Ona Baraka za Umoja wa Ufalme!
“Wote wawaonao watakiri ya kuwa wao ni kizazi kilichobarikiwa na [Yehova].”—ISAYA 61:9.
1. (a) Ni uandalizi gani wa Yehova wa kisasa unaoonyesha ukarimu wake kuelekea umati mkubwa usiomjua bado? (b) Watu wake mwenyewe waliobarikiwa wanatambulishwaje?
TANGU mwaka wa 1914 Mfalme wa kimbingu amewekwa juu ya kiti cha ufalme akapewa uwezo wa kutawala. Na uandalizi umetolewa wa tengenezo la kidunia lililo chini ya “wana wa kifalme” ambao wanatawala kwa ajili ya haki yenyewe. (Isaya 32:1, 2, NW) Katika hayo yote, Yehova amekuwa mkarimu kwa wale wote wenye njaa na kiu ya uadilifu. Na wenye njaa na kiu wanamiminikia watu ambao Yehova amebariki hivyo. Lakini wanawatambuaje? Je! wao ni mashuhuri katika mambo ya kijamii, kisiasa au kifedha? Hapana, hawatambuliki kwa yo yote ya sababu hizo. Wanatambulika kwa sababu wanaonyesha alivyo Mungu wao mkarimu kwa nia yao ya kushiriki na wengine baraka ambazo tayari wamepokea.
2. Kwa kupatana na Isaya 32:8, ni sifa gani iliyo wazi kati ya watumishi wa Yehova duniani leo, na hiyo ni kwa sababu wametii shauri gani la Kiongozi wao?
2 Mungu huyo mkarimu amefunza watumishi wake wawe wakarimu pia. Kuhusu mtu mwenye elekeo la kuwa mkarimu andiko la Isaya 32:8, NW, linasema: “Kwa habari ya mkarimu, ametoa shauri kwa ajili ya mambo makarimu; na yeye mwenyewe atainuka kwa kupendelea mambo makarimu.” Kama vile tu Yesu alivyoweka kando mapenzi yake mwenyewe na kujinyima mambo mengi ili atimize mgawo aliopewa na Mungu wa kushiriki habari njema tukufu za Ufalme pamoja na wengine, ndivyo wafuasi wake walivyoazimia kufanya jambo ilo hilo. Wanasikiliza shauri la Yesu: “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.” (Luka 6:38) Yehova na Kristo Yesu ndio wanaoweza na ndio watakaorudisha ukarimu huo wa watumishi wao kwa kuwapa uradhi, amani ya akili na furaha katika matunda ya utumishi wao wa ushikamanifu unaohusu faida za Ufalme.
3. Nia ya watumishi washikamanifu wa Yehova inatofautianaje na ile ya watu wa Jumuiya ya Wakristo na wenye kuiunga mkono?
3 Nia ya ukarimu, ya bidii ya waenezaji wasio wanyimivu wa habari njema inatofautiana na ile ya wengine. Nabii wa Mungu anasema juu ya msiba kwa wanawake ambao walikuwa ‘wapenda raha’ wasiojali katika Yerusalemu wenye kukosa uaminifu. (Isaya 32:9-14) Nia yao huenda ikatukumbusha juu ya wengine wanaodai kuwa watumishi wa Mungu na Kristo, lakini ambao hawana bidii au juhudi kwa ajili ya utumishi wa Yehova. Hakika, huenda tukawafikiria wale waliomo katika Jumuiya ya Wakristo na wale ambao hawahangaikii kweli kweli umati mkubwa wenye njaa na kiu. Kushughulikia kwao mambo ya kimwili, bila kufikiria kujishughulisha na kazi aliyoamuru Yehova ifanywe katika wakati huu hasa wa historia, mwisho wake utakuwa wenye msiba tu kwao, kama vile msiba unavyoshirikishwa na ukosefu wa mavuno.
4. Ni wakati gani ujao unaowangojea wale wote wanaoendelea kushughulikia Neno la Mungu kwa udanganyifu?
4 Kuna huzuni na uharibifu tu mbele ya Jumuiya ya Wakristo na wenye kuisaidia na kuiunga mkono. Njaa kubwa ya kiroho na kwa hiyo watu kupunguka yatakuwa ndiyo matokeo ya Jumuiya ya Wakristo kukosa ukarimu na kukosa kuzaa matunda katika utumishi wa Yehova. Kwa kuwa Wakristo wote hao wa bandia wameshindwa kupanda na kunyunyiza maji vizuri, wakakosa kutumia Neno la Mungu kwa unyofu, Yehova hana jukumu la ‘kukuza.’—Linganisha 1 Wakorintho 3:6-9.
