Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 6/1 kur. 3-7
  • Kutangaza Habari Njema za Jambo Zuri Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutangaza Habari Njema za Jambo Zuri Zaidi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Mungu Wako Anamiliki!”
  • Tengenezo la Mungu Lafanya Kazi!
  • Mpanuko wa Ajabu!
  • ‘Imbeni Pamoja kwa Shangwe’!
    Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
  • Kutoa Ushuhuda Kunaleta Ongezeko la Ufalme
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Yehova ‘Ayahimiza’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Uungaji-Mkono wa Duniani Pote kwa Suala la Ufalme
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 6/1 kur. 3-7

Kutangaza Habari Njema za Jambo Zuri Zaidi

“Amka, amka, jivike nguvu zako, Ee Sayuni”!—ISAYA 52:1.

1. (a) Ni kwa njia gani vyombo vya habari vya ulimwengu vimeshindwa? (b) Chanzo kilicho na hekima kuliko vyanzo vyote kinawezesha nini kijulikane?

MLIO huu wa wa tarumbeta ulilia mapema katika karne yetu ya 20. Kwa sababu gani? Kwa sababu wakati ulikuwa umefika wa kutangaza habari njema za mambo mazuri zaidi kwa wanadamu. Je! tunasoma habari njema hizo katika magazeti ya ulimwengu? Hapana, kwa maana vyombo hivyo vya habari vinapendelea zaidi kuripoti mambo yatakayosisimua watu kwa njia ya kilimwengu au kutangaza ongezeko la uovu na ukosefu wa maadili. Lakini, wao hawawezi kuonyesha kitu kitakachotatua tatizo lililopo. Leo, watu wengi wanaogopa kupatwa na uharibifu katika maangamizi makubwa yenye moto mkali sana, ambao utawashwa na mlipuko wa makombora ya nyukilia yaliyotengenezwa na mwanadamu kumaliza watu. Lakini Mtu Fulani mwenye hekima nyingi sana kuliko mwanadamu mwenye kufa anatupasha habari za kwamba mwisho wa ulimwengu utakapofika utakuwa umeletwa na chanzo tofauti kabisa. Utaletwa na hukumu ya Mungu mwenyewe juu ya wanadamu waovu na mataifa maovu. (Zaburi 110:5, 6) Chanzo hicho cha habari kinatuambia pia juu ya mileani nzuri ajabu itakayofuata ya kutengeneza mambo upya, wakati dunia yetu, na wanadamu walio juu yake, watafikishwa kwenye hali ya ukamilifu mtukufu. Hakika hizo ni habari njema!—Ufunuo 20:6; Zaburi 72:16, 18, 19; Warumi 8:21.

2. Ni kilio (mwito) gani cha haraka kinachotokezwa sasa, na ni lazima kijibiwe namna gani?

2 “Amka, amka!’ Isaya anapaza sauti. Uharaka huo ni wa nini? Ni kwa vile mambo mbalimbali yanayotukia kutimiza unabii wa Biblia tangu mwaka wa 1914 na kuendelea yanaonyesha kwamba Ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo Yesu, yaani, “mji wa Mungu aliye hai, Yerusalemu wa mbinguni,” sasa unatawala katika mbingu. Ni lazima wajumbe waliopo duniani wa Sayuni, tengenezo la kimbingu la Mungu, waamke wafanye utendaji wenye juhudi. Ni lazima watangaze habari njema hizi kwa nguvu ambazo Mungu anawapa wale wanaomtii yeye kuwa mtawala.​—Waebrania 12:22, UV; Matendo 5:32, NW.

3. Isaya anasema na nani, na kwa ukaribishaji gani?

3 “Jivike mavazi yako mazuri, Ee Yerusalemu, mji mtakatifu; kwa maana tokea sasa hataingia ndani yako asiyetahiriwa, wala aliye najisi. Jikung’ute mavumbi; uondoke, uketi, Ee Yerusalemu; jifungulie vifungo vya shingo yako, Ee binti Sayuni uliyefungwa.”​—Isaya 52:1, 2.

