Woga Ni Ishara ya Ule Mwisho?
JE! SISI tunaishi katika machweo ya kizazi chenye mashaka na masumbuko ambapo ‘wanadamu wanazimia moyo kwa sababu ya hofu na kwa kutazamia mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu’? Kurudia kujikumbusha kwa ufupi tu matukio ya ulimwengu na mambo yenye kusababisha woga tangu mwaka wa 1914 kutatuburudisha akilini na kutusaidia tuone kama tunaukaribia ule “mwisho” uliotabiriwa.—Luka 21:9, 25, 26.
Woga na Vita
Nguzo za kuwakumbuka wafu wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika Ufaransa zimeandikwa maneno yanayosema “la Grande Guerre.” Ndiyo, ile ambayo sisi sasa tunaiita vita ya ulimwengu ya kwanza (1914-18) ilikuwa ikiitwa ile Vita Kuu hapo kwanza. Ilikuwa kubwa sana na yenye kuogopesha sana katika wingi wa waliouawa na wa uharibifu uliofanywa mpaka wanadamu wakaiita kwa matumaini mazuri kuwa ile vita ya kukomesha vita vyote. Baada ya kupatwa na tukio hilo la kutia woga mwingi, hakika ilifikiriwa kwamba mwanadamu aliyestaarabika ‘hangejifunza vita tena kamwe.’ (Isaya 2:4) Ilichukua muda wa miaka 18 tu baadaye halafu ndoto hiyo ikafagiliwa mbali wakati kulipotokea kwa ghafula ile Vita ya Raia wa Spania (1936-39) iliyokuwa mbaya sana. Katika vita hiyo Waspania zaidi ya nusu-milioni walikufa. Wajeremani na Waitalia walishiriki katika pigano hilo, na hayo yakawa ni kama mazoezi kwa ajili ya ile iliyolazimika kuitwa vita ya ulimwengu ya pili (1939-45). Hayo maangamizi makubwa ya ulimwengu yalimalizika kwa kutokeza uharibifu mbaya sana wa miji ya Hiroshima na Nagasaki.
Wakati milipuko hiyo ya makombora ya atomi ilipotokea juu ya Japani, chanzo kipya cha woga na masumbuko kilitokea kwa ghafula ulimwenguni, yaani, woga unaohusu kutokea kwa vita ya atomi. Hakika Albert Einstein alisema maneno ya kweli kabisa mwezi Desemba wa 1945: “Ulimwengu uliahidiwa kupata uhuru wa kutokuwa na woga, lakini kusema kweli woga umeongezeka ajabu tangu vita hiyo ilipokoma”! Halafu akaongeza kusema, “Hali za ulimwengu wetu wa baada ya vita hazionyeshi kuna matumaini mazuri.”
Woga huo unaoendelea kuongezeka unaonyeshwa leo na mamilioni ya watu ulimwenguni pote ambao wanafanya maandamano ya kupinga silaha za nyukilia. Hata viongozi wa kidini wanajiingiza katika suala hilo. Ndiyo, silaha za nyukilia zimegeuza siasa za ulimwengu na maarifa ya kijeshi. Ni kama vile mwanahistoria E. P. Thompson alivyosema katika kitabu chake cha hivi juzi kinachoitwa Beyond the Cold War: “Silaha hizo zinafanya kazi kwa kutumia siasa, maoni ya kuwazia na mbinu za kutafuta kuungwa mkono kisiasa; zinafahamiwa kuwa zenye kuogopesha na zimekusudiwa zifanye hivyo; zinatia watu woga na wakati uo huo zinaongeza na kuchochea maoni ya kutaka kuanzisha vita.”—Mwandiko wa italiki ni wetu.
