Mtu Kutenda Mwenzake Unyama
ILITOKEA katika nchi iliyoko Magharibi ya Afrika, mwaka wa 1961. Polisi wanaopambana na wafanya ghasia walikatiza kwa ghafula mkutano wa Kikristo wenye amani wakiwa na bunduki zilizochomekwa visu virefu. Waliwafunga pingu wanaume waliokuwapo kisha wakawapiga kinyama mpaka wakawa “kama nyama tu zilizorundikana pamoja.” Kiongozi wa mkutano huo alipata mapigo mengi sana ya rungu mpaka akatapika damu muda wa siku 90. Polisi walitazamia wanaume hao wafe.
“Mtu kutenda mwenzake unyama” ni sikitisho ambalo limetukia mara nyingi katika historia. Waashuri wa kale walitundika wafungwa wao wa vita kwenye miti iliyotumiwa kutoboa tumbo na kuingizwa moja kwa moja mpaka kwenye kifua. Warumi walikuwa na njia yao wenyewe ya kuutumia mti. Wateswa wao kwanza walipigwa vikali sana kwa mijeledi hata kwamba ngozi ya miili yao ikachanwa kutoka mifupani. Kisha walifungwa au wakapigiliwa misumari kwenye miti iliyoinuka na kuachwa wafe—polepole, kwa maumivu makali sana.
Ukatili na uhasama wa kutisha umeonyeshwa mara nyingi na makuhani wa kidini. Waazteki wa Meksiko walitolea mungu wao Huitzilopochtli wanadamu wawe dhabihu kwa kuwapasua na kung’oa mioyo ya watu hao wakiwa hai. Katika karne ya 16, hata hivyo, Hernan Cortes wa Spania aliwashinda Waazteki kwa vita. Je! dini yake ilikuwa nzuri kuliko ya watu hao? Siku hizo Baraza la Kidini la Kispania lilisimamia vyumba vya mateso ya kuogofya kisha likachoma likaua “wazushi” kwa moto. Wateswa walifungwa kwenye chombo chenye fito ambazo zilipozunguka zilivuta sana mikono na miguu yao mpaka ikaachana na sehemu za mwili zenye kuishikilia. Njia nyingine zilizotumiwa zilikuwa za kugutusha sana—lakini afadhali tusizitaje.
‘Lakini yote hayo yalitendeka wakati uliopita,’ watu wengine wanafikiri hivyo. ‘Leo watu wana huruma zaidi ya kibinadamu tena wamestaarabika.’ Je! ndivyo?
Tendo la kutesa-tesa watu halijamalizika. Ni kweli kwamba matendo mabaya sana ya kuchoma watu mbele ya umati wa wengine waliokuwa wakifurahishwa na mambo hayo bila huruma yameisha. Lakini kwa siri katika vyumba vya magereza, bado watu wanateswa-teswa kwa ukawaida—mara nyingi kwa maarifa ya hali ya juu ambayo hata hayaachi nyuma ushuhuda wa kwamba waliteswa. Katika nchi moja ya Amerika ya Kusini, mteswa aliyekuwa ameteswa-teswa kwa njia ya kisasa yenye jeuri ya kutumia nguvu za umeme alisema hivi: “Jambo moja tu linaloingia akilini ni kwamba:wanararua ngozi ya mwili wangu. Lakini hawakurarua ngozi yangu. . . . Hata hawakuacha alama zo zote mwilini kuonyesha walinitesa.”
Ripoti moja ya magazetini inadai kwamba nchi nyingi ‘zinajulikana sana kwa sifa mbaya ya kutesa-tesa na kuua wafungwa wa kisiasa.’ Ripoti hiyo inaendelea kusema:“Watu ‘wametoweka’ pia baada ya kukamatwa—wasionekane tena.” Halmashauri ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Kibinadamu imepanga orodha ya mataifa zaidi ya 100 yaliyo washiriki wa Umoja wa Mataifa kuwa “waonezi na wakatili.”
Mauaji makubwa ya ukatili yamefanywa mara nyingi katika muda wote wa karne hii ya 20. Mwaka wa 1915-16 jeshi lenye kushambulia lilitumiwa kuhamisha kwa nguvu sehemu iliyo kubwa ya Waarmenia, na wakati wa shughuli hiyo labda Waarmenia milioni moja waliuawa. Inakadiriwa kwamba kwa sababu ya mapinduzi ya utawala katika Urusi, raia milioni 14 walikufa kati ya mwaka wa 1914 na 1926. Katika China, kuanzia mwaka wa 1949 mpaka 1958, kati ya watu milioni 15 na 30 waliangamia katika “shughuli za kumaliza watu wasiotakwa kisiasa.” Mauaji makubwa ya kuangamiza Wayahudi yamefanywa sana kwa karne nyingi; lakini hakuna yo yote ya hayo yaliyokuwa ya unyama sana au ya muda mrefu kama yale machinjo yaliyofanywa juu ya Wayahudi zaidi ya milioni sita chini ya utawala wa Hitler.
Lakini, kuna dhambi za kuepuka kutenda mambo fulani na pia za kutenda mambo fulani hasa. Unyama unaweza kujifunua wenyewe kwa kujifanya huoni hali ya wenye shida. Katika kisa cha kujaribia tu kilichofanyika hivi majuzi katika Afrika Kusini, mwanamke mmoja alilala fofofo kando ya motakaa yake aone kama mtu ye yote angesimama amsaidie. Hakuna aliyefanya hivyo kwa muda wa siku mbili.
Unyama unaonekana wazi pia katika nchi zenye masazo ya chakula. Chakula hicho kinafanywaje? Kiasi kingi kinaharibiwa. Na hata hivyo, kulingana na ripoti ya Umoja wa Mataifa ya mwaka wa 1982, watoto wadogo 40,000 wanakufa kwa ukosefu wa chakula kinachofaa na kwa kuambukiwa na magonjwa—kila siku!
Basi, “mtu kutenda mwenzake unyama” kunaendelea hata katika kizazi chetu “chenye nuru ya elimu.” Lakini mambo yalianzia wapi? Je! kuna mtu anayeweza kuyakomesha?