4. Unabii huo umekuwaje na utimizo wa karne ya 20?

4 Unabii huo umekuwa na utimizo wa kusisimua wa karne ya 20! Wakati wa ile Vita Kuu ya miaka ya 1914-18, Wakristo wapakwa mafuta waliingia katika hali ya kuwa mateka (wafungwa) kwa njia ya kiroho, na wengine wao, kutia ndani maafisa wa Sosaiti, walitupwa ndani ya magereza halisi. Lakini mwaka wa 1919 walifunguliwa. Wakiwa wanawakilisha Sayuni ya kimbingu, Wakristo hao ndipo walipovaa “mavazi” yenye uzuri wa kupendeza kulingana na maoni ya Mungu, yaani, mavazi ya kutambulika kwao kuwa watumishi wa Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote. Walijitenga na uchafu wa kutokuwa na maadili na wa kiroho.​—Linganisha 2 Wakorintho 6:17, ambapo mtume Paulo anatumia maneno ya Isaya 52:11.

5. Watu wa Mungu wametii namna gani mwito wa Isaya na mfano wa Yesu?

5 Hivyo watu wa Mungu mwenyewe walipata uhuru kamili wakaacha mafundisho na mazoea ya dini ya uongo. Walifuata mfano ambao Yesu aliweka alipokuwa duniani, hata wao wakajitangaza kuwa “si sehemu ya ulimwengu huu,” kutia ndani siasa chafu za ulimwengu wenyewe na jeuri yao yenye kuongezeka sana. (Yohana 18:36; Ufunuo 18:2, 4) Lakini walipoinuka wakaiacha hali yao ya kukanyagiwa chini na kufikia msimamo wenye kukubaliwa mbele za Mungu, iliwalazimu kufuata hatua za Bwana wao kwa njia yenye mwelekeo mzuri zaidi, kama tutakavyoona sasa.​—1 Petro 2:21.

“Mungu Wako Anamiliki!”

6. Sasa ni “miguu” ya nani inayoleta habari njema, na ni kwa kusudi gani yeye anafika sasa?

6 Sikiliza kwa makini maneno ya nabii yanayofuata: “Jinsi ilivyo mizuri juu ya milima miguu yake aletaye habari njema, yeye aitangazaye amani, aletaye habari njema ya mambo mema [ya jambo zuri zaidi, NW], yeye autangazaye wokovu, auambiaye Sayuni, Mungu wako anamiliki [amekuwa mfalme, NW]!” (Isaya 52:7) Mjumbe huyo wa amani si mwingine ila Mfalme Yesu Kristo. Alipokuwa duniani alipakwa mafuta kwa roho ya Mungu atangaze habari njema kwa maskini, wenye kupondeka mioyo. Lakini sasa, baada ya “majira ya Mataifa” kutimizwa mwaka wa 1914, yeye ‘anakuja katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye,’ ili achukue uufalme na kuhukumu mataifa na watu wa dunia.​—Luka 4:18; 21:24; Mathayo 25:31, 32.

7. Mjumbe analeta habari gani?

7 Katika maono yako mwone Mjumbe huyo anaporuka kwa njia ya mfano kutoka mlima mmoja na kukanyaga mwingine, akiwa na hamu nyingi ya kutangaza habari njema za mambo bora kwa wale wanaomtafuta Mungu. Jinsi ilivyo mizuri “miguu” yake! Ni myepesi sana katika kumharakisha akapeleke ujumbe wake wa amani. Kwa juhudi, yeye anatangazia wokovu “binti Sayuni” aliyekuwa ametekwa, yaani, mabaki walioachwa huru wa washiriki 144,000 wa Israeli wa kiroho, halafu wanatangazia ‘mkutano mkubwa usio na hesabu kutoka mataifa yote.’​—Ufunuo 7:4, 9, 10.