Woga huo unaohusu vita ya nyukilia uko kote kote ulimwenguni. Kijitabu cha juzi-juzi cha Urusi kilisema hivi: “Urusi inashikilia maoni ya kwamba vita ya nyukilia ingekuwa maafa ya ulimwengu mzima, na inaelekea zaidi kuwa kwamba hiyo ndiyo ingekuwa mwisho wa ustaarabu. Huenda ikaongoza kwenye uharibifu wa wanadamu wote.” Sasa zile pande mbili zilizo kubwa-kubwa zinakabiliana moja na nyingine zikiwa katika hali ya kushindwa kuamua kupigana kwa kutegemea kile kinachoitwa Angamizano Hakika. Si ajabu basi kwamba wanadamu wamo katika ‘hofu na katika kutazamia mambo yanayokuja juu ya dunia’—sawasawa na vile Yesu alivyotabiri.
Woga na Uhalifu
Kuna woga wa namna nyingine unaofika karibu zaidi na nyumbani. Ni woga gani? Ni wa kuogopa uhalifu katika ujirani wako mwenyewe. Kulikuwa na wakati ambao mwivi mwenye kuvunja nyumba, au mnyang’anyi, alipochukua mali tu. Sasa wanachukua hata uhai. Watu hawaogopi sana sheria, na kufanya uhalifu kunawaletea watu wengi faida nyingi. Hivyo woga mwingi sana unapenya ndani sana ya majiji na maeneo ya mijini wanakoishi matajiri. Kwa mfano, sasa ni watu wachache kabisa wanaotumia reli ya New York inayopita chini ya ardhi, tangu mwaka wa 1917. Kwa sababu gani? Moja ya sababu zilizo kubwa zaidi ni woga wa kutendwa unyang’anyi au kuuawa. Habari moja ya kutoka Uingereza inasema: “Ile roho ya ushirikiano inayohitajiwa sana kati ya watu wa mitaa inaharibiwa na woga unaohusu uhalifu ambao unafanya watu wengi wakae nyumbani.” Hata katika miji iliyokuwa salama hapo zamani kama Barcelona, Spania, milango migumu zaidi inaendelea kuuzwa kwa wingi mkubwa zaidi, na sasa nyumba nyingi zina kufuli zisizopungua mbili au tatu na milango ya nyumba hizo ina makomeo. Katika United States (Amerika) wanawake wengi wanajifunza kutumia bunduki za mkononi ili wajue kujikinga. Uchunguzi mmoja unaonyesha kwamba asilimia 52 ya jamaa za Kiamerika zina bunduki! Habari iyo hiyo inaonya kwamba, “Woga unaohusu uhalifu unaendelea kuipoozesha jamii ya watu wa Amerika pole kwa pole.”
Waandikaji wa Biblia walioongozwa na Mungu walijua kwamba hali hizo za kupita kiasi zingetokeza katika wakati wa mwisho. Hivyo mtume Paulo alionya hivi: “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema.” (2 Timotheo 3:1-3) Ni uhalifu mwingi kama nini unaochochewa na mambo ambayo mtume anataja hapo! Na ni woga mwingi kama nini unaoenezwa na hesabu ya wahalifu wanaozidi kuongezeka nyakati zote!
Woga na Ukosefu wa Kazi
Jambo jingine linalopanda woga na masumbuko katika karne ya 20 ni ukosefu wa uthabiti wa uchumi wa ulimwengu, ambao umeletea watu fulani ufanisi wa kiasi na kufanya mamilioni wakose kazi. Hata wale walio na kazi wanajisikia mara nyingi wakiwa bila usalama. ‘Safari ile itakayofuata itakuwa zamu ya nani kupiga miguu akitafuta kazi?’ Hilo ndilo ulizo lenye kuvuruga sana akili. Kwa kuwa ni watu wengi wanaojipatia chakula kwa kukopa, tatizo kubwa hilo linaleta masumbuko kila siku. Katika mataifa ya Wazungu tu kuna watu zaidi ya milioni 30 wasio na kazi. Mwelezaji mmoja hata alitoa onyo lenye uzito akasema kwamba huenda wengi wa wasio na kazi wakakosa kupata kazi hata siku moja!
