Wewe Unatumia Jina Gani Kutaja Mungu?
Wewe unajua ni jina gani ambalo Biblia inatumia mara nyingi sana kuliko jina jingine lo lote? Je! ungesema ni Daudi? Abrahamu? au Yesu?
Ikiwa lo lote la majina hayo ndilo umefikiria, bila shaka mfululizo wa makala hizi utakupendeza sana, kwa maana jina lililo la maana kupita majina yote katika Biblia linatumiwa mara nyingi sana kuliko majina yote hayo yakijumlishwa pamoja.
KICHAPO kimoja cha kidini kinaonyesha kwamba wakati unaposema unapenda mtu, unaita mtu huyo kwa jina lake. Hungesema: “Ewe mwanamume, mimi nakupenda.” Wala hungesema: “Ewe mwanamke, mimi nakupenda.” Badala yake, ungesema: “John, mimi nakupenda.” Au: “Margaret, mimi nakupenda.” Halafu kichapo hicho kinauliza: “Ni jina gani ambalo wewe unaweza kumpa Mungu ili uonyeshe kwamba una uhusiano wa kibinafsi na wa ndani zaidi pamoja naye? ”
Kinazungumza ulizo hilo katika ukurasa mzima, lakini hakitaji hata mara moja lile jina ambalo Mungu anajiita mwenyewe. Kinamalizia hivi: “Jina ambalo wewe unachagua kuonyesha una uhusiano wa ndani pamoja na Mungu linapasa kuamuliwa kwa kutegemea maoni yako binafsi.” Lakini, Je! haingekuwa vizuri zaidi kutumia jina ambalo Mungu alijichagulia mwenyewe, ambalo linatumiwa mara elfu nyingi katika Biblia?
Kweli Mungu Ana Jina?
Ndivyo, analo. Katika Kiebrania na Kigiriki ambamo hapo kwanza Biblia iliandikwa, neno “mungu” halikumaanisha yule Mungu wa kweli sikuzote. Kama ilivyo katika Kiswahili, neno hilo lingeweza kutumiwa kwa miungu ya uongo na sanamu. Kwa hiyo Mungu wa kweli aliye Muumba pia angetofautishwaje na miungu inayotengenezwa na wanadamu? Ni kwa kutumia jina la kibinafsi. Hata hivyo watu wengi hawajui jina la Mungu, na ni wachache sana wanaotumia jina hilo leo.
Kwa kweli, huenda ikawa wewe hujaliona kamwe jina la Mungu katika Biblia yako mwenyewe. Kwa sababu gani? Kwa sababu watu waliotafsiri nakala yako ya Biblia huenda wakawa walilibadili. Huenda wakawa hawakukubaliana na waandikaji wa Biblia ambao Mungu aliwaongoza watumie jina hilo mara elfu nyingi katika Maandiko ya Kiebrania.
Biblia ya Union Version, ambayo imetumiwa kwa muda mrefu na watu wanaosema Kiswahili, ina jina la Mungu, si zile mara karibu 7,000 ambazo linaonekana katika Kiebrania, bali mara kumi na mbili hivi likiwa peke yalo —kwenye Kutoka 6:2, 3, 6-8; Zaburi 68:20; 83:18; Isaya 12; 26:4; 49:14; Yeremia 16:21 na Habakuki 3:19. Kuna tafsiri nyingine zisiotumia jina la Mungu hata kidogo. Zimeliondoa jina la Mungu katika kitabu chake mwenyewe!
Ni wazi kwamba JINA hilo lilikuwa la maana zaidi ya maneno ambayo watafsiri waliweka badala yalo, kwa hiyo tafsiri nyingine zinachapisha maneno hayo yaliyowekwa badala yalo yakiwa ya herufi kubwa, ili kujulisha wasomaji wenye ujuzi mahali jina la Mungu lipo katika maandishi yale ya kwanza kabisa. Kitabu ensaiklopedia kinachojulikana sana kinaeleza hivi: “Inapasa kukumbukwa kwamba jina la Kiebrania Yehova linatafsiriwa kwa ujumla katika tafsiri ya Kiingereza kwa neno BWANA (nyakati nyingine MUNGU), na kuchapwa kwa herufi kubwa za namna ndogo.” Kwa hiyo wakati unapoona neno “BWANA” likiwa limechapwa kwa njia hiyo, mtafsiri anakuwa akikuambia wewe kwamba jina la Mungu mwenyewe, YEHOVA, limetumiwa katika ile lugha ya kwanza kabisa.—Cyclopedia ya McClintock na Strong, ya 1981, Buku la 4, ukurasa wa 811.
Kama wewe umeona au hujaona jina hilo katika Biblia yako, jina hilo lilikuwako katika maandishi ya kwanza kabisa ya Kiebrania. Wanachuo Wajeremani, Keil na Delitzsch, wanaonyesha kwamba usemi “Yehova Elohim” (Yehova Mungu) unaonekana mara 20 katika mistari inayopungua 50 ya Mwanzo sura ya 2 na ya 3. Wanasema kwamba usemi huo “unatumiwa kwa mkazo usio wa kawaida, ili kutokeza wazi uhakika wa kwamba kwa kweli Yehova ni Elohim,” au Mungu.—Commentary on the Old Testament, kilichotayarishwa na Keil na Delitzsch, 1973, Buku la Kwanza, kurasa 72, 73.
Kwa kweli, jina la Yesu mwenyewe linamaanisha “Wokovu wa Yah [Yehova].” Na wakati wo wote unaposema “Haleluya,” unakuwa ukitumia namna fupi ya kishairi ya jina la Yehova. Unaweza kutazama neno Hallelujah (Haleluya) katika kamusi (ya Kiingereza) ujionee mwenyewe kwamba neno hilo linamaanisha ‘Sifu Yah,’ au ‘Sifu Yehova.’
Kumbuka, Yehova ni jina la Mungu mwenyewe. Ndilo jina ambalo kwalo YEYE alichagua atambulike. Je! ungependa kujua namna matumizi ya jina hilo yanavyoweza kapanua hali yako ya kuthamini Mungu na makusudi yake? Hiyo ndiyo habari inayozungumzwa na makala zinazofuata.