Habari Njema kwa Washikamanifu
5. Ni nini yaliyotabiriwa katika Isaya 32:15, na ni matukio gani mazuri ajabu yaliyopo mpaka mwaka huu wa 1984?
5 Jambo lenye kutia moyo wale wanaomngojea Yehova kwa subira huku wakifanyiza kazi faida za Ufalme walizoaminishwa, ni habari njema. Zimeandikwa katika Isaya 32:15 kwa maneno haya: “Hata roho itakapomwagwa juu yetu kutoka juu; hata jangwa litakapokuwa shamba lizaalo sana; nalo shamba lizaalo sana litakapohesabiwa kuwa msitu.” Roho takatifu ya Mungu imemwagwa juu ya mashahidi wake wa kisasa, sawa na ilivyomwagwa juu ya mitume na wanafunzi waliokuwa wakingojea katika Pentekoste ya mwaka 33 W.K. (Matendo 2:1-4, 14-18; Yoeli 2:28, 29) Matokeo yamekuwa kwamba watumishi washikamanifu wa Yehova duniani wamejishughulisha katika kazi ya kufanya wanafunzi zaidi. Kama walivyofanya katika Pentekoste ndivyo wanavyofanya sasa. Hasa katika mwaka wa 1919 na 1922 roho ya Yehova ilimwagwa juu ya watu wake, na kuanzia sana-sana mwaka wa 1922 mkazo mkubwa ulitiwa katika kazi ya kuhubiri Ufalme. Utendaji huo umeendelea na kupanuka mpaka katika mwaka huu, wa 1984, zijapokuwa hali zenye msukosuko zenye kuenea duniani. Hesabu ya watangazaji wakarimu wa habari njema imefurika kutoka hesabu ndogo ya watangazaji 7,000 au 8,000 mwaka wa 1922 ikawa kilele kikuu cha 2,652,323 leo.
6. Kumekuwako matokeo gani mengine mazuri ajabu kutokana na kumwagwa kwa roho takatifu juu ya tengenezo la kidunia la Yehova?
6 Hakika ‘roho takatifu iliyomwagwa’ imetokeza uzaaji wa matunda. Hatushiriki tena hali ya jangwa ya ulimwengu wa Shetani, wala njaa ya kiroho ya kutaka kusikia Neno la Yehova. (Ezekieli 36:29, 30) Tangu Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. na kuendelea, Mungu amepanda “miti mikubwa”—Wakristo walio imara, kakawana—katika shamba la kiroho la watu wake. “Miti” hiyo yenye heshima, yenye kuzaa matunda, ‘iliyopandwa na Yehova,’ imekua na kufanikiwa ikawa msitu kamili kwa kuwa tengenezo linaloonekana la waabudu wa Yehova linawapa wote wenye nia uvuli wenye kuburudisha na chakula na maji ya kiroho kutoka kwa Mungu.—Isaya 61:3, NW.
7. Ni nini kimesukuma mkutano mkubwa wa watu wenye mioyo minyofu wamiminike kwenye tengenezo linaloonekana la Yehova?
7 Watu wenye mioyo minyofu wanaomiminika sasa kwenye tengenezo la kitheokrasi la Yehova linaloonekana wanavutiwa na maajabu ya paradiso ya kiroho. Hakuna mahali penginepo duniani wameona uadilifu na haki. Wamechoka na viongozi wa kidini wasio na imani, wanasiasa wenye kujitumikia na matajiri-wakubwa wa biashara yenye pupa. Macho yao yamefunguliwa wakaona jamii ya wanaume na wanawake wenye kumwogopa Mungu ambao kati yao wapumbavu na watu wasioongozwa na kanuni hawapakwi kwa chokaa nyeupe ili waonekane kuwa watu wa heshima; katika jamii hiyo mwenendo usio wa kimungu na usio wa Kikristo unakaripiwa na wazoeaji wa uchafu na uovu wanachukuliwa hatua upesi sana.