8. Sasa ni tangazo gani lenye kuchochea linalotolewa, na kwa sababu gani?

8 Habari inayokaziwa katika utangazaji wa amani na habari njema ni tangazo hili lenye kuchochea: “Mungu wako anamiliki!” Mungu huyu ni nani, naye anakuwaje Mfalme? Yeye ndiye yule Mungu ambaye jina lake linadharauliwa na kutajwa mara chache sana kati ya dini za Jumuiya ya Wakristo, yaani, Bwana Mwenye Enzi Kuu YEHOVA. Yeye ndiye anayetangaza hivi katika mistari inayotangulia ya Isaya 52: “Jina langu linatukanwa daima mchana kutwa. Kwa hiyo watu wangu watalijua jina langu.” Jina lake lisilo na jingine la kulingana nalo lazima sasa liondolewe malawama kwa sababu saa yake ya kuyahukumu mataifa imefika. Lazima hayo pia yaje kumwogopa yeye kuwa “mfalme wa mataifa.”​—Yeremia 10:7; Ufunuo 14:7.

9. (a) Ni vyeo gani vinavyohusiana vya “Bwana wetu” na “Kristo wake”? (b) Wasifaji wote wa Mungu wanaweza kuwa wenye shukrani kwa sababu ya nini?

9 Mfalme mkuu huyo ndiye Bwana ambaye sauti kubwa mbinguni zimekuwa zikimtaja kuhusiana na matukio ya tangu mwaka wa 1914 na kuendelea, zikisema: “Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atamiliki hata milele na milele.” Waabudu wengine wa Mungu wanaongeza kwenye maneno hayo mengine ya kutoa sifa inayotoka, moyoni: “Tunakushukuru wewe, Bwana Mungu Mwenyezi, uliyeko na uliyekuwako, kwa sababu umeutwaa uweza wako ulio mkuu, na kumiliki. Na mataifa walikasirika, hasira yako nayo ikaja.” Katika siku hii ya ule Ufalme, Kristo Yesu anatawala akiwa Mfalme-Mshirika pamoja na Baba yake, Bwana Yehova, ambaye Yesu anafikiliza hukumu yake ya uadilifu.​—Ufunuo 11:15,17 18 12:10; Yohana 5:30.

10. Katika kutumia maneno ya Yoeli 2:32 na Isaya 52:7, Paulo alionyesha nini?

10 Huyo Mfalme-Mjumbe hayuko peke yake katika kutangaza amani. Mtume Paulo anaeleza sababu, akitumia maneno ya Yoeli 2:32 kama yafuatavyo: “Kila atakayeliitia Jina la [Yehova] ataokoka.” Halafu Paulo anauliza mfululizo wa maulizo na kuyafikisha kwenye upeo kwa kutaja maneno ya Isaya 52:7, akisema: “Basi wamwiteje yeye wasiyemwamini? Tena wamwaminije yeye wasiyemsikia? Tena wamsikieje pasipo mhubiri? Tena wahubirije, wasipopelekwa? Kama ilivyoandikwa, Ni mizuri kama nini miguu yao wahubirio habari ya mema!”​—Warumi 10:13-15.

11. Watu wengi leo wameonyeshaje kwamba wana ‘miguu mizuri’ ya kupendeza?

11 Kwa hiyo, wengine pia wana ‘miguu mizuri.’ Watu hao wametii habari njema zilizotangazwa na Mjumbe wa Mungu. Nao pia wamekuwa wahubiri wa habari njema​—jeshi la wahubiri wa Ufalme. Leo hesabu yao ni karibu milioni mbili na nusu, na kati ya hao kuna wanaume, wanawake na watoto kutoka mataifa yote ya wanadamu! Loo, ni pendeleo kubwa kama nini ulilo nalo ikiwa wewe ni mmoja wao, ikiwa unahubiri “habari njema ya mambo mema [jambo fulani lililo zuri zaidi, NW]”! Nayo miguu yako halisi ina thamani kubwa ikiwa inakupeleka kwa ukawaida nyumba kwa nyumba unapotangaza wokovu! Kwa maana katika njia hiyo wewe unakuwa na ushiriki katika utimizo wa Zaburi 19:4, ambayo Paulo anatumia maneno yake kwenye Warumi 10:18, akisema: “Sauti yao imeenea duniani mwote, na maneno yao hata miisho ya ulimwengu.”​—Ona pia Zaburi 99:1-3; 148:12, 13.