Wenye kuhifadhi pesa katika benki za mataifa yote wanashindwa kujua la kufanya wanapotazama nchi baada ya nchi nyingine ikifilisika kabisa. Kama ilivyoripotiwa na gazeti The Guardian, “Kwa ujumla katika muda wa miaka mitatu iliyopita karibu nchi 25 zimelazimika kuomba mabenki na serikali mbalimbali ziongezwe wakati wa kulipa madeni yazo, na nyingi kati yazo zimerudi kukopa zaidi ya mara moja.” Basi hali ya uchumi ni jambo moja jingine linalotimiza maneno ya Yesu kwamba ‘wanadamu watazimia moyo kwa sababu ya hofu na kwa kutazamia mambo yanayokuja juu ya dunia.’
Woga na Anga za Juu
Woga wa mwanadamu wa namna nyingi za masumbuko yake hautokani na matatizo yake ya kidunia tu. Tangu mwaka wa 1914 silaha za kuogopesha na kuleta maangamizi zimemiminika chini kutoka angani katika vita vya ulimwengu viwili na katika mapigano mengine mengi makubwa-makubwa. Lakini sasa tisho lenyewe linatokana na kitu kingine kilicho juu zaidi ya anga—kimejificha katika anga za juu zaidi. Hivi majuzi gazeti la Kispania la kila siku linaloitwa El País lilikuwa na kichwa cha habari yenye kusema “Anga za Juu, Karibu Kugeuzwa Ziwe Uwanja wa Shughuli za Kijeshi.” Makala hiyo iliendelea kusema hivi: “Kwa njia hiyo United States na hata Urusi inapiga hatua moja zaidi katika kushindania mamlaka ya anga za juu, na katika miezi ya majuzi imeonekana kwa njia ya kustaajabisha sana kwamba kusudi lao ni kufanya shughuli za kijeshi huko. Inaweza kusemwa kwamba kipindi cha kutumia anga za juu kwa njia ya kutaka vita kimeanza.”
Tisho linalotoka kwenye anga za juu linahakikishwa na maneno yaliyosemwa na Luteni-Jenerali Richard C. Henry, naibu wa amiri wa Kikosi cha Anga za Juu cha United States (Amerika), aliyesema hivi: “Anga za Juu si mahali pa kupeleka vyombo tu na kurudi, ni mahali pa kukaliwa. Ni uwanja wa kuendeshea shughuli za kijeshi. Sasa wakati umefika tunaopaswa kupachukua kama uwanja wa kuendeshea shughuli za kijeshi.” Naye Jenerali Robert T. Marsh, amiri wa Kikosi cha Mifumo ya Jeshi la Hewani, alihakikisha hivi: “Safari za kwenda-kwenda kwenye anga za juu zitabadili njia tunayotumia kufanya kazi yetu. Tutazitegemea ili kusafirisha vifurushi vyetu vyote vya kitaifa vya malipo ya kujisaidia wakati wa uzee [yaani, vifaa vya kijeshi].” Maneno hayo yanaonyesha kwamba anga za juu haziwezi tena kuchukuliwa kuwa nafasi tupu tu isiyoleta madhara. Ni kama vile katibu-mkuu wa Umoja wa Mataifa alivyoonya: “Ni lazima sisi tupinge kwa juhudi nyingi lile ongezeko kubwa la kufanya anga za juu ziwe mahali pa kuwekea vifaa vya kijeshi. Tuna wakati—lakini mchache sana.” Kupita kwa wakati tu ndiko kutakakoonyesha ni ishara gani nyingine zitakazoonekana katika makao ya ‘jua na mwezi na nyota’ ili kuleta woga na tazamio la mambo yatakayotendeka.—Luka 21:25.
Je! Ni Tofauti na Vizazi Vilivyotangulia?