8. Andiko la Isaya 32:16 limetimizwaje juu ya watu wa Yehova leo?
8 Nabii huyo anaendelea na ujumbe wake uliotolewa na Mungu, akisema: “Ndipo hukumu itakaa katika jangwa, na haki itakaa katika shamba lizaalo sana.” (Isaya 32:16) Bila shaka, haki na uadilifu vinakaa katika tengenezo la kitheokrasi la Yehova linaloonekana. Kwa wazi, watumishi wote wa kweli wa Mungu wanatambua kwamba kila walicho nacho na wanachofurahia, kutia ndani msimamo wao wenye pendeleo pamoja na Yehova, wamekipata kama fadhili zisizostahilika. Uadilifu wao ni wa Mungu.
9. Kazi za mashahidi waaminifu wa Yehova zinatofautianaje na kazi na nia za viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo?
9 Jambo hilo ni tofauti sana na msimamo wa kujionyesha wenye haki na watakatifu ulio wa watu mashuhuri katika Jumuiya ya Wakristo. Huo ni uadilifu unaothibitishwa na matendo—matendo yanayomletea Yehova sifa na faida kwa viumbe wake watiifu wa jamii na lugha zote. Tendo moja kubwa kati ya hayo ni kutangaza Mfalme ambaye anatawala sasa kulingana na mapenzi ya Mungu. Hakuna tengenezo jinginelo la watu linaloshiriki kutangaza jambo hilo la hakika lenye kufurahisha. Na kila msikiaji wa ujumbe huo mwenye moyo mnyofu, naye, ana tamaa ya kuwapasha jirani zake habari inayohusu baraka za umoja wa Ufalme.
Baraka za Amani
10. Isaya anaendelea kueleza nini katika unabii kwenye sura ya 32, mstari wa 17?
10 Kazi hii ya duniani pote yenye kuenea, utumishi mtakatifu, inasonga mbele ikiwa katika mazingira ya kitengenezo yenye amani, utulivu na usalama kama Isaya anavyoendelea kueleza katika sura ya 32, mstari wa 17, wa unabii wake, akisema: “Na kazi ya haki itakuwa amani; na mazao ya haki yatakuwa ni utulivu na [usalama] daima.” Uadilifu huo wa kweli ndio ambao watu wenye kumwogopa Mungu wa jamii na lugha zote wamekuwa wakitafuta, na sasa wanauona katika tengenezo la Mashahidi wa Yehova. Humo kuna amani, kwa maana kila mtu anashirikiana, akiwa na ‘mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.’—1 Wakorintho 15:58, NW.
11. (a) Ni nani ambao hawana mahali katika tengenezo la Yehova? (b) Wanakusanywaje na kutolewa nje, na matokeo yanakuwa nini kwa watumishi washikamanifu wa Yehova?
11 Kati ya watu wa Mungu, hakuna mahali pa watu wanaosema-sema na huku wanajikalia tu wala wasiotaka kufanya kazi katika utumishi wa Yehova. Kwa kweli, ahadi iliyodokezwa katika mfano wa Yesu katika Mathayo 13:24-30, 39, 41 sasa inatimizwa. Wavunaji wa kimalaika ‘wanakusanya kweli kweli kutoka tengenezo lake la Ufalme vitu vyote vyenye kuchukiza na watu watendao maasi.’ Malaika wanaweza kutambua ni nani walio watumishi wa Yehova wa kweli na walio wa uongo. Wanaweza kabisa kutokeza hali ambazo katika hizo watenda uovu wanafunuliwa na kufukuzwa kutoka ushirika wa Wakristo wa kweli. Na matokeo yanakuwa nini? Tengenezo lenye afya, lenye kutenda ili kumletea Yehova sifa na kusogeza mbele Ufalme wake chini ya Yesu Kristo.
12. (a) Yehova anawapa watu wake mahakikisho gani yenye nguvu kama inavyoelezwa katika Isaya 32:18? (b) Ni matukio gani yanayokuja ambayo yametangulia kuonyesha dalili, na washikamanifu wa Yehova wanapatwaje na hayo?
12 Isaya anaendelea kutangaza hivi (32:18): “Na watu wangu watakaa katika kao la amani; na katika maskani zilizo salama, na katika mahali pa kupumzikia penye utulivu.” Kweli kweli Yehova amewapa watumishi wake waaminifu duniani mahali na kazi ambayo hakuna mtu atakayeruhusiwa awafukuze wasiifanye. Wataendelea kuwapo mpaka Yehova atimize kusudi lake kwao katika upande huu wa Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Katika kisa chao, Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, imekwisha kuanguka. Nguvu zake zinapungua haraka sana. Hata sasa, sehemu-sehemu za mnyama-mwitu anayesimuliwa katika Ufunuo sura ya 17 zinamtazama, zikijitayarisha kula nyama yake na kumteketeza kabisa kwa moto. (Ufunuo 17:16) Lakini mashahidi wa Ufalme hawatiwi wasiwasi hata na matukio hayo yaliyo karibu kutokea. Wao hawashiriki woga na kuvunjika moyo kwa watu wa ulimwengu. Kwa kuwa Yehova ametubariki kwa kutupa maarifa ya kimbele ya matukio yanayokuja, tunaweza kukabili wakati ujao tukiwa na uhakika matokeo yatakuwa nini. “Wana amani nyingi waipendao sheria yako [Yehova], wala hawana la kuwakwaza.”—Zaburi 119:165.