Tengenezo la Mungu Lafanya Kazi!

12. (a) Huu ndio wakati ulio wa maana zaidi ya nyakati zote wa kufanya nini? (b) Ni kweli gani zenye kutokeza zilizofanywa zikajulikana katika mwaka wa 1925?

12 Ndiyo, Mungu wako anamiliki!” Kwa hiyo sasa ndio wakati unaopita nyakati zote wa kuliinua juu jina la Mungu aliye hai, Yehova, na kumtukuza yeye kuwa ndiye Bwana Mwenye Enzi Kuu. Katika miaka ya 1920 mabaki ya watumishi wapakwa mafuta wa Mungu walishukuru sana kwamba nuru inayohusu Ufalme wa Mungu iliendelea ‘kuzukia wenye haki.’ Na hatua kubwa ilifikiwa wakati Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Machi 1, 1925 ulipochapishwa. Makala kuu ya gazeti hilo, yenye kuitwa “Uzawa wa lile Taifa,” ilieleza wazi unabii mbalimbali wenye kuonyesha kwamba Ufalme ulioahidiwa wa Mungu ulikuwa umezaliwa katika mbingu mwaka wa 1914, kwamba Mfalme wa Kimasihi alikuwa amevurumisha Ibilisi na malaika zake huku chini duniani, na kwamba ni lazima kuwe na vita ya kukata maneno kati ya tengenezo la Mungu na tengenezo la Shetani.​—Zaburi 97:11; Ufunuo 12:1-12.

13. (a) Watu wa Mungu walifanya maendeleo gani mpaka mwaka wa 1938? (b) Ni tukio gani lililotukia kwa wakati wake mwaka wa 1938?

13 Vita hiyo ya kiroho ilipokuwa ikiendelea, wale waliokuwa wakitumikia pamoja na tengenezo la Yehova waliburudishwa na miangaza-miangaza ya ufahamu wa Biblia, na hesabu yao iliongezeka mpaka katika mwaka wa 1938 watu 50,769 wakaripoti utumishi wa Ufalme wakati wa kipindi cha kutolea mataifa yote ushuhuda. Ukuzi huo wa haraka haraka ulitokeza uhitaji wa kufanya usimamizi mzuri zaidi wa mambo ya tengenezo, na Yehova aliwezesha jambo hilo katika wakati unaofaa kabisa! Matoleo mawili ya Mnara wa Mlinzi (katika Kiingereza) ya Juni 1 na 15, 1938, yalikuwa na kichwa cha habari ya kujifunza inayosema: “Tengenezo.” Yalifuatwa katika Julai na Agosti na mfululizo wenye sehemu nne wenye kusema “Vita Yake.” Mpango ulio wa kitheokrasi kweli kweli uliingizwa kati ya Mashahidi wa Yehova, na jambo hilo liliwatia nguvu wafanye vita ya kiroho ya kujikaza kweli kweli. Kama vile unabii wa Isaya, kwenye sura ya 60 mistari 17 na 22, ulivyokuwa umeonyesha, hali iliyopata maendeleo kati ya watu wa Mungu ingechochea kazi ya Ufalme wa Yehova ifanywe haraka zaidi.

14. (a) Ni nini katika nyakati za kisasa kililingana na shughuli ya ujenzi wa Sulemani? (b) Kwa sababu hiyo, ni ulizo gani linaloulizwa?

