Yohana 11:26, Yesu alisema nini juu ya kutokufa kamwe? (b) Ni tendo gani la mataifa linaloyaunganisha, na wanafanya hivyo kabla ya wao kupatwa na nini kwenye Har–Magedoni?
19 Hapa ndipo inapofaa kuyafikiria yale maneno ya Yesu Kristo kwenye Yohana 11:25, 26: “Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele.” Kulingana na mashuhuda yote ambayo yameonekana tangu mwaka ule wenye vita wa 1914, tunajikuta tukiwa hai katika “wakati wa mwisho,” ndiyo, katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Danieli 12:1-4; Mathayo 24:1-3, NW) Ingawa Mashahidi wa Yehova wamezitangaza “habari njema hizi za ufalme” ulimwenguni pote tangu mwaka wa 1919, mataifa, hata yale ya Jumuiya ya Wakristo, yamekataa kujiweka chini ya huo Ufalme wa Kimasihi uliosimamishwa katika mbingu tangu mwaka wa 1914. Upinzani kwa Ufalme wa Mungu unaostahili na kwa mahubiri ya Ufalme huo ndio unaoyaunganisha mataifa pamoja, na kwa njia hiyo yanakusanywa kwenye “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni. “Vita” hiyo ya duniani pote itayaletea mataifa hayo yasiyo na imani uharibifu kamili. Huo ndio utakaokuwa mwisho wa huu mfumo wa mambo.—Ufunuo 16:14-16; Mathayo 24:14, NW.
20. (a) Wakati huo watu wenye mfano wa kondoo hapa duniani watapata nini? (b) Watataka majina yao yaandikwe katika kitabu gani, na jambo hilo litawahakikishia nini kabisa?
20 Wakati huo watu wenye imani walio mfano wa kondoo, wale walio wa lile “kundi moja” la Mchungaji Mwema, ndio peke yao watakaoepuka kifo. Hiyo ni kutia ndani na ule “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine.” Kwenye Ufunuo 7:9-17 walitangulia kuonwa katika njozi ‘wakitoka katika ile dhiki kubwa’ wakiwa hai na kuingia katika mfumo wa mambo ya Mileani hapa duniani. (Mathayo 24:21, 22) Hao hawana tena uhitaji wa kufa watoke duniani. Chini ya utawala wa Kristo watapewa nafasi ya kupata uzima usio na mwisho katika Paradiso itakayorudishwa duniani. (Ufunuo 20:1-6) Mpaka sasa hatujui ni mashahidi wangapi wa Yehova kati ya wale zaidi ya 2,000,000 walio hai leo waliojiweka wakf na kubatizwa, watakaohifadhiwa hai kuipita “dhiki kubwa” itakayozingira dunia yote. Lakini watakuwa ni “mkutano mkubwa” usio na hesabu kutoka katika mataifa na lugha ambazo ni nyingi. Watu hao wenye imani watasisimuka kwa kuukanyaga mfumo wa mambo utakaoifuata Har–Magedoni kuliko vile Noa na jamaa yake walivyosisimuka walipotoka katika safina wakaikanyaga dunia safi baada ya ile Gharika ya dunia nzima. Kwa watu hao wa kisasa wenye imani maneno ya Yesu yatatimia katika maana halisi kabisa: “Naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele.” (Yohana 11:26) Waokokaji hao wa Har–Magedoni watataka majina yao ‘yaandikwe katika kitabu cha uzima’ ambacho Mungu aliye mpaji-uzima atakiweka. (Ufunuo 20:7-15) Kuandikwa namna hiyo kwa majina yao kutawapa uhakikisho kamili kwamba wataishi milele juu ya dunia-Paradiso.
21. Ni nini ambacho waokokaji hao wa Har–Magedoni hawatahitaji wakati wa Mileani, na wakati huo watakuwa mashahidi kwa akina nani kwa sababu watakuwa wamekwisha kuwa mashahidi washika-ukamilifu wa Yehova wakati wa sasa?
21 Pasipo shaka hata kidogo, katika muda huu ambao umepita sana wa “wakati wa mwisho” tangu kikomo cha Majira ya Mataifa mwaka wa 1914, kuna wanaume na wanawake wengi wenye imani na ukamilifu walio hai ambao hawatakufa kamwe watoke katika uso wa dunia hii, ambayo ni kikanyagio cha Mungu. Lo! wana pendeleo kubwa kama nini mbele yao! Kwa sababu wao hawatakufa kamwe wala kuzikwa, hawatahitaji ufufuo wa wafu wakati wa utawala wa Yesu Kristo wa miaka elfu. Kwa kweli, wao watakuwa hai wakaribishe wenye kurudi kutoka kwa wafu ambao wamelala usingizi katika mavumbi ya ardhi, wale ambao Mfalme Yesu Kristo aliwatolea uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uwe dhabihu ya ukombozi. Waokokaji wa Har–Magedoni watakuwa na pendeleo la kuyatolea ushuhuda mabilioni hayo ya wanadamu wafufuliwa juu ya mambo yote ambayo Yehova Mungu atakuwa amefanya kupitia Yesu Kristo wakati wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo.” Basi, katika muda wote huu ulio wa maana kupita nyakati zote zilizotangulia, waacheni hao wenye pendeleo kubwa wajithibitishe kuwa mashahidi washika-ukamilifu wa Yehova Mungu ili enzi kuu yake ya ulimwengu wote iondolewe malawama.—Kutoka w7/1/83.
[Maelezo ya Chini]
a Ona toleo la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1918 (Kiingereza), ukurasa wa 80 chini, katika habari inayosema “Makusanyiko Kuhutubiwa na Ndugu J. F. Rutherford”’; Jehovah’s Witnesses in the Divine Purpose, ukurasa wa 76, fungu la mwisho; pia, toleo la Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 1924 (Kiingereza), ukurasa wa 280, chini ya kichwa kidogo “Sababu Mamilioni Hawatakufa Kamwe.”
b Ona ukurasa wa 345, mafungu 577, 578, ya kitabu The Harp of God, kilichochapishwa mwaka wa 1921; pia toleo la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 15, 1923 (Kiingereza), ukurasa wa 310, fungu la 33, la makala inayosema “Mfano wa Kondoo na Mbuzi.”
Je! Wewe Unakumbuka?
□ Ni kwa njia gani mabaki wapakwa mafuta walikuwa wamekuwa kama wafu?
□ Yehova alifufua mashahidi wake wapakwa mafuta wakawa na nafasi gani za kutumia katika muda ulioifuata vita?
□ Kurudishwa hivyo katika hali inayofaa kulitimiza unabii gani mbalimbali?
□ Waokokaji wa kidunia wa Har–Magedoni hawatahitaji kupatwa na nini wakati wa Mileani?
[Picha katika ukurasa wa 14]
Mashahidi waliopakwa mafuta wa Yehova na wenzi wao wenye mfano wa kondoo wanashirikiana kwa moyo wote katika kueneza ujumbe wa Ufalme