Watu wengine wana maelekeo ya kupuuza maonyo ya Biblia, wakisema kwamba vizazi vilivyotangulia vimepatwa na hatari za namna hii na kwamba woga na masumbuko yaliyopo sasa si ishara ya ule mwisho uliotabiriwa na Yesu. Kwa uhakika ni kweli kwamba vizazi vilivyotangulia vimepatwa na misiba. Karne ya 14 ilikuwa wakati wa ile Tauni Nyeusi, wakati watu katika sehemu zote za Ulaya waliishi wakiogopa sana magonjwa ya kipuku, ukosefu wa vyakula na pia vita. Lakini sasa linganisha wingi wa mambo katika karne yetu.
Mwanasayansi René Dubos aliandika majuzi hivi: “Mimi ninavurugwa sana moyoni sawasawa na mtu mwingine ye yote na yale maovu mengi sana sana yanayoletwa na matatizo hatari ya kijamii, kiufundi na ya kimazingira. . . . Mimi pia natambua kwamba pande kadha za matatizo ya sasa ya ulimwengu zinayafanya yatofautiane na yale ya zamani kwa wingi na kwa ubora. Kwa mfano:... Matatizo ya leo si ya watu wachache-wachache kama zamani.” (Mwandiko wa italiki ni wetu.) Alipanga pia madhara ya ulimwenguni pote yanayoletwa na vitu fulani kama ukali wa miale yenye nguvu nyingi inayotokezwa na madini fulani, mvua kali ya asidi na dawa za kuua wadudu. Jambo jingine ni kwamba mataifa yameongeza utegemeano wayo hivi kwamba yote yanapatwa kwa umoja na hatari kama ile iliyotokea mwaka wa 1973 kwa sababu ya ongezeko katika bei ya mafuta ya kuchimbwa ardhini. Haikuwa hivyo katika vizazi vilivyopita.
Basi si jambo la kweli hata kidogo kwamba vizazi vilivyotangulia vimeumizwa kwa kiasi kile kile na woga na masumbuko yanayopata kizazi hiki, wala havikuumia kwa sababu zile zile ambazo Yesu alitaja katika Luka sura ya 21. Hakuna kizazi kilichotangulia kile cha 1914 kimepata kuwa na vita ya ulimwengu hata moja, achia mbali vita viwili. Hakuna kizazi kilichotangulia kimepata kuelekeana na wazimu wa “angamizano hakika” kwa kutumia silaha za nyukilia. Hakuna kizazi kilichotangulia kimepata kuiharibu dunia kwa takataka na uchafuzi wenye kuenea sana kama ule wa sasa.—Ufunuo 11:18.
Halafu kuna jambo jingine moja la maana kabisa—hakuna kizazi kilichotangulia ambacho kimepata kuhubiriwa kwa mapana na marefu ‘habari njema hizi za ufalme katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda’ kama kizazi cha sasa. (Mathayo 24:14, NW) Sasa Mashahidi wa Yehova wanafanya hivyo kwa matokeo mazuri katika nchi zaidi ya 200, katika kila taifa ambako Mungu amewezesha jambo hilo. Hiyo ni sababu moja inayofanya wewe usome gazeti hili sasa hivi. Ujumbe wa Mungu wa tumaini na hukumu unatangazwa katika wakati unaofaa. Hiyo ni ishara hakika ya kwamba pasipo shaka mwisho utakuja karibuni. Halafu ni jambo gani litabaki? Yesu anajibu hivi: “Mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.”—Luka 21:29-33.
Ikiwa wewe ungependa kupata habari zaidi juu ya jambo hili la kupendeza, jisikie huru kuandikia wachapishaji wa gazeti hili au uende kwenye kundi la kwenu la Mashahidi wa Yehova katika Jumba la Ufalme lao. Maulizo yako yatajibiwa bila ya wewe kuombwa ulipe cho chote.
[Blabu katika ukurasa wa 6]
“Kipindi cha kutumia anga za juu kwa njia ya kutaka vita kimeanza”
[Picha katika ukurasa wa 5]
Kulingana na uchunguzi mmoja, asilimia 52 ya jamaa za Kiamerika zina bunduki
[Picha katika ukurasa wa 7]
‘Anga za juu si mahali pa kupeleka vyombo tu na kurudi—ni uwanja wakuendeshea shughuli za kijeshi’