14 Makala hizo za Mnara wa Mlinzi juu ya “Tengenezo” zilionyesha ulinganifu kati ya utawala wa Sulemani wa karne ya 11 K.W.K. na ule wa Yesu aliyeketishwa juu ya kiti cha ufalme, ambao ulianza mwaka wa 1914 W.K. Sulemani alianza shughuli yake ya ujenzi katika mwaka wa nne wa utawala wake. Ilichukua miaka 7 kulijenga hekalu, na miaka mingine 13 kuimaliza nyumba ya mfalme. Vivyo hivyo, Bwana Yesu Kristo anaonekana kuwa alitimiza kazi ya ujenzi yenye kuhusiana hasa na kurudisha ibada ya kweli na kuhusiana na ujenzi wa “nyumba ya Mungu” ya kiroho wakati wa miaka ya 1918-38. (1 Petro 4:17) Gazeti la mwisho la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) lenye kusema juu ya “Tengenezo” lilimalizia kwa maelezo haya:

“Maandiko yanaonyehsa kwamba, baada ya ile miaka ishirini ya shughuli ya ujenzi wa Sulemani kama ulivyotangulia kuonyeshwa sasa hivi, yeye alianza shughuli ya ujenzi wa taifa lote. (1 Fal. 9:10, 17-23; 2 Nya. 8:1-10) Ndipo alipokuja malkia wa Sheba ‘kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya Sulemani.’ (Mt. 12:42; 1 Fal. 10:1-10; 2 Nya. 9:1-9, 12) Jambo hilo linatokeza ulizo hili: Ni nini kitakachotokea karibuni sana kwa ajili ya watu wa Yehova waliopo duniani? Sisi tutangoja tukiwa na uhakika kamili, halafu tutaona ni kitu gani.”

Basi, sisi tunaona nini sasa, miaka 46 baadaye?

Mpanuko wa Ajabu!

15. (a) Ni nani “malkia wa Sheba” wa kisasa ambaye ametokea? (b) Ni mipango gani ya kitengenezo imesaidia jamii hii, na kwa sababu gani?

15 Jamii ya “malkia wa Sheba” (NW) wa kisasa, “kondoo wengine” wa Bwana, wamekuwa wakimiminika kwa wingi “kutoka pande za mwisho za dunia” ili wasikilize hekima ya Mfalme aliyeketishwa juu ya kiti cha ufalme, Yesu Kristo. Hakika yeye ni “mkuu kuliko Sulemani.” Kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” yaani, kile kikundi cha Wakristo wapakwa mafuta ambao Bwana amekifanya kiwe tengenezo na akakipa jambo la kufanya hapa duniani, yeye amekuwa akitoa karamu ya chakula kingi cha kiroho. (Mathayo 12:42; 24:45-47) Na hata wakati Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipokuwa imewaka kufikia upeo, “mtumwa” huyo alisonga mbele akatangaze habari njema kwa mapana zaidi. Mwaka wa 1943 Shule ya Gileadi ya Mnara wa Mlinzi na Biblia ilifunguliwa huko South Lansing, New York, U.S.A. Wahudumu (maminista) wenye kustahili walipewa mazoezi wawe wamisionari, na kila miezi sita wenye kuhitimu karibu mia moja walitumwa kwenye miisho ya dunia.

16. (a) Orodha inayoambatana na habari hii inaonyesha nini juu ya mpanuko tangu mwaka wa 1943? (b) Ni matukio gani yametukia katika muda wa miaka kumi iliyopita?