13. Ni maendeleo gani makubwa ambayo Yehova ameleta katika tengenezo lake linaloonekana, na yamekuwa na matokeo gani juu ya nia na kazi ya watu wake?
13 Katika Isaya 60:17 nabii huyo alitabiri kwamba utaratibu wa kitheokrasi na njia za kufanya mambo kati ya watumishi wa kidunia wa Yehova zingefanyiwa maendeleo. Alionyesha jambo hilo kwa kuweka shaba, fedha na dhahabu mahali pa vitu vinavyoteketea kwa moto na vyuma vya hali ya chini. Kisha twasoma: “Tena nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, na hao [wakupao kazi] kuwa haki.” Wote katika tengenezo hili lenye kuutangaza Ufalme wanafurahi kutumikia pamoja kwa amani, kwa maana kazi zao zote, hata wawe wanashiriki katika sehemu gani ya utumishi, zinakamatana na utangazaji wa Ufalme duniani pote. Wote wanaona jicho kwa jicho, na wote wanahangaikia kuimaliza kazi. Ni tofauti kama nini na vita vyenye kuendelea vya choyo kati ya wafanya kazi na matajiri wao, vita vinavyotokeza matatizo mengi sana katika ulimwengu unaotuzunguka! Wote katika tengenezo la Yehova, hata wawe wana cheo gani, wanafundishwa na Yehova na kwa hiyo wanaweza kuendelea na kazi yao katika amani na utaratibu mzuri.—Isaya 54:13.
14. Ni wakati gani ujao ulio tofauti kabisa unaokabili (a) watu wa Yehova wenye bidii? (b) Jumuiya ya Wakristo na marafiki wake wote wa kisiasa?
14 Watu hao waliobarikiwa na wenye bidii wataendelea kuwa katika hali ya utulivu hata mwisho wa mfumo wa mambo wa Shetani unapofika kwa ughafula wenye kushangaza. Utekelezaji wa hukumu ya Yehova, kama dhoruba ya mvua kubwa ya mawe juu ya Jumuiya ya Wakristo na ulimwengu wote, utaangamiza adui kabisa. Lakini watu wa Mungu watakuwa salama chini ya ulinzi wake wakati “msitu” mkubwa wa majeshi yenye silaha ya Shetani utakapofyekwa kabisa, kama andiko la Isaya 32:19 linavyotabiri: “Mvua ya mawe itakunya, wakati wa kuangushwa miti ya msituni; na huo mji utadhilika.” Kupitia hali hiyo yote yenye kutetemesha ulimwengu, watumishi wa Yehova watakuwa wenye utulivu kwa sababu ya uhakikisho wa kwamba “malaika wa [Yehova] hufanya kituo, akiwazunguka wamchao na kuwaokoa.”—Zaburi 34:7.
Kazi Kubwa Sana Itamalizwa
15. Ni kazi gani ambayo ingali ifanywe na watu wa Yehova?
15 Kwa sasa, kuna kazi kubwa sana ambayo ingali itamalizwa maadamu Yehova angali anatoa nafasi kwa umati mkubwa katika mataifa yote waje wafunguliwe macho na masikio yao ili waelewe umaana wa ujumbe wa wokovu. Kweli kweli wenye furaha ni wale wanaojitoa wenyewe bila unyimivu kwa ajili ya utumishi huo wa Ufalme, kwa bidii sana wakipanda mbegu za ukweli wa Ufalme kati ya watu wa mataifa yote! Ubarikiwa huo ni kama ule unaosimuliwa katika mstari wa mwisho wa Isaya 32, unaosema: “Heri ninyi mpandao mbegu kando ya maji yote, na kuiacha miguu ya ng’ombe na punda waende ko kote.” Wanyama hao walikuwa wanyama wa kubeba mizigo ambao walitumiwa na watu wa kale wa Mungu ili kulima nchi wapande mbegu. Vivyo hivyo leo, Yehova ametoa vyombo vinavyohitajiwa na mashahidi wake wa kisasa ili upandaji wa ukweli wa Ufalme utimizwe kwa haraka sana na kwa matokeo, wakiwa na tumaini lenye uhakika kwamba Yehova ataongeza baraka zake kwa kutokeza mavuno makubwa.
