1914—Mahali pa Makutano
“MAMBO ambayo yangetokea barabara katika 1914 sisi hatukujua wakati huo, lakini tulikuwa na uhakika juu ya jambo moja: Mwaka 1914 ndipo ungeanza wakati mbaya zaidi wa taabu ambao haukuwa umetokea duniani mpaka wakati huo; kwa maana unabii mwingi sana wa Biblia ulitabiri hivyo. Imani yetu ilikuwa yenye nguvu na matumaini yetu yalitegemea zaidi ya kuwazia-wazia kwa kibinadamu tu.”
Kwa maneno hayo, A. H. Macmillan, mbuni wa kitabu chenye kuuzwa sana cha 1957, Faith on the March, akasimulia usadikisho wake wa mapema kwamba mwaka 1914 ungekuwa mahali pa makutano ya unabii wa Biblia. Miaka zaidi ya 40 baada ya 1914, usadikisho wake haukuwa umedhoofika.
Matukio Yanapokuja Pamoja
“Mahali pa makutano” panaelezwa kuwa “mahali pa katikati pa utendaji au faida: mahali ambapo mistari ya tendo inapokuja pamoja.” Je! mwaka 1914 ulikuwa mahali pa makutano kwa maana hiyo? Ndiyo. Ebu yafikirie yale ambayo Macmillan na Wanafunzi wa Biblia wengi wengine walitazamia katika mwaka huo.
Toleo la Machi 1880 la Mnara wa Mlinzi wa Sayuni na Kutangaza Kuwapo kwa Kristo (Kiingereza) lilisimulia matukio mawili yenye umaana wa kutikisa dunia ambayo yalitazamiwa kuwa yangetokea katika mwaka 1914: “‘Nyakati za Mataifa’ zitaendelea mpaka mwaka wa 1914, na ufalme wa kimbingu hautatawala kikamili mpaka wakati huo.” Kwa hiyo, Wanafunzi wa Biblia wengi walitazamia Ufalme wa Mungu usimamishwe kikamilifu katika mwaka huo. Hiyo ingemaanisha kuanza kwa wakati wa Kristo ‘kwenda hali akitiisha katikati ya adui zake.’ Kwa lazima pia, ingemaanisha mwanzo wa “Umalizio wa mfumo [mbovu] wa mambo.”—Zaburi 110:1, 2, NW; Mathayo 24:3, NW; Ufunuo 12:10, 12.
Wanafunzi wa Biblia hao wanyofu walifikia kukata maneno hivyo baada ya kurudia kuchunguza elimu ya tarehe ya Biblia.a Lakini elimu ya tarehe za Biblia ilikuwa mstari mmoja tu wa ushuhuda—shahidi mmoja. Kulingana na Biblia, Ufalme wa Mungu ungekuwa wa kimbingu, na kwa hiyo usioonekana. Kwa hiyo wanafunzi wa Biblia wangejuaje kama matumaini yao yalikuwa yametimizwa au hayakutimizwa? Wangehitaji uthibitisho wenye kuonekana, ishara.
Wanafunzi wa Yesu walikuwa wameomba ishara hiyo waliposema: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3, NW) Kwa kutoa ishara hiyo, Yesu alitoa ushuhuda wa shahidi wa pili kuonyesha wazi mwaka wa 1914. Jambo hilo lilipatana na kanuni ya Biblia “kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike.”—Mathayo 18:16.
Ingawa vidokezo vya tarehe za Biblia vinaelekeza mbele kwenye mwaka wa 1914, ishara yenye sehemu mbalimbali iliyotolewa na Yesu ilikusudiwa ielekeze nyuma kwenye mwaka wa 1914 kuwa mwanzo wa kipindi kipya cha wakati. Kwa hiyo mwaka wa 1914 ulipasa kuwa “mahali ambapo mistari ya tendo inakuja pamoja.”
Je! ndivyo ulivyokuwa? Je! ishara ambayo Yesu alitoa kweli kweli inaweza kutambuliwa katika matukio ya tangu mwaka 1914? Tunakukaribisha uchunguze jambo hilo halafu ujijibu mwenyewe.
[Maelezo ya Chini]
a Hesabu ya wakati yenye kuonyesha kwamba “Nyakati za Mataifa” zilikwisha mwaka 1914 ilizungumzwa kirefu katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1984.