16 Je! Yehova amefanikisha utendaji wa mashahidi wake uliopangwa kwa njia ya tengenezo? Orodha iliyo katika ukurasa wa 5, yenye kuonyesha wastani ya wahubiri wa Ufalme walioripoti utumishi waliompa Yehova katika vipindi vilivyotengana kwa miaka kumi-kumi tangu mwaka wa 1943, inatoa jibu. Maendeleo yaliyopatikana katika muda wa kile kipindi cha mwisho kabisa cha miaka kumi yanafaa kufikiriwa nasi kwa njia ya pekee sasa. Hiyo ilikuwa miaka ya kujaribiwa na kuchujwa (kuchungwa), kwa kuwa waasi fulani wa imani wasiotosheka waliliacha tengenezo. Lakini imekuwa miaka mizuri sana pia ya ujenzi na urekebishaji wa usimamizi wa tengenezo ulimwenguni pote, na ya kuwatia akina ndugu nguvu kwa ajili ya kazi iliyoko mbele. Sababu ni kwamba hakuna shaka kuwa ni lazima kuwe na ukusanyaji zaidi wa “kondoo” kabla ‘miji haijabomoka iwe magofu.’​—Isaya 6:11, NW; linganisha Luka 22:31, 32; Mathayo 25:31-33.

17. Kwa sababu gani sasa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wana sababu ya kufurahi?

17 Wakati wa mwaka wa 1983 kazi ya Ufalme ilifikia kilele kizuri ajabu. Kuzunguka dunia yote, nchi baada ya nchi ilianza kuripoti vilele vipya vya wahubiri katika shamba. Sanduku lililoonyeshwa hapa juu linaonyesha kadiri fulani ya furaha ambayo akina ndugu wanapata wakati Yehova anapoleta ongezeko. Kulikuwa na ukuzi mkubwa sana wakati wa miezi ya masika na ya kiangazi, mpaka ikawa kwamba shamba la ulimwengu wote sasa limefikia kilele chenye kusisimua kisichopata kuonekana tena, cha wahubiri 2,652,323​—ongezeko la 174,715 juu ya kilele cha mwaka wa 1982—katika nchi 205 mbalimbali. Sisi tunamsifu Yehova kwa sababu ya baraka hiyo!—Malaki 3:10; Kumbukumbu la Torati 28:12, 13.

18. Ile ripoti inayohusu waliobatizwa inapasa ituchochee kufanya nini?

18 Pia limekuwa jambo la kuchangamsha sana moyo kuona watu wengi zaidi wakionyesha wakf wao kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji. Kwenye “Umoja wa Ufalme” Makusanyiko ya Wilaya ya 1983, wapya wengi wameingizwa hivyo ndani ya umoja wa Kikristo katika tengenezo la Mungu. Jumla ya watu 161,896 walibatizwa mwaka wa 1983, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 17 (%) juu ya mwaka uliotangulia. Yehova na atupe sisi ‘uvuaji na uwindaji’ mkubwa tena wakati wa mwaka wa 1984! (Yeremia 16:16) Nasi tunapopata wanaostahili, acheni tuwalishe kupitia matumizi ya ustadi ya Neno la Mungu, pamoja na kutumia vile vitabu viwili vizuri vinavyoitwa Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani na United in Worship of the Only True God.​—Mathayo 10:7, 11.

19. Ripoti ya Ukumbusho wa mwaka wa 1983 inaonyesha nini?

19 Yenye kusisimua zaidi ya mambo yote ni ripoti ya Ukumbusho, uliofanywa jioni ya Machi 29,1983, katika makundi karibu 46,235 kuzunguka dunia yote. Ni watu 9,292 tu walioonyesha wana tumaini la kuishi mbinguni kwa kuishiriki mifano, wakaonyesha kwamba “kondoo wengine” ndio waliokuwa wengi zaidi kati ya wale wahudhuriaji 6,767,707—ongezeko la watu 514,920 juu ya hesabu ya mwaka wa 1982. Hakika ni halaiki kubwa ya watu wapole inayoonyesha kuwa inapendezwa na makusudi ya Ufalme wa Yehova!

20. Sasa inatupasa tukaze fikira gani kuelekea washirika wapya, na pia kuelekea watu ambao wamekuwa si watendaji, na kwa sababu gani?