16. Tuna ushuhuda gani kwamba sasa Yehova anabariki sana mashahidi wake wa Ufalme duniani pote?
16 Tunapokagua shamba, ambalo ni ulimwengu, je, hatuoni baraka za wazi za Yehova juu ya jitihada zetu za kuhubiri ujumbe wa Ufalme kwa juhudi na kwa ukawaida? Makao ya tawi makubwa zaidi na yaliyofanyiwa maendeleo ni maskani ya hesabu yenye kuongezeka ya wahudumu-wafanyi kazi wenye nia ambao wanahitajiwa ili kuangalia kazi kubwa ya Betheli katika nchi nyingi. Vifaa vya uchapaji vya kisasa na njia zenye kuokoa wakati zimeanzishwa katika nchi baada ya nchi, hata utengenezaji wa Biblia, vitabu vya Biblia na magazeti ukaongezeka sana. Hesabu zenye kuongozeka za watumishi wa Mungu walio wakfu na kubatizwa wanajitoa kwa moyo wa kupenda watumikie wakiwa mapainia wa kawaida na wasaidizi, wakitumia wakati kila siku katika utumishi wa lazima wa kupanda ukweli wa Ufalme katika mioyo ya wengi. Watangazaji wa Ufalme katika karibu makundi yote wanajitahidi kuongeza huduma yao, wakifanya hivyo kwa kuthamini sana baraka ambazo tayari amewamiminia.
17. Ni jambo gani la pekee sana juu ya Mashahidi wa Yehova na kazi yao katika siku zetu?
17 Ni Mashahidi wa Yehova peke yao wanaoshiriki katika kazi hiyo ya kutoa uzima kwa niaba ya serikali ya Ufalme wa Mungu. Ni wao peke yao wanaofurahia mavuno ambayo hata sasa yanaonekana. Pia, mbegu ambayo Yehova anatoa kwa wafanyi kazi wake wa shambani wenye nia imekaguliwa vizuri sana na kuchaguliwa vizuri sana! Vifaa vyetu vya funzo la Biblia vimetayarishwa vikiwa na kusudi la kuchochea mioyo ya wengi ambao wangali wavunwe na kuletwa katika tengenezo lenye amani la Yehova, kundi la Kikristo, ambalo katika Mathayo 13:30 linafananishwa na ‘ghala’ la Mwanaye.
18. Kwa sababu gani twapaswa kuazimia kuendelea mbele katika utumishi wetu wa Ufalme tukiwa na uradhi na furaha?
18 Kweli kweli, tumo katika siku ya Yehova, siku ya kuona utimizo wa “ahadi kubwa mno, za thamani” kwa watu wake waliojitoa. (2 Petro 1:4) Amani na umoja zinasitawi kati yetu. Tumepewa ufahamu ulio wazi wa makusudi ya Mungu wetu. Tuna amani ya akili katikati ya watu wa ulimwengu wenye hofu na wasiwasi. Wakati ujao wenye kujawa na baraka kubwa zaidi unatungojea. Je! hatuna furaha nyingi sana kuwa wapokeaji wa baraka hizo zote za umoja wa Ufalme? Na je, si tumeazimia kusonga mbele na kazi yetu ya Ufalme imletee sifa Yehova milele?—Kutoka w5/15/84.
Jibu Lako Ni Nini?
◻ Nia ya watumishi wa Yehova inatofautianaje na ile ya waliomo katika Jumuiya ya Wakristo?
◻ Kumiminwa kwa roho takatifu ya Mungu kumetokeza nini?
◻ Kupatana na Isaya 32:17, 18, watu wa Yehova wanafurahia baraka gani sasa?
◻ Tuna uthibitisho gani kwamba Yehova anabariki mashahidi wake wa Ufalme?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Uhitaji wa ‘kutangaza Mfalme na Ufalme’ ulikaziwa katika kusanyiko la watu wa Yehova huko Cedar Point, Ohio mwaka wa 1922
[Picha katika ukurasa wa 19]
Yehova amebariki watu wake kwa kuwapa amani na umoja wa ulimwenguni pote