20 Akiwa chini ya uongozi wa roho ya Mungu, Mfalme Daudi alitangaza hivi: “Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:11; ona pia Mathayo 5:5.) Acheni Mashahidi wa Yehova kila mahali watie bidii katika kuwajenga wapole wanaoingia katika ushirika pamoja nao, kama vile wahudhuriaji wa Ukumbusho, na pia wawatolee msaada wa kiroho wa upendo wale waliokuwa washirika wao zamani ambao huenda wakawa wameanguka katika hali ya kutokutenda. Maisha yao yana thamani kubwa kwa Yehova. (Mathayo 18:14) Ili wapate wokovu kwa kuipita dhiki kubwa, ni lazima watu hao sasa ‘wafue mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo,’ kisha waendelee kuyaweka katika hali ya weupe. “Mkutano mkubwa” na uendelee kuongezeka wakati wapole wengi zaidi na zaidi wanapoendelea kuamka wajitambulishe wenyewe kuwa watumishi wa Yehova walio wakf na kushiriki kwa furaha pamoja na watu wake katika ‘kutangaza habari njema za kitu kizuri zaidi.’​—Ufunuo 7:9, 14.

Wewe Ungejibuje?

◻ Andiko la Isaya 52:1,2 limekuwa na utimizo gani wa kisasa unaostaajabisha?

◻ Andiko la Isaya 52:5-7 linatumikaje kwa wahubiri wa Ufalme?

◻ Yehova alitayarishaje watu wake kwa ajili ya mpanuko wa wakati ujao?

◻ Kuna ushuhuda gani wa kuonyesha kwamba baraka ya Yehova imekuwapo muda wa makumi ya miaka iliyopita, na hasa wakati wa mwaka wa 1983?

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Inayofuata ni mifano tu ya ripoti za mwaka wa 1983 zilizopokewa kutoka matawi ya Sosaiti

▪ Kanada: Mwaka umekuwa wenye vilele vingi, kutia ndani wahubiri 77,003, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 13 juu ya wastani ya mwaka uliopita.

▪ Chile: Katika Agosti kilele kipya chetu cha wahubiri ambacho hakijapata kuonekana zamani kilikuwa 21,344, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 25; tulikuwa na watu 70,522 wenye kuhudhuria Ukumbusho.

▪ El Salvador: Kuanzia Januari mpaka Agosti kumekuwa na mfululizo wa vilele vya wahubiri wapya, mpaka kukaja kuwa na 12,008 wenye kuripoti, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 25, na watu 44,967 walihudhuria Ukumbusho.

▪ Ireland: Tulipanda tukafikia kilele kipya cha wahubiri 2,215 katika Agosti; wale watu 127 waliobatizwa ni ongezeko la asilimia 17.

▪ Israeli: Kilele chetu kisichopata kuonekana tena cha wahubiri 297 katika Aprili kilikuwa ongezeko la asilimia 14.

▪ Visiwa vya Ufilipino: Baada ya makusanyiko ya wilaya ya 1982, hesabu ya wahubiri iliruka kutoka 60,000 ikawa zaidi ya 70,000.

▪ Sri Lanka: Tuliripoti vilele vitano vya wahubiri vyenye kufuatana mfululizo, tukawa na kilele kisichopata kuonekana tena cha wahubiri 764 katika Mei​—ongezeko la asilimia 14.

▪ Nchi moja ya Kiafrika iliyo chini ya marufuku: Hudhurio zuri la Ukumbusho la watu 25,430 ni karibu mara mbili na nusu za wastani ya hesabu ya wahubiri.

[Grafu katika ukurasa wa 5]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Ongezeko la Ufalme Baada ya Miaka Kumi-Kumi

Wastani ya Hesabu ya Wahubiri Wanaoripoti

1943 109,794

1953 468,106 Ongezeko: 358,312

1963 956,648 Ongezeko: 488,542

1973 956,648 Ongezeko: 488,542

1983 2,501,722 Ongezeko: 